Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 6/01 kur. 3-5
  • Je, Waweza Kujitolea?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Waweza Kujitolea?
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kutazama “Nyumba ya Mungu” kwa Uthamini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kazi Njema Ambazo Haziwezi Kusahauliwa
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
  • Watu Wote Wanaalikwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2001
km 6/01 kur. 3-5

Je, Waweza Kujitolea?

1 Tukio lisilo la kawaida latokea mwaka wa 778 K.W.K. Katika njozi, nabii Isaya anamwona “Bwana [“Yehova,” NW], ameketi katika kiti cha enzi, kilicho juu sana na kuinuliwa sana.” Kisha Isaya asikia maserafi wakipaaza sauti kuhusu utukufu wa Yehova, wakisema: “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, ni BWANA [“Yehova,” NW] wa majeshi.” Lilikuwa jambo lenye kutia kicho kama nini! Katika kikao hicho, Yehova atokeza mwito huu: “Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu?” Hakuna maelezo yanayotolewa kuonyesha ni mgao wa aina gani wala faida gani atakayopata mwenye kujitolea. Ingawa hivyo, bila kusitasita, Isaya aitikia hivi: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isa. 6:1, 3, 8.

2 Watu wa Yehova huwa na roho hiyo ya kuwa tayari kufanya yoyote ambayo anawaamuru. (Zab. 110:3) Na sasa kuna mwito wa pekee kwa wale wanaoweza kujitolea. Je, uko tayari kuitikia kwa roho kama ile ya Isaya?

3 Bado kuna uhitaji mkubwa wa akina ndugu wa kutumikia Betheli. Lazima wawe na tamaa kubwa ya kutanguliza masilahi ya Ufalme na kuwa tayari kufanya chochote wanachotakikana kufanya ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri. (Mt. 6:33) Kutumikia kama mshiriki wa familia ya Betheli humpa mtu fursa isiyo na kifani ya kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Jinsi gani?

4 Kazi Inayofanywa Betheli: Fikiria yote yanayotimizwa kwa kawaida katika ofisi za Betheli zilizo katika nchi mbalimbali za Afrika Mashariki. Ndugu na dada wa familia ya Betheli katika sehemu hizo wana pendeleo la kuhusika karibu-karibu katika kuitegemeza jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza lake Linaloongoza katika kugawanya Biblia na vichapo vya Biblia vya kutumiwa shambani na katika funzo la kibinafsi. (Mt. 24:45) Kwa mfano, mwaka wa utumishi uliopita, makutaniko yaliweza kupokea vitabu, vijitabu, broshua, magazeti, na kaseti. Wanajitahidi sana kufanya utafiti na kuteua “maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli” ya vichapo hivyo. (Mhu. 12:9, 10) Wale wanaotumikia Betheli wanafurahi kushiriki katika kazi ya kusaidia wahubiri wapate vichapo vya kutumia shambani na kwa ajili ya funzo lao la kibinafsi. Kuna watafsiri katika ofisi hizi ambao husaidia kutokeza vichapo katika lugha mbalimbali. Mengi yanatimizwa ili kusimamia kazi katika nchi kadhaa za Afrika Mashariki. Wajitoleaji wengine wanahitajiwa ili kushughulikia Huduma za Habari za Kihospitali, Ofisi ya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme, usafi, udumishaji, kutayarisha chakula, ununuzi, utunzaji wa afya, na kazi nyingine katika Betheli.

5 Ni kazi kubwa mno kutimiza hayo lakini ni yenye kuridhisha kiroho. Kujua kwamba nguvu zako zote zinatumiwa kutegemeza kazi ya kuhubiri na kufundisha huleta shangwe nyingi. Utumishi wa Betheli hutusaidia tujue tengenezo la Yehova kwa undani zaidi. Tunakumbushwa kwamba mtunga-zaburi aliwatia moyo Waisraeli wajue zaidi kituo cha kidunia cha utawala wa kitheokrasi katika siku zao.—Zab. 48:12, 13.

