Zaburi
Wewe Unapenda Kadiri Gani Utawala Wenye Haki Ya Adili?
UTAWALA wenye kuhangaikia sana raia zao wote unaweza kutamaniwa sana! Kama umaskini, uonezi na mambo ya udhalimu yangeweza kuondolewa, wakaaji wa dunia wangeburudika kweli kweli.
Katika Zaburi ya 72, ambayo inaonekana wazi kwamba iliandikwa na Daudi (mstari wa 20), tunapata maelezo juu ya utawala utakaotimiza mambo hayo. Huo ndio ufalme wa Mungu kupitia Yesu Kristo. Mfano mdogo wa namna utawala huo utakavyokuwa ulionyeshwa na utawala wenye amani na ufanisi wa Mfalme Sulemani wakati alipoendelea kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu. Yakielekeza kwenye utimizo wa kwanza, maelezo ya juu yanayoitangulia Zaburi ya 72 yanasema “Kwa habari ya Sulemani” (katika tafsiri ya New World).
Mstari wa kwanza unafunua kwamba utawala huo wenye haki ya adili hauwezi kuwapo kusipokuwapo kanuni za milele za haki ya hukumu ya kimungu. Tunasoma hivi: “Ee Mungu, mpe mfalme hukumu zako, na mwana wa mfalme haki yako.” (Zaburi 72:1) Maneno hayo ni ombi la sala kwamba mfalme aweze kutoa hukumu za Yehova anapofanya maamuzi. Tena, haki ya adili anayoionyesha sana Mungu wa kweli inapasa iwe sifa ya mwana wa mfalme pia.
Maneno “mwana wa mfalme” yanamfaa Sulemani na Yesu Kristo pia. Sulemani alikuwa mwana wa Mfalme Daudi, hali Yesu ndiye Mwana wa yule Mfalme mkuu Yehova Mungu. (Isaya 33:22) Kwa habari ya Sulemani, raia zake walipata kujua “ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake, ili afanye hukumu.” (1 Wafalme 3:28) Na Yesu Kristo alisema: “Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.”—Yohana 5:30.
Bila shaka, ili haki ya adili isitawi, lazima watu wote wazipokee faida zinazotokana na haki ya hukumu isiyo na upendeleo. Zaburi ile inaendelea kusema: “Atawaamua watu wako [Mungu] kwa haki, na watu wako walioonewa kwa hukumu. Milima itawazalia watu amani, na vilima navyo kwa haki. Atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa [kuwakomboa katika uonezi] wahitaji, atamseta mwenye kuonea.” (Zaburi 72:2-4) Wakati haki ya hukumu inapofikilizwa kwa wote bila upendeleo, kutia na wenye kutaabishwa hata maskini na wazao wao, kunakuwa na amani na usalama. Kisha hakuna mtu anayelazimika kuishi akiogopa kunyang’anywa vitu vyake kwa njia ya udanganyifu wala kutokutimiziwa haki zake. Inaposemwa milima na vilima vilivyo katika uso wa nchi ‘vizalie watu amani’ maana yake ni kwamba amani hiyo ingefikia sehemu zote za nchi. Ni sawa na wakati vijito na mito inayoanzia vilimani na milimani inapopeleka maji yenye kuendeleza uhai kwenye mabonde na nyanda. Wale wanaotaabishwa kwa ukawaida na utawala mpotovu watafurahia usalama, kwa maana wanadamu wote walio waonezi na wenye kunyang’anya watu vitu vyao kwa udanganyifu ‘watasetwa’ (watapondwa), waadhibiwe au waletwe hukumuni.
