Wenye Furaha Ni Walio Wanyenyekevu
“Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”—1 PETRO 5:5.
1, 2. Katika Mahubiri yake juu ya Mlima Yesu alihusianishaje jambo la kuwa mwenye furaha na jambo la kuwa mnyenyekevu?
JE! KUWA mwenye furaha na kuwa mnyenyekevu kunahusiana? Katika mahubiri yake yanayojulikana zaidi, Yesu Kristo, yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, asimulia furaha au neema tisa. (Mathayo 5:1-12) Je! Yesu alihusianisha kuwa mwenye furaha na kuwa mnyenyekevu? Ndiyo, alifanya hivyo, kwani kuwa mnyenyekevu kunahusika katika furaha kadhaa alizotaja. Kwa kielelezo, ni lazima mtu awe mnyenyekevu ili atambue uhitaji wake wa kiroho. Ni wanyenyekevu tu walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu. Na wenye kiburi si wenye hali pole na si wenye rehema, wala si wafanya-amani.
2 Wanyenyekevu ni wenye furaha kwa sababu kuwa mnyenyekevu ni jambo lifaalo na lenye kufuatia haki. Zaidi ya hayo, wanyenyekevu ni wenye furaha kwa sababu kuwa mnyenyekevu ni jambo lenye hekima; huchangia mahusiano mazuri na Yehova Mungu na Wakristo wenzetu. Juu ya hayo, wanyenyekevu ni wenye furaha kwa sababu kuwa wanyenyekevu ni wonyesho wa upendo kwa upande wao.
3. Kwa nini kufuatia haki hutuwajibisha tuwe wanyenyekevu?
3 Kwa nini kufuatia haki hutaka tuwe wanyenyekevu? Kwanza, kwa sababu sisi sote twarithi kutokukamilika na twaendelea kufanya makosa. Mtume Paulo alisema hivi juu yake mwenyewe: “Najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati.” (Warumi 7:18) Ndiyo, sisi sote tumetenda dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu. (Warumi 3:23) Uwazi utatuzuia tusiwe wenye kiburi. Kukiri kosa hutaka unyenyekevu, na kufuatia haki kutatusaidia tukubali lawama wakati wowote tufanyapo makosa. Kwa kuwa sisi hupungukiwa daima kutimiza tunachojitahidi kufanya, tuna sababu nzuri ya kuwa wanyenyekevu.
4. Ni sababu gani inayotolewa kwenye 1 Wakorintho 4:7 inayotufanya tuwe wanyenyekevu?
4 Mtume Paulo atupa sisi sababu nyingine kwa nini kufuatia haki kwapasa kutufanya wanyenyekevu. Yeye asema hivi: “Ni nani anayekupambanua na mwingine? nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea?” (1 Wakorintho 4:7) Bila shaka, lisingekuwa jambo la kufuatia haki kwa sisi kujipa wenyewe utukufu, kuwa wenye kiburi juu ya mali zetu, uwezo wetu mbalimbali, au mambo ambayo tumetimiza. Kufuatia haki huchangia kuwa kwetu na dhamiri njema mbele ya Mungu, ili tuweze ‘kujiendesha wenyewe kwa kufuatia haki katika mambo yote.’—Waebrania 13:18, NW.
5. Kufuatia haki kutatusaidiaje pia wakati ambapo tumefanya kosa?
5 Kufuatia haki hutusaidia tuwe wanyenyekevu tunapokosea. Kutatufanya tuwe tayari zaidi kukubali lawama, badala ya kujaribu kujitetea wenyewe au kumwekea mtu mwingine lawama hilo. Hivyo, ingawa Adamu alimlaumu Hawa, Daudi hakumlaumu Bath-sheba, akisema, ‘Asingalipaswa kuoga hadharani. Nisingaliweza kuepuka kushawishwa.’ (Mwanzo 3:12; 2 Samweli 11:2-4) Kwa kweli, yaweza kusemwa kwamba kwa upande mmoja, kuwa wenye kufuatia haki hutusaidia kuwa wanyenyekevu; kwa upande ule mwingine, kuwa wanyenyekevu hutusaidia tuwe wenye kufuatia haki.
Imani Katika Yehova Hutusaidia Tuwe Wanyenyekevu
6, 7. Imani katika Mungu hutusaidiaje tuwe wanyenyekevu?
