Je! Wewe Huwaheshimu Wengine Utoapo Shauri?
JINSI lilivyo jambo zuri na lenye manufaa kushauriwa kwa heshima! “Shauri lenye fadhili, lenye ufikirio, lenye kujali hutokeza mahusiano mazuri,” asema Edward. “Unapohisi kwamba mshauri akuheshimu na akustahi kwa kuonyesha kutaka kusikiliza upande wako, shauri linakuwa rahisi zaidi kukubali,” adai Warren. “Mshauri anitendeapo kwa staha, nahisi huru kumkaribia, kumwomba shauri,” asema Norman.
Haki ya Binadamu ya Asili ya Kuonyeshwa Heshima
Shauri changamfu, la kirafiki, na lenye upendo linakubaliwa kwelikweli. Kuwashauri wengine kwa njia ambayo wewe wataka kushauriwa kuna manufaa. (Mathayo 7:12) Mshauri mzuri huchukua wakati kusikiliza na kujaribu kuelewa yule anayeshauriwa—kufikiri kwake, msimamo wako, na hisia zake—badala ya kuchambua na kushutumu.—Mithali 18:13.
Washauri wa leo, kutia ndani wazee Wakristo, wahitaji kuwa macho kuwaheshimu wengine watoapo shauri. Kwa nini? Kwa sababu ya msingi kwamba mtazamo wenye kuenea katika jamii ni kushughulika na wengine kwa njia isiyoonyesha heshima. Huo ni wenye kuambukiza. Mara nyingi sana wale unaotazamia watakutendea kwa heshima ndio wale ambao hushindwa kufanya hivyo, wawe ni wenye ustadi fulani wa kazi, viongozi wa kidini, au wengine. Ili kutoa kielezi, kufutwa kazi ni jambo linalofadhaisha na lenye kuleta mkazo wa akili kwa mwajiri na kwa mwajiriwa pia. Hilo huharibu kujistahi kwa mtu, hasa ikiwa yule anayefutwa kazi haonyeshwi heshima. Wafanyapo hivyo ni lazima wasimamizi wajifunze jinsi ya kutoa “ujumbe huo mgumu waziwazi, bila kusema mengi, na kwa ustadi, na kudumisha heshima ya mtu huyo,” laripoti The Vancouver Sun. Ndiyo, wanadamu wote wastahili kutendewa kwa heshima.
Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lapiga mbiu hivi: “Wanadamu wote wamezaliwa huru na wenye usawa katika heshima na haki. Wamepewa uwezo wa kusababu na dhamiri na wapaswa kutenda kuelekea mmoja na mwenzake katika roho ya udugu.” Kwa kuwa heshima ya mwanadamu inashambuliwa, ni kwa sababu nzuri kwamba Hati ya Katiba ya Umoja wa Mataifa na dibaji ya Julisho ya Ulimwengu Wote Mzima la Haki za Kibinadamu zatambua sifa hiyo. Zahakikisha “imani katika haki za kibinadamu za msingi, katika heshima na ustahifu wa binadamu.”
Yehova Alimwumba Mwanadamu Akiwa na Heshima ya Asili
Yehova ni Mungu mwenye heshima. Neno lake lililopuliziwa lataarifu hivi kwa usahihi, “Heshima na adhama ziko mbele zake,” na, “heshima [Yake] inasimuliwa juu ya mbingu.”—1 Mambo ya Nyakati 16:27; Zaburi 8:1, NW.
Akiwa Mungu mwenye heshima na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, yeye atoa heshima kwa uumbaji wake wote, wa kimbingu na wa kidunia. Mwenye kutokeza zaidi miongoni mwa wale wenye kuheshimiwa hivyo ni Mwana wake aliyetukuzwa na anayetawala, Mfalme, Kristo Yesu. “Heshima na adhama waweka juu yake,” Daudi akaandika kiunabii.—Zaburi 21:5; Danieli 7:14.