Utawala wenye haki ya adili kama huo ungemletea Yehova Mungu utukuzo mwingi. Ni kama vile zaburi hiyo inavyosema: “Watakuogopa wakati wote wa kudumu jua, na wakati wa kung’aa mwezi kizazi hata kizazi.” (Zaburi 72:5) Kwa kuwa mfalme anatoa hukumu za Yehova, raia watamwogopa yule Aliye Juu Zaidi kwa woga unaofaa. Woga huo ungeendelea kuwapo maadamu jua na mwezi vinaendelea kuwapo, katika vizazi vyote. Kwa mfano, wakati Sulemani alipoamua kesi ya makahaba wawili, watu ‘walimwogopa mfalme’ kwa kuiona hekima ya kimungu ikifanya kazi. (1 Wafalme 3:28) Inafaa pia kukumbuka kwamba miujiza iliyofanywa na Yesu Kristo alipokuwa angali duniani ilijaza watu wengi woga unaofaa na ukawafanya wamsifu Yehova Mungu.—Mathayo 9:8; Luka 7:16.
Burudisho la utawala wenye haki ya adili linaelezwa kwa njia hii: “Atashuka kama mvua juu ya majani yaliyokatwa, kama manyunyu yainyweshayo nchi. Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia.” (Zaburi 72:6-8) Utawala wa mfalme wenye haki ya adili ungekuwa wenye kuburudisha kama mvua nyingi inayohitajiwa isitawishe majani yaliyokatwa. Kwa sababu ya amani na usalama uliopo, mtu aliyekuwa na haki ya adili angeweza ‘kusitawi,’ yaani, avuvumke au afanikiwe. Kama vile mwezi usivyoweza kuondoka usiwepo tena, vivyo hivyo amani yenye kuletwa na utawala huu wenye haki ya adili isingeweza kumalizika.—Linganisha Mathayo 5:18.
Inastahili kuangaliwa kwamba utawala wa Sulemani ulikuwa wenye amani isiyo na kifani. Biblia inaeleza hivi: “Naye alikuwa na amani pande zake zote. Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Wafalme 4:24, 25) Chini ya utawala wa Yesu Kristo, yule “Mwana wa Kifalme wa Amani,” tunaweza kutazamia utimizo mkubwa kuliko huo wa maneno ya mtunga zaburi.—Isaya 9:6, NW.
Utawala wa Sulemani ulianzia Bahari Nyekundu (ya Shamu) mpaka Bahari ya Kati, na kuanzia Mto Frati mpaka nchi ile iliyoko kusini na iliyoko magharibi. (Linganisha Kutoka 23:31.) Lakini Yesu Kristo atatawala dunia nzima.—Zekaria 9:9, 10; linganisha Danieli 2:34, 35, 44, 45; Mathayo 21:4-9; Yohana 12:12-16.
Kwa habari ya makundi ya watu ambao wangekuwa chini ya mamlaka ya mfalme, Zaburi 72 inasema: “Mbele yake wakaaji wa majimbo yasiyo na maji watainama chini, na wale wale walio adui zake watayalamba mavumbi yenyewe. Wafalme wa Tarshishi na wa visiwa—watakuja wamtolee heshima. Wafalme wa Sheba na Seba—zawadi watatoa. Na kwake wafalme wote watasujudu wao wenyewe; mataifa yote, kwa upande wao, watatumikia yeye.” (Mistari 9-11, tafsiri ya New World) Maneno hayo yanaonyesha nini? Kwamba wahamahamaji wenye kupiga hema katika jimbo la jangwa upande wa mashariki wa nchi ya Israeli wangejitolea ushinde wamnyenyekee mfalme huyu. Adui zake wangemsujudia kwa kumtii, nyuso zao zikiwa zimeyagusa mavumbi yenyewe. Zawadi za kumheshimu zingeletwa kutoka mapana na marefu ya nchi. Unaweza kusoma kwenye Wafalme wa Kwanza 10:22-25 uone ni kwa kadiri gani zaburi hiyo ilitimizwa wakati wa utawala wa Sulemani.
Walakini, ukilinganishwa na utawala wa Yesu Kristo, utawala na utukufu wa Sulemani utafifia uwe jambo lisilokumbukwa sana. Si kwamba Mwana wa Mungu amerithi utawala wa dunia nzima tu, bali hata malaika wa mbinguni wanautambua ubwana wake.—Wafilipi 2:9, 10; Waebrania 1:3-9; 2:5-9.