6 Imani katika Yehova itatusaidia pia tuwe wanyenyekevu. Kuthamini jinsi Muumba, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, alivyo mkuu sana kutatuzuia tusijione wenyewe kuwa wa maana mno. Nabii Isaya atukumbusha hilo vizuri kama nini! Kwenye Isaya 40:15, 22, twasoma hivi: “Tazama, mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani. . . . [Kuna Mmoja, NW] anayeketi juu ya duara ya dunia na hao wanaokaa ndani yake huwa kama panzi.”
7 Imani katika Yehova itatusaidia pia tunapohisi tumeteseka isivyohaki. Badala ya kujisumbua juu ya jambo hilo, tutamngojea Yehova kwa unyenyekevu, kama vile mtunga-zaburi atukumbushavyo kwenye Zaburi 37:1-3, 8, 9. Mtume Paulo aonyesha jambo lilo hilo: “Wapenzi msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana [Yehova, NW].”—Warumi 12:19.
Unyenyekevu —Mwendo Wenye Hekima
8. Kwa nini unyenyekevu huchangia uhusiano mzuri na Yehova?
8 Kuna sababu nyingi kwa nini kuwa mnyenyekevu ni mwendo wenye hekima. Moja ni kwamba, kama ilivyoonyeshwa tayari, huo huchangia mahusiano mazuri na Mfanyi wetu. Neno la Mungu husema hivi kwa wazi kwenye Mithali 16:5: “Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA [Yehova, NW].” Twasoma hivi pia kwenye Mithali 16:18: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” Hatimaye wenye kiburi hupatwa na majonzi. Kwa kweli ni lazima iwe hivyo kwa sababu ya yale tusomayo kwenye 1 Petro 5:5: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu [wa akili, NW], mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.” Utaona jambo lilo hilo katika kielezi ambacho Yesu alitoa juu ya Farisayo na mtoza ushuru ambao kila mmoja wao alikuwa akisali. Ni yule mtoza ushuru mnyenyekevu aliyethibitishwa kuwa mwadilifu zaidi.—Luka 18:9-14.
9. Unyenyekevu husaidiaje katika nyakati za msiba?
9 Unyenyekevu ni mwendo wenye hekima kwa sababu unyenyekevu hufanya iwe rahisi zaidi kwetu kutii shauri lipatikanalo kwenye Yakobo 4:7: “Basi mtiini Mungu.” Ikiwa sisi ni wanyenyekevu, hatutaasi Yehova aturuhusupo kupatwa na msiba. Unyenyekevu utatuwezesha turidhike na hali zetu na kuvumilia. Mtu mwenye kiburi haridhiki, hutaka zaidi sikuzote, na kuasi apatwapo na hali ngumu. Kwa upande ule mwingine, mtu mnyenyekevu huvumilia magumu na majaribu, sawa na vile Ayubu alivyofanya. Ayubu alipoteza mali zake zote na alipatwa na ugonjwa wenye maumivu, kisha mke wake hata alimshauri achukue mwendo wa kiburi, akisema: “Umkufuru Mungu ukafe.” Yeye aliitikiaje? Masimulizi ya Biblia hutuambia hivi: “Yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.” (Ayubu 2:9, 10) Kwa sababu Ayubu alikuwa mnyenyekevu, yeye hakuasi lakini alijitiisha kwa hekima kwa lolote ambalo Yehova aliruhusu limpate. Na mwishowe alipokea thawabu bora.—Ayubu 42:10-16; Yakobo 5:11.
Unyenyekevu Huchangia Mahusiano Mazuri na Wengine
10. Unyenyekevu huboreshaje mahusiano yetu na Wakristo wenzetu?
10 Unyenyekevu ni mwendo wenye hekima kwa sababu huchangia mahusiano mazuri na Wakristo wenzetu. Mtume Paulo hutushauri vema hivi: “Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.” (Wafilipi 2:3, 4) Unyenyekevu utatuzuia kwa hekima tusishindane na wengine au kujaribu kuwa bora zaidi ya wengine. Mitazamo hiyo ya akilini husababisha matatizo kwetu na kwa Wakristo wenzetu.
