Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 10/1 kur. 24-28
  • Kumtumikia Yehova Tukiwa Familia Iliyoungana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Yehova Tukiwa Familia Iliyoungana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Kweli ya Biblia
  • Mwenye Furaha Katika Utumishi wa Wakati Wote
  • Kufurahia Mabadiliko Maishani Mwangu
  • Machaguo ya Watoto Wetu
  • Njia ya Mafanikio
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Watu Wote Wanaalikwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kutegemezwa na Uhakika Wangu Katika Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 10/1 kur. 24-28

Kumtumikia Yehova Tukiwa Familia Iliyoungana

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ANTONIO SANTOLERI

Baba yangu alikuwa mwenye miaka 17 alipoondoka Italia mwaka wa 1919. Alihamia Brazili akitafuta maisha bora. Hatimaye, akaja kuwa na duka la kinyozi katika mji mdogo sehemu za ndani za jimbo la São Paulo.

SIKU moja mwaka wa 1938, nilipokuwa mwenye umri wa miaka saba, baba alipata tafsiri ya Biblia ya Brasileira kutoka kwa mtu aliyetembelea duka lake. Miaka miwili baadaye mama akawa mgonjwa mahututi akaendelea akiwa mwele hadi kifo chake. Baba akawa mgonjwa pia, kwa hiyo sisi sote—mama, baba, dada yangu Ana, nami—tukaenda kuishi pamoja na watu wa ukoo katika jiji la São Paulo.

Wakati wa kuelimishwa kwangu katika São Paulo, nilikuwa msomaji mwenye bidii, hasa wa maandishi ya kihistoria. Nilivutiwa kwamba mara kwa mara Biblia ilitajwa ndani yayo. Kitabu cha hadithi zenye kubuniwa, nilichokuwa nimeazima kutoka maktaba ya umma ya São Paulo, kilitaja Mahubiri ya Mlimani mara kadhaa. Ndipo nilipoamua kupata Biblia ili nijisomee mahubiri hayo. Niliitafuta Biblia ambayo baba alikuwa amejipatia miaka kadhaa iliyopita na hatimaye nikaipata ikiwa chini katika sanduku kubwa, ilikokuwa imekaa kwa miaka saba.

Familia yetu ilikuwa ya Kikatoliki, kwa hiyo sikuwa nimetiwa moyo kamwe kuisoma Biblia. Sasa, peke yangu, nikajifunza kutafuta sura na mistari. Nilisoma kwa furaha sana si yale Mahubiri ya Mlimani pekee bali pia kitabu chote cha Mathayo na pia vitabu vingine vya Biblia. Jambo lililonivutia zaidi lilikuwa ile kweli iliyoonyeshwa na mafundisho na miujiza ya Yesu.

Nikitambua jinsi dini ya Katoliki ilivyokuwa tofauti sana na yale niliyokuwa nikisoma katika Biblia, nilianza kuhudhuria Kanisa la Presbiteri, na Ana akajiunga nami. Hata hivyo, bado nilihisi hali ya utupu moyoni mwangu. Kwa miaka kadhaa nilikuwa nimemtafuta Mungu kwa bidii. (Matendo 17:27) Usiku mmoja mwangavu, nilipokuwa katika hali ya kufikiria sana, nilijiuliza, ‘Kwa nini niko hapa? Kusudi la uhai ni nini?’ Nilitafuta mahali pa upweke uwanjani, nikapiga magoti, na kusali, ‘Bwana Mungu! Wewe ni nani? Naweza kupataje kukujua?’ Jibu likaja upesi baadaye.

Kujifunza Kweli ya Biblia

Siku moja mwaka wa 1949, mwanamke kijana alimfikia baba alipokuwa akitoka katika gari la reli la barabarani. Alimtolea magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baba alifanya uandikishaji wa Mnara wa Mlinzi akamwomba mwanamke huyo atutembelee nyumbani, akimweleza kwamba alikuwa na watoto wawili waliohudhuria Kanisa la Presbiteri. Wakati wa ziara ya mwanamke huyo, alimwachia Ana kitabu Children na kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Baadaye nilijiunga na funzo hilo.

Katika Novemba 1950 tulihudhuria mkusanyiko wetu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova. Huko kitabu “Let God Be True” kilitolewa, nasi tukaendelea na funzo letu la Biblia tukitumia kitabu hicho kikiwa mwongozo wetu. Upesi baadaye tulitambua kwamba tulikuwa tumeipata kweli, na katika Aprili 1951 tukabatizwa kwa ufananisho wa wakfu wetu kwa Yehova. Baba alijiweka wakfu miaka kadhaa baadaye na alikufa akiwa mwaminifu kwa Mungu katika mwaka wa 1982.

