Tumeutafuta Ufalme Kwanza
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA OLIVE SPRINGATE
Mama alikuwa ametoka tu kuuzima mshumaa na alikuwa ameondoka chumbani baada ya kusikia sala zetu. Ndugu yangu mchanga zaidi akaniuliza hivi mara iyo hiyo: “Olive, Mungu aweza kutuona na kutusikiaje kupitia kuta za matofali?”
“MAMA asema Yeye aweza kuona kupitia kitu chochote,” nikajibu, “hata ndani kabisa ya mioyo yetu.” Mama alikuwa mwanamke mcha Mungu na msomaji wa Biblia mwenye bidii, naye alitia ndani yetu sisi watoto staha yenye kina kuelekea Mungu na kuelekea kanuni za Biblia.
Wazazi wetu walikuwa washiriki wa Kanisa Anglikana katika mji mdogo wa Chatham, Jimbo la Kent, Uingereza. Ingawa mama alikuwa mhudhuria-kanisa wa kawaida, aliamini kwamba kuwa Mkristo kulimaanisha zaidi ya kuketi kitako tu na kusikiliza kanisani kila juma. Alikuwa na hakika pia kwamba ni lazima Mungu awe ana kanisa moja tu la kweli.
Uthamini Kuelekea Kweli ya Biblia
Katika 1918, nilipokuwa na miaka mitano hivi, mama alipata mabuku yenye kichwa Studies in the Scriptures, yaliyoandikwa na Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society. Miaka michache baadaye, tulipokuwa tukiishi katika sehemu ndogo iliyoitwa Wigmore, mama alitembelewa na mmoja wa Wanafunzi wa Biblia kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Alikubali msaada wa funzo la Biblia The Harp of God, na kutokana nao alianza kupata majibu kwa maswali yake mengi ya Biblia. Kila juma kadi nyekundu-nyeupe yenye maswali yaliyochapishwa juu ya kila sura ilikuja kwa posta. Kadi hiyo ilionyesha pia ni mahali papi katika kitabu majibu yangeweza kupatikana.
Katika 1926 wazazi wangu, dada yangu mchanga zaidi, Beryl, na mimi tuliacha kuhudhuria Kanisa Anglikana kwa sababu tulichukizwa na jinsi kanisa lilivyojiingiza katika siasa, pamoja na mafundisho yalo mengi yasiyofaa. Fundisho kuu lilikuwa kwamba Mungu angetesa watu kwa umilele wote katika helo yenye moto. Mama yangu, aliyekuwa akitafuta kweli ya Biblia kwelikweli, alisadiki kwamba Kanisa Anglikana halikuwa lile la kweli.
Muda mfupi baadaye, kwa jibu la sala la mama lenye bidii, Bi. Jackson, aliyekuwa Mwanafunzi wa Biblia, alituzuru. Kwa karibu muda wa saa mbili, alisema pamoja na mama na mimi, akijibu maswali yetu yote kutoka Biblia. Tulifurahi sana kujifunza, miongoni mwa mambo mengine, kwamba sala zetu zapaswa kuelekezwa kwa Yehova Mungu, Baba ya Yesu Kristo, na si kwa Utatu fulani wa kifumbo. (Zaburi 83:18; Yohana 20:17) Lakini kwangu swali lisilosahaulika zaidi ambalo mama aliuliza ni hili: “Ni nini maana ya kuutafuta Ufalme kwanza?”—Mathayo 6:33.
Jibu lenye msingi wa Biblia liliathiri maisha zetu sana. Tangu juma lilo hilo, tulianza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia na kushiriki na wengine mambo tuliyojifunza. Tulisadiki kwamba tulikuwa tumepata kweli. Miezi michache baadaye, katika 1927, mama alibatizwa kwa ufananisho wa wakfu wake kumtumikia Yehova, na katika 1930, mimi pia nilibatizwa.
Kuingia Katika Utumishi wa Painia
Familia yetu ilihudhuria Kutaniko la Gillingham, lililokuwa na watu 25 hivi. Watu kadhaa kati yao walikuwa wahudumu wa wakati wote, walioitwa mapainia, na wote walikuwa na tumaini la kimbingu. (Wafilipi 3:14, 20) Bidii yao ya Kikristo iliambukiza. Nikiwa tineja bado, nilipainia kwa muda mfupi nikiwa Ubelgiji katika miaka ya mapema ya 1930. Hilo lilichochea tamaa yangu ya kufanya utumishi zaidi wa Ufalme. Wakati huo tulishiriki katika kugawia kila kasisi nakala ya kijitabu The Kingdom, the Hope of the World.