11. Kwa nini unyenyekevu waweza kutusaidia tuepuke kufanya makosa?
11 Mara kwa mara unyenyekevu utatusaidia tuepuke kufanya makosa. Kwa jinsi gani? Kwa sababu unyenyekevu utatuzuia tusiwe wenye uhakika kupita kiasi. Badala ya hivyo, tutathamini shauri la Paulo kwenye 1 Wakorintho 10:12: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” Mtu mwenye kiburi hujiamini mno, kwa hiyo yeye huelekea kufanya makosa kwa sababu ya uvutano mbalimbali wa nje au udhaifu mbalimbali wake mwenyewe.
12. Unyenyekevu utatusukuma tutimize wajibu upi wa Kimaandiko?
12 Unyenyekevu utatusaidia kutimiza takwa la kuwa katika ujitiisho. Kwenye Waefeso 5:21, (NW) twashauriwa: “Mwe katika ujitiisho kwa mmoja na mwenzake katika hofu ya Kristo.” Kwa kweli, je, sisi sote hatuhitaji kuwa katika ujitiisho? Watoto huhitaji kujitiisha kwa wazazi wao, wake kwa waume zao, na waume kwa Kristo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:22; 6:1) Kisha, katika kutaniko lolote la Kikristo, wote, kutia na watumishi wa huduma, wapaswa kuonyesha ujitiisho kwa wazee. Je! si kweli pia kwamba wazee wamo katika ujitiisho kwa jamii ya mtumwa mwaminifu, hasa kama ilivyowakilishwa na mwangalizi wa mzunguko? Halafu pia, mwangalizi wa mzunguko huhitaji kujitiisha kwa mwangalizi wa wilaya, na mwangalizi wa wilaya kwa Halmashauri ya Tawi ya bara anakotumikia. Lakini namna gani washiriki wa Halmashauri ya Tawi? Ni lazima wawe “katika ujitiisho kwa mmoja na mwenzake” na pia kwa Baraza Linaloongoza linalowakilisha jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambalo, pia, lawajibika kutoa hesabu kwa Yesu, Mfalme aliyetawazwa. (Mathayo 24:45-47) Kama vile katika baraza lolote la wazee, washiriki wa Baraza Linaloongoza wapaswa kustahi maoni ya wengine. Kwa kielelezo, huenda mmoja akafikiri ana wazo zuri. Lakini isipokuwa idadi ya kutosha ya washiriki wale wengine yakubaliana na dokezo lake, ni lazima aache jambo hilo. Kwa kweli, sisi sote twahitaji unyenyekevu, kwani sisi sote tumo katika ujitiisho.
13, 14. (a) Unyenyekevu utatusaidia katika hali gani hasa? (b) Petro aliweka kielelezo kipi kwa habari ya kukubali shauri?
13 Unyenyekevu huonwa kuwa mwendo wenye hekima hasa katika jambo la kwamba unyenyekevu hufanya iwe rahisi zaidi kwetu kukubali shauri na nidhamu. Kila mmoja wetu huhitaji nidhamu nyakati fulani, na twapaswa kutii shauri hili kwenye Mithali 19:20: “Sikiliza mashauri, ukapokee mafundisho, upate kuwa na hekima siku zako za mwisho.” Kama vile imesemwa vema, unyenyekevu huondolea mbali uchungu wa kukaripiwa au wa kutiwa nidhamu. Kwa kuongezea, mtume Paulo, kwenye Waebrania 12:4-11, atushauri juu ya hekima ya kujitiisha kwa nidhamu tukiwa na unyenyekevu. Ni jinsi hiyo tu tuwezavyo kutumaini kuelekeza kwa hekima mwendo wetu wa wakati ujao kisha kupata ile zawadi ya uhai wa milele. Hilo litakuwa tokeo lenye furaha kama nini!
14 Kwa habari hiyo twaweza kuelekezea kielelezo cha mtume Petro. Yeye alipokea shauri kali kutoka kwa mtume Paulo, kama tuarifiwavyo katika simulizi kwenye Wagalatia 2:14: “Nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi.” Je! mtume Petro alihisi kuudhika? Si kwa kudumu, ikiwa hata alihisi hivyo, kama iwezavyo kuonwa katika rejezeo lake la baadaye kwa “ndugu yetu mpenzi Paulo” kwenye 2 Petro 3:15, 16.
