Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 4/1 kur. 29-31
  • “Kataa Hadithi Zisizo za Kweli”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kataa Hadithi Zisizo za Kweli”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujaribu Maneno ya Kweli
  • Hadithi Juu ya Mambo Yapitayo Uwezo wa Kibinadamu
  • Kukataa Ushuhuda wa Mashetani
  • Dokezo la Kujifunza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Mpingeni Ibilisi
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 4/1 kur. 29-31

“Kataa Hadithi Zisizo za Kweli”

BIBLIA imejaa mambo yaliyoonwa na hadithi juu ya watu. Sisi hatufurahii tu kuzisoma bali pia twanufaika kutokana nazo. Mtume Paulo aliandikia kutaniko la Kikristo katika Roma hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”—Warumi 15:4.

Paulo mwenyewe alishiriki katika kusimulia mambo yaliyoonwa. Biblia husema hivi juu ya Paulo na Barnaba mwishoni mwa safari yao ya kwanza ya mishonari: “Hata walipofika [Antiokia ya Siria] wakalikutanisha kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani.” (Matendo 14:27) Bila shaka ndugu walitiwa moyo sana na mambo hayo yaliyoonwa.

Hata hivyo, si mambo yote yaliyoonwa ambayo ni yenye kujenga. Chini ya upulizio, Paulo alimwonya Timotheo hivi: “Bali kataa hadithi zisizo za kweli ambazo huhalifu kilicho kitakatifu na ambazo wanawake wazee hueleza.” (1 Timotheo 4:7, NW) Na alimwandikia Tito kwamba Wakristo waaminifu-washikamanifu hawapaswi “kutoa uangalifu kwa hekaya za Kiyahudi na amri za watu ambao hujigeuza mbali wenyewe kutoka kwenye ile kweli.”—Tito 1:14, NW.

Hizo hadithi au hekaya zisizo za kweli zilikuwa nini? Maneno yote mawili hutokana na neno la Kigiriki myʹthos (“ngano”). The International Standard Bible Encyclopaedia yasema kwamba neno hilo laeleza “hadithi (ya kidini) ambayo haihusiani hata kidogo na mambo halisi.”

Ulimwengu wa siku za Paulo ulijaa hadithi za jinsi hiyo. Kielelezo kimoja ni kile kitabu cha apokrifa cha Tobiti, ambacho labda kiliandikwa zaidi ya miaka mia mbili kabla ya wakati wa Paulo. Hadithi hiyo yasimulia juu ya Tobiti, Myahudi mchaji Mungu, anayepofushwa wakati kinyesi cha ndege kiangukapo machoni mwake. Baadaye, yeye amtuma mwana wake, Tobiasi, aende kukusanya deni fulani. Akiwa njiani, Tobiasi apata moyo, ini, na nyongo ya samaki, kwa mwelekezo wa malaika. Kisha akutana na mjane, ambaye ingawa ameolewa mara saba, angali bikira kwa sababu kila mume aliuawa na roho mwovu katika usiku wa arusi. Kwa kuchochewa na malaika huyo, Tobiasi amwoa mjane huyo na amfukuza yule shetani kwa kuchoma ule moyo na lile ini la samaki. Baadaye Tobiasi arudisha uwezo wa kuona wa babake kwa ile nyongo ya samaki.

Kwa wazi, hadithi hiyo si ya kweli. Zaidi ya hali yayo ya kuwa yenye kuwaziwa tu na uvutio wayo wa kishirikina, hiyo si sahihi. Kwa kielelezo, simulizi hilo lasema kwamba Tobiti alishuhudia uasi wa makabila ya kaskazini na pia kuhamishwa kwa Waisraeli hadi Ninawi, matukio katika historia ya Israeli yaliyotengwa na muda wa miaka 257. Lakini, hadithi hiyo yasema kwamba Tobiti alikuwa na miaka 112 wakati wa kifo chake.—Tobiti 1:4, 11; 14:1, The Jerusalem Bible.

Hekaya za jinsi hiyo ni tofauti sana na “kiolezo cha maneno yenye afya” yanayopigwa mbiu na watumishi waaminifu wa Mungu. (2 Timotheo 1:13, NW) Hayo ni matokeo ya mawazo, tofauti na mambo hakika ya kihistoria, jambo linalosimuliwa na wanawake wazee wasiomwogopa Mungu. Hizo ndizo hadithi zilizopaswa kukataliwa na Wakristo.

Kujaribu Maneno ya Kweli

Hadithi izo hizo zimeenea sana leo. Paulo aliandika hivi: “Utakuja wakati [watu] watakapoyakataa mafundisho yenye uzima [afya, NW]; ila . . . watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo [zisizo za kweli, NW].” (2 Timotheo 4:3, 4) Katika sehemu nyinginezo za dunia, hadithi juu ya mambo yapitayo uwezo wa kibinadamu zimeenea sana na zapendwa na watu wengi. Kwa hiyo, Wakristo hutenda kwa hekima kwa ‘kujaribu maneno’ ya hadithi za kidini ili kuona ikiwa yanapatana na Biblia.—Ayubu 12:11.