Mwenye Furaha Katika Utumishi wa Wakati Wote

Katika Januari 1954, nilipokuwa mwenye umri wa miaka 22 tu, nilikubaliwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, iitwayo Betheli. Nilipowasili huko, nilishangaa kupata kwamba mwanamume mmoja aliyekuwa mkubwa wangu kwa miaka miwili tu, Richard Mucha, alikuwa ndiye mwangalizi wa tawi. Mwaka wa 1955, uhitaji ulipotokea wa watumishi wa mzunguko, kama vile waangalizi wasafirio walivyokuwa wakiitwa wakati huo, nilikuwa miongoni mwa wanaume watano walioalikwa kushiriki katika utumishi huo.

Mgawo wangu ulikuwa jimbo la Rio Grande do Sul. Kulikuwa na makutaniko 8 tu ya Mashahidi wa Yehova nilipoanza, lakini kabla ya miezi 18 kuisha makutaniko 2 mapya na vikundi 20 vya mbali vilianzishwa. Katika eneo hilo leo, kuna mizunguko 15 ya Mashahidi wa Yehova, kila mmoja ukiwa na makutaniko 20 hivi! Mwishoni mwa mwaka 1956, niliarifiwa kwamba mzunguko wangu ulikuwa umegawanywa kuwa minne midogo ambayo ingetumikiwa na watumishi wanne wa mzunguko. Wakati ule nilielekezwa kurudi Betheli ili kupewa mgawo mpya.

Kwa mshangao na furaha yangu, nilipewa mgawo kwenda kaskazini mwa Brazili nikiwa mtumishi wa wilaya, mhudumu asafiriye anayetumikia mizunguko kadhaa. Wakati huo Brazili ilikuwa na wahudumu 12,000 wa Mashahidi wa Yehova, na kulikuwa na wilaya mbili nchini. Richard Wuttke alitumikia kusini, nami nilikuwa na wilaya ya kaskazini. Huko Betheli tulizoezwa kutumia projekta ya kuonyesha filamu zilizotokezwa na Mashahidi wa Yehova, The New World Society in Action na The Happiness of the New World Society.

Siku hizo kusafiri kulikuwa tofauti sana. Hakuna Shahidi aliyekuwa na gari, kwa hiyo tulisafiri kwa mtumbwi, mashua ya kuendeshwa kwa makasia, gari la ng’ombe-dume, farasi, gari la kuburutwa, lori, na wakati mmoja kwa ndege. Ilisisimua kuruka kwa ndege juu ya msitu wa Amazon ili kutua katika Santarém, jiji lililoko kwenye nusu ya njia kati ya Belém kwenye mwanzo wa mto Amazon na Manaus, jiji kuu la Jimbo la Amazonas. Wakati huo watumishi wa wilaya walikuwa na makusanyiko machache ya mizunguko ya kutumikia, kwa sababu hiyo nilitumia wakati wangu mwingi nikionyesha filamu za Sosaiti. Katika majiji makubwa zaidi, mamia ya watu yalihudhuria.

Jambo lililonivutia zaidi katika kaskazini mwa Brazili lilikuwa ule mkoa wa Amazon. Nilipokuwa nikitumikia huko katika Aprili 1957, Mto Amazon na vijito vyao vilifurika kingo zao. Nilikuwa na pendeleo la kuonyesha mojapo filamu hizo msituni, kwa kunyoosha kati ya miti miwili, kiwambo cha kufanyizwa papo hapo. Nguvu za kuiendesha projekta zilitoka kwenye mashua yenye mota iliyotiwa nanga katika mto ulio karibu. Ilikuwa filamu ya kwanza ambayo walio wengi kati ya wasikilizaji walipata kuona wakati wowote ule.

Upesi baadaye nilirudi kwenye utumishi wa Betheli, na mwaka uliofuata, wa 1958, nilikuwa na pendeleo la kuhudhuria ule mkusanyiko maarufu katika historia ulioitwa “Mapenzi ya Kimungu” Kusanyiko la Kimataifa la Mashahidi wa Yehova, katika New York City. Wajumbe kutoka nchi 123 walikuwa miongoni mwa wale 253,922 waliojaza Yankee Stadium na Polo Grounds karibu na hapo, siku ya mwisho ya mkusanyiko huo wa siku nane.

