Usalama wa Duniani Pote Jinsi Gani?
WAZIA ukiishi katika dunia isiyo na hatari na shida. Hiyo ndiyo maana ya usalama wa duniani pote. Je! ni ndoto tu?
Sivyo. Fikiria siku za Mfalme Sulemani wa kale. Kwa habari ya utawala wake wenye hekima, Biblia hutaarifu hivi: “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake . . . siku zote za Sulemani.”—1 Wafalme 4:25.
Somo Kutoka Utawala wa Sulemani
Masimulizi ya Biblia yasiyo ya kikawaida, kama hayo yaliyotangulia, hupuuzwa na watia-shaka kuwa yameongezewa chumvi. Hivyo, huenda mtu fulani akauliza hivi: ‘Nawezaje kuwa na uhakika kwamba utawala wa Sulemani si hadithi ya kutungwa tu?’ Uthibitisho wa akiolojia usio wa moja kwa moja unatokezwa baada ya makala hii. Bila shaka, uthibitisho mzuri kabisa wa uhalisi wa utawala wa Sulemani ni kwamba umeripotiwa katika Neno lisilokosea la Mungu aliye hai, Yehova.—Yohana 17:17; 1 Petro 1:24, 25.
Siri ya kupata usalama ulioonewa shangwe chini ya utawala wa Sulemani ilikuwa katika kutumia sheria adilifu za Yehova. Kabla Waisraeli hawajaingia Bara la Ahadi, Mungu alikuwa amesema: ‘Mkiendelea kutembea katika sheria-katiba zangu na kushika amri zangu, kwa kweli bara litatoa mazao yalo. Na kwa kweli nyinyi mtakaa katika usalama katika bara lenu. Na mimi nitaweka amani katika bara, na kwa kweli nyinyi mtalala, bila mtu wa kufanya mteteme.’—Walawi 26:3-6, NW.
Kwa kuhuzunisha, baada ya Sulemani kufa Waisraeli waliacha kutii Yehova; waligeukia ibada ya sanamu na ibada chafu ya ngono. Tokeo ni kwamba, walipoteza usalama wao, na bara likavamiwa na Farao Shishaki wa Misri. (1 Wafalme 14:21-26) “Ninyi mmeniacha mimi, kwa hiyo nami nimewaacha ninyi mkononi mwa Shishaki,” Yehova akaeleza kusanyiko la watawala katika Yerusalemu.—2 Nyakati 12:5.
Mtu Aliye Mkubwa Kuliko Sulemani
Yesu Kristo alithibitisha ukweli wa kihistoria juu ya Sulemani na “fahari yake yote.” (Mathayo 6:29) Lakini kwa habari yake mwenyewe, Yesu alisema: “Hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.” (Mathayo 12:42) Alimaanisha nini? Usalama ulioonewa shangwe chini ya utawala wa Sulemani ulikuwa na mipaka. Mfalme huyo wa kibinadamu hakuweza kuwaweka huru raia zake na ugonjwa, dhambi, na kifo. Hata hivyo, Yesu alifundisha wanadamu wenye dhambi jinsi wangeweza kufikia uhai mkamilifu katika usalama wa milele.—Yohana 10:10; 13:34, 35; 17:3.
Msingi wa kufikia usalama kamili huo uliwekwa na kifo na ufufuo wa Yesu. (Yohana 3:16; 1 Wakorintho 15:20) Akiwa kwenye mkono wa kulia wa Mungu mbinguni, karibuni atawaletea wote wenye kujitiisha kwa utawala wake usalama wa duniani pote. Mfalme Daudi wa zamani alivuviwa aandike juu ya jambo hilo katika Zaburi ya 72 iliyo ya kishairi. Maneno hayo yalikuwa na utimizo wa kisehemu wakati wa utawala wa mwana wa Daudi, na ndiyo sababu utangulizi-wa-juu husema, “Kuhusu Sulemani.” (NW) Hata hivyo, utimizo ulio mkubwa wahusu utawala wa Ufalme wa Sulemani Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo.
