Kutegemezwa na Uhakika Wangu Katika Yehova
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA AGENOR DA PAIXÃO
Mwana wetu pekee, Paul, alikufa kutokana na mchochota wa mirija ya mapafu alipokuwa na umri wa miezi 11 tu. Miezi mitatu baadaye, Agosti 15, 1945, mke wangu mpendwa alikufa kutokana na nimonia. Nilikuwa na miaka 28, na mapigo hayo yaliniacha mwenye huzuni na mwenye msononeko. Hata hivyo, uhakika katika Yehova na ahadi zake zilinitegemeza. Acheni nisimulie jinsi nilivyopata kuwa na uhakika huo.
TANGU wakati wa kuzaliwa kwangu katika Salvador, Jimbo la Bahia, Brazili, Januari 5, 1917, mama alinifundisha kuwaabudu “watakatifu” wa Kanisa la Katoliki. Hata aliwaamsha ndugu zangu nami mapema asubuhi ili tuweze kusali pamoja. Hata hivyo, wazazi wangu walihudhuria pia vipindi vya sherehe za ibada za kiuchawi za Wabrazili wenye asili ya Kiafrika. Niliheshimu itikadi hizo, lakini sikuwa na uhakika katika wale wenye kuitwa isivyofaa watakatifu wa Ukatoliki au katika sherehe za ibada za kiuchawi za Wabrazili wenye asili ya Kiafrika. Kilichonitamausha hasa ni ule ubaguzi wa rangi ulioonyeshwa ndani ya dini hizo.
Baada ya muda kaka zangu wawili waliondoka nyumbani ili kutafuta kazi. Baadaye baba yangu aliiacha familia. Kwa hiyo nikiwa na umri wa miaka tisa, nililazimika kutafuta kazi ili kumsaidia mama na dada yangu mchanga. Miaka ipatayo 16 baadaye, mazungumzo pamoja na mfanyakazi mwenzangu kiwandani yalithibitika kuwa yenye kuleta badiliko la maana katika maisha yangu.
Kupata Uhakika Katika Yehova
Nilikutana na Fernando Teles katika mwaka wa 1942. Mara nyingi alisema kwamba ilikuwa makosa kuabudu “watakatifu.” (1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21) Mwanzoni sikumkazia uangalifu wowote. Lakini weupe wake wa moyo na upendezi wake katika watu, bila kujali rangi yao kulinivutia, na nilikuja kuvutiwa na ujuzi wake wa Biblia, hasa yale aliyosema juu ya Ufalme wa Mungu na dunia iliyo paradiso. (Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4) Alipoona upendezi wangu, alinipatia Biblia na fasihi kadhaa za Biblia.
Majuma machache baadaye, nilikubali mwaliko kwenye funzo la Biblia la kutaniko. Hicho kikundi kilikuwa kikijifunza kitabu Religion, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Nilifurahia hilo funzo, nikaanza kuhudhuria mikutano yote ya kutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Nilipendezwa hasa na kutokuwapo kwa ubaguzi wa rangi na jinsi nilivyokubaliwa mara moja. Karibu na wakati huo nilianza kutafuta uchumba kwa Lindaura. Nilipoongea naye juu ya yale niliyokuwa nikijifunza, alianza kuhudhuria mikutano pamoja nami.
Jambo lingine lililonivutia kwenye hiyo mikutano lilikuwa ule mkazo uliowekwa juu ya kazi ya kuhubiri. (Mathayo 24:14; Matendo 20:20) Kwa kutiwa moyo na mapainia, kama waitwavyo watumishi wa wakati wote, nilianza kuzungumza kivivi hivi na wengine kwenye gari la moshi niliposafiri kwenda na kurudi kazini. Nilipopata yeyote aliyependezwa, nilikuwa nikichukua anwani yake na kumtembelea ili kujaribu kusitawisha upendezi huo.
Wakati huohuo, uhakika wangu katika Yehova na katika tengenezo analotumia ulizidi kukua. Hivyo, baada ya kusikiliza hotuba ya Biblia juu ya wakfu wa Kikristo, nilibatizwa, katika Bahari-Kuu ya Atlantiki, katika Aprili 19, 1943. Siku hiyohiyo, nilishiriki kwa mara ya kwanza katika huduma ya nyumba hadi nyumba ya kawaida.