6 Matakwa ya Utumishi wa Betheli: Inafaa wale wanaoomba kutumikia Betheli wawe tayari kufanya kazi kwa bidii, si kuwa “wenye kuzipenda raha.” (2 Tim. 3:4; 1 Kor. 13:11) Washiriki wa familia ya Betheli wanapaswa kuwa wanaume na wanawake wa kiroho ambao wamesitawisha mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi na wamezoeza nguvu zao za kufikiri ili “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” (Ebr. 5:14) Ukomavu wao wa Kikristo wapaswa kuwa tayari umeonyeshwa katika sehemu zote za maisha, kutia ndani mavazi, mapambo, na uchaguzi wao wa muziki na tafrija. Washiriki wa familia ya Betheli wako tayari kutumikia popote wanapohitajiwa. Mara nyingi washiriki vijana hupewa migao inayohusu kazi ya kutumia nguvu za kimwili, kutia ndani uchapaji, kutayarisha na kutuma vichapo, udumishaji, utunzaji wa vyumba, usafi, udobi, na kupika. (Mit. 20:29) Ingawa hivyo, tofauti na kazi ya kuajiriwa, kila mgao huleta uradhi kwa sababu ni utumishi mtakatifu unaomletea Yehova utukufu.—Kol. 3:23.

7 Kwa kawaida, wale wanaoitwa Betheli huhitajiwa kukaa huko kwa angalau mwaka mmoja ili waweze kuzoezwa kuwa wafanyakazi wenye matokeo. Inatumainiwa kwamba wataweza kukaa Betheli. Upendo kwa Yehova ndio huwachochea washiriki wa familia ya Betheli kutanguliza kazi ya Ufalme badala ya mambo yao ya kibinafsi, jambo ambalo lampendeza Yehova.—Mt. 16:24.

8 Mahitaji ya Sasa: Kwa sababu ya namna ya kazi inayofanywa Betheli, uhitaji wetu mkubwa kwa sasa ni wa akina ndugu waseja. Ijapokuwa si takwa, wale wanaopewa nafasi ya kwanza ni mapainia wa kawaida, kwa kuwa tayari wako katika utumishi wa wakati wote. Wakati mwingine dada waseja na wenzi waliooana wenye umri wa miaka 19 hadi 35 ambao huenda wakawa na ustadi fulani unaohitajiwa Betheli, wanaweza kuitwa. Kwa kuongezea, akina ndugu na dada ambao wamepita umri wa miaka 35 na wana ustadi na mazoezi ya pekee ambayo yanaweza kutumika Betheli wanatiwa moyo kujaza fomu ya ombi. Kwa mfano hao wanatia ndani madaktari wa meno, madaktari wa kawaida, wajuzi wa hesabu waliopata cheti, wahandisi, wauguzi waliosajiliwa, mekanika wa magari, au mafundi wa umeme. Hata hivyo, hatuwatii moyo watu wakapate elimu ya pekee kwa kuwazia kwamba hiyo itaongeza uwezekano wao wa kuitwa Betheli. Wale ambao tayari walipokea mazoezi ya pekee labda kabla ya kuingia katika kweli, wanaweza kuandika muhtasari wa mambo hayo na kuunganisha muhtasari huo pamoja na fomu ya ombi la Betheli.

9 Ukijaza fomu ya ombi na usiitwe Betheli, usivunjike moyo. Unaweza kufikiria kujaza fomu hiyo upya kila mwaka. Ndugu wengine ambao wana ujuzi wa kipekee na ustadi ambao labda unahitajiwa Betheli wamejitolea kutumikia kwa muda. Wanaweza kujitolea kutumikia Betheli kwa muda wa juma moja, mawili, matatu, au manne au hadi miezi mitatu. Mwandishi wa kutaniko anaweza kuomba fomu ya ombi la kujitolea kwa muda kutoka kwenye ofisi.