Kulingana na Zaburi 72:7, 8, usalama utakaoonewa shangwe chini ya utawala wa Kristo utakuwa wa duniani pote na wa milele pia. “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia.”—Linganisha Zekaria 9:9, 10.
Raia za utawala wa Kristo wataonea shangwe pia uhuru wa kutokuwa na upungufu wa mahitaji, kwa maana Zaburi 72:16, NW, hutuhakikishia hivi: “Kutakuja kuwa na utele wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mfuriko.” Kiasili, kutakuwako pia uhuru wa kutokuwa na ubaguzi, uonevu, na jeuri. “Kwa maana atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12, 14.
Kama ilivyokuwa wakati wa Mfalme Sulemani, msingi wa usalama huo wa duniani pote utakuwa ni utumizi wenye hekima wa sheria za Yehova za ulimwengu wote mzima. Hiyo itakuwa kwa kujibu ombi hili la kiunabii la Daudi: “Ee Mungu, umjalie mfalme uamuzi wako . . . Mfalme awatetee wanyonge wa taifa, awasaidie watoto wa fukara, na kuwaangamiza watu waonevu.”—Zaburi 72:1, 4, HNWW.
Namna Gani Mahitaji Yetu ya Wakati Uliopo?
‘Yote hayo ni mambo mazuri sana,’ mtu angeweza kusema hivyo, ‘lakini mimi nahitaji usalama wa kimwili sasa.’ Ni kweli kwamba bado Wakristo hupasishwa hali zisizo salama zinazokumba ainabinadamu—uhalifu, magonjwa, maafa ya kiasili, uzee, na kifo. Hata hivyo, yaliyoonwa kuzunguka tufe lote yaonyesha kwamba wakiwa na maarifa ya Biblia, wao huwezana na hali vizuri zaidi. (Mithali 15:1; 22:3) Pia, wana uradhi wa tumaini halali. Mwanafunzi mpya wa Biblia mwenye kutoka kitongoji kimoja chenye uhalifu mwingi cha Johannesburg, Afrika Kusini, alieleza njia moja ambayo Maandiko yalimsaidia: “Sasa mimi najua kwamba uhalifu si wa kudumu; ni wa muda tu.”
Naam, hata kuna tumaini kwa wale ambao wamekufa kwa kutolewa mhanga na jeuri ya uhalifu. “Mimi ndimi ule ufufuo na ule uhai,” Yesu akaahidi, halafu akaongezea hivi: “Yeye ajizoezaye imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.”—Yohana 11:25, NW.
Ili uonee shangwe hisia hiyo ya usalama, wewe wahitaji imani imara, ambayo huja kwa kujifunza Neno la Yehova. Kwa kuweka kando kila siku wakati wa kujifunza Biblia, waweza kujionea utimizo wa ahadi hii nzuri ajabu: “Kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.”—Mithali 1:33; 2:21, 22.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
“Chini ya Sulemani, utamaduni wa Kiisraeli wa vitu vya kimwili ulistawi kwa muda wa miongo mitatu kuliko vile ulivyokuwa umefanya katika miaka mia mbili iliyotangulia. Katika tabaka za ardhi ya maeneo ya wakati wa Sulemani twapata mabaki ya mijengo ya kudumu, majiji makubwa yenye kuta kubwa sana, vuvumko la maskani zenye vikundi-vikundi vya makao ya watu wenye ufanisi, usitawi wa ufundi wa mfinyanzi na taratibu zake za utengenezaji. Pia, twapata mabaki ya sanaa ya vitu vilivyofanyizwa mahali pa mbali sana, vikiwa ni ishara za kwamba kulikuwako biashara na ubadilishanaji mwingi wa bidhaa za kimataifa.”—The House of David, kilichotungwa na Jerry M. Landay.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]
Foto ya NASA