Ukuu wa utawala wa mfalme haumaanishi kwamba yeye hatakuwa na wakati wa kushughulikia mahitaji ya raia mmoja mmoja. Imesemwa angekuwa mtu anayeweza kufikiwa na watu wote wakiwa na shida, naye angewahangaikia kwa huruma nyingi sana. Mistari 12 mpaka 14 ya Zaburi 72 inatuambia hivi: “Kwa maana atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”
Ndiyo, hata raia wenye hali za chini zaidi wangeweza kutimiziwa mahitaji yao na mfalme huyo, naye angekuja kuokoa wote wanaohitaji msaada. Angewahurumia maskini na wenye mahitaji, kwa kuwakomboa katika mabaya wanayotendwa. Kwake yeye, damu, inayosimamia uhai wa kibinadamu, ingekuwa na thamani kubwa sana, wala isingekuwa kitu cha kumwagwa bila sababu nzuri. Wakati wa utawala wa Sulemani, raia walipewa ruhusa ya kufika mbele ya kiti cha kifalme wahukumiwe. Jambo hilo linaonekana wazi kwa kuwa makahaba wawili waliweza kuja mbele yake asikie kesi yao, kisha wakasikia uamuzi wenye haki ya hukumu ukitangazwa siku hiyo hiyo. (1 Wafalme 3:16-27) Lo, alikuwa tofauti namna gani na wafalme wa Kiajemi wa nyakati zilizofuata! Hata mtu aliye malkia asingeweza kuja mbele ya mumewe bila ruhusa, ama sivyo angetia uhai wake hatarini. (Esta 4:11) Alipokuwapo duniani, yule aliye mkubwa kuliko Sulemani, Yesu Kristo, alionyesha kwa matendo mara nyingi kwamba alihurumia wanadamu. Alipoyaona makundi ya watu, “aliwaonea huruma kwa sababu walikuwa hoi na wenye wasiwasi kama kondoo wasio na mchungaji.” (Matayo 9:36, Habari Njema kwa Watu Wote) Hata alitolea wanadamu uhai wake.—Mathayo 20:28.
Kwa habari ya mfalme kama huyo anayeelezwa na mtunga zaburi, moja kwa moja mtu angepaza sauti ya shangwe akisema: ‘Maisha marefu kwa mfalme!’ Anapaswa kupokea heshima kwa raia zake, tena mtawala wa namna hiyo angestahili kuombewa sala za kumfaidi yeye. Angehitaji baraka, si laana. Mawazo haya yamekaziwa katika mstari wa 15 wa Zaburi 72: “Basi na aishi; na wampe dhahabu ya Sheba; na wamwombee daima; na kumbariki mchana kutwa.”
Tunaweza kutendaje kwa kupatana na roho ya Zaburi 72:15 kumwelekea Yesu Kristo? Tunaweza kufanya hivyo kwa kujiweka chini yake kishikamanifu, ‘kumkiri mbele ya watu kwamba yeye ni Bwana kwa utukufu wa Mungu aliye Baba.’ (Wafilipi 2:11) Angalia namna misisimuko ya moyoni inayotajwa na Zaburi 72:15 inavyolingana na maneno haya ya Ufunuo 5:13, 14: “Kila kiumbe kilichoko mbinguni na juu ya nchi na chini ya nchi [wafu watakaofufuliwa] na juu ya bahari, na vitu vyote vilivyomo ndani yake, nalivisikia, vikisema, Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye [Yehova Mungu] aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo [Yesu Kristo], hata milele na milele. Na wale wenye uhai wanne [makerubi] wakasema, Amina. Na wale wazee wakaanguka, wakasujudu.”
Ikiueleza ufanisi ambao ungefuatana na utawala wenye haki ya adili, Zaburi 72 inaendelea kusema: “Uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni, na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi.”—Mstari 16.
