Ulimwengu Bora Zaidi—U Karibu!
“KUTAMANI sana paradiso ni mojayapo tamaa zenye nguvu zaidi zinazoonekana kufikiriwa na wanadamu daima. Huenda ikawa hiyo ni mojayapo tamaa zenye nguvu zaidi na zenye kudumu zaidi ya zote. Kadiri fulani ya kutamani paradiso inaonekana katika kila kiwango cha maisha ya kidini,” yasema The Encyclopedia of Religion.
Yaonekana tamaduni zote hushiriki tamaa ya kuishi katika ulimwengu bora zaidi, kana kwamba zaombolezea hali bora ya awali ambayo haiko tena. Hilo ladokeza uwezekano wa paradiso ya awali, lakini wapi? Mchanganuzi wa hisiamoyo huenda akasema kwamba matumainio hayo hufunua tamaa ya kupata tena ule usalama ambao mtu alifurahia akiwa katika tumbo la uzazi la mama. Lakini, elezo hilo haliwasadikishi wasomi wajifunzao historia ya dini.
“Kutamani Sana Paradiso” —Kwa Nini?
Je! kuwako kwa tamaa ya jinsi hiyo ni ili tu kufanya hali ngumu na maisha mafupi ya wanadamu yavumilike, kama vile wengine hudokeza? Au kuna elezo jingine?
Kwa nini wanadamu hutamani ulimwengu bora zaidi? Biblia hutoa elezo lililo wazi na sahili: Wanadamu wametoka katika ulimwengu bora zaidi! Paradiso ya awali ilikuwako kwelikweli. Neno la Mungu laiita “bustani” iliyokuwa sehemu hususa huko Mashariki ya Kati, iliyobarikiwa kwa “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” Mungu aliikabidhi kwa mume na mke wa kwanza. (Mwanzo 2:7-15) Hiyo ilikuwa hali bora ambamo wanadamu wangaliweza kuwa na furaha kwelikweli.
Kwa nini hali hizo za Paradiso hazikudumu? Kwa sababu ya uasi wa kwanza wa kiumbe kimoja cha roho na kisha cha wale mume na mke wa kibinadamu. (Mwanzo 2:16, 17; 3:1-6, 17-19) Hivyo, mwanadamu hakupoteza Paradiso tu bali pia ukamilifu, afya, na uhai usio na kikomo. Hali zilizoanza kuenea hazikuboresha hata kidogo maisha ya kibinadamu. Kinyume cha hilo, hali imezidi kuwa mbaya hatua kwa hatua hadi kiwango cha chini kabisa tuonacho leo.—Mhubiri 3:18-20; Warumi 5:12; 2 Timotheo 3:1-5, 13.
Kutafuta-Tafuta Paradiso —Historia ya Wazo
Kama iwezavyo kuwaziwa, “kutamani sana paradiso” kuna historia ndefu sana. Wasumeria walikumbuka wakati ambapo upatano ulikuwako katika ulimwengu wote mzima: “Hakukuwa na hofu, wala ogofyo, mwanadamu hakuwa na mshindani. . . . Ulimwengu wote mzima, watu wote pamoja, walimpa Enlili sifa kwa lugha moja,” kakumbusha shairi moja la Mesopotamia ya kale. Wengine, kama vile Wamisri wa kale, walitumaini kufika kwenye ulimwengu bora zaidi baada ya kifo chao. Waliamini kwamba nafsi isiyoweza kufa ilifika kwenye zile zilizoitwa nyanja za Aaru. Lakini angalau mwanzoni, tumaini hilo lilikuwa la wakuu pekee; maskini hawakuweza kuwa na tumaini la ulimwengu bora zaidi.
Katika eneo tofauti la kidini, Wahindu wamengojea kuja kwa enzi bora zaidi ya ulimwengu (yuga) kwa karne nyingi. Kulingana na mafundisho ya Kihindu, yuga nne hurudia-rudia katika kawaida yenye kuendelea, na kwa sasa tunaishi katika ile iliyo mbaya zaidi. Kwa kusikitisha, Yuga hii iitwayo Kali (enzi yenye giza), yenye mateso na uovu, itadumu kwa muda wa miaka 432,000, kama wengine wasemavyo. Hata hivyo, Wahindu waaminifu wangojea enzi bora, ile Yuga iitwayo Krita.
Kwa upande mwingine, Wagiriki na Waroma walitamani kufika kwenye vile Visiwa vya Ufanisi vya kingano, katika Bahari ya Atlantiki. Na waandikaji wengi, kama vile Hesiod, Virgil, na Ovid, walisema juu ya enzi bora ya awali iliyo nzuri ajabu, wakitumaini kwamba ingerudishwa siku moja. Kuelekea mwisho wa karne ya kwanza K.W.K., mtunga-mashairi Mlatini Virgil alitabiri kuja kwa aetas aurea (enzi bora) mpya na yenye kudumu kulikokuwa karibu. Katika karne zilizofuata, “maliki Waroma wasiozidi kumi na sita walidai kwamba tawala zao zilianzisha upya ile Enzi Bora,” yasema The Encyclopedia of Religion. Lakini kama vile tujuavyo vema leo, hiyo ilikuwa propaganda ya kisiasa tu.
Waselti wengi walitumainia lile walilofikiria kuwa bara jangavu kwenye kisiwa (au katika kikundi cha visiwa) ng’ambo ya bahari, ambako waliamini kwamba watu waliishi katika furaha kamilifu. Kulingana na hekaya moja, ingawa Mfalme Arthur alikuwa na majeraha ya kusababisha kifo, aliendelea kuishi baada ya kupata kile kisiwa kizuri ajabu kilichoitwa Avalon.
Katika nyakati za kale na katika Enzi za Kati, wengi walifikiri kwamba bustani yenye mambo halisi yaliyo mazuri, bustani ya Edeni, bado ilikuwako mahali fulani, “juu ya mlima usiofikika au ng’ambo ya bahari isiyovukika,” aeleza mwanahistoria Jean Delumeau. Hata ingawa yule mtunga-mashairi Mwitalia Dante aliamini katika paradiso ya kimbingu, aliwazia kwamba bado paradiso ya kidunia ilikuwako juu ya mlima wa Purgatori yake, kwenye ng’ambo ile nyingine ya jiji la Yerusalemu. Wengine waliamini kwamba hiyo ingeweza kupatikana katika Asia, katika Mesopotamia, au katika Milima ya Himalaya. Na hekaya za enzi ya kati kuhusu paradiso ya Kiedeni zilikuwa nyingi sana. Wengi waliamini kwamba karibu na hiyo paradiso, kulikuwa na ufalme mzuri ajabu uliotawalwa na Padri John aliyekuwa mchaji Mungu. Kwa sababu ya mahali pa paradiso hiyo ya kidunia, maisha katika ufalme wa Padri John yalidhaniwa kuwa marefu na yenye baraka, chanzo cha daima cha wingi na utajiri. Wengine, wakiwa na ufahamu wa zile hekaya za Kigiriki, bado walifikiri kwamba visiwa vya paradiso vingepatikana katika Atlantiki. Ramani za enzi ya kati zilionyesha kwamba watu walikuwa na hakika sana juu ya kuwako kwa bustani ya Edeni, hata zikionyesha mahali palipodhaniwa kuwa hapo.
Katika karne za 15 na 16, nahodha waliovuka Atlantiki kwa kweli walikuwa wakitafuta ulimwengu ambao wakati uleule ulikuwa mpya na wa kale. Walifikiri kwamba kwenye ng’ambo ile nyingine ya bahari, wangepata kuvumbua Visiwa vya Hindi na pia bustani ya Edeni. Kwa kielelezo, Christopher Columbus, aliitafuta bustani hiyo miongoni mwa ile milima ya mabara ya Amerika Kusini na ya Kati yenye halijoto ya kiasi na ya kitropiki. Wavumbuzi kutoka Ulaya waliowasili Brazili walikuwa na hakika kwamba ni lazima ile paradiso iliyopotea ilikuwa huko kwa sababu ya hiyo halijoto ya kiasi na wingi wa chakula na mimea. Lakini, upesi walilazimika kutambua ukweli wenye kuhuzunisha.
Utopia—Mahali Penye Hali Bora?
