Wakati Ambapo Njaa Haitakuwapo tena
HUENDA ikawa hujapatwa na njaa yenye kuendelea kwa siku nyingi inayosokota tumbo sana. Hata hivyo hali hiyo ndiyo wanaume, wanawake na watoto milioni nyingi wanayolazimika kukabili (kuelekea). Kulingana na kadirio moja, wakaaji wa dunia milioni 460 hawapati chakula cha kutosha. Makadirio mengine yangeionyesha hesabu hii kuwa zaidi ya mamilioni milioni moja. Sana sana watoto ndio wanaotaabika sana. Njaa inayowapata inaweza kutokeza upofu, kuzuia ukuzi wa miili yao, kupoteza uwezo wa mwili wa kujikinga na magonjwa na, hata, kuleta kifo cha mapema sana.
Bila shaka msaada wa kuondoa njaa unahitajiwa. Walakini je! msaada huo utakuja? Ndiyo, Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, amekusudia kumaliza njaa. Kwa mfano, unabii wa Isaya, ulionyesha kimbele karamu ya dunia yote, ikiwa na chakula cha kutosha kwa wote. Tunasoma hivi: “[Yehova] wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono.”—Isa. 25:6.
Ahadi hiyo huenda ikawa jambo lisilosadikika kwa wale mamilioni wanaokufa njaa. Huenda wakafikiri kwamba dunia haiwezi kutoa chakula cha kutosha kila mtu. Lakini hivyo si ndivyo ilivyo. Katika toleo lake la Septemba 1974, gazeti Scientific American lilisema kwamba: “Inaelekea kwamba dunia pamoja na ufundi inaweza kutoa chakula kwa idadi ya watu mamilioni milioni 40 mpaka 50.” Ni kwa sababu gani, basi, watu wengi sana wanakufa njaa? Kukosa ushirikiano kati ya watu, matengenezo ya kiuchumi yakiwa na kusudi la kupata faida kubwa, pamoja na kutumiwa vibaya kwa mali za dunia ni mojawapo mambo yanayoleta hali yenye kuhuzunisha iliyopo leo.
Yote haya yanatokana na kushindwa kwa wanadamu kupendezwa na hali njema ya wanadamu wenzao. Kushindwa huku hakupatani na vile Mwana wa Mungu, Yesu Kristo alivyotutia moyo: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Kwa kuwa mafundisho ya Yesu yalitoka kwa Baba yake, ni wazi kwamba, kutotii sheria ya Mungu ndiko kumetokeza tatizo (gumu) hili la njaa.—Yohana 7:16.
Inafaa kuangalia kwamba karne nyingi zilizopita Yehova Mungu aliwafunulia Waisraeli kwamba uhuru kutokana na njaa ungetegemea utii wao kwa amri zake. Waliambiwa hivi: “Mtakaposikiliza kwa bidii maagizo yangu niwaagizayo leo kwa kumpenda [Yehova], Mungu wenu, na kumtumikia . . . , utakula na kushiba.”—Kum. 11:13-15.
Historia ya Waisraeli inahakikisha maneno hayo. Kwa mfano, wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, Waisraeli walikuwa na ufanisi na usalama kwa sababu ya kushikilia sheria ya Mungu kwa uaminifu. Biblia inaripoti hivi: “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-Sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Fal. 4:25) Maneno ya Zaburi 72 ambayo kwanza yalisemwa kuonyesha mambo ambayo yangetazamiwa wakati wa utawala wa Sulemani yalitimizwa: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zab. 72:16.
Hali iliyokuwapo wakati wa utawala wenye fanaka wa Sulemani ilikuwa mfano wa unabii wa hali kubwa zaidi zitakazoenea duniani pote chini ya utawala wa aliye mkuu kuliko Sulemani, Yesu Kristo. (Mt. 12:42) Twajua hili kwa kuwa maneno ya Zaburi 72:8 yanarudiwa katika Zekaria 9:10, ambapo utawala wa Masihi unatajwa waziwazi. Tunasoma hivi: “Naye atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia.”—Linganisha Zekaria 9:9 na Mathayo 21:4, 5.
Kwa kuwa dunia yote itakuwa chini ya mamlaka yake, Yesu Kristo anaweza kuhakikisha kwamba raia zake wote wanafaidika na mazao mengi ya dunia. Zaidi ya hayo, atawaondoa wale wote wasiotaka amani ambayo anatoa, wale wanaoendelea kufuata njia zao wenyewe, ambazo zinawaumiza wanadamu wenzao. Alipokuwa duniani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba yeye angekuja akiwa mfishaji wakati wa wasiwasi na taabu kubwa kati ya wanadamu. (Luka 21:25-36) Kwa kuwa taabu ya ulimwengu inaendelea kuongezeka, lazima wakati huo uwe umekaribia sana.
Kuchukua hatua juu ya wale wanaoendelea kufuata mapendezi yao ya kichoyo na wanaopinga utawala wake kutamaanisha mwisho wa matengenezo ya kibiashara yenye pupa, matumizi mabaya ya mali za dunia, ugawaji wa chakula usiosawazika na mambo mengine yote yanayosababisha hali hizi mbaya za watu wanaokufa njaa.
Baada ya hapo Yesu Kristo atakaza fikira zake katika kuwasaidia raia zake wapate mambo yaliyo mema kabisa ya maisha. Kupendezwa kwake na hali njema ya watu alikoonyesha alipokuwa mwanadamu duniani, kunatuhakikishia hilo. Kwa mfano, kuna wakati alipowaita wanafunzi wake akawaambia: “Nawahurumia makutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije wakazimia njiani.” (Mt. 15:32) Huruma hii ilimsukuma Yesu afanye mwujiza. Akitumia vipande saba vya mkate na samaki wachache, alitoa chakula kwa wanaume elfu nne, licha ya wanawake na watoto. (Mt. 15:34-38) Wakati fulani kabla ya hapo , alikuwa amefanya mwujiza kama huo kwa vipande vitano vya mkate na samaki wawili.—Mt. 14:17-21.
Kuzidishwa huku kwa mkate na samaki kimwujiza huenda kukaonekana kuwa jambo lisilosadikika. Lakini je! haitupasi kutazamia mambo ya namna hiyo kutoka kwa mtu ambaye si mwanadamu wa kawaida bali ni Mwana wa Mungu? Na ikiwa angeweza kufanya miujiza ili atoe mahitaji ya lazima, bila shaka ana uwezo wa kuifanya dunia ‘itoe mazao yake’ kwa wingi wakati ambapo watu wenye pupa wanaoichafua na “waiharibuyo” sayari hii watakapoondolewa!—Zab. 67:6; Ufu. 11:18.
Basi, twaweza kutazamia kwa uhakika wakati ujao usio mbali sana wakati njaa itakapokuwa jambo la zamani. Ikiwa unataka kuuona wakati huo, chukua hatua ifaayo uonyeshe kwamba unataka kuwa mtumishi mtiifu wa Mungu na Kristo. Ndipo wewe, kama ilivyokuwa kwa Waisraeli katika siku za utawala wa Sulemani, huenda ukawa kati ya wengi ambao wataona wakati wa amani, usalama na ufanisi.
[Andiko katika ukurasa wa 3]
“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zab. 72:16.