Baada ya muda baba yangu alipinga sana utendaji wetu wa Kikristo, na hiyo ikiwa sababu moja, nilihamia London katika 1932 ili kwenda kwenye chuo. Baadaye nilikuwa mwalimu wa shule kwa miaka minne na katika wakati huo nilishirikiana na Kutaniko la Blackheath, mojayapo yale manne pekee katika London wakati huo. Ni wakati huo kwamba tulianza kusikia ripoti juu ya kufungwa gerezani na kuteseka kwa ndugu na dada zetu Wakristo katika Ujerumani wa Hitler kwa sababu walikataa kuunga mkono jitihada za vita za Hitler.
Katika 1938, ule mwezi hasa nilipomaliza kulipa deni ya vitabu nilivyokuwa nimepata, niliacha kazi yangu ili kutimiza tamaa yangu ya kuwa painia. Dada yangu Beryl alianza kupainia katika London wakati uo huo, lakini yeye aliishi katika makao tofauti ya mapainia. Painia mwenzi wangu wa kwanza alikuwa Mildred Willett, aliyeolewa baadaye na John Barr, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Pamoja na wengine katika kikundi chetu, tulikuwa tukienda kwa baiskeli hadi eneo na kubaki huko siku nzima, ijapokuwa mvua mara nyingi.
Tayari vita ilikuwa ikikaribia katika Ulaya. Mazoezi ya kutumia vifuniko vya uso vya kuzuia gesi yalikuwa yakifanywa kwa ajili ya raia, na matayarisho yalikuwa yakiendelea kuwapeleka watoto maeneo ya mashambani ya Uingereza au kwenye miji midogo vita itokeapo. Nilikuwa nimeweka akiba fedha za kutosha tu kununua jozi ya viatu, na hakukuwa na uwezekano wa kupata msaada wa kifedha kutoka kwa wazazi wangu. Lakini je, Yesu hakuwa amesema ‘Hayo yote mtazidishiwa mkiutafuta ufalme kwanza’? (Mathayo 6:33) Nilikuwa na imani kamili kwamba Yehova angeniandalia mahitaji yangu yote, naye amefanya hivyo kwa wingi miaka hiyo yote. Katika wakati wa vita nyakati nyingine niliongeza kwa posho zangu ndogo mboga nilizookota kando ya barabara baada ya malori yaliyopakiwa nazo kupita. Na mara nyingi nilipata chakula kwa kubadilisha fasihi ya Biblia na matunda na mboga.
Dada yangu Sonia alizaliwa katika 1928. Alikuwa na miaka saba tu alipoweka maisha yake wakfu kwa Yehova. Sonia asema kwamba hata akiwa mchanga hivyo, kupainia kulikuwa kumekuwa mradi wake. Katika 1941, upesi baada ya yeye kuufananisha wakfu wake kwa ubatizo wa maji, alitimiza mradi wake wakati yeye na mama walipogawiwa kwenda Caerphilly, Wales Kusini, wakiwa mapainia.
Huduma Yetu Katika Miaka ya Vita
Katika Septemba 1939, Vita ya Ulimwengu 2 ilianza, na dada na ndugu zetu Wakristo katika Uingereza walikuwa wakifungwa gerezani kwa sababu ileile ambayo waamini wenzao katika Ujerumani wa Nazi walikuwa wakifungwa—msimamo wao wa kutokuwamo kwa habari ya kushiriki katika vita. Mashambulizi ya mabomu katika Uingereza yalianza katikati ya mwaka wa 1940. Usiku baada ya usiku, mashambulizi hayo yalikuwa ya sauti ya juu mno, lakini kwa msaada wa Yehova tuliweza kulala usingizi na kuburudishwa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya siku iliyofuata.