Majuma mawili baadaye, katika Mei 5, Lindaura nami tulioana. Kisha, katika Agosti 1943, akabatizwa katika kusanyiko la kwanza kufanywa na Mashahidi wa Yehova katika jiji la Salvador. Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1973 (cha Kiingereza) kilisema hivi kuhusu kusanyiko hilo: ‘Hatua ya makasisi ilifaulu kusimamisha hotuba ya watu wote Salvador, lakini si kabla ya kuwe na utangazaji mwingi mzuri.’ Uthibitisho wa mwongozo wa Yehova tulipokabili mnyanyaso mkali ulitia nguvu uhakika wangu katika yeye.
Kama nilivyosimulia mwanzoni, miaka miwili tu baada ya ubatizo wa Lindaura’—na miezi mitatu baada ya kifo cha mwana wetu—mke wangu mpendwa alikufa. Alikuwa na miaka 22 tu. Lakini uhakika niliokuwa nao katika Yehova ulinitegemeza katika miezi hiyo migumu.
Kuimarishwa na Utendaji wa Kiroho
Katika mwaka wa 1946, mwaka mmoja baada ya kupoteza mke na mwana wangu, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa funzo la Biblia katika lile kutaniko moja lililokuwako Salvador wakati huo. Mwaka huohuo Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilianza katika makutaniko Brazili, nami nikawa kiongozi wa shule wa kwanza katika jimbo la Bahia. Kisha katika Oktoba 1946, Kusanyiko la Kitheokrasi “Mataifa Yenye Nderemo” lilifanywa katika jiji la São Paulo. Mwajiri wangu wa miaka kumi alisema kwamba alinihitaji naye akanisonga nisiende. Hata hivyo, baada ya kumweleza jinsi kuhudhuria kusanyiko hilo kungekuwa na maana kubwa kwangu, alinipatia zawadi kubwa na kunitakia mema safarini.
Vipindi vya kusanyiko katika Municipal Theater ya São Paulo viliongozwa katika Kireno—lugha ya Brazili—na pia Kihungaria, Kiingereza, Kijerumani, Kipolandi na Kirusi. Kwenye kusanyiko hilo gazeti Amkeni! lilitolewa katika Kireno. Nilichochewa sana na hilo kusanyiko—watu wapatao 1,700 walihudhuria hotuba ya watu wote—hivi kwamba nilijaza ombi la kuanza upainia katika Novemba 1, 1946.
Wakati huo tulitumia sana kinanda cha gramafoni katika kazi yetu ya upainia. Ile hotuba “Ulinzi” ilikuwa moja tuliyowachezea wenye nyumba mara nyingi. Baada ya kuicheza hiyo hotuba, tulikuwa tukisema hivi: “Ili kujilinda dhidi ya adui asiyeonekana, twahitaji kushikamana na rafiki asiyeonekana pia. Yehova ndiye rafiki yetu mkuu na ni mwenye uwezo mwingi zaidi ya adui yetu, Shetani. Hivyo twapaswa kushikamana karibu na Yehova ili kujilinda dhidi ya Shetani.” Kisha tulitoa kijitabu Protection, kilichoandaa habari zaidi.
Nilikuwa nimepainia kwa muda uliopungua mwaka mmoja nilipopata mwaliko wa kutumikia nikiwa painia wa pekee pamoja na Kutaniko la Carioca katika Rio de Janeiro. Nyakati nyingine tulikabili upinzani mkali huko. Mwenzangu, Ivan Brenner, wakati mmoja alishambuliwa kihalisi na mwenye nyumba. Majirani waliita polisi, nasi sote tukapelekwa kwenye kituo cha polisi.
Wakati wa kuhojiwa, yule mwenye nyumba mwenye ghadhabu alitushtaki kuwa wenye kuvuruga amani. Mkuu wa polisi alimwamrisha anyamaze. Kisha huyo mkuu wa polisi akatugeukia na kwa sauti ya upole akasema tulikuwa huru kwenda. Alimzuia mshtaki wetu, akamshtaki kuwa mpiganaji. Hali kama hizo zilitegemeza uhakika wangu katika Yehova.