Kwa sababu ya kutokuwapo kwa uharibifu mwingi unaoletwa na vita na wasiwasi unaoletwa na udhalimu na uonezi, raia wangeweza kufanya ukulima wakiwa na amani. Udongo ungezaa vitu vingi kwa kubarikiwa na Mungu. Ingekuwa kama kwamba nafaka ilikuwa ikikua kando za mlima, moja kwa moja mpaka juu ya mlima wenyewe. Kwa kuwa si kawaida nafaka kuwa nyingi juu ya vilele vya milima, maneno yanayosema ‘uwepo wingi wa nafaka juu ya milima’ ni wonyesho unaopendeza wa namna nafaka itakavyokuwa nyingi sana. Matunda yake yangevuvumka kama Lebanoni, ndiyo, kama miti-mierezi ya Lebanoni iliyo mingi sana, ambayo inakua sana. Labda hilo lina maana ya kwamba mashina ya mimea yangekuwa mrefu na manene, yaweze kuyategemeza majani mazito ya mimea hiyo. Hata wakaaji wa mji wangevuvumka, wawe wengi sana kama majani. Ndivyo mambo yalivyokuwa wakati wa utawala wa Sulemani, kwa maana tunasoma hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi.” (1 Wafalme 4:20) Hali bora zaidi ya hizo zitakuwa katika “dunia mpya” chini ya utawala wa Yesu Kristo.
Kwa kweli, utawala wenye haki ya adili na baraka nyingi unapasa ufanye mtu ashukuru sana, ashukuru kwa shukrani za namna inayoelezwa katika Zaburi 72:17: “Jina lake na lidumu milele, pindi ling’aapo jua jina lake liwe na wazao; mataifa yote na wajibariki katika yeye, na kumwita heri.” Jina la mfalme anayetawala kwa haki ya adili linastahili kuwapo kwa wakati usiojulikana. Kwa habari ya Sulemani, maneno ya mtunga zaburi yanautakia mema ukoo wake wa kifalme uendelee kuwapo na kusitawi sana. Inaposemwa “jina lake liwe na wazao” maana yake ni kwamba mfalme awe na watoto wa kuendeleza ukoo wake wa kifalme. Na inaposemwa watu wajibariki kwa jina la mfalme maana yake ingekuwa ni kumtaja yeye kwa kutakia watu wale wengine pia baraka. Ni wazi kwamba watu wa mataifa yale mengine walimtangaza Sulemani kuwa mwenye furaha kutokana na maneno ya malkia wa Sheba: “Heri watu wako, na heri watumishi hawa wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako.”—1 Wafalme 10:8.
Maneno ya mtunga zaburi yanatimizwa kwa njia kubwa sana katika Yesu Kristo ambaye Yehova Mungu alimpa ‘jina lile lipitalo kila jina.’ (Wafilipi 2:9) Yeye hahitaji watu wa kumrithi kwa sababu ndiye Mwana wa Mungu asiyeweza kufa. Kwa kuwa ana uwezo wa kuwapa watu nzima, anaweza kuwarudisha wafu wapate uhai tena na hivyo awe ndiye baba ya mamilioni mengi ya watu. (Isaya 9:6, 7; Yohana 5:26, 28; 1 Timotheo 6:15, 16) Hapo jina lake litapata ongezeko kubwa sana! Akiwa ndiye mkuu katika ‘uzao wa Ibrahimu,’ yeye ndiye kupitia kwake “mataifa yote ya dunia yatajibariki yenyewe pasipo shaka.”—Mwanzo 22:18, NW.
Utawala wenye haki ya adili wa Mwana wa Mungu utapendeza weee! Malkia wa Sheba alimwambia Sulemani: “Na ahimidiwe [Yehova], Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa [Yehova] amewapenda Israeli.” (1 Wafalme 10:9) Hata sisi nasi tumhimidi (tumbariki) Yehova kwa kumchagua Mwanawe awe mfalme, na kuyafuata maneno ya mtunga zaburi yanayosema: “Na ahimidiwe [Yehova], Mungu, Mungu wa Israeli, atendaye miujiza Yeye peke yake; jina lake tukufu na lihimidiwe milele; dunia yote na ijae utukufu wake. Amina na Amina.”—Zaburi 72:18, 19.