Yehova Alibariki Uamuzi Wangu wa Kupiga Moyo Konde
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RICHARD WUTTKE
“Wewe utakufa katika muda wa miezi mitatu!” “Wamaanisha nini?” “Hivyo ndivyo daktari uliyeona katika Assis alivyoniambia,” William ndugu yangu akajibu.
LAKINI mimi nilitaka kuishi, si kufa. Kwa mara ya kwanza, nilisali kwa Mungu nipate msaada. Kwa kufurahisha, miaka 46 baadaye, naweza kusema kwamba ingawa daktari huyo hakusema tatizo langu lilikuwa nini, upimaji wake ulikosea. Hata hivyo, ogofyo hilo lilifanya nifikirie kusudi langu maishani na uhitaji wa kutumikia Muumba wetu.
Familia Yagura
Nilipozaliwa Novemba 11, 1921, wazazi wangu walikuwa wakiishi katika Grosen, mji mdogo katika Ujeremani mashariki. Walizaliwa katika Urusi na wahamiaji Wajeremani. Lakini, mapinduzi ya Bolsheviki yalipoleta Ukomunisti katika 1917, wao pamoja na wengine wenye asili ya Kijeremani walihamishwa na kupoteza mali zao zote. Baada ya safari ndefu kwa gari-moshi la mizigo, wazazi wangu na watoto wao wadogo waliwasili kwenye mpaka wa Ujeremani. Hata hivyo, walikatazwa kuingia na kulazimika kufunga safari ya kurudi Urusi. Huko wakakatazwa kuingia tena, kwa hiyo wakalazimika kurudi Ujeremani. Baada ya miezi ya magumu, mwishowe waliruhusiwa kuingia nchini.
Nilipokuwa na miaka kumi, baba yangu alikufa. Miaka miwili baadaye, katika 1933, Hitler alipata mamlaka, nami nikashurutishwa kujiunga na harakati ya Vijana wa Nazi. Wakati wa milki ya Hitler, kulikuwako matatizo kwa Wajeremani waliozaliwa katika nchi nyinginezo, na kulikuwa na uthibitisho wa kwamba Ujeremani ilikuwa ikijitayarisha kwa ajili ya vita nyingine. Kwa hiyo tukaamua kuhamia humu Brazili, kwa kutiwa moyo na wengine waliokuwa tayari wamehamia huko. Tuliwasili katika Santos, Brazili, katika Mei 1936.
Baada ya kufanya kazi miezi michache katika shamba la kahawa, tulinunua shamba dogo katika jimbo lenye rutuba karibu na Maracaí katika mkoa wa São Paulo. Tulipokuwa tukijenga nyumba yetu, tuliweza kukaa katika makao ya mhudumu Mlutheri. Alitutia moyo tuhudhurie kanisa lake lakini wakati yeye, na baadaye mwandamizi wake, alipoanza kuongea siasa katika mahubiri yake, tuliacha kanisa hilo.
Kukutana na Ukweli wa Biblia Mara ya Kwanza
Karibu na wakati huu ndipo ndugu yangu aliponiambia juu ya upimaji wenye kuogofya uliofanywa na daktari. Hivyo basi nikaenda São Paulo nikapate maoni ya pili. Nilipokuwa huko, familia niliyokuwa nikiishi nayo ilipata ziara kutoka kwa rafiki yao, Otto Erbert. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye akaanza kututolea ushahidi. Hata hivyo, familia hiyo haikuthamini aliyokuwa akisema, na mmoja kwa mmoja wakaondoka chumbani wote, wakiniacha mimi na mgeni wao.
Otto aliongea nami kwa muda wa karibu saa mbili juu ya habari za moto wa helo; kutokufa kwa nafsi; Mungu wa kweli, Yehova; Ufalme wake; na tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso. Alisimulia wakati ujao ulio mwangavu kama nini! Ulitofautiana kama nini na mambo niliyokuwa nimejifunza katika Kanisa la Kilutheri! Mwishowe, Otto aliuliza hivi: “Je! wewe waamini katika mafundisho bandia ya Jumuiya ya Wakristo au katika Biblia?”
“Katika Biblia,” nikajibu.