Kufurahia Mabadiliko Maishani Mwangu

Punde baada ya kurudi Betheli, nilifahamiana na Clara Berndt, tukafunga ndoa Machi 1959. Tulipewa mgawo kufanya kazi ya mzunguko katika jimbo la Bahia, tulimotumikia kwa karibu mwaka mmoja. Clara nami tungali twakumbuka kwa shangwe ule unyenyekevu, ukaribishaji-wageni, bidii, na upendo wa ndugu huko; walikuwa maskini kimwili lakini matajiri katika matunda ya Ufalme. Kisha tukahamishwa hadi Jimbo la São Paulo. Hapo ndipo, mke wangu alipata kuwa mja-mzito mwaka wa 1960, tukalazimika kuacha huduma ya wakati wote.

Tuliamua kuhamia mahali fulani katika jimbo la Santa Catarina, ambako mke wangu alizaliwa. Mwana wetu, Gerson, alikuwa wa kwanza kati ya watoto wetu watano. Alifuatwa na Gilson mwaka wa 1962, Talita mwaka wa 1965, Tárcio mwaka wa 1969, na Janice mwaka wa 1974. Kwa sababu ya Yehova na lile shauri jema analoandaa, tuliweza kukabiliana na ugumu wa kuwalea katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4, NW.

Twamwona kila mmoja wa watoto wetu kuwa mwenye thamani. Mtunga-zaburi alieleza hisia zetu vizuri sana: “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA.” (Zaburi 127:3) Yajapokuwa matatizo, tumewatunza watoto wetu kama vile tungetunza “urithi [wowote] wa BWANA,” tukikumbuka maagizo yanayopatikana katika Neno lake. Thawabu zimekuwa nyingi. Tulipata shangwe isiyoelezeka wakati wote watano kwa mfululizo, wakiwa mmoja-mmoja, na kwa hiari yao wenyewe walipoonyesha tamaa yao ya kubatizwa kwa ufananisho wa wakfu wao kwa Yehova.—Mhubiri 12:1.

Machaguo ya Watoto Wetu

Tulishangilia sana wakati Gerson, upesi baada ya kumaliza mtaala wa kompyuta wa mchakato wa data, aliposema alitaka kutumikia Betheli, hivyo akichagua huduma ya wakati wote badala ya kazi-maisha yenye malipo. Hata hivyo maisha ya Betheli hayakuwa rahisi mwanzoni kwa Gerson. Baada ya kumtembelea alipokuwa amekuwa Betheli kwa miezi minne pekee, niliathiriwa sana na huzuni iliyoonekana usoni pake tulipokuwa tukiondoka. Katika kioo cha kuangalia nyuma cha gari letu, nilimwona akituangalia mpaka tulipopita mpindo wa kwanza barabarani. Macho yangu yalijaa machozi sana hivi kwamba nililazimika kutua kando ya barabara kabla ya kuendelea na safari yetu ya kilometa 700 kurudi nyumbani.

Gerson alikuja kufurahia sana Betheli. Baada ya kuwa hapo karibu miaka sita, alimwoa Heidi Besser, na walitumikia Betheli pamoja kwa miaka miwili. Heidi akawa mja-mzito, wakalazimika kuondoka. Binti yao Cintia, mwenye umri wa miaka sita sasa, huandamana nao katika utendaji wao mbalimbali wa Ufalme.

Muda mfupi baada ya kumtembelea Gerson kwa mara ya kwanza Betheli, Gilson, aliyekuwa ametoka tu kumaliza mwaka wake wa kwanza katika usimamizi wa biashara, alisema kwamba yeye pia alitaka kutumikia hapo. Mipango yake ilikuwa kuanza upya mtaala wake wa biashara baada ya kutumikia Betheli kwa mwaka mmoja. Lakini mipango yake ilibadilika, naye akaendelea katika utumishi wa Betheli. Mwaka wa 1988 alimwoa Vivian Gonçalves, aliyekuwa painia, kama vile wahudumu wa wakati wote wanavyoitwa. Tangu wakati huo, wamekuwa wakitumikia Betheli pamoja.

Shangwe zetu ziliendelea wakati mtoto wetu wa tatu, Talita, alipochagua kuingia utumishi wa painia mwaka wa 1986 baada ya kufanya mtaala wa urasimu. Miaka mitatu baadaye yeye pia alialikwa Betheli. Katika 1991 aliolewa na José Cozzi, aliyekuwa ametumikia Betheli kwa miaka kumi. Wanaendelea huko wakiwa mume na mke.