Kwa huzuni, haki hiyo ya msingi ya kibinadamu imetumiwa vibaya sana muda wote wa historia. Malaika mmoja mwenye nguvu, ambaye kwa matendo yake alikuwa Shetani Ibilisi, alipinga haki, uadilifu, na ustahili wa enzi kuu ya Mungu. Kwa kufanya hivyo hakuonyesha staha kwa Yehova na alifedhehesha jina lake lenye heshima huku akipinga haki Yake ya kutawala. Alijipa heshima nyingi mno. Kama vile Ibilisi, wafalme wa kibinadamu wenye mamlaka, kama vile Nebukadreza wa nyakati za Biblia, wamejivunia ‘uwezo na nguvu zao.’ Wameshambulia heshima ya Yehova, wakijipa heshima isiyofaa. (Danieli 4:30) Utawala wa Shetani wenye uonevu, uliolazimishwa juu ya ulimwengu wa ainabinadamu umeshambulia na waendelea kushambulia heshima ya watu.
Je! heshima yako imepata kudhoofishwa wakati wowote? Wakati umeshauriwa, je, umefanywa uhisi kuwa na hatia, aibu, kufedheheka, au kushushiwa heshima kupita kiasi? “Sikuhisi nimeonyeshwa ufikirio, huruma, wala heshima. Nilifanywa nihisi sifai kitu,” adai André, akiongeza hivi: “Hilo liliongoza kwenye hisia za kukata tamaa na kuhangaika, hata kushuka moyo.” “Ni vigumu kukubali shauri kutoka kwa mtu ambaye wahisi hajali hali njema yako,” asema Laura.
Kwa sababu hiyo, waangalizi Wakristo wanaonywa kwa upole watendee kundi la Mungu kwa staha na heshima. (1 Petro 5:2, 3) Ikiwa hali zatokea ambazo ni lazima na yafaa kushauri wengine, waweza kujilindaje dhidi ya njia ya kufikiri na ya kutenda ya walimwengu ambao hushambulia heshima ya wengine bila kusita? Ni nini kiwezacho kukusaidia uhifadhi heshima ya Wakristo wenzako, pamoja na yako mwenyewe?—Mithali 27:6; Wagalatia 6:1.
Kanuni Zinazohifadhi Heshima
Neno la Mungu halibaki kimya kwa habari hiyo. Mshauri stadi ataweka tumaini kamili katika shauri la Neno la Mungu, badala ya kutafuta hekima ya ulimwengu. Maandishi Matakatifu yana mawaidha yenye thamani. Yanapofuatwa, hayo huheshimu mshauri na pia yule anayeagizwa. Hivyo, mwelekezo wa Paulo kwa mwangalizi Mkristo Timotheo ulikuwa: “Mzee usimkemee, bali umwonye kama baba; na vijana kama ndugu; wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote.” (1 Timotheo 5:1, 2) Ni kiasi kikubwa kama nini cha huzuni, udhia, na aibu kiwezacho kuepukwa kinachoepukwa kwa kushikamana na viwango hivyo!
Angalia kwamba ufunguo wa kutoa shauri kwa mafanikio ni staha ifaayo kwa yule mtu mwingine na haki yake ya kutendewa katika njia yenye heshima, ya kumjali. Wazee Wakristo, kutia na waangalizi wasafirio, wapaswa wajitahidi kufuata mawaidha hayo, wakijaribu kujua ni kwa nini yule anayehitaji rekebisho afikiri na kutenda kama atendavyo. Wao wapaswa watake kusikia maoni yake, na kufanya kila jitihada ili kuepuka kuaibisha, kushushia heshima, au kufedhehesha yule anayesaidiwa.
Ukiwa mzee, acha ndugu yako ajue kwamba wamjali na wataka kumsaidia na matatizo yake. Ndivyo daktari hufanya uzurupo ofisi yake ili kuchunguzwa kitiba. Wazo la kuvua mavazi katika chumba chenye ubaridi, bila uchangamfu, laweza kukufanya uaibike na kufedheheka. Wathamini kama nini daktari aonyeshaye kwamba afikiria sifa yako ya kujistahi na akuheshimu kwa kukupa wewe mavazi ya kujifunika anapokuchunguza ili kuamua ni nini kinachosababisha maradhi yako! Kwa njia iyo hiyo, mshauri Mkristo aonyeshaye staha ifaayo kwa mtu ni mwenye fadhili na mwenye uthabiti, hata hivyo humvika heshima yule anayepokea shauri. (Ufunuo 2:13, 14, 19, 20) Tofauti na hilo, shauri isiyo na huruma, yenye ubaridi, na bila hisia ni kama kuvua mavazi kitamathali kunakokufanya uhisi aibu, kufedheheka, na kunyang’anywa heshima yako.
Waangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni waangalifu hasa kutoa shauri kwa heshima. Wanaposhauri wazee-wazee, wanaonyesha upendo uleule ambao wangeonyesha wazazi wao wa kimwili. Wao ni wenye ufikirio, wenye urafiki, na wachangamfu. Ufikirio huo ni wa lazima. Unatokeza hali ambayo ni nzuri sana kwa shauri kutolewa na kupokewa ifaavyo.
Wazee, zingatieni kwamba shauri lifaalo linachangamsha, linatia moyo, linajenga, na linafaa. Waefeso 4:29 lasema hivi: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.”
Hakuna haja ya kutumia maneno, lugha, au kusababu kwa njia ya ukali. Badala ya hivyo, staha kwa yule mtu mwingine na tamaa ya kuhifadhi hisia zake za kujithamini na kujistahi hukuchochea ueleze mambo kwa njia ifaayo, ya kujenga. Tanguliza maneno yoyote kwa pongezi ya kweli, yenye weupe wa moyo kwa ajili ya sifa zake njema, badala ya kukazia maoni ambayo yamfanya ahisi kukata tamaa na kutofaa kitu. Ikiwa watumikia ukiwa mzee, tumia ‘mamlaka yako upate kujenga wala sikuangusha.’—2 Wakorintho 10:8.
Ndiyo, tokeo la shauri lolote kutoka kwa waangalizi Wakristo lapasa kuwa kutoa kitia-moyo kinachohitajiwa, kutoa jambo lenye kupendeleka. Halipasi kuvunja moyo au “kuwaogofya.” (2 Wakorintho 10:9) Hata mtu ambaye amefanya kosa zito ahitaji kupewa kadiri fulani ya sifa ya kujistahi na heshima. Ni lazima shauri lisawazishwe na maneno ya kukaripia yenye fadhili, na bado yenye uthabiti ili kumsukuma afikie hatua ya toba.—Zaburi 44:15; 1 Wakorintho 15:34.
Ni jambo la maana kwamba, Sheria ya Mungu kwa Israeli ilitia ndani kanuni izo hizo. Iliruhusu shauri na hata nidhamu ya kimwili, wakati uleule ikihifadhi haki ya mtu ya kupata kadiri fulani ya heshima ya kibinafsi. Kupiga kwa mapigo “kwa kadiri ya uovu wake” kuliruhusiwa, lakini hilo halikupaswa kupita kiasi. Mpaka uliwekewa idadi ya mapigo yaliyotolewa ili mtenda mabaya ‘asionekane amedharauliwa.’—Kumbukumbu la Torati 25:2, 3.
Ufikirio kwa ajili ya hisia za watenda mabaya wenye toba ulikuwa sifa moja ya Yesu pia. Isaya alitabiri hivi juu yake: “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli.”—Isaya 42:3; Mathayo 12:17, 20; Luka 7:37, 38, 44-50.
Maneno ya Yesu katika Mahubiri juu ya Mlima yanakazia zaidi uhitaji wa kuwa na hisia-mwenzi: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.” (Mathayo 7:12) Kanuni hiyo ni ya kimsingi katika kuendeleza mahusiano mazuri hivi kwamba kwa ukawaida huitwa Kanuni ya Kidhahabu. Ukiwa mzee Mkristo, hiyo yaweza kukusaidiaje kuwatendea wengine kwa fadhili na heshima utoapo shauri?
Kumbuka kwamba wewe pia hufanya makosa. Kama vile Yakobo alivyoonelea, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.” (Yakobo 3:2) Kukumbuka hilo kutakusaidia kupunguza ukali wa maneno yako na kudhibiti hisia zako iwapo ni lazima kuongea na wengine juu ya upungufu wao mbalimbali. Tambua mambo yanayowaudhi upesi. Hilo litakusaidia uepuke kuchambua kupita kiasi, kuelekeza fikira kwenye makosa au kasoro ndogo-ndogo. Yesu alikazia hilo aliposema hivi: “Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimacho, ndicho mtakachopimiwa.”—Mathayo 7:1, 2.