“Basi jifunze hiyo!” akahimiza, akiongezea hivi: “Ikiwa wataka kusikia mengi zaidi juu yayo, uje unione.” Kwa kuwa nilipenda niliyoyasikia, hasa juu ya kuishi milele duniani, nilienda kumwona kesho yake. Mazungumzo hayo ya pili yalinisadikisha kwamba nilikuwa nimeupata ‘ukweli uwekao ainabinadamu huru.’ (Yohana 8:32) Niliondoka na kijitabu kimoja, Health and Life, na mwaliko wa funzo la Biblia katika Kijeremani.
Kutimiza Tamaa Yangu ya Kina Kirefu Kabisa
Kwa wakati huo, nilipata matibabu yafaayo na nikaweza kurudi nyumbani. Nilimchukua Otto Erbert kwenda likizoni. Mama alifurahi sana kwamba nilikuwa ninajifunza Biblia, kitabu ambacho sikuzote kilikuwa juu ya meza yetu lakini kisisomwe kamwe. Baada ya Otto kurudi São Paulo, nilifanya funzo la Biblia pamoja na familia yetu karibu kila usiku, kwa kadiri ambayo ningeweza. Niliona shangwe mno wakati mama yangu, Robert ndugu yangu, na Olga dada yangu walipokubali wote ujumbe wa ukweli. Sikuzote nyumba yetu ilikuwa imekuwa kitovu cha starehe za kijamii, lakini baada ya karibu miezi miwili ya kutoa kwetu ushahidi, ilikuwa karibu tupu. Mmoja wa wale waliokuwa wakija nyumbani kwetu alisema: “Mkiendelea na mambo haya, mwisho wenu utakuwa katika makao ya wakichaa!”
Hata hivyo, tamaa yangu kutumikia Yehova iliendelea kukua. Nilijipatia vichapo zaidi, nikawa nikisoma hadi usiku sana. Lakini fasihi zote zilikuwa katika Kijeremani, nami niling’amua kwamba ikiwa ningefundisha wengine, ningelazimika kujifunza Kireno. Hivyo basi, katika 1945, nilihamia São Paulo kusomea Kireno. Niliishi na Otto Erbert, ambaye baadaye alimwoa Olga dada yangu.
Pamoja na wengine karibu 50, nikaanza kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme moja tu katika São Paulo. Kundi moja hilo sasa limekua likawa makundi zaidi ya 510 katika São Paulo iliyo kubwa zaidi, likiwa na wahubiri wa Ufalme zaidi ya 50,000. Siku ya Januari 6, 1946, nilibatizwa kwa ufananisho wa wakfu wangu kufanya mapenzi ya Mungu. Mwaka uo huo nilihudhuria “Mataifa Yenye Kuterema” Kusanyiko la Kitheokrasi katika São Paulo, kusanyiko langu kubwa la kwanza. Ulikuwa msisimuko ulioje kuona watu 1,700 wakiwapo Jumapili! Kwenye mkusanyiko huu nilikutana na Otto Estelmann, aliyenitia moyo, akisema: “Richard, wewe ni mchanga; wewe una afya; hivyo basi uwe painia.”
Nilikuwa nimefikiria huduma ya wakati wote kabla ya hapo, lakini sasa nilifanya hivyo kwa uzito zaidi. Nikiwa pamoja na wawili wengine, niliweka wakati fulani wa kuanza miezi sita ijayo. Wakati huo ulipofika, niliuliza hivi: “Je! mko tayari kwenda?” Hakuna yeyote wa hao aliyekuwa tayari. Hivyo basi nikawaambia mimi ningeanza tu. “Utakuwa na matatizo,” wakaonya. Lakini mimi nikashikamana na uamuzi wangu. Siku ya Mei 24, 1947, nilipokea mgawo wangu niwe painia wa kawaida.
Milango Mipya ya Utumishi Yafunguka
Eneo langu lilikuwa kubwa sana, kutia na sehemu za makao na za biashara za São Paulo. Niliangusha mamia ya vitabu na vijitabu kila mwezi. Asubuhi moja niliingia chumba kikubwa ambamo wanaume kadhaa walikuwa wakifanya kazi. Nilimwendea mwanamume wa kwanza nikamtolea kitabu “The Truth Shall Make You Free.”