Utumishi wa Wakati Wote Uliopanuka
Katika Julai 1, 1949, nilisisimuka kualikwa kutumikia Betheli, kama vile ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova katika nchi fulani-fulani ziitwavyo. Siku hizo Betheli katika Brazili ilikuwa kwenye 330 Licínio Cardoso Street katika Rio de Janeiro. Wakati huo, kulikuwa na watu 17 tu katika familia yote ya Betheli. Kwa muda fulani nilihudhuria Kutaniko la Engenho de Dentro la karibu na hapo, lakini baadaye nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi-msimamizi katika kutaniko pekee katika Belford Roxo, jiji lililoko kilometa chache kutoka Rio de Janeiro.
Miisho-juma ilikuwa na kazi nyingi sana. Jumamosi nilisafiri kwenda Belford Roxo kwa gari la moshi, nilishiriki katika huduma ya shambani alasiri, kisha nikaenda kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi jioni. Nilikaa pamoja na akina ndugu usiku kucha na kushiriki huduma ya shambani asubuhi iliyofuata. Alasiri hiyo ya Jumapili nilihudhuria hotuba ya Biblia ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi na kurudi Betheli karibu saa tatu na nusu usiku. Leo kuna makutaniko 18 Belford Roxo.
Katika mwaka wa 1954, baada ya miaka mitatu na nusu ya ratiba hiyo, nilipewa mgawo wa kurudi Rio de Janeiro kuwa mwangalizi-msimamizi katika Kutaniko la São Cristóvão. Kwa miaka kumi iliyofuata, nilitumikia pamoja na kutaniko hilo.
Migawo Yangu ya Betheli
Mgawo wangu wa kwanza katika Betheli ulikuwa kujenga mahali pa kuwekea gari pekee la Sosaiti, gari kubwa la mizigo la aina ya Dodge 1949 lililobandikwa jina Chokoleti kwa sababu ya rangi yalo ya kikahawia. Mahali hapo pa kuwekea gari palipomalizika, nilipewa mgawo wa kufanya kazi jikoni, nilimofanya kazi kwa miaka mitatu. Kisha nikahamishwa kwenda katika Idara ya Matbaa ya Kazi ambamo nimekuwa sasa kwa miaka zaidi ya 40.
Vingi vya vifaa vya kupigia chapa tulivyokuwa navyo vilikuwa vimekwisha kutumika. Kwa kielelezo, kwa miaka mingi tulikuwa na matbaa tambarare ya zamani tuliyoita kwa shauku Sara, kama mke wa Abrahamu. Ilikuwa imetumiwa kwa miaka mingi katika kiwanda cha makao makuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York. Kisha katika miaka ya 1950, ikapelekwa kwa meli Brazili. Hapa, kama mke wa Abrahamu, katika miaka yayo ya uzeeni ilizaa matunda—ya namna ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
Sijapata kamwe kuacha kushangazwa na ongezeko la idadi ya vichapo vitolewavyo na kiwanda cha uchapaji cha Brazili. Katika mwaka mzima wa 1953, tulichapa magazeti 324,400, lakini sasa utokezaji ni zaidi ya milioni tatu kwa mwezi!
Majengo Yetu ya Betheli
Limekuwa jambo la kusisimua katika miaka ambayo imepita kuona upanuzi wa majengo yetu ya Betheli Brazili. Katika mwaka wa 1952 tulijenga kiwanda chenye orofa mbili nyuma ya makao yetu ya Betheli katika Rio de Janeiro. Kisha katika 1968, Betheli ilihamishwa hadi jengo jipya katika jiji la São Paulo. Tulipohamia huko, kila kitu kilionekana kikubwa na chenye nafasi kwa familia yetu ya Betheli yenye washiriki 42. Kwa kweli tulifikiria kwamba jengo hilo lingetosha kwa ukuzi wetu wote wa wakati ujao. Hata hivyo, katika mwaka wa 1971 maongezeo mawili yenye orofa tano yalijengwa, na kiwanda kilichokuwa karibu kikanunuliwa, kikajengwa upya, na kuunganishwa na majengo hayo. Lakini baada ya miaka michache, ongezeko lenye kuendelea la wapiga-mbiu wa Ufalme—tulipita alama ya 100,000 katika mwaka wa 1975—lilihitaji nafasi zaidi.