Badala ya kujitahidi kupata ulimwengu bora katika sehemu ya mbali sana duniani wengine wamejaribu kuupanga. Hivyo, katika 1516, mchunguzi mmoja Mwingereza wa hali za kibinadamu Thomas More alisimulia kisiwa cha Utopia, kuwa mahali pazuri ajabu, penye amani, na penye uvumilivu, tofauti sana na ulimwengu aliojua ulioshuka kiadili. Wengine pia walikuwa wamejaribu kupanga ulimwengu mbalimbali ulio bora zaidi, wenye furaha zaidi: katika karne ya sita K.W.K., kulikuwa na Plato na Jamhuri yake; katika 1602, kulikuwa na mwanadini Mwitalia Tommaso Campanella na jiji lake City of the Sun lililopangwa kwa utaratibu sana; miaka michache tu baadaye, kulikuwa na mwanafalsafa Mwingereza Francis Bacon akisimulia juu ya “ile jamii yenye furaha na yenye kusitawi” ya jiji lake la New Atlantis. Kwa muda wa karne kadhaa, wenye kufikiria mambo ya aina zote (iwe ni waamini wa dini fulani au la) wamesimulia juu ya Utopia nyingi sana. Ni wachache walioaminiwa ikiwa kuna wowote walioamini.
Hata kumekuwa wale ambao wamejaribu kufanyiza Utopia zao. Kwa kielelezo, katika 1824 tajiri Mwingereza, Robert Owen, aliamua kuhamia Indiana, U.S.A., ili kutimiza mawazo yake ya Kiutopia katika kijiji alichoita New Harmony. Akiwa amesadiki kwamba watu wangeboreka wakiwa chini ya hali zifaazo, alitumia karibu mali zake zote akijitahidi kuanzisha ule alioona kuwa ulimwengu mpya wa kiadili. Lakini matokeo yalionyesha kwamba hali mpya za kuishi hazitoshi ili kutokeza watu wapya.
Karibu mawazo yote ya kisiasa husisitiza kwamba ni lazima mwanadamu apange ulimwengu kulingana na ujuzi wake mwenyewe na hisi yake mwenyewe juu ya yale yaliyo ya kweli ili kutokeza ile paradiso inayotamaniwa sana duniani. Lakini, tofauti na hilo, majaribio ya kutimiza matumaini hayo yametokeza vita na mapinduzi, kama yale Mapinduzi ya Ufaransa katika 1789 na Mapinduzi ya Bolsheviki katika 1917. Badala ya kutokeza hali za paradiso, mara nyingi jitihada hizo zimeongoza kwenye maumivu na kuteseka zaidi.
Matumaini, mipango, Utopia, na majaribio ya kuzitimiza—yasimulia kisa kimoja cha kukatishwa tamaa baada ya kingine. Kwa sasa, wengine husema juu ya “ndoto isiyotimia” na “mwisho wa enzi ya utopia,” wakitualika tujifunze “kuishi bila utopia.” Je! kuna tumaini lolote la kuona ulimwengu bora zaidi, au huo utaendelea kuwa ndoto tu?
Wakristo na Ulimwengu Bora Zaidi
Ulimwengu mpya si ndoto hata kidogo—ni tumaini hakika! Yesu Kristo, aliye Mwanzilishi wa Ukristo, alijua kwamba ulimwengu huu wa sasa si ulimwengu bora zaidi ya mwingine wowote. Alifundisha kwamba dunia ingerithiwa na watu wenye tabia-pole na kwamba mapenzi ya Mungu yangetendeka huko. (Mathayo 5:5; 6:9, 10) Yeye na wanafunzi wake walijua kwamba ulimwengu huu unatawalwa na adui wa Mungu, Shetani Ibilisi, na kwamba hiyo ndiyo sababu kuu ya ole nyingi za wanadamu. (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:12) Wayahudi waaminifu walingojea siku ambayo mara moja kwa wakati wote Mungu angeweka dunia huru na vita, maumivu, na ugonjwa ili aijaze watu wapendao amani na haki. Kwa njia iyo hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza walingojea kwa hakika ulimwengu huu uliopo ambao mahali pao pangechukuliwa na mfumo mpya wa mambo, “mbingu mpya na dunia mpya.”—2 Petro 3:13, New World Translation; Zaburi 37:11; 46:8, 9; Isaya 25:8; 33:24; 45:18; Ufunuo 21:1.