“Una vitabu vingapi katika mkoba wako?” akauliza.
“Karibu 20,” nikajibu. Alichukua vyote na kumpa kimoja kila mwanamume aliyepo. Kumbe lilikuwa ni jumba la jiji!
Hata hivyo, shangwe yangu iliyo kubwa kabisa ilikuwa katika kuongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia. Katika muda wa miaka minne, kwa msaada wa Yehova, 38 kati ya wale niliojifunza nao walibatizwa. Baadhi yao walianza huduma ya wakati wote. Mmoja wao alikuwa Afonso Grigalhunas, aliyetumikia kwa miaka zaidi ya kumi akiwa painia msaidizi, mpaka kifo chake katika 1988—tena akiwa na mguu wa kufanyizwa. Halafu ilikuwako ile familia ya akina Ciuffa. Francisco, mwana mmoja, alitumikia kwa miaka mingi akiwa mwangalizi anayesafiri, na dada yake, Ângela, angali painia.
Katika 1951 nilialikwa niwe mwangalizi anayesafiri. Mgawo wangu ulihusisha maeneo makubwa ya mikoa ya Rio Grande do Sul na Santa Catarina. Maelfu ya watu wenye asili ya Ulaya waliishi huko katika kusini mwa Brazili. Zilizo nyingi za ziara zilifanywa kwa watu na vikundi vilivyo peke yavyo, kwa maana kulikuwa na makundi machache wakati huo. Kulikuwako mito mingi lakini madaraja machache, jambo lililomaanisha kuvuka kwa miguu ile iliyo midogo huku mkoba wangu wa nguo ukiwa mgongoni na taipureta yangu na mkoba wa vitabu ukiwa mikononi. Barabara zilikuwa zisizotandazwa na zilijaa mashimo. Ili kulinda nguo zangu na mavumbi hayo, nilivaa kanzu nyepesi ya juu. Hiyo iliongoza watu fulani kufikiri nilikuwa padri wao mpya, nao wakajaribu kubusu mkono wangu.
Kutetea Masilahi ya Ufalme
Nilipokuwa nikijaribu kuyachukua matatizo kwa maoni yafaayo, nilifuata kanuni hii: Ikiwa wengine waweza kuishi mbali sana na majiji, watembee katika mapito haya na kuvuka mito hii, mbona mimi nisiweze kufanya hivyo hivyo, hasa kwa kuwa mimi nina ujumbe wa maana sana kuwaletea?
Mara nyingi matatizo ya hali tofauti yalitokea katika miji midogo zaidi. Kwa kielelezo, wakati mmoja tulifanya mipango ya kufanya mkutano katika shule moja ya mahali hapo karibu na bustani fulani. Upande ule mwingine wa bustani ilikuwako nyumba ndogo ya pombe na kanisa la Kikatoliki. Mwalimu alipokosa kuja kuifungua shule, niliamua kutoa hotuba katika ile bustani. Upesi baada ya hotuba kuanza, wanaume nusu dazani walitoka ndani ya nyumba ya pombe wakaanza kupiga makelele na kupungapunga mikono. Tulipata habari baadaye kwamba walikuwa wamelipwa na padri ili wafanye hivyo.
Mimi nilianza kusema kwa sauti kubwa zaidi, nikisema nao moja kwa moja. Waliacha, na mmoja akasema: “Yeye anaongea juu ya Mungu. Padri angewezaje kusema kwamba yeye ni wa Ibilisi?” Padri alipoona kwamba wanaume hao hawangeuvunja mkutano, aliingia ndani ya gari lake aina ya jeep akazunguka-zunguka bustani, akipaaza sauti hivi: “Mtu yeyote aliye Mkatoliki hapaswi kuhudhuria mkutano huu!” Hakuna aliyebanduka hapo, na mkutano uliendelea kwa amani.