15. Ni nini uhusiano kati ya kuwa kwetu wanyenyekevu na kuwa kwetu wenye furaha?
15 Pia kuna lile jambo la kuridhika, kutosheka. Hatuwezi kuwa wenye furaha hata kidogo tusiporidhika na fungu letu, mapendeleo yetu, baraka zetu. Mkristo mnyenyekevu huwa na mtazamo huu: “Ikiwa Mungu aruhusu hilo, naweza kulivumilia,” ambalo kwa kweli ndilo jambo mtume Paulo asema, kama tusomavyo kwenye 1 Wakorintho 10:13: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” Kwa hiyo twaona tena jinsi ambavyo unyenyekevu ndio mwendo wenye hekima, kwani huo hutusaidia tuwe wenye furaha haidhuru fungu letu ni nini.
Upendo Utatusaidia Tuwe Wanyenyekevu
16, 17. (a) Ni kielelezo kipi cha Kimaandiko kikaziacho ile sifa kuu zaidi katika kutusaidia tuwe wanyenyekevu? (b) Ni kielelezo kipi cha kilimwengu kionyeshacho jambo hilo pia?
16 Zaidi ya jambo jingine lolote, upendo usio na ubinafsi, a·gaʹpe, utatusaidia tuwe wanyenyekevu. Kwa nini Yesu aliweza kuvumilia kwa unyenyekevu sana ono lake la mti wa mateso ambalo Paulo asimulia kwa Wafilipi? (Wafilipi 2:5-8) Kwa nini hakufikiria kuwa sawa na Mungu? Kwa sababu, kama vile yeye mwenyewe alivyosema: “Nampenda Baba.” (Yohana 14:31) Ndiyo sababu nyakati zote alielekeza utukufu na heshima kwa Yehova, Baba yake wa kimbingu. Hivyo, kwenye pindi nyingine alikazia kwamba ni Baba yake wa kimbingu aliyekuwa mwema.—Luka 18:18, 19.
17 Tukio moja linaloonyesha jambo hilo ni lile katika maisha ya mmoja wa watunga-shairi wa mapema wa Amerika, John Greenleaf Whittier. Mwanamume huyo alikuwa na mpenzi alipokuwa kijana, na wakati mmoja katika shindano la kuendeleza herufi za maneno, mpenzi wake aliendeleza herufi za neno fulani kwa usahihi, ilhali yeye alikosea. Mpenzi huyo alihisi vibaya sana juu ya hilo. Kwa nini? Kama vile mtunga-shairi huyo alivyokumbuka, mpenzi huyo alisema: “Nasikitika kwamba niliendeleza herufi za neno hilo. Nachukia sana kuwa bora kuliko wewe . . . waona, ni kwa sababu nakupenda.” Ndiyo, ikiwa twampenda mtu, tutataka yeye awe bora kuliko sisi, si chini yetu, kwa sababu upendo ni mnyenyekevu.
18. Unyenyekevu utatusaidia tutii shauri jipi la Kimaandiko?
18 Hilo ni somo zuri kwa Wakristo wote, hasa ndugu. Kwa habari ya pendeleo la utumishi la pekee, je, tutafurahia kwamba ndugu yetu alilipokea badala ya sisi, au tutahisi wivu na kijicho kidogo? Ikiwa twampenda ndugu yetu kikweli, tutashangilia kwamba alipata mgawo huo wa pekee au utambuzi au pendeleo la utumishi. Ndiyo, unyenyekevu utafanya iwe rahisi kutii shauri hili: “Katika kuonyeshana heshima, ongozeni.” (Warumi 12:10, NW) Tafsiri nyingine husomwa hivi: “Heshimianeni kuliko nafsi zenu wenyewe.” (New International Version) Halafu pia, twashauriwa hivi na mtume Paulo: “Tumikianeni kwa upendo.” (Wagalatia 5:13) Ndiyo, ikiwa tuna upendo, tutafurahi kuwahudumia ndugu zetu, kuwatumikia, kutanguliza mapendezi na hali yao njema mbele ya yetu wenyewe, jambo litakalo unyenyekevu. Unyenyekevu utatuzuia pia tusijivune na hivyo kuepuka kuamsha ndani ya wengine roho ya wivu au kijicho. Paulo aliandika kwamba upendo “haujigambi; haujivimbishi kwa kiburi.” Kwa nini sivyo? Kwa sababu kusudi la kujigamba na kujivimbisha ni lenye ubinafsi, la kujiona, ilihali upendo ndio kiini chenyewe cha kutokuwa na ubinafsi.—1 Wakorintho 13:4.