10 Kumtumikia Yehova kwa kushirikiana na ndugu za Kristo ni pendeleo la pekee kwa wale wanaotumikia Betheli. Baraza Linaloongoza linathamini roho hiyo ya kujitolea ya wote wanaojitoa kuhudumia mahitaji ya udugu wetu wa ulimwenguni pote.—Flp. 2:20-22; 2 Tim. 4:11.

11 Vijana–Jitayarisheni Sasa Kwa Ajili ya Utumishi wa Betheli: Kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa Betheli huanza mapema kabla ya umri unaotakikana wa miaka 19. Vijana wanaweza kufanya nini ili wajitayarishe kwa ajili ya utumishi wa Betheli? Yesu alisema: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama?” (Luka 14:28) Kwa kuwa kujitayarisha na kupanga ni kwa maana ili mradi wowote wa ujenzi ufanikiwe, ni jambo la maana kama nini vijana kufikiria kwa uangalifu jinsi wanavyoweza kujenga wakati wao ujao katika utumishi wa Yehova! Msingi unaofaa lazima ujengwe mapema maishani ili wafikie miradi ya kiroho. Ukiwa kijana, unajengaje msingi wako? Ikiwa ungependa kutumika Betheli, utanufaika kwa kuchunguza mambo yafuatayo kwa uangalifu.

12 ‘Fanyia Nafasi’ Pendeleo Hili la Pekee la Utumishi: Kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 19:12, Yesu alitia moyo wanafunzi wake ‘wafanyie nafasi’ useja. Kwa nini? Si kwa sababu za kibinafsi, lakini “kwa sababu ya ufalme wa mbingu.” Paulo vilevile, alitia moyo watu wafuatie hali hiyo ya “kuhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.” (1 Kor. 7:32-35) Kwa kusikitisha, wengine hupoteza fursa ya pendeleo la kutumikia wakiwa wanaume waseja huko Betheli kwa sababu ya kufunga ndoa wakiwa na umri mdogo. Twataka kuwatia moyo akina ndugu vijana watumie nishati zao kufuatia huduma ya wakati wote kabla hawajapata majukumu ya familia. Kisha baada ya muda fulani wakiamua kuoa, watakuwa waume bora zaidi kwa sababu ya ujuzi waliopata maishani wakiwa katika huduma ya Kikristo. Baada ya kutumikia kwa miaka kadhaa Betheli, wengine wameoa na wakaweza kuendelea kutumikia huko pamoja na wenzi wao wa ndoa. Baadaye wakiwa na mapendeleo mengine, kama vile kazi ya kusafiri, au utumishi wa mishonari, kwa kweli hawajuti kamwe kwamba walitumikia Betheli.

13 Usikengeushwe na Vitu vya Kimwili: Inafaa kila kijana ajiulize hivi: ‘Je, mradi wangu baada ya kumaliza shule ni kufuatia kazi ya kimwili au ni kumtumikia Yehova wakati wote?’ Kuchukua msimamo wa kumtumikia wakati wote kwahitaji kujitoa mhanga. Lakini ndivyo ilivyo pia na kufuatia kazi ya kimwili! Hatimaye, ni mwendo upi utakaokuwa na matokeo yenye faida na yenye kudumu? Yesu alitoa jibu lililo wazi. Kulingana na Mathayo 6:19-21, alisema: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala ya hivyo, jiwekeeni akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” Tusiache mioyo yetu ituongoze kufuatia kazi-maisha za kilimwengu na kutafuta vitu vya kilimwengu badala ya kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Ili tuufurahishe moyo wa Yehova, sisi sote lazima tutambue kwamba mradi wenye thamani unaostahili kutafutwa ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. (Mit. 27:11) Kwa kumtanguliza Yehova maishani mwetu tukiwa tungali vijana, twaonyesha mahali hazina yetu ilipo na jinsi Ufalme ulivyo wa maana kwetu. Kumbuka kwamba, “baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.” (Mit. 10:22) Vijana wana fursa nzuri zaidi ya kuonyesha mahali ilipo mioyo yao kwa kumrudishia Yehova kitu chenye thamani kwa yote ambayo amewapa. Utumishi wa Betheli hutoa fursa hiyo nzuri ajabu kwa wale wanaofikia sifa zenye ustahili.