Nyakati nyingine tulikuwa tukienda kwenye eneo letu la kuhubiri kupata tu kwamba nyumba nyingi zilikuwa magofu. Katika Novemba bomu moja liliangushwa meta chache tu kutoka makao ambamo sisi kadhaa tulikuwa tukiishi, likivunja-vunja madirisha katika maelfu ya vipande. Ule mlango wa mbele ulio mzito ulianguka kwa kishindo, na dohari ikabomoka. Baada ya kutumia sehemu iliyobaki ya usiku huo tukiwa katika mahali pa salama dhidi ya mabomu, tulitawanyika na kwenda kuishi katika makao ya Mashahidi tofauti-tofauti.
Muda mfupi baadaye nilipokea mgawo kwenda Croydon, katika London na viunga vyake. Painia mwenzi wangu alikuwa Ann Parkin, ambaye ndugu yake Ron Park baadaye alikuja kuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi katika Puerto Rico. Baadaye nilihamia Bridgend, Wales Kusini, nilikoendelea kupainia, nikiishi kwa miezi sita katika gari lenye kuburutwa kwa farasi. Kutoka hapo tulikuwa tukienda kwa baiskeli umbali wa kilometa sita hadi kutaniko kubwa la karibu zaidi, katika Port Talbot.
Kufikia wakati huo watu walikuwa wenye uhasama sana kuelekea sisi wakituita conchies (wakataaji kidhamira). Hilo lilifanya iwe vigumu kwetu kupata makao, lakini Yehova alitutunza kama ilivyoahidiwa.
Baadaye, wanane kati yetu tuligawiwa kuwa mapainia wa pekee katika Swansea, mji wenye bandari katika Wales Kusini. Kadiri vita ilipochacha, ndivyo na ile chuki dhidi yetu isiyokuwa na msingi ilivyochacha. Maneno “panya” na “waoga” yaliandikwa kwa rangi ukutani pa kao letu la mapainia. Uhasama huo ulichochewa hasa na ripoti za magazeti ya habari zilizotushutumu kwa ajili ya msimamo wetu wa kutokuwamo. Hatimaye, watu saba kati yetu tulifungwa jela, mmoja baada ya mwingine. Nilitumia mwezi mmoja katika jela ya Cardiff katika 1942, na baadaye dada yangu Beryl alitumia wakati humo pia. Ingawa tulikuwa na machache kimwili na tulipatwa na dhihaka na kulaumiwa, tulikuwa tajiri kiroho.
Wakati uo huo, mama na Sonia walikuwa wakipainia katika Caerphilly na walikuwa na maono yaleyale. Funzo la Biblia la kwanza kabisa ambalo Sonia aliongoza alikuwa mama mmoja ambaye Sonia alipanga kumzuru Ijumaa moja jioni. Sonia alikuwa na hakika kwamba mama angeandamana naye, lakini mama alieleza hivi: “Nina miadi nyingine. Umepangia hilo, kwa hiyo ni lazima uende peke yako tu.” Hata ingawa Sonia alikuwa na miaka 13 pekee, alienda peke yake, na mama huyo alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na baadaye akawa Shahidi aliyejiweka wakfu.
Utendaji wa Baada ya Vita —Halafu Gileadi
Wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipoisha katika 1945, nilikuwa nikifanya kazi katika eneo lisilogawiwa kutaniko katika Whaley Bridge, Derbyshire. Katika asubuhi ambayo tangazo lilitolewa juu ya kukoma kwa mapigano, tulizuru na kufariji watu ambao kufikia wakati huo walikuwa wamechoshwa na vita—matokeo yayo ya mayatima, wajane, na miili iliyokatwa-katwa.
Miezi kadhaa baadaye, Sosaiti iliomba wajitoleaji waende kuhubiri katika Ailandi, kile Kisiwa cha Zumaridi. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wapatao 140 tu kwenye kisiwa hicho, kwa hiyo lilionwa kuwa eneo la mishonari. Katika muda wa miezi michache, mapainia wa pekee 40 hivi waligawiwa kwenda huko, nami nilikuwa miongoni mwao.
Baada ya kufanya kazi kwa muda fulani katika Coleraine na Cookstown upande wa kaskazini, niligawiwa, pamoja na wengine watatu, kwenda Drogheda kwenye pwani ya mashariki. Ingawa Waailandi kwa asili ni watu wachangamfu na wakaribishaji-wageni, kulikuwa na chuki nyingi ya kidini. Hivyo, katika mwaka mzima mmoja, tuliweza kugawia watu misaada michache tu ya funzo la Biblia (kwa kweli kitabu kimoja tu na vijitabu kadhaa).