19. Ni vielelezo vipi vya Biblia vionyeshavyo kwamba unyenyekevu na upendo huhusiana kwa ukaribu, kama vile kiburi na ubinafsi?
19 Uhusiano wa Daudi na Mfalme Sauli na mwanae Yonathani ni kielelezo chenye kutokeza cha jinsi ambavyo upendo na unyenyekevu huhusiana kwa ukaribu na jinsi ambavyo kiburi na ubinafsi vilevile huhusiana kwa ukaribu. Kwa sababu ya mafanikio ya Daudi vitani, wanawake wa Israeli waliimba hivi: “Sauli amewaua elfu zake, na Daudi makumi elfu yake.” (1 Samweli 18:7) Tangu wakati huo, kwa sababu ya kutokuwa mnyenyekevu hata kidogo, lakini, kuwa na kiburi kingi mno, Sauli aliendeleza chuki ya kuua kimakusudi kuelekea Daudi. Hilo lilitofautiana kama nini na roho ya mwanae Yonathani! Twasoma kwamba Yonathani alimpenda Daudi kama nafsi yake mwenyewe. (1 Samweli 18:1) Kwa hiyo Yonathani aliitikiaje, ilipokuwa wazi katika mwendo wa matukio, kwamba Yehova alikuwa akimbariki Daudi na kwamba yeye, wala si Yonathani, angekuwa mwandamizi wa Sauli akiwa mfalme wa Israeli? Je! Yonathani alihisi wivu au kijicho? Hasha! Kwa sababu ya upendo wake mkubwa kuelekea Daudi, aliweza kusema, kama tusomavyo kwenye 1 Samweli 23:17: “Usiogope, kwa maana mkono wa Sauli, babangu, hautakupata; na wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli; na mimi nitakuwa wa pili wako; ndivyo ajuavyo hata Sauli, babangu.” Upendo mkubwa wa Yonathani kuelekea Daudi ulimsababisha akubali kwa unyenyekevu yale aliyoyatambua kuwa mapenzi ya Mungu kwa habari ya ni nani angekuwa mwandamizi wa baba yake akiwa mfalme wa Israeli.
20. Yesu alionyeshaje ule uhusiano wa karibu kati ya upendo na unyenyekevu?
20 Jambo linalokazia zaidi uhusiano kati ya upendo na unyenyekevu ni lile lililotukia katika usiku wa mwisho ambao Yesu Kristo alikuwa pamoja na mitume wake kabla ya yeye kufa. Kwenye Yohana 13:1, twasoma kwamba Yesu, “ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo.” Baada ya hayo, twasoma kwamba Yesu aliosha miguu ya mitume wake, akitenda akiwa mtumishi wa kazi yenye umaana mdogo. Hilo lilikuwa somo lenye nguvu kama nini la unyenyekevu!—Yohana 13:1-11.
21. Kwa ufupi, kwa nini tuwe wanyenyekevu?
21 Kwa kweli, kuna sababu nyingi za kuwa mnyenyekevu. Kuwa mnyenyekevu ni jambo lifaalo, jambo lenye kufuatia haki. Ni mwendo wa uaminifu. Huchangia mahusiano mazuri na Yehova Mungu na waamini wenzetu. Ni mwendo wenye hekima. Zaidi ya yote, ni mwendo wa upendo na huleta furaha ya kweli.
Ungejibuje?
◻ Kufuatia haki husaidia kwa njia zipi katika kuwa mnyenyekevu?
◻ Kwa nini imani katika Yehova hutusaidia tuwe wanyenyekevu?
◻ Ni nini kionyeshacho kwamba kuwa mnyenyekevu ni mwendo wenye hekima?
◻ Kwa nini upendo ni wenye msaada hasa kwa kuwa kwetu wanyenyekevu?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Ayubu alijitiisha kwa Yehova kwa unyenyekevu. Yeye ‘hakumkufuru Mungu afe’
[Picha katika ukurasa wa 23]
Petro alijitiisha kwa unyenyekevu Paulo alipomshauri hadharani