14 Wale Wanaotumikia Betheli Lazima Wawe Safi Kiadili: Mtunga-zaburi aliuliza: “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” Alijibu hivi: “Kwa kutii, akilifuata neno [la Yehova].” (Zab. 119:9) Hilo latia ndani kuepuka kufisidiwa na ulimwengu wa Shetani. Ponografia ya Internet, mwenendo usiofaa pamoja na watu wa jinsia tofauti, muziki wenye kushusha heshima, vitumbuizo visivyofaa na kunywa vileo kabla ya umri unaokubaliwa ni baadhi ya mitego anayotumia Shetani ili kuwazuia vijana wetu wasifikie miradi ya kiroho. Azimio lenye nguvu lahitajiwa ili kukinza mbinu hizo. Kama kijana, ikiwa wajipata unahusika na yoyote ya mambo haya, zungumza na wazee katika kutaniko lenu na utatue mambo hayo kabla ya kuomba kutumikia Betheli. Kuwa na dhamiri njema ni muhimu ili kumtumikia Yehova kikamili.—1 Tim. 1:5.

15 Jifunze Kupatana na Wengine: Takwa muhimu ili ufanikiwe katika utumishi wa Betheli ni kujifunza kupatana na wengine. Familia ya Betheli ina ndugu na dada kutoka malezi mbalimbali. Ijapokuwa nyutu hizi mbalimbali huongezea uzuri wa Betheli, nyakati nyingine pia zaweza kutokeza magumu. Ikiwa unafikiria kutumikia Betheli, itafaa kujiuliza hivi: ‘Je, mimi huudhika upesi wengine wasipokubaliana na maoni yangu? Je, mimi hupatana na wengine kwa urahisi?’ Ikiwa wahitaji kufanyia kazi sehemu hizo, anza sasa. Kufanya hivyo kutakusaidia ujirekebishe kwa urahisi unapoishi na kufanya kazi na washiriki wa familia ya Betheli.

16 Jitahidi kuwa mtu wa kiroho kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Sitawisha programu nzuri ya funzo la kibinafsi, ambayo itatia ndani kusoma Biblia kila siku. Uwe na bidii ya kuwahubiria wengine habari njema. Kwa kufanya mambo hayo, utakuwa unadhihirisha maendeleo yako ya kiroho. (1 Tim. 4:15) Ni matarajio mazuri ajabu kama nini yanayowangojea wale wanaofanya utumishi wa wakati wote uwe mradi wao maishani!

17 Wazazi, Funzeni Watoto Wenu: Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwatia moyo vijana wafuatie huduma ya wakati wote? Yesu alisema: “Kila mtu aliyefunzwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40) Bila shaka, mwanafunzi aliyefunzwa vilivyo ataonyesha sifa njema za mwalimu wake aliyejitoa kwa bidii. Wazazi Wakristo wanapaswa kuweka akilini kanuni hiyo wanapojitahidi kufundisha watoto wao huku “ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha [yao].” (1 Tim. 4:7) Kwa kuwa watoto huelekea kuiga mtazamo wa wazazi wao kuhusu mambo ya kiroho, basi nyinyi wazazi jiulizeni hivi: ‘Je, sisi wenyewe twathamini kazi inayofanywa Betheli ya kuendeleza masilahi ya ibada ya kweli ya Yehova? Je, twatambua kwamba Yehova anaubariki mpango wa Betheli? Je, twaamini kwamba kumtumikia Yehova ndiyo kazi bora zaidi maishani ambayo watoto wetu wanaweza kufanya?’ Uthamini wetu wa kutoka moyoni kwa ajili ya utumishi wa Betheli na kazi inayofanywa huko utatusaidia tuwatie moyo watoto wetu wawe na uthamini huohuo.