Kwa hivyo, majengo mapya yalijengwa karibu kilometa 140 kutoka São Paulo karibu na mji mdogo wa Cesário Lange. Katika mwaka wa 1980 familia yetu ya Betheli yenye washiriki 170 ilihamishwa kwenda kwenye majengo hayo mapya. Tangu wakati huo kazi ya Ufalme imekua kwa njia ya kutazamisha. Sasa tuko na watu zaidi ya 410,000 wanaoshiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Brazili! Kushughulikia mahitaji ya kiroho ya wapiga-mbiu hawa wote wa Ufalme, tumelazimika kuendelea kujenga viwanda vipya vya kuchapia fasihi za Biblia na makao mapya ili kuwapa malazi wajitoleaji wa Betheli. Sasa tuna washiriki wapatao 1,100 wa familia ya Betheli!
Mapendeleo Yenye Kuhazini
Nauona utumishi wa Betheli kuwa pendeleo lenye thamani. Hivyo, ijapokuwa katika miaka ya mapema nilifikiria kuoa tena, nilichagua kukazia fikira kabisa mapendeleo yangu katika Betheli na kazi ya kuhubiri. Hapa nimekuwa na furaha ya kutumikia pamoja na vijana wasiohesabika katika matbaa na kuwazoeza katika migawo yao. Nimejaribu kushughulika nao kana kwamba wao ni wana wangu. Bidii yao na hali yao ya kutokuwa na ubinafsi zimekuwa chanzo cha kitia-moyo kikubwa kwangu.
Pendeleo lingine limekuwa kufurahia ushirika wa wanachumba wazuri kwa miaka ambayo imepita. Ni kweli, nyakati nyingine tofauti za nyutu zimetokeza ugumu. Hata hivyo nilijifunza kutokutarajia ukamilifu kutoka kwa wengine. Nimejitahidi kuepuka kufanya mambo madogo kuwa makubwa au kujihisi kuwa wa maana sana. Huko kutojihisi kuwa mwenye umaana sana kumenisaidia kuvumilia makosa ya wengine.
Pendeleo lingine nililofurahia lilikuwa lile la kuweza kuhudhuria mikusanyiko mikubwa ya kimataifa Marekani. Mojawapo ya hiyo lilikuwa Kusanyiko la “Habari Njema Idumuyo Milele” lililofanywa Yankee Stadium, New York, katika mwaka wa 1963, na lile lingine lilikuwa “Amani Duniani” Kusanyiko la Kimataifa lililofanywa mahali hapohapo katika mwaka wa 1969. Nikiwa huko, nilikuwa na shangwe ya kutembelea makao makuu ya ulimwengu yaliyokuwa karibu na hapo ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York!
Lilikuwa pendeleo langu pia kushiriki kwa miaka kumi—kwa kupokezana zamu na wengine—kusimamia ibada ya asubuhi ya familia ya Betheli. Hata hivyo, pendeleo lililo tukufu zaidi, ambalo limeniletea shangwe kuu na kitia-moyo, ni lile la kupelekea wale wenye mioyo ya haki ujumbe wa Ufalme, sawa na vile Bwana-Mkubwa wetu, Yesu Kristo, alivyofanya.
Katika miaka ya majuzi nimekabili ugumu wa kuishi na maradhi ya Parkinson. Utunzi wenye upendo wa ndugu na dada katika mahali pa kutunzia wagonjwa pa Betheli umekuwa sikuzote chanzo cha msaada na faraja kwangu. Nikiwa na uhakika kamili, nasali kwamba Yehova aweze kunipa nguvu za kuendelea kufanya vizuri niwezavyo kwa ajili ya ibada yake ya kweli.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nikiwa na mke wangu, aliyekufa 1945
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ofisi ya tawi ya Brazili ambako naishi sasa