Yesu Kristo alipokuwa akining’inia kwenye mti wa mateso, alirudia ahadi ya ulimwengu bora zaidi kwa mtenda-maovu mmoja aliyeonyesha kadiri fulani ya imani katika Yeye. “[Yesu] akamwambia: ‘Kweli mimi nakuambia wewe leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.’” (Luka 23:40-43, NW) Mtenda-maovu huyo alielewaje maneno hayo? Je! Yesu alidokeza kwamba mtenda-maovu huyo ‘angekuwa pamoja naye’ mbinguni siku iyo hiyo, kama vile yaonekana kuonyeshwa na tafsiri fulani za Biblia za Katoliki na Protestanti? La, Yesu hakumaanisha hilo, kwa kuwa baada ya ufufuo wake, Yesu alimwambia Mariamu Magdalene kwamba Yeye ‘hakuwa amepaa kwenda kwa Baba.’ (Yohana 20:11-18) Ingawa walifundishwa na Yesu kwa muda wa miaka mitatu na nusu, kabla ya Pentekoste 33 W.K. hata mitume wake hawakufikiria paradiso ya kimbingu. (Matendo 1:6-11) Mtenda-maovu huyo alielewa yale ambayo walio wengi wa Wayahudi waliokuwa wakiishi wakati huo wangalielewa: Yesu alikuwa akiahidi juu ya ulimwengu bora zaidi ambao ungekuja katika dunia-paradiso. Msomi mmoja Mjerumani alikiri hivi: “Fundisho juu ya malipo katika maisha baada ya kifo halionekani hata kidogo katika Agano la Kale.”
Jambo la kwamba kutakuwa na paradiso juu ya dunia yetu linathibitishwa na mtume Paulo katika barua yake kwa Waebrania. Alipokuwa akiwatia moyo waamini wenzake ‘wasipuuze wokovu wa ukubwa ulioanza kusemwa kupitia Yesu Kristo,’ Paulo athibitisha kwamba Yehova Mungu alimpa Yesu mamlaka juu ya “dunia ijayo inayokaliwa [Kigiriki, oi·kou·meʹne].” (Waebrania 2:3, 5, NW) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, sikuzote neno oi·kou·meʹne hurejezea dunia yetu ikiwa imekaliwa na wanadamu, si ulimwengu wa kimbingu. (Linganisha Mathayo 24:14; Luka 2:1; 21:26; Matendo 17:31.) Kwa hiyo Ufalme wa Mungu ukiwa unatawalwa na Kristo Yesu utatawala juu ya dunia inayokaliwa. Kwa kweli mahali hapo patakuwa bora pa kuishi!
Hata ingawa Ufalme wenyewe ni wa kimbingu, hata hivyo huo utaingilia mambo ya dunia. Matokeo yatakuwa nini? Maradhi, ukatili mbalimbali, umaskini, na kifo yatakuwa mambo ya zamani. Hata kufadhaika na kutoridhika kutatokomea. (Ufunuo 21:3-5) Biblia husema kwamba ‘Mungu ataufumbua mkono wake na kukishibisha kila kilicho hai matakwa yake.’ (Zaburi 145:16) Matatizo kama vile ukosefu wa kazi za kuajiriwa na uchafuzi yatakuwa na suluhisho lenye mafaa na lenye kudumu. (Isaya 65:21-23; Ufunuo 11:18) Lakini zaidi ya yote, kwa sababu ya baraka ya Mungu, kweli, haki, na amani vitashinda—sifa ambazo yaonekana kama zimetokomea!—Zaburi 85:7-13; Wagalatia 5:22, 23.
Je! hayo yote ni ndoto, Utopia? La, wakati huu tunamoishi ulio mgumu zaidi ya mwingine wowote waonyesha kwamba tumo katika “siku za mwisho” za ulimwengu huu na kwamba ulimwengu mpya u karibu. (2 Timotheo 3:1-5) Je! wewe ungependa kuishi huko? Jifunze jinsi inavyowezekana kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ulimwengu bora zaidi u karibu, ulio bora zaidi ya vile tulivyowazia. Huo si Utopia—ni jambo halisi!
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ulimwengu bora zaidi —litakuwa jambo halisi karibuni