Mke wangu nami tulifurahia tena wakati Tárcio, anayefuata, aliporudia fungu lilelile la maneno tulilokuwa tumesikia mara tatu tayari, “Baba, nataka kwenda Betheli.” Ombi lake lilikubaliwa, na mwaka wa 1991 yeye pia akaanza utumishi wa Betheli, alikokaa hadi mwaka wa 1995. Tunafurahi kwamba alitumia nguvu zake za ujana ili kuendeleza masilahi ya Ufalme wa Yehova kwa njia hiyo kwa miaka zaidi ya mitatu.

Mtoto wetu mchanga zaidi, Janice, alifanya uamuzi wake wa kumtumikia Yehova, akabatizwa akiwa na umri wa miaka 13. Wakati wa kuelimishwa kwake, alitumikia kwa mwaka mmoja akiwa painia-msaidizi. Kisha, Septemba 1, 1993, akaanza kutumikia akiwa painia wa kawaida katika kutaniko letu hapa katika jiji la Gaspar.

Njia ya Mafanikio

Ni nini kilicho siri ya kudumisha familia ikiwa yenye muungano katika ibada ya Yehova? Siamini kwamba kuna kanuni fulani za pekee ziwezazo kutatua kila tatizo. Yehova ameandaa shauri katika Neno lake la kufuatwa na wazazi Wakristo, kwa hiyo sifa zote zapaswa zimwendee kwa ajili ya matokeo mazuri ambayo tumefurahia. Tumejaribu tu kufuata mielekezo yake. (Mithali 22:6) Watoto wetu wote walirithi hisiamoyo za Walatini kutoka kwangu na mtazamo wa Kijerumani wa kufikiria mambo kutoka kwa mama yao. Lakini jambo la maana zaidi ambalo wamepokea kwetu lilikuwa urithi wa kiroho.

Maisha yetu ya nyumbani yalikazia masilahi ya Ufalme. Kutanguliza masilahi hayo hakukuwa jambo rahisi. Mathalani, sikuzote ilikuwa vigumu kwetu kudumisha funzo la Biblia la familia la kawaida, hata hivyo hatukuacha kamwe. Tangu siku zao za kwanza za uhai, kila mtoto alipelekwa kwenye mikutano ya Kikristo na pia kwenye makusanyiko na mikusanyiko. Ni ugonjwa pekee au hali nyingine za dharura zilizotuzuia tusihudhurie. Kwa kuongezea, kwenye umri mchanga, watoto waliandamana nasi katika huduma ya Kikristo.

Walipokuwa na umri wa karibu miaka kumi, watoto walianza kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Tuliwasaidia kutayarisha hotuba zao za kwanza, tukiwatia moyo watumie muhtasari badala ya hati. Baadaye, kila mmoja alitayarisha hotuba yake mwenyewe. Pia, walipokuwa kati ya miaka 10 na 12, kila mmoja wao alianza kushiriki kwa ukawaida katika huduma. Hiyo ilikuwa ndiyo njia pekee ya maisha waliyojua.

Mke wangu, Clara, alikuwa na fungu la maana katika kuwalea watoto wetu. Kila usiku, walipokuwa wachanga sana—wakati mtoto afyonzapo mambo yote afundishwayo kama sifongo—Clara aliwasomea hadithi ya Biblia na alisali na kila mmoja wao. Alitumia kwa faida nzuri vitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana, Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.a Ilipopatikana, tulitumia pia misaada ya kusikilizwa na ya kuonwa iliyoandaliwa na Mashahidi wa Yehova.

Mambo ambayo tumeona tukiwa wazazi Wakristo huthibitisha kwamba watoto wanahitaji uangalifu wa kila siku. Upendo mwingi, upendezi wa kibinafsi, na wakati mwingi ni miongoni mwa mahitaji ya msingi ya wachanga. Hatukuliona jambo la kutosheleza mahitaji hayo kwa uwezo wetu bora zaidi kuwa tu daraka letu la kiuzazi bali pia tulivuna furaha kubwa kwa kufanya hivyo.

Kwa kweli, inaridhisha kwa wazazi kuona utimizo wa maneno haya kwenye Zaburi 127:3-5: “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA, uzao wa tumbo ni thawabu. Kama mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani. Heri mtu yule aliyelijaza podo lake hivyo.” Kumtumikia Yehova tukiwa familia yenye muungano kwa kweli kumetufanya tushangilie!

[Maelezo ya Chini]

a Vyote vimetangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Antonio Santoleri pamoja na familia yake ya karibu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki