Uvumilivu Huongoza Kwenye Maendeleo
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JOSÉ MAGLOVSKY
Polisi aliponishika mkono, nilimtafuta baba yangu. Hata hivyo, bila mimi kujua, alikuwa tayari amepelekwa kwenye kituo cha polisi. Nilipofika huko, polisi wakachukua vichapo vyetu vyote, kutia ndani Biblia zetu, na kuzitupa sakafuni. Baba yangu alipoona hilo, akauliza: “Nyinyi huweka hata Biblia sakafuni?” Mkuu wa polisi akaomba msamaha, kisha akazichukua Biblia hizo na kuziweka mezani.
TULIFIKAJE katika kituo cha polisi? Tulikuwa tukifanya nini? Je, tulikuwa katika utawala wa mabavu wa polisi wasiotambua kuwapo kwa Mungu, ili kwamba hata tunyang’anywe Biblia zetu? Ili kujibu maswali haya, tutahitaji kurudi nyuma hadi 1925, hata kabla sijazaliwa.
Katika mwaka huo baba yangu, Estefano Maglovsky, na mama yangu Juliana, walihama iliyokuwa Yugoslavia wakati huo na kwenda Brazili, wakikaa katika São Paulo. Ingawa baba alikuwa Mprotestanti na mama Mkatoliki, dini haikuwa kitu cha kuwatenganisha. Kwa kweli, miaka kumi baadaye kitu fulani kilifanyika kilichowaunganisha pamoja kidini. Shemeji ya baba alimletea kijitabu chenye picha nyingi cha Kihungaria kilichozungumzia hali ya wafu. Shemeji yake alikuwa amekipokea kijitabu hicho kikiwa zawadi, naye akamuuliza baba akisome na ampe maoni yake juu ya yaliyomo, hasa sehemu ile juu ya “helo.” Baba alitumia usiku mzima akikisoma tena na tena kijitabu hicho, na siku iliyofuata, shemeji yake alipokuja kusikia maoni yake, kwa kufaa baba alijibu: “Kweli ipo hapa!”
Mianzo Midogo
Kwa kuwa kichapo hicho kilitokana na Mashahidi wa Yehova, wote wawili waliwatafuta ili wajifunze mengi kuhusu itikadi na mafundisho yao. Mwishowe walipowapata, washiriki kadhaa wa familia yetu wakaanza kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na Mashahidi. Mwaka huo huo, 1935, funzo la Biblia la kawaida la Kihungaria lilianzishwa, kukiwa na wastani wa watu wanane wakishiriki, na tangu wakati huo tumekuwa na mafunzo ya Biblia ya kawaida nyumbani kwetu.
Baada ya miaka miwili ya kujifunza Biblia, baba alibatizwa katika 1937 naye akawa Shahidi wa Yehova mwenye shauku, akishiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba pia akitumika akiwa mtumishi aliyewekwa na kiongozi wa funzo. Alisaidia katika kufanyiza kutaniko la kwanza katika São Paulo, kitongojini mwa Vila Mariana. Kutaniko hilo baadaye lilihamishwa kitovuni mwa jiji na kuwa Kutaniko la Central. Miaka kumi baadaye kutaniko la pili lilifanyizwa, katika eneo la Ypiranga, na baba akawekwa kuwa mtumishi wa kutaniko huko. Katika 1954 kutaniko la tatu lilifanyizwa, katika sehemu ya Moinho Velho, ambapo alitumika akiwa mtumishi wa kutaniko vilevile.
Mara tu kikundi hicho kilipojisimamia, alianza kusaidia kikundi kilichokuwa karibu-karibu katika São Bernardo do Campo. Yote hayo kwa ajili ya baraka za Yehova juu ya jitihada ya vikundi hivi vidogo vya Mashahidi wakati wa miaka hiyo, ukuzi umekuwa wenye kutokeza, hivi kwamba katika 1994 kulikuwa na zaidi ya wahubiri 70,000 katika makutaniko 760 katika São Paulo iliyo kubwa kidogo. Kwa kusikitisha, baba hakuishi aone ukuzi huu. Alikufa katika 1958 akiwa na umri wa miaka 57.
Kujitahidi Kufuata Kielelezo cha Baba
Sifa iliyotokeza ya baba, kama ilivyo kwa Wakristo wakomavu, ilikuwa ukaribishaji wake wa wageni. (Ona 3 Yohana 1, 5-8.) Kama tokeo, tulipendelewa kuwakaribisha Antonio Andrade, mkeye na mwana wao, waliokuja Brazili kutoka Marekani pamoja na Ndugu na Dada Yuille katika 1936. Pia wageni nyumbani kwetu walikuwa wahitimu wawili wa Watchtower Bible School of Gilead, Harry Black na Dillard Leathco, waliokuwa wamishonari wa kwanza waliogawiwa Brazili katika 1945. Wengine wengi waliwafuata. Ndugu na dada hawa walikuwa chanzo cha kitia moyo wakati wote kwa kila mmoja katika familia yetu. Kwa uthamini wa hayo na kwa manufaa ya familia yangu, nimejitahidi kuiga kielelezo cha baba yangu kuhusu sifa ya Kikristo ya ukaribishaji wa wageni.