Wakati tulipokuwa tukiishi Drogheda, nilikuwa nikiendesha baiskeli kutoka shamba moja hadi jingine wakati mfanyakazi mchanga mmoja wa shambani alipotokea kwenye ua kwa ghafula hadi barabarani. Alitazama huku na huku barabarani, kisha akauliza kwa sauti ya chini: “Je! wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Nilipojibu kwamba nilikuwa mmoja, aliendelea hivi: “Jana usiku nilibishana sana na mchumba wangu juu ya nyinyi wasichana, tukavunja uchumba wetu. Yeye alisisitiza kwamba nyinyi ni Wakomunisti, kama vile mapadri Wakatoliki na magazeti ya habari husema, lakini nilibisha kwamba hilo lisingeweza kuwa kweli hata kidogo, kwa kuwa nyinyi huenda nyumba kwa nyumba waziwazi.”
Nilimpa kijitabu asome, ambacho alificha mfukoni mwake, na tulipanga kukutana na kuongea zaidi giza lilipoingia, kwa kuwa alisema hivi: “Nikionwa nikiongea nawe, nitapoteza kazi yangu.” Usiku huo wawili kati yetu tulikutana naye na kujibu maswali yake mengi. Alionekana amesadikishwa kwamba hilo lilikuwa ndiyo kweli, na aliahidi kuja nyumbani kwetu usiku mwingine ili kujifunza zaidi. Hakuja kamwe, kwa hiyo tulihisi kwamba ni lazima awe alitambuliwa na waendesha-baiskeli fulani waliopitia usiku huo wa kwanza na labda alipoteza kazi yake. Mara nyingi sisi hujiuliza ikiwa yeye alipata kuwa Shahidi.
Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya katika Brighton kwenye pwani ya kusini ya Uingereza katika 1949, kadhaa kati yetu tulipokea mialiko ya kwenda Watchtower Bible School of Gilead katika Jimbo la New York. Jumla ya 26 kutoka Uingereza walihudhuria darasa la 15, lililohitimu katika Julai 30, 1950, wakati wa mkusanyiko wa kimataifa kwenye Stediamu ya Yankee.
Huduma Yetu Katika Brazili
Mwaka uliofuata niligawiwa kwenda São Paulo, Brazili, mojayapo majiji yenye kukua kwa kasi zaidi ulimwenguni. Wakati huo lilikuwa na makutaniko matano pekee ya Mashahidi wa Yehova, lakini sasa kuna karibu 600 yayo! Ilikuwa tofauti kama nini na kufanya kazi Ailandi! Makao yaliyo mengi katika eneo letu katika São Paulo yalikuwa makubwa mno, yakizingirwa na nyua za chuma zenye kimo kirefu zilizo na malango yenye usanii ya chuma kilichofuliwa. Tulikuwa tukimwita mwenye nyumba au mjakazi kwa kupiga makofi.
Miaka ilipopita, kulikuwa na migawo mipya. Nilikuwa na pendeleo la kusaidia kufanyiza makutaniko mapya katika mahali mbalimbali katikati ya jimbo la São Paulo, kutia na moja katika Jundiaí katika 1955 na jingine katika Piracicaba katika 1958. Baadaye, katika 1960, dada yangu Sonia alikuwa mwenzi wangu wa mishonari, na tuligawiwa kwenda Pôrto Alegre, jiji kuu la jimbo la Rio Grande do Sul. Huenda ukajiuliza, alipataje kuja Brazili?
Sonia na mama waliendelea kupainia pamoja katika Uingereza baada ya Vita ya Ulimwengu ya 2. Lakini katika miaka ya mapema ya 1950, mama alifanyiwa upasuaji wa kansa uliofanya awe dhaifu sana asiweze kwenda nyumba kwa nyumba, ingawa aliweza kuongoza mafunzo ya Biblia na kuandika barua. Sonia aliendelea katika kazi ya painia, na wakati uo huo alisaidia kumtunza mama. Katika 1959, Sonia alikuwa na pendeleo la kuhudhuria darasa la 33 la Gileadi akagawiwa kwenda Brazili. Wakati uo huo, Beryl alimtunza mama hadi kifo chake katika 1962. Kufikia wakati huo Beryl alikuwa ameolewa, na yeye na familia yake wanamtumikia Yehova kwa uaminifu.
Katika Brazili, Sonia na mimi tulisaidia watu kadhaa kufikia wakfu na ubatizo. Hata hivyo, mojayapo matatizo ambalo Wabrazili wengi walikuwa nalo ni lile la kuhalalisha ndoa yao. Kwa sababu ya ugumu wa kupata talaka katika Brazili, lilikuwa jambo la kawaida kwa mwanamume na mwanamke kuishi pamoja tu bila kuoana. Hilo lilikuwa kweli hasa wakati mwenzi mmoja alikuwa ametengana na mwenzi wa zamani wa halali.
Mama mmoja, aliyeitwa Eva, alikuwa katika hali hiyo nilipomtembelea. Mwenzi wake halali aliondoka na haikujulikana alikokwenda, kwa hiyo ili kumpata, tulitoa tangazo kupitia redio. Mume wake alipopatikana, niliandamana naye hadi jiji jingine ili kupata sahihi yake kwenye hati ambayo ingemweka huru ili aweze kuhalalisha muungano pamoja na yule mwanamume asiyeoa ambaye alikuwa akiishi naye. Katika kesi mahakamani mbele ya hakimu, yeye aliuliza Eva nami pia tueleze kwa nini alitaka kurekebisha hali yake ya ndoa. Hakimu alionyesha mshangao na pia uradhi alipoelezwa hilo.
Katika pindi moja, nilienda pamoja na mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia kufanya mipango ili wakili ashughulikie kesi yake. Tena ushahidi mzuri ulitolewa kuhusu ndoa na viwango vya Mungu vya kiadili. Wakati huu gharama ya kutaliki ilikuwa ya juu sana hivi kwamba wenzi wote wawili walilazimika kufanya kazi ili kulipia ada. Lakini kwa wanafunzi hao wapya wa Biblia, jitihada hiyo ilistahili. Sonia nami tulikuwa na pendeleo la kushuhudia ndoa yao, na baadaye, pamoja na watoto wao matineja watatu, tulisikiliza hotuba fupi ya Biblia nyumbani mwao.
Maisha Yenye Baraka Tele, na Yenye Kuthawabisha
Sonia na mimi tulipoyaweka maisha yetu wakfu kwa Yehova na kuwa mapainia, tulinuia, ikiwa ingewezekana, kwamba huduma ya wakati wote ingekuwa kazi-maisha yetu. Hatukupata kufikiria sana ni nini kingetukia katika maisha yetu ya baadaye au iwapo tungepatwa na ugonjwa au matatizo ya kifedha. Lakini, kama vile Yehova alivyoahidi, hatujaachwa kamwe.—Waebrania 13:6.
Oh, ndiyo, ukosefu wa fedha umekuwa tatizo nyakati nyingine. Wakati mmoja, mwenzi wangu na mimi tulikula mkate na pasile (mboga yenye majani yaliyofinyana) ukiwa chakula cha mchana kwa mwaka mzima, lakini hatujapata kamwe kuwa na njaa, wala hatujakosa mahitaji ya msingi.
Kadiri miaka imepita, ndivyo nishati zetu zimepungua. Katika miaka ya katikati ya 1980, sote wawili tulikuwa na upasuaji mkubwa uliotokeza jaribu gumu kwetu, kwa kuwa utendaji wetu wa kuhubiri ulikatizwa sana. Katika Januari 1987, tulialikwa kuwa washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brazili.
Familia yetu kubwa ya wahudumu zaidi ya elfu moja iko kilometa 140 hivi nje ya São Paulo katika majengo yenye kupendeza, ambako sisi huchapisha fasihi ya Biblia kwa ajili ya Brazili na sehemu nyinginezo za Amerika Kusini. Huko sisi hupokea utunzaji wenye upendo kutoka kwa watumishi wa Mungu wenye kujitoa. Nilipokuja Brazili kwa mara ya kwanza katika 1951, kulikuwa na wahubiri 4,000 hivi wa ujumbe wa Ufalme, lakini sasa kuna zaidi ya 366,000! Baba yetu wa kimbingu mwenye huruma kwa kweli ametuongezea ‘mambo mengine yote’ kwa sababu tumeutafuta Ufalme wake kwanza.—Mathayo 6:33.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Olive pamoja na Mildred Willett kando ya gari la kutoa habari, 1939
[Picha katika ukurasa wa 25]
Olive na Sonia Springate