Yehova Anatulinda Sisi
Kama ilivyosimuliwa na Erich Kattner
PAAH! Kitabu kikapiga kichwa changu. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara yangu ya kwanza kukutana na Biblia, na ilikuwa mkononi mwa kasisi Mkatoliki. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya swali nililokuwa nimeuliza.
Kasisi huyo alikuwa akifundisha katikisimu na dini na alikuwa akijaribu kututia moyo sisi wavulana tuchukue kazi ya ukasisi. Katika jitihada yake ya kufanya hilo, alitumia andiko la 1 Wathesalonike 4:17, mahali pasemapo juu ya wale ‘wenye kunyakuliwa pamoja nao katika mawingu kumlaki Bwana hewani.’
Sikuzote mimi nilijaa maswali, kwa hiyo nikauliza: “Kwa sababu gani unasema makasisi huenda moja kwa moja mbinguni, hali, kama isemavyo Imani, Yesu alilazimika kwenda kuzimuni?” (Matendo 2:31) Huo ndio wakati Biblia ilipopiga kichwa changu.
Tamaa ya Kujua
Lakini kwa unyofu nilitaka majibu. Nilikuwa sana na mwelekeo wa kumwabudu Mungu, hata nilipokuwa kivulana. Nilizoea kuingia kusali karibu kila kanisa nililopita karibu nalo. Hata hivyo sikuridhika. Kwa njia fulani sikuzote nilikasirishwa na mambo niliyoona, kama vile zoea baya sana la ibada ya sanamu la watu wengine au mwenendo wa makasisi fulani.
Nilipokuwa karibu miaka minane tu, nilisoma kitabu changu cha kwanza. Kiliitwa The Christianization of Brazil. Nilishtushwa kwa mshangao. Kwangu mimi ilionekana kama hadithi ya mauaji ya kukusudia, mauaji ya kukusudia ya Wahindi katika jina la dini. Kujifunza juu ya mambo hayo kulitosha kubadili akili yangu juu ya mambo mengi.
Yote hayo yalitukia huko nyuma katika miaka ya 1920. Mimi nilizaliwa Vienna, Austria, Agosti 19, 1919, mtoto pekee wa wazazi wangu. Nilipokuwa na karibu umri wa miaka sita, baba yangu, mhadisi wa umeme, alikubali kazi kaskazini mwa Chekoslovakia, katika sehemu ya Sudetenland yenye kusema Kijeremani. Basi jamaa yangu ikahamia huko, na mwishowe tukakaa kijiji kiitwacho Warnsdorf.
Nilitambua sasa jinsi nilivyokuwa nimedanganywa na Kanisa Katoliki. Siku moja, nikiwa na uchungu sana kwa sababu ya adhabu niliyokuwa nimepewa tena kutoka kwa yule kasisi, nililia nilipokuwa njiani kwenda nyumbani kutoka shuleni. Nilipokuwa nikitembea kupitia mashamba fulani, nilifikiria kwamba haiwezekani kwamba kuna Mungu, kwa sababu ya mambo mengi yaliyopotoka niliyokuwa nimeyaona na kufundishwa.
Ndipo nyimbo za ndege zikanifikia, nami nikaangalia maua, vipepeo, na uzuri wote wa uumbaji. Nami nilianza kufahamu kwamba ni lazima kuwe na Mungu mwenye upendo lakini kwamba wale wanaoitwa eti watu wa Mungu huenda wasiwe watu wa Mungu hata kidogo. Na pengine Mungu alikuwa ameachilia wanadamu. Huo ndio wakati nilipotoa sala yangu ya kwanza halisi ya kujisikia, nikimwomba Mungu anisaidie kumjua ikiwa angepata kupendezwa tena kamwe na mwanadamu. Huo ulikuwa mwaka 1928.
Mwezi mmoja hivi baadaye mama yangu alisafiri kuungana na washiriki wa jamaa katika Vienna; ilikuwa ni siku ya kuzaliwa ya mama yake ya mwaka wa 60. Huko mama yangu alimwona ndugu yake, Richard Tautz, ambaye wakati huo alikuwa akiishi katika Maribor, Yugoslavia. Alikuwa amekuwa mmoja wa Wanafunzi wa Biblia hivi karibuni, kama walivyoitwa Mashahidi wa Yehova wakati huo. Mama alirudi nyumbani akiwa amesisimuka sana akiwa na kweli mpya za Biblia alizokuwa amejifunza. Mambo aliyonisimulia yalikuwa na maana kwangu. Ilionekana kwamba mkono wa Yehova ulikuwa ukifanya kazi.—Zaburi 121:5.
Kufanya Yale Niliyokuwa Nikijifunza
Baadaye, Wanafunzi wa Biblia wakaja kutoka Ujeremani, na kazi ya kuhubiri ikaanza katika eneo letu. Miezi fulani baadaye, mikutano ya kawaida ikaanza kufanywa katika mji jirani katika Ujeremani, nasi tulitembea maili chache na kuvuka mpaka tukaihudhuria. Ni katika wakati huo nilipokutana na Otto Estel-mann, ambaye katika miaka ya baadaye nilifanya kazi pamoja naye kwa ukaribu karibu.
Katika 1932 jamaa yetu ilihamia Bratislava, mji mkuu wa Slovakia, karibu kilometa 72 kutoka Vienna. Hakukuwa na Mashahidi wo wote huko wakati huo, niliamua ilikuwa lazima nianze kutenda katika kazi ya kuhubiri. Kwa hiyo nilichagua lile nililodhani kuwa eneo gumu kupita yote, jengo la orofa lenye nyumba nyingi lililokaliwa zaidi na jamaa za maafisa wa serikali. Lugha nne zilizungumzwa wakati huo katika Bratislava: Kislovaki, Kizeki, Kijeremani, na Kihangari.
Huku nikibeba kadi zilizokuwa na mahubiri mafupi yaliyokuwa yamepigwa chapa juu yazo katika lugha nne, nilienda peke yangu nikipiga kengele kwenye milango ya nyumba hizo. Nyakati nyingine babangu, ambaye wakati huo hakuwa amekuwa Shahidi, alikuwa akisimama ng’ambo ile nyingine ya barabara, akinitazama na kutikisa kichwa chake. Muda mfupi baadaye yeye pia alichukua msimamo imara kwa ajili ya Yehova.
Februari 15, 1935, kwenye mkutano wa pekee pamoja na mwangalizi asafiriye katika nyumba yetu, mimi, pamoja na wengine, tulibatizwa katika birika la kuogea. Nilihitimu katika shule ya biashara mwaka huo nami nikapewa toleo la kazi yenye kuvutia, lakini wakati uo huo nilialikwa nikafanye kazi kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Prague, Chekoslovakia. Baada ya mazungumzo mazito pamoja na wazazi wangu, tulimpelekea Yehova habari hiyo katika sala. Hivyo, muda mfupi kabla ya kuwa na miaka 16, mimi niliingia katika utumishi wa wakati wote Juni 1, 1935.
Kutumikia Katika Nyakati za Magumu
Kwenye afisi ya Sosaiti huko Prague, nilijifunza kuendesha mashine za kupiga chapa na kuunganisha vipande vya madini vyenye maandishi kwa kurasa. Tulitokeza trakti kwa ajili ya ndugu zetu katika Ujeremani, waliokuwa chini ya marufuku ya Hitler, na pia tulitokeza Mnara wa Mlinzi katika lugha kadha. Hata hivyo, hizo zilikuwa siku za magumu kwa kazi yetu katika Ulaya, na mwishowe wenye mamlaka walifunga tawi letu katika Desemba 1938.
Nilirudi nyumbani Bratislava, ambako serikali ilikuwa imeingia mikononi mwa wenye kuunga mkono Nazi, nami nilifanya kazi bila ya kuzuiwa kwa miezi miwili nikihubiri nyumba kwa nyumba. Karibu na wakati huo ile afisi ya Ulaya ya Kati ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Bern, Switzerland, ikaniandikia kwamba ikiwa nilikuwa ninataka kutumikia kama painia mahali po pote ulimwenguni, inanipasa nije Bern.
Nilikubali mwaliko huo na kuondoka nyumbani. Ulikuwa ndio wakati wa mwisho nilipomwona babangu, na ingechukua miaka 30 kabla sijamwona mama yangu tena. Lakini Yehova alitulinda sisi wote watatu kupitia magumu mengi yaliyofuata. Kwa mfano, nilijifunza baadaye kwamba Hlinka Guarda mwenye sifa mbaya sana (namna ya askari wa SS wa Slovakia) alikuwa akinitafuta siku nilipoondoka Bratislava. Na nilipokuwa njiani, wakati wajumbe wa Nazi walipojua kwamba mimi nilikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, walijaribu kufanya nikamatwe kwenye mipaka ya Yugoslavia na Italia. Lakini Yehova aliendelea kunilinda mimi.—Zaburi 48:14; 61:3.
Huko Bern nilijifunza kwamba ningetumwa Shanghai, China, lakini baadaye mgawo huo ulibadilishwa ukawa Brazili. Nilifanya kazi katika tawi katika Bern mpaka nilipopokea hati yangu ya kusafiri kwenda Brazili. Kufikia wakati huo matata katika Ulaya yalikuwa yakiongezeka. Mipaka ilikuwa ikifungwa, kwa hiyo katika Agosti 1939 Sosaiti ilinihimiza niende Ufaransa. Ile meli ya kibiashara ya Brazili Siqueira Campos ilikuwa ikiondoka Le Havre, Ufaransa, Agosti 31, nami nilipaswa kuwa ndani yake. Masaa manne tu kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kufyatuka, meli hiyo ilianza safari.
Nilijifunza baadaye kwamba, abiria karibu kumi na wawili niliosafiri pamoja nao katika sehemu ya chumba cha daraja la pili, wote walikuwa wajumbe wa Nazi. Wao hawakupenda kuhubiri kwangu hata kidogo. Mara kadha walijaribu kufanya niondolewe melini. Huko Vigo, Hispania, nahodha aliyekuwa mwenye urafiki alinionya nisitoke ndani ya meli tulipokuwa huko. Katika Lisbon, Ureno, wale wajumbe wa Nazi waliweka katika ubao wa matangazo maandishi yasiyo ya kweli juu ya wakati wa meli kuondoka ili niachwe huko. Lakini tena Yehova alikuwa akinilinda. (Zaburi 121:3) Nilifika katika Santos, Brazili, jioni ya Septemba 24, 1939. Siku iliyofuata nilisafiri kwenda Sao Paulo, ilikokuwa afisi ya tawi ya Sosaiti.
Kutumikia Katika Brazili
Katika Septemba 1939 kulikuwa Mashahidi 127 tu katika Brazili, ambao wakati huo ilikuwa na idadi ya watu wapatao milioni 41. Baada ya kuwa katika Sao Paulo kwa karibu juma moja, niliondoka kwenda kwa mgawo wangu wa painia katika jimbo lililo upande wa kusini zaidi, Rio Grande do Sul. Nilikuwa nikae pamoja na Mashahidi wenye kusema Kijeremani wa asili ya Polandi walioishi katika eneo la mbali sana la msituni.
Safari ya garimoshi ilichukua siku nne. Mwisho wa njia ya reli ilikuwa Girua, uliofanana na mji wa Magharibi wenye jeuri ya siku za mapema za Amerika Kaskazini. Kutoka Girua ningali nilikuwa na kilometa 32 za kusafiri kwenda msituni kufika mahali walipoishi Mashahidi. Lori la kusafirisha bidhaa lilinibeba, likaniacha kwenye barabara ya mchanga. Nikiendelea na safari kwa miguu kwa maili moja hivi kupitia msitu bikira na kuvuka kijito, mwishowe nilifika.
Kwa sababu ya eneo kuwa mbali sana na watu, utumishi wangu wa painia ulikuwa wa nyakati ambazo mtu fulani angenichukua kwa kigari chenye kukokotwa na farasi. Kufikia watu kulihusu kusafiri kwa siku nyingi, kulala kwenye barabara za mchanga kuepuka nyoka au chini ya gari kuliponyesha. Tulihubiri pia katika miji kama vile Cruz Alta.
Katika 1940 Sosaiti ilinipa mgawo mwingine kwenye Porto Alegre, mji mkuu wa jimbo la Rio Grande do Sul. Huku nilijiunga na rafiki wa siku za utoto wangu Otto Estel-mann, ambaye pia alikuwa amepewa mgawo kuja Brazili. Wenye mamlaka huko walionekana kuwa waungaji mkono wa Nazi. Tulikamatwa na kupewa uchaguzi wa kutia sahihi kikaratasi cha kukana imani yetu au kuondo-ka jioni hiyo tukiwa katika gari-moshi kwenda kwenye kizuizi kwenye mpaka wa Urugwe. Tulikuwa katika gari-moshi jioni hiyo.
Chini ya Kizuizi
Hapo mpakani tulitumia karibu miaka miwili tukiwa chini ya kizuizi katika nyumba. Lakini kwa mara nyingine tena Yehova alitutolea msaada. Wanabiashara fulani wa Kiyahudi walitoa msaada wao. Kama matokeo, badala ya kuwekwa gerezani, niliruhusiwa kufanya kazi ya kilimwengu, lakini tuliwekwa chini ya ulinzi mkali. Hatukuweza kuwasiliana na afisi ya tawi.
Hata hivyo, siku moja barabarani tulikutana na ndugu painia kutoka Ulaya aliyekuwa amepewa mgawo kuja Urugwe. Ilikuwa kwamba alikuwa akizuru mpakani. Kulikuwa kuunganishwa tena kulikoje! Yeye alitupatia Biblia ya Kijeremani na Mnara wa Mlinzi wa Kiingereza. Ndipo nilipoanza kujifunza Kiingereza kweli kweli.
Kisha, katika Agosti 22, 1942, Brazili ikatangaza vita juu ya Ujeremani na Italia, jambo lililomaanisha badiliko la hali yetu. Tulirudishwa Porto Alegre, na baada ya kuhojiwa, mimi nikaachiliwa. Baadaye, nilikutana na vijana Mashahidi ambao nilikuwa nimewajua hapo mapema katika eneo la msituni ambapo nilikuwa nimepewa mgawo wangu wa kwanza. Kwa hiyo niliweza kuwasiliana na afisi ya tawi, na nikaanza tena kupainia. Wanne wa vijana hao walijiunga nami katika kazi ya upainia, nasi tulipata watu walioukubali ujumbe wa Ufalme, ambao baadhi yao wangali wanahubiri.
Hao wenye mamlaka wapya walitupendelea, kwa hiyo katika 1943 tulipanga tuwe na kusanyiko dogo la kwanza katika Porto Alegre. Jumla ya hudhurio ilikuwa 50, karibu nusu yao walikuwa mapolisi wenye mavazi ya kiraia. Mwaka mmoja baadaye, katika 1944, tulipanga kuwe kusanyiko jingine. Baada ya hapo niliitwa nikatumikie kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti, iliyokuwa imehamishwa kutoka Sao Paulo kwenda Rio de Janeiro.
Shule ya Gileadi na Baadaye
Katika 1950 nilialikwa kuhudhuria darasa la 16 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi huko South Lansing, New York. Baada ya kuhitimu katika Februari 1951, nilipokea mgawo wa muda wa painia wa pekee nishirikiane na Kundi la South Bronx, New York, lakini baadaye nikarudi Brazili.
Kwa karibu mwaka mmoja na nusu nilitumikia nikiwa mjumbe anayesafiri wa Sosaiti, kama mwangalizi wa mzunguko na wilaya pia. Halafu, katika Februari 1953, niliitwa nirudi kwenye afisi ya tawi katika Rio de Janeiro na nikapewa mgawo wa kufanya kazi ya kutafsiri. Baadaye, kuanzia Septemba 1961 kufikia Septemba 1963, nilikuwa na pendeleo la kufanya kazi ya mgawo wa pekee wa kutafsiri kwenye makao makuu ya Sosaiti huko Brooklyn, New York. Nikiwa huko, nikutana na wenzi waliooana niliokuwa nimejuana nao huko Brazili. Mume alikubali kujifunza Biblia pamoja nami katika hoteli walimokuwa wakikaa naye akasadikishwa juu ya ukweli.
Miezi michache baadaye, tulipokuwa tumerudi Brazili, nilionana naye tena. Lakini kidogo alionekana kukinai. Kwa hiyo nikamwa-mbia: “Tazama, Paul, wewe ni mhadisi wa ujenzi. Lakini tuseme ni mimi niliyekuwa mhadisi wa ujenzi na nikakuambia kwamba paa liko tayari kukuangukia. Ungefanya nini? Basi, mimi nikiwa ‘mhadisi’ wa Biblia, mimi nakuambia kwamba usipotenda kulingana na yale unayojua, umo matatani.”
Katika muda mfupi alibatizwa naye amekuwa akitumikia akiwa mzee Mkristo kwa miaka kadha sasa. Pia yeye alisaidia sana katika ujenzi wa yale makao mapya makubwa ya tawi katika Cesario Lange, Sao Paulo, ambapo sisi 480 tunafanya kazi sasa tukitumikie mahitaji ya kiroho ya hesabu inayokuwa ya Mashahidi katika Brazili.
Maongezeko Yenye Kuendelea
Katika 1945 tulikuwa na ziara ya kwanza ya msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Nathan H. Knorr, na pia ya aliyekuwa wakati huo kaimu wa msimamizi, Frederick Franz. Mkusanyiko ulipangwa katika jumba la michezo ya kuzoeza viungo katika Mji wa Sao Paulo, nami nilitumikia nikiwa mtafsiri kwa hao ndugu wenye kuzuru. Kilele cha hudhurio letu kilikuwa 765.
Nakumbuka Ndugu Knorr akiutazama uwanja wa mchezo mkubwa ulio karibu na kustaajabia kama tungeweza kamwe kuujaza. Basi, tulifanya hivyo katika Desemba 1973, wakati 94,586 walipojaa Uwanja wa Mchezo wa Paca-embu kwenye Mkusanyiko wa “Ushindi wa Kimungu”. Idadi hiyo ilipitwa katika Agosti 1985 kwenye Mkusanyiko wa “Washika-Ukamilifu” katika Uwanja wa Michezo wa Morumbi, Mji wa Sao Paulo, ambapo 162,941 walikuwapo. Na wakati uo huo, wengine 86,410 walikuwa wakihudhuria kwenye uwanja wa mchezo katika Rio de Janeiro. Baadaye, mikutano mingine zaidi 23 iliinua jumla ya hudhurio la Mikusanyiko ya “Washika-Ukamilifu” katika Brazili kuwa 389,387!
Kwa muda wa miaka iliyopita, nimependelewa kutafsiri kwa ajili ya wasemaji wenye kuzuru kutoka makao makuu ya Brooklyn, New York. Hivi karibuni mmoja wao, alipokuwa akitembea pamoja nami na kuona watu wengi niliokuwa nimejifunza nao kwa muda wa miaka iliyopita wakija kunisalimu, alisema hivi kwa ucheshi: “Sijapata kamwe kuona mwanamume mseja mwenye watoto wengi hivyo.”
Nyakati nzuri kabisa katika maisha yangu zimekuwa pia ile mikusanyiko ya kimataifa niliyoweza kuhudhuria katika nchi nyinginezo. Kwenye mkusanyiko huko Nuremberg katika 1969, nilimwona mama yangu kwa mara ya kwanza kwa muda wa miaka 30. Alikufa akiwa mwaminifu katika 1973. Baba hakuruhusiwa kusafiri nje ya nchi kwa ajili ya mkusanyiko, nami sikumwona tena kamwe baada ya kuondoka nyumbani. Katika 1978 nilikuwa na pendeleo la kutoa hotuba ya watu wote kwenye mkusanyiko wa kimataifa katika Vienna, Austria, uliokuwa mkusanyiko wa kwanza mkubwa niliopata kuhudhuria katika mji wa uzaliwa wangu.
Katika muda wa miaka hii mingi katika Brazili, nimeshuhudia kwamba Yehova Ndiye “akuzaye.” (1 Wakorintho 3:7) Katika 1948 tulipita kiwango cha wahubiri 1,000. Baada ya hapo, hesabu ya wahubiri iliruka kufika 12,992 katika 1958 na kufika 60,139 katika 1970. Badala ya wale wahubiri wa Ufalme 127 tuliokuwa nao katika Septemba 1939, walikuwako 196,948 katika Agosti 1986. Hakika, ‘mdogo amekuwa taifa hodari’ pia katika nchi hii.—Isaya 60:22.
Lakini idadi ya watu wa Brazili imeongezeka pia, kutoka milioni 41 katika 1939 kufika zaidi ya milioni 135 sasa. Kwa hiyo tungali na shamba kubwa la utendaji. Imekuwa furaha yangu binafsi kuhusika katika maongezeko ya ajabu tuliyopewa na Yehova, na limekuwa jambo lenye kusisimua kama nini! Basi mimi naweza kupendekeza hivi kwa ye yote anayetaka kumtumikia Yehova kwa wakati wote: Endelea! Usiogope linaloweza kutokea, kwa kuwa “Yehova mwenyewe atalinda kuondoka kwako na kuingia kwako.”—Zaburi 121:7, 8, NW.
[Blabu katika ukurasa wa 26]
“Nakuambia kwamba usipotenda kulingana na yale unayojua, umo matatani”
[Picha katika ukurasa wa 25]
N. H. Knorrakisema, pamoja na Erich Kattnerakiwa mkalimani, katika Sao Paulo, Brazili, 1945