Katika Mirante do Paranapanema, São Paulo, nilizuru mkuu wa polisi kueleza hali ya kazi yetu na kuomba utumizi wa jumba moja kwa ajili ya hotuba ya peupe. Alitupangia tutumie jumba moja la klabu. Tulimwambia tungekuwa pia tukitayarisha vikaratasi vya ukaribishaji ili kuvumisha hotuba hiyo. “Mtakuwa mkivigawanya katika sehemu gani ya mji?” akauliza. Baada ya sisi kumwambia, aliomba kwamba baadhi yetu wagawanye katika sehemu nyingine ya mji. Alikuja kwenye hotuba Jumapili, akiwa pamoja na polisi wawili, kama alivyosema, “ili kudumisha utaratibu.”
“Je! wataka mimi nitoe utangulizi wa hotuba yako?” akauliza.
“Nitafurahi,” mimi nikajibu, “lakini acha nikueleze jinsi sisi hutoa utangulizi wa kujulisha wasemaji wetu.” Baada ya kunitolea utangulizi, aliketi jukwaani ili asikilize. Mimi nakuambia kwamba, wasikilizaji walijiendesha vizuri ajabu. Hatukupata matata huko, kwani je! si walikuwako polisi wawili mlangoni na mkuu wao akiwa ameketi jukwaani!
Katika Machi 1956 niliwekwa kuwa mwangalizi wa wilaya na nikatumikia makusanyiko kotekote Brazili. Umbali wa kusafiri ulikuwa mkubwa. Wakati mmoja ilichukua siku tatu kutoka kusanyiko moja hadi lililofuata. Katika sehemu ya kaskazini ya nchi, nyakati fulani usafiri ulikuwa kwa magari-mkokoteni. Yalikuwa bila dirisha, na kwa sababu hiyo yalikuwa na nafasi nyingi za kupitishia hewa, hilo likiwa wazo zuri, kwa maana abiria walikuwa ni kutia na kuku na nguruwe!
Gileadi Yaimarisha Uamuzi Wangu wa Kupiga Moyo Konde
Ulikuwa msisimuko ulioje katika 1958 kuhudhuria Watchtower Bible School of Gilead! Darasa letu lilihitimu kiangazi hicho wakati wa ule mkusanyiko uliofanywa Yankee Stadium na Polo Grounds, ambako watu 253,922 kutoka nchi tofauti-tofauti 123 walihudhuria hotuba ya watu wote. Lo, tamasha iliyoje! Ndipo nikarudi Brazili, nikiwa nimeazimia zaidi ya wakati wowote kufuliza kutangaza Ufalme wa Yehova.
Katika 1962 nilifunga ndoa na Ruth Honemann, ambaye tayari alikuwa amekuwa akitumikia kwa zaidi ya miaka sita akiwa misionari katika Brazili. Tangu wakati wa ndoa yetu nimekuwa nikiendelea kupata shangwe ya mapendeleo zaidi ya utumishi, nikiongoza mitaala katika Shule ya Huduma ya Ufalme na Shule ya Utumishi wa Painia, na pia kuongoza katika kupanga mikusanyiko ya kitaifa na ya kimataifa na katika kujenga Jumba la Kusanyiko la kwanza la São Paulo.
Wakati wa sasa sisi twalionea shangwe pendeleo kubwa kabisa la kazi-maisha zetu za kitheokrasi tukiwa washiriki wa familia ya Betheli ya Brazili. Ninapotazama nyuma kwenye miaka zaidi ya 40 ya utumishi wa wakati wote, 35 kati yayo nikiwa mwangalizi anayesafiri, naweza kusema kwamba imekuwa yenye kujaa utendaji mbalimbali wenye kufurahisha na kuthawabisha. (Mithali 10:22) Nimejifunza mengi kutokana na tengenezo la Yehova, kutia na uhitaji wa kuonyesha hisia-mwenzi, kuwa rafiki wala si bwana-mkubwa, na kutokuwa mwenye shughuli nyingi mno nisiweze kuhudumia mahitaji ya wengine. Kwa umalizio, ningependa kusema, hasa kwa walio wachanga zaidi, yale ambayo Ndugu Estelmann alisema kwangu miaka mingi iliyopita: “Wewe ni mchanga; wewe una afya; hivyo basi uwe painia!”
[Picha katika ukurasa wa 29]
Makao yetu ya wakati wa sasa, Betheli ya Brazili