18 Elkana na Hana walithamini sana ibada ya kweli. Waliweka kielelezo kinachostahili kuigwa na wazazi Wakristo leo. Katika Israeli ya kale, ni wanaume Waisraeli tu waliotakikana ‘kuhudhuria mbele ya Bwana MUNGU’ mara tatu kwa mwaka kwenye hema ya kukutania. Hata hivyo, “mwaka kwa mwaka” Elkana alisafiri umbali wa kilometa 30, labda kwa miguu, akiwa na familia yake yote kutoa dhabihu hekaluni mwa ibada ya Yehova. (Kut. 23:17; 1 Sam. 1:3, 4, 9, 19; 2:19) Ni wazi kwamba kichwa huyo wa familia alitaka familia yake yote ihangaikie mambo ya kiroho kama yeye.

19 Hana alishiriki mapendezi ya mume wake ya ibada ya kweli. Aliona kwa uzito wajibu wake wa kutegemeza ibada ya kweli kwenye hema ya kukutania. Hana alitoa nadhiri kwamba ikiwa Yehova angembariki kwa kumpa mwana, angemtoa kwa ajili ya utumishi wa hema ya kukutania. (1 Sam. 1:11) Sheria ya Kimusa ilimpa mume haki ya kuitangua nadhiri ya mke wake iliyosemwa pasipo kufikiri. (Hes. 30:6-8) Hata hivyo, Elkana aliikubali nadhiri ya Hana, akionyesha kwamba yeye pia aliunga mkono tendo hilo la ibada ya kweli!—1 Sam. 1:22, 23.

20 Je, mwana wao Samweli alinufaishwa na uthamini na mtazamo mzuri ulioonyeshwa na wazazi wake? Ndiyo, bila shaka. Akiwa mvulana mchanga, Samweli alifanya kazi zake kwa hiari na kwa uaminifu naye alizoezwa kwa ajili ya mapendeleo mengine zaidi ya utumishi wa Mungu. Upendezi ambao Elkana na Hana walionyesha katika utumishi wa Samweli kwenye hema ya kukutania haukuisha baada ya yeye kuanza kufanya kazi huko. Waliendelea kumtembelea kwa ukawaida wakimtia moyo na kumtegemeza huku akiendelea na utumishi wa wakati wote.—1 Sam. 2:18, 19.

21 Elkana na Hana waliweka kielelezo bora kama nini kwa wazazi Wakristo leo! Watoto wetu wanaposikia maelezo yenye uthamini ya kutoka moyoni kwa ajili ya pendeleo la utumishi wa Betheli na kuona roho ya kujitolea tunayoonyesha katika kuendeleza masilahi ya Ufalme, wao pia watasitawisha moyo wa kupenda kutumikia wengine. Wazazi wengi wanafanikiwa kutia moyo watoto wao wawe na mtazamo huo wenye kupendeza. Mtoto mmoja mwenye umri wa miaka saba alisema hivi: “Nitakapokuwa mkubwa, ningetaka kutumikia Betheli, na ningependa kufanya mambo haya nikiwa huko. (1) Kupiga chapa za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, (2) kufanya kazi katika idara yenu ya uchoraji, (3) kukunja nguo baada ya kufuliwa. Yoyote ya kazi hizo. Si hoja, yoyote ile nitakayopata.” Inachangamsha moyo kama nini kuona mtazamo huo ukistawi mioyoni mwa watoto wetu!

22 Vijana, kumbukeni kwamba “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Endeleeni kufuatia miradi ya kiroho, kutia ndani pendeleo la pekee la utumishi wa Betheli. Wazazi, igeni kielelezo cha waaminifu wa kale ambao walitia moyo watoto wao wasitawishe ujitoaji-kimungu. (2 Pet. 3:11) Sisi sote, na tufanye sehemu yetu kusaidia ndugu na dada zetu vijana wamtumikie Muumba wetu Mtukufu kadiri wawezavyo, kwa kuwa ujitoaji huo “una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Tim. 4:8; Mhu. 12:1.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki