Usalama Sasa na Milele
MUUMBA wetu, anayejua ubora wa kila kitu, aliongoza watu kwa roho yake watoe shauri hili: “Azitegemeaye mali zake ataanguka.” “Hakuna mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu.” “Farasi hafai kitu kwa wokovu, wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake” (Mit. 11:28; Zab. 33:16, 17) Yesu Kristo alisema kweli kwamba “hata mtu anapokuwa na vingi na kusaza, mali yake haimpi uzima.”—Luka 12:15, The New English Bible.
Bila shaka, katika hali yenye kuharibika zaidi na zaidi ya uhalifu, huenda tukachukua hatua fulani zinazofaa ili tulinde uzima na mali zetu. Walakini twapaswa kukubali kwamba hatua hizo ni za muda nazo hazitoi uhakika wa usalama kwa njia yo yote. Jambo ambalo tunatamani kweli kweli ni uhakikisho wa kwamba hakuna hali kadha wa kadha za kutoka nje zitakazotuletea madhara ya kudumu. Je! inawezekana kuishi tukiwa na uhakika huo? Je! kuna chanzo cho chote cha nguvu na chenye mamlaka kinachoweza kufanya maisha yetu yawe salama sasa na hata milele? Je! tunaweza kuishi kwa usalama hata tunapotishwa na jeuri, upungufu wa chakula au kuharibika kwa hali ya uchumi?
Usalama wa Kweli Waonyeshwa
Hapa kuna jambo la kufikiria: Sababu gani katika Israeli ya kale, jamaa zingeweza kuondoka nyumbani na vijijini mwao bila kuacha ulinzi na kufunga safari kwenda Yerusalemu kwenye sikukuu zao za kidini hata ingawa walikuwa wamezungukwa na mataifa adui? Inawezekanaje kwamba wakati Yerusalemu ulipoelekea kuzingirwa na jeshi lenye nguvu la Ashuru hakuna hata tone moja la damu ya Mwisraeli lililomwagika na hali askari adui 185,000 walikufa usiku mmoja? (2 Fal. 19:32-35) Inawezekanaje kwamba taifa la wanaume, wanawake na watoto milioni tatu liliishi kwa miaka 40 katika “jangwa kubwa na baya sana lenye nyoka wenye sumu na nge, nchi ya kiu na ukavu”?—Kum. 8:15, NE.
Yehova Mungu wao, Muumba wa vitu vyote, ndiye aliyekuwa akifanya maisha yao kuwa salama. Ikawa kama vile tu mtunga zaburi Daudi aliyeongozwa na Mungu alivyosema: “Katika amani nitajilaza na kulala usingizi, kwa kuwa wewe peke yako, Ee Yehova, wanifanya nikae katika usalama.”—Zab. 4:8, NW.
Je! una mashaka kwamba Yehova Mungu, Baba yetu wa kimbinguni, anaweza kutuangalia katika karne ya 20 katika njia ile ile aliyowaangalia Israeli nyuma kule? Tuseme mkuu wa benki ya kwenu angekuambia hivi: “Sitaki uwe na wasiwasi wa jambo lo lote. Niambie tu unayohitaji nami nitakupa.” Je! ahadi hiyo isingeondoa wasiwasi wako juu ya usalama? Bila shaka, haielekei kwamba mkuu wa benki anaweza kutoa uhakikisho huo. Hata hivyo, Yehova Mungu amekwisha kuhakikishia watumishi wake wote waaminifu kwamba atayaangalia mahitaji yao yote. (Mt. 6:31-33) Twaweza kuwa na uhakika kamili katika jambo hilo kwa sababu Aliye Juu Zaidi sikuzote anatimiza ahadi zake, kama inavyoonyeshwa na mifano, ya wakati uliopita na wa sasa.—Yos. 21:45.
Mfalme Sulemani mwenye hekima alikuja kutambua ubora wa kadiri wa vitu vya kimwili na wakati uo huo akapata uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu uliomwezesha kuishi katika usalama. Sulemani aliandika hivi: “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake.” (Mit. 18:11) Ni kweli kama nini—“katika mawazo yake”! Mtu tajiri anawaza kwamba mali hiyo itamlinda msiba unapokuja. Lakini mambo yaliyotokea yameonyesha mara nyingi kama nini kwamba “ukuta” huo wa ulinzi ni jambo lisilo la kweli nao hautoi ulinzi wo wote katika nyakati za kuharibika kwa uchumi, infuleshoni isiyozuilika, msukosuko wa kisiasa au maradhi yenye kuua!
Katika Mithali 18:10, Sulemani anatofautisha kwa njia hii: “Jina la [Yehova] ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Hakuna hatari ya kadiri yo yote wala hali fulani zinazoweza kumweka mtumishi wa Mungu katika mahali asipoweza kupata msaada wa kimungu. Hapa, basi, ndipo palipo chanzo cha usalama wa kweli—uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Baba yetu mwenye upendo.—Zab. 59:16, 17; 62:5-8.