Heshimu Wengine—Mpingeni Ibilisi
Mbinu za Shetani zimekusudiwa kukunyang’anya heshima, kutokeza hisia za kufedheheshwa, kuhisi kutofaa kitu, na kukata tamaa. Angalia jinsi alivyotumia wakili wa kibinadamu kuchochea hisiamoyo zisizofaa ndani ya Ayubu mwaminifu. Elifazi mwenye unafiki alidai hivi: “Yeye [Yehova] hawategemei watumishi wake; na malaika zake [watakatifu] huwahesabia upuzi; je! si zaidi sana hao wakaao katika nyumba za udongo, ambazo misingi yao i katika mchanga, hao waliosetwa mbele ya nondo!” (Ayubu 4:18, 19) Kwa hiyo kulingana na yeye, kwa Mungu, Ayubu hakuwa na thamani zaidi ya nondo. Kwa kweli, mbali na kuwa lenye kujenga, shauri la Elifazi na waandamani wake lingalimwacha Ayubu hata bila kumbukumbu la nyakati zilizokuwa bora zaidi. Kwa maoni yao uaminifu wake, mazoezi ya familia yake, uhusiano wake na Mungu, na zawadi zake za rehema za wakati uliopita hazikufaa kitu.
Leo vilevile, ni rahisi sana kwa watenda mabaya wenye toba kupatwa na hisia za jinsi hiyo, na kuna hatari ya wao ‘kumezwa katika huzuni yao ipitayo kiasi.’ Wazee, mtoapo shauri kwa watu wa jinsi hiyo, ‘thibitisheni upendo wenu’ kwao kwa kuwaruhusu wahifadhi kadiri fulani ya heshima. (2 Wakorintho 2:7, 8) “Kutendewa bila heshima hufanya kuwe vigumu kukubali shauri,” akiri William. Ni muhimu kuimarisha imani yao kwamba wao ni wenye thamani machoni pa Mungu. Wakumbushe kwamba Yehova “si dhalimu hata aisahau kazi [yao], na pendo lile [walilo]lidhihirisha kwa jina lake” katika miaka yao iliyopita ya utumishi mwaminifu.—Waebrania 6:10.
Ni mambo gani zaidi yawezayo kukusaidia uwaheshimu wengine utoapo shauri? Tambua kwamba wanadamu wote wana haki ya asili ya kuonyeshwa heshima, kwa kuwa wamefanyizwa katika mfano wa Mungu. Wao wanathaminiwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo; yale maandalizi mawili ya fidia na ufufuo yathibitisha uhakika huo. Yehova aongezea Wakristo heshima zaidi kwa ‘kuwaweka katika utumishi wake,’ akiwatumia kusihi kizazi chenye uovu kifanye amani pamoja na Mungu.—1 Timotheo 1:12.
Wazee, kumbukeni kwamba walio wengi wa ndugu zenu Wakristo huenda wakawa washiriki wa kwanza wa ile jamii mpya ya kibinadamu katika dunia iliyosafishwa. Wakiwa watu mmoja-mmoja waliothaminiwa na wenye ubora hivyo, wanastahili kuheshimiwa. Mtoapo shauri, kumbukeni jinsi Yehova na Yesu pia huwaonyesha ufikirio, na endeleeni kufanya sehemu yenu kusaidia ndugu zenu wahifadhi hisia yao ya heshima na kujithamini wakabilipo upinzani wa Shetani.—2 Petro 3:13; linganisha 1 Petro 3:7.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
Shauri Liheshimulo
(1) Toa pongezi ya kweli na yenye weupe wa moyo. (Ufunuo 2:2, 3)
(2) Uwe msikilizaji mzuri. Tambulisha tatizo na sababu ya shauri waziwazi na kwa fadhili. (2 Samweli 12:1-14; Mithali 18:13; Ufunuo 2:4)
(3) Tegemeza shauri lako juu ya Maandiko. Uwe mwenye maoni yafaayo, mwenye kusababu, na mwenye kutia moyo, na kuonyesha hisia-mwenzi. Dumisha heshima na sifa ya kujithamini ya yule anayepokea shauri. (2 Timotheo 3:16; Tito 3:2; Ufunuo 2:5, 6)
(4) Thibitishia mwenye kupokea shauri kwamba baraka hutokana na kukubali na kutumia shauri. (Waebrania 12:7, 11; Ufunuo 2:7)
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wazee Wakristo wahitaji kuwaheshimu wengine watoapo shauri