Ingawa nilikuwa na umri wa miaka tisa tu baba alipojifunza kweli katika 1935, nikiwa mtoto wa kwanza wa kiume, nilianza kuandamana naye katika utendaji wake wa kitheokrasi. Sisi wote tulihudhuria mikutano pamoja naye kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa kwenye makao makuu ya Mashahidi katika São Paulo kwenye Barabara ya Eça de Queiroz, Nambari 141. Kwa sababu ya ufundishaji na mazoezi aliyonipa baba, nilikuza tamaa yenye nguvu ya kumtumikia Yehova, na katika 1940, nilijiweka wakfu kwa Yehova, na kufananisha huo kwa uzamisho wa maji katika Mto Tietê uliochafuliwa sasa, uteremkao kupitia kitovuni mwa São Paulo.
Baada ya muda mfupi nikajifunza kilichomaanisha kuwa mhubiri wa kawaida wa habari njema, kupanda na kutia maji ujumbe wa kweli ndani ya wengine na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani pamoja nao. Sasa, nionapo yale maelfu ya Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu katika Brazili, nahisi shangwe ya kina sana nikijua kwamba nilitumiwa Naye kuwasaidia wengi wao kufikia ujuzi wa ile kweli au kuzidisha uthamini wao kwayo.
Kati ya wale niliosaidia alikuwa Joaquim Melo, niliyekuta katika huduma ya mlango kwa mlango. Nilikuwa nikisema na wanaume wengine watatu waliokuwa wakisikiliza bila upendezi mwingi. Kisha nikagundua kijana mmoja aliyekuwa ameungana nasi naye alisikiliza kwa makini sana. Nilipoona upendezi wake, nilimwelekezea uangalifu wangu, baada ya ushahidi mzuri, nikamkaribisha kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Hakuhudhuria funzo hilo, lakini alikuja kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na baadaye akahudhuria mikutano kwa kawaida. Alifanya maendeleo mazuri, akabatizwa, na kwa miaka kadhaa ametumika akiwa mhudumu asafiriye, akiandamana na mkeye.
Kisha alikuwako Arnaldo Orsi, niliyekutana naye mahali nilipofanya kazi. Nilimhubiria kwa kawaida mfanyakazi mwenzi lakini nikagundua kwamba kijana mmoja mwenye madevu alisikiliza kila wakati, hivyo nikaanza kuzungumza moja kwa moja naye. Alikuwa wa familia moja iliyoshikilia sana Ukatoliki lakini akauliza maswali mengi kuhusu mambo kama vile uvutaji sigareti, kutazama filamu za ponografia, na mazoezi ya ufundi wa kupigana mwereka. Nilimwonyesha yale Biblia iliyosema, na kwa mshangao wangu wenye shangwe, siku iliyofuata alinikaribisha kutazama akivunja kiko na kiberiti chake cha gesi pamoja na msalaba wake, akaharibu filamu zake za ponografia, na kukata madevu yake. Mtu aliyebadilika kwa dakika chache! Pia aliacha kufanya mazoezi ya mwereka akaniomba nisome naye Biblia kila siku. Ijapokuwa upinzani kutoka kwa mkeye na babaye, alifanya maendeleo mazuri kiroho kwa msaada wa ndugu walioishi karibu naye. Baada ya muda mfupi, alibatizwa na leo anatumika akiwa mzee wa kutaniko. Mkeye na watoto pia waliikubali kweli.
Kushiriki Katika Utumishi wa Ufalme
Nilipokuwa karibu na umri wa miaka 14, nilianza kufanya kazi katika kituo cha utangazaji, nilipojifunzia jinsi ya kupaka rangi ishara. Hili lilithibitika kuwa la maana sana, na kwa miaka kadhaa ni mimi tu katika São Paulo niliyekuwa nikipaka rangi mabango na alama za barabarani za kutangaza hotuba za watu wote na makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Kwa karibu miaka 30, nilikuwa na pendeleo la kutumika nikiwa mwangalizi wa Idara ya Ishara kwenye mkusanyiko. Sikuzote nilikuwa nikihifadhi likizo yangu ili nifanye kazi kwenye mikusanyiko, hata nikilala katika jumba la mkusanyiko ili niweze kupaka rangi ishara kwa wakati.
Pia nilipata fursa ya kufanya kazi na gari lenye kikuza sauti la Sosaiti, kilichokuwa kitu kipya wakati huo. Tungeweka vichapo vyetu vya Biblia jukwaani, huku gari lenye kikuza sauti likitangaza ujumbe uliorekodiwa, tulikuwa tukizungumza na watu waliotoka nyumbani kuona ni nini kilichokuwa kikitendeka. Njia nyingine tuliyotumia kujulisha habari njema za Ufalme ilikuwa kwa gramafoni yenye kubebeka, na bado nina rekodi zilizotumiwa kutoa vichapo vya Sosaiti. Kama tokeo fasihi nyingi za Biblia ziliangushwa.
Katika siku hizo Kanisa Katoliki lilifanya milolongo katika barabara za São Paulo, mara nyingi kukiwa na wanaume mbele wakiondoa watu njiani. Jumapili moja, baba na mimi tulikuwa tukiangusha Mnara wa Mlinzi na Amkeni! barabarani mlolongo mrefu ulipotokea. Baba alikuwa amevalia kofia, kama ilivyokuwa desturi yake. Mtu mmoja mbele ya mlolongo huo akapaaza sauti: “Vua kofia yako! Huoni mlolongo unakuja?” Baba alipokataa kuvua kofia yake, watu zaidi walikuja, wakitusukuma kando dhidi ya dirisha la duka na kufanya fujo. Jambo hili lilimtahadharisha polisi mmoja, aliyekuja kuona ni nini kilichokuwa kikitendeka. Mmoja wa watu hao akamshika mkono polisi huyo, akitaka kuzungumza naye. “Ondoa mkono wako kwenye yunifomu yangu!” polisi huyo akaamuru, akiupiga kofi mkono wa mtu huyo. Kisha akauliza ni nini kilichokuwa kikiendelea. Mtu huyo akaeleza kwamba baba alikataa kutoa kofia kwa ajili ya mlolongo, akiongeza: “Mimi ni mfuasi wa Katoliki ya Kiroma.” Jibu lisilotazamiwa lilikuwa: “Unasema wewe ni Mroma? Basi rudi Roma! Huku ni Brazili.” Kisha akatugeukia, akiuliza: “Nani aliyekuwa hapa kwanza?” Baba alijibu kwamba ni sisi, polisi huyo akawafukuza watu hao na kutuambia tuendelee na kazi yetu. Alisimama kando yetu hadi mlolongo wote ulipopita—na baba hakutoa kofia!
Visa kama hivi havikuwa vya kawaida. Lakini vilipotokea, ilitia moyo kujua kwamba kulikuwa na watu walioshikilia haki kwa watu wa hali ya chini na wasiounga mkono Kanisa Katoliki.
Katika pindi nyingine, nilikutana na tineja mmoja aliyeonyesha kupendezwa na akaniomba nirudi juma lililofuata. Niliporudi alinikaribisha vizuri na kuniomba niingie. Nilishangaa kama nini kujikuta nimezungukwa na genge la vijana wakinidhihaki na kujaribu kuniudhi! Hali hiyo ikawa mbaya sana, na nikahisi kwamba watanishambulia mara hiyo. Nilimwambia aliyekuwa amenikaribisha kwamba ikiwa chochote kitanipata, atakuwa mwenye daraka lote na kwamba familia yangu ilijua nilipokuwa. Niliwaomba waniache, nao wakakubali. Hata hivyo, kabla ya kuondoka, niliwaambia kwamba ikiwa yeyote wao angetaka kuongea nami peke yangu, ningepatikana. Baadaye, nilijua kwamba walikuwa kikundi cha washupavu, marafiki wa kasisi wa mahali hapo aliyekuwa amewatia moyo kufanya mkutano huo. Nilifurahi kuondoka mikononi mwao.
Bila shaka, mwanzoni, maendeleo katika Brazili yalikuwa ya polepole, karibu yasionekane. Tulikuwa katika sehemu ya kwanza ya “upandaji,” tukiwa na wakati mchache wa “upaliliaji” na “uvunaji” matunda ya kazi yetu. Sikuzote tulikumbuka yale mtume Paulo aliyoandika: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (1 Wakorintho 3:6, 7) Wahitimu wawili wa Gileadi walipofika katika 1945, tulihisi kwamba wakati ulikuwa umefika wa ukuzi huu uliongojewa kwa muda mrefu.
Moyo Mkuu Mbele ya Upinzani
Hata hivyo, ukuzi haungepatikana bila upinzani, baada ya Vita ya Ulimwengu ya 2 kuanza Ulaya. Kulikuwa mnyanyaso wa moja kwa moja kwa sababu watu kwa jumla na wengine katika mamlaka hawakuelewa msimamo wetu wa kutokuwamo. Katika pindi moja, katika 1940, tulipokuwa tukifanya kazi ya barabarani tukiwa na mabango kitovuni mwa São Paulo, polisi mmoja akaja nyuma yangu, akayapasua mabango hayo, na kunishika mkono kunipeleka kwenye kituo cha polisi. Nikamtafuta baba yangu, lakini hakuonekana popote. Nikiwa sijui, yeye pamoja na ndugu na dada kadhaa wengineo, kutia ndani Ndugu Yuille, aliyekuwa msimamizi wa kazi katika Brazili, walikuwa tayari wamepelekwa kwenye kituo cha polisi. Kama ionyeshwavyo kwenye fungu la kwanza, huko nikakutana na baba tena.
Kwa kuwa nilikuwa mdogo, singeweza kuzuiliwa mara moja nikarudishwa nyumbani na polisi mmoja nikakabidhiwa mama yangu. Jioni hiyo hiyo akina dada pia waliachiliwa. Baadaye polisi wakaamua kuwaachilia ndugu wote, karibu kumi, ila Ndugu Yuille. Hata hivyo, ndugu walisisitiza: “Ama twende sote ama tubaki sote.” Polisi walikataa kabisa, hivyo wote walilala sakafuni ndani ya chumba chenye baridi. Siku iliyofuata wote waliachiliwa bila matakwa. Mara kadhaa ndugu walifungwa kwa kuhubiri wakiwa na mabango. Ishara hizo zilitangaza hotuba ya watu wote na pia kijitabu chenye kichwa Fascism or Freedom, na wenye mamlaka fulani wakadhani kwamba tulikuwa tukipendelea Ufashisti, jambo ambalo kwa wazi lilitokeza kutoelewana.
Utumishi wa kijeshi wa kulazimishwa pia uliletea ndugu vijana shida. Katika 1948, nilikuwa wa kwanza katika Brazili kufungwa gerezani kwa sababu ya suala hili. Wenye mamlaka hawakujua la kunifanya. Nilihamishwa kwenye kambi ya jeshi katika Caçapava na kupewa kazi ya kupanda na kutunza mboga bustanini na vilevile kusafisha chumba kilichotumiwa na maofisa wa ulinzi. Nilikuwa na fursa nyingi za kutoa ushahidi na kuangushia watu hao vichapo. Ofisa aliyekuwa kazini alikuwa wa kwanza kuchukua nakala ya kitabu cha Sosaiti Children. Baadaye, hata niligawiwa kufundisha mambo ya dini kwa wanajeshi 30 au 40 walioshindwa kufanya mazoezi nao wakafungiwa ndani ya chumba fulani. Mwishowe, baada ya karibu miezi kumi katika jela, nilipelekwa mahakamani na kuachiliwa. Namshukuru Yehova, aliyenipa uwezo wa kukabili matisho, jeuri, na dhihaka niliyopokea kutoka kwa watu fulani.
Msaidizi Mwaminifu-Mshikamanifu
Katika Juni 2, 1951, nilimwoa Barbara, na tangu wakati huo amekuwa mwandamani mwaminifu-mshikamanifu katika kufundisha watoto wetu na kuwalea katika “adabu na maonyo ya Bwana.” (Waefeso 6:4) Kati ya watoto wetu watano, wanne wanamtumikia Yehova kwa shangwe katika migawo mbalimbali. Tumaini letu ni kwamba, pamoja nasi, wataendelea kuvumilia katika kweli na kuchangia maendeleo ya tengenezo na kazi inayofanywa. Washiriki wote wa familia walioko kwenye picha iliyoandamanishwa ni watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu ila yule mdogo kabisa, mtoto aliyeshikwa mkononi. Wanne ni wazee wa kutaniko na wawili kati yao ni mapainia wa kawaida, likitoa kielelezo cha ukweli wa Mithali 17:6: “Wana wa wana ndio taji ya wazee, na utukufu wa watoto ni baba zao.”
Sasa, nikiwa na umri wa miaka 68, afya yangu si nzuri sana. Katika 1991, mishipa yangu mitatu ya damu ilirekebishwa na baadaye nikafanyiwa upasuaji wa mishipa hiyo. Hata hivyo, nafurahi kuweza kuendelea kutumika nikiwa mwangalizi-msimamizi katika kutaniko moja katika São Bernardo do Campo, nikifuata hatua za baba yangu, aliyekuwa wa kwanza kuanzisha kazi hapa. Kizazi chetu kwelikweli ni cha pekee, kuwa na fursa ya kushiriki katika pendeleo lisilorudiwa kamwe la kutangaza kusimamishwa kwa Ufalme wa Kimesiya wa Yehova. Hivyo tusisahau kamwe maneno ya Paulo kwa Timotheo: “Bali wewe, . . . fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.”—2 Timotheo 4:5.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Wazazi wangu, Estefano na Juliana Maglovsky
[Picha katika ukurasa wa 26]
José na Barbara pamoja na washiriki wa familia yao ya watumishi waliojiweka wakfu kwa Yehova