Tunaweza Kuhakikishiwaje Ulinzi?
Uhakika huo hausitawi mara moja Kama vile mti unaokuwa na nguvu mwaka baada ya mwaka, wenye kuwa imara baada ya kila upepo mkali, imani yetu kwa Yehova inatiwa nguvu tunapoona njia zake za haki zikitenda kwa ajili ya mambo bora zaidi maishani mwetu. Kujifunza kwetu Neno lake kila siku, wakati tunaotumia tukihubiri “habari njema,” kumfikia kwa sala kwa ukawaida—yote hayo yanatokeza kifungo hicho cha kibinafsi.
Isaya alisimulia namna ya usalama ambao tunatamani kwa maneno haya: “Huyu ndiye atakayekaa juu; majabali ni ngome yake; atapewa chakula chake; maji yake hayatakoma.” (Isa. 33:16) Hata hivyo, usalama huo ni wa wale wanaotamani kuishi maisha yanayotokeza hali njema ya wengine. Isaya aliandika hivi pia: “Ni yeye aendaye kwa haki, anenaye maneno ya adili; ni yeye anayedharau faida ipatikanayo kwa dhuluma; akung’utaye mikono yake asipokee rushwa; azibaye masikio yake asisikie habari za damu; afumbaye macho yake asitazame uovu.” (Isa. 33:15) Matakwa hayo ili kupata ulinzi wa Mungu yanahusuje katika nyakati za kisasa?
‘Haki yenye kuendelea’ (NW) inaonyesha kufuata kila siku kanuni za haki za Yehova au unyofu. Maneno ‘kudharau faida ipatikanayo kwa dhuluma’ yanatukumbusha kwamba hatupaswi kuiga njia za kutajirika haraka za ulimwengu. Pamoja na kukataa kukubali rushwa, kutokukubali kamwe zawadi au faida ya kimwili iharibu uamuzi, mtu anayetaka kuwa na kibali ya Yehova anapaswa kuwa mtu ‘azibaye masikio yake asisikie habari za umwagaji wa damu; afumbaye macho yake asitazame uovu.’ Sinema za karne ya ishirini, vitabu na magazeti vyote hivyo manabii hawakuwa navyo, lakini mtu anayetamani urafiki wa karibu pamoja na Yehova ataepuka tafrija zenye jeuri na za uasherati za leo.
Kushikamana kwetu na kanuni za haki kunatokeza kufurahia kwetu usalama. Mfalme Sulemani mwenye hekima alijumlisha jambo hilo kwa maneno machache: “Aendaye kwa unyofu huenda salama.”—Mit. 10:9.
Nyakati nyingine, baadhi ya Mashahidi wa Yehova pia wameona jambo ambalo wamechukua kuwa ni ulinzi wa kimungu. Chukua, kwa mfano, Ndugu Z——. Alikuwa akisoma Mnara wa Mlinzi katika gari lake siku moja wakati mtu alipomkamata shingo kwa ghafula. Aliomba Yehova kwa bidii. Mshambuliaji huyo aliduwaa, nayo mikono yake ikalegea. Ndugu Z—— akatia gari moto, akampa kwa heri naye akamwacha mtu huyo akiwa amesimama kama sanamu katikati ya barabara.
Halafu alikuwako misionari kutoka Kenya. Wazazi wake walikuwa wanapinga vikali alipoanza kutumikia Yehova. Baba yake alimtisha na kifo kama asingewaacha wale “nyani weupe,” kama alivyowaita Mashahidi. Alikodisha wahuni wamwumize. Yeye anaripoti hivi: “Ulinzi wa Yehova uliniwezesha nisikamatwe nao kamwe.”
Kama ambavyo mambo hayo yaliyoonwa yanavyoonyesha, Wakristo wanalazimika kuelekeana na hali zenye hatari. Hata hivyo, kwa tumaini kamili katika Yehova, twaweza kuwa na hakika kwamba hakuna cho chote kitakachoweza kutuletea madhara yenye kudumu hata kidogo. Baba yetu wa kimbinguni ameahidi hivi: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, [Yehova] ndiye anisaidiaye, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?”—Ebr.13:5, 6.
Hivi karibuni jamaa yote ya kibinadamu itapatwa na hatari ambayo itaharibu zinazoonekana kuwa kuta zenye kutoa ulinzi zinazotolewa na mali, uweza wa kijeshi au uwezo wa kisiasa. Ni wale tu ambao wametumaini mkono wa Yehova usioonekana wenye nguvu ndio watakaookoka na kufurahia usalama milele chini ya utawala wenye haki wa ufalme wa Mungu. (Ufu. 21:1, 4) Hilo na liwe fungu lako lenye furaha kwa kuwa ulisitawisha kifungo cha kibinafsi cha karibu pamoja na Aliye Juu Zaidi.