Kwa wazi, nyingi hazipatani na Biblia. Kwa kielelezo, katika sehemu nyingi za ulimwengu, ni kawaida kusikia hadithi zinazounga mkono wazo la kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa. Hadithi hizo zasimulia jinsi mtu anavyokufa, kisha arudi baadaye ama katika mwili wa mtoto mchanga aliyezaliwa karibuni, ama akiwa roho, ama akiwa mnyama, ama akiwa mtu katika mahali tofauti.

Hata hivyo, Neno la Mungu laonyesha kwamba nafsi za kibinadamu si zenye hali ya kutoweza kufa; nafsi hufa. (Ezekieli 18:4) Zaidi ya hayo, Biblia husema kwamba wafu wamo kaburini bila uhai, wasiweze kufikiri, kusema, wala kufanya jambo lolote. (Mhubiri 9:5, 10; Warumi 6:23) Hivyo, wale wanaoshawishwa na hadithi zisizo za kweli zinazoendeleza wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa, ‘wamejiepusha’ na “mafundisho yenye uzima [afya, NW]” ya Biblia, kama vile Paulo alivyosema.

Hadithi Juu ya Mambo Yapitayo Uwezo wa Kibinadamu

Hadithi nyinginezo zakazia matendo ya wachawi wa kike na walozi. Kwa kielelezo, katika sehemu fulani za Afrika, hao wawakilishi wa maovu husemwa kuwa na nguvu nyingi sana za kuweza kujigeuza au kuwageuza wengine wawe wanyama watambaazi, tumbili, na ndege; wenye uwezo wa kuruka hewani ili kutimiza kazi zao; wenye uwezo wa kutokea na kutoweka; wenye uwezo wa kupitia ukutani; wenye uwezo wa kuona vitu vilivyozikwa ardhini.

Wingi wa hadithi za jinsi hiyo, pamoja na kuaminiwa kwazo na watu wengi, kwaweza kuwavuta wengine katika kutaniko la Kikristo waamini pia kwamba hizo ni kweli. Huenda wakasababu kwamba ingawa wanadamu wa kawaida hawawezi kufanya mambo ya jinsi hiyo, wale wapokeao nguvu zinazopita za kibinadamu kutoka kwa viumbe wa roho, mashetani, waweza kufanya mambo hayo. Unaoonekana kuwa msingi wa mkataa huo ni 2 Wathesalonike 2:9, 10, lisemalo: “Yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa.”

Ingawa ni kweli kwamba andiko hilo laonyesha kwamba Shetani ana uwezo wa kazi zenye nguvu, hilo lataja kwamba Shetani pia ndiye mwanzilishi wa “ishara na ajabu za uongo” na pia “madanganyo yote ya udhalimu.” Kwa upatano, Biblia yamwonyesha Shetani kuwa mdanganyi mkuu “audanganyaye ulimwengu wote.” (Ufunuo 12:9) Yeye ni bwana-mkubwa katika kufanya watu waamini mambo yasiyo ya kweli.

Kwa sababu hiyo, mara nyingi hata ushuhuda na maungamo ya wale ambao wamehusika katika uwasiliani-roho na uchawi hayategemeki hata kidogo. Huenda watu hao wakaamini kwa moyo mweupe kwamba wameona, wamesikia au kupatwa na mambo fulani; lakini, kwa kweli hawajapatwa nayo. Kwa kielelezo kuna wale wafikirio wamewasiliana na roho za wafu. Lakini wao wamekosea, wamedanganywa, ni wenye kuathiriwa na udanganyifu wa kishetani. Biblia husema kwamba wafu ‘wanashuka kwenye kimya.’—Zaburi 115:17.

Kwa sababu ya historia ya Ibilisi ya udanganyifu, ukweli wa hadithi juu ya nguvu zipitazo uwezo wa kibinadamu wapaswa kushukiwa sikuzote. Nyingi zatokana na ubuni wa mawazo ya kishirikina, yaliyotiwa chumvi kwa kusimuliwa-simuliwa daima.

Kurudia-rudia hekaya hizo kwaendeleza masilahi ya baba wa uwongo, Shetani Ibilisi. (Yohana 8:44) Hizo huchochea upendezi katika mazoea yanayohusu mafumbo ya kishetani ambayo humchukiza Yehova. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Zinatega watu katika utando wa hofu na ushirikina. Si ajabu kwamba Paulo aliwashauri Wakristo “wasiangalie hadithi . . . zisizo na ukomo [zisizo za kweli, NW].”—1 Timotheo 1:3, 4.

Kukataa Ushuhuda wa Mashetani

Lakini, namna gani ikiwa hadithi zaonekana kuwa za kweli? Nyakati nyingine mambo yaliyoonwa yanasimulia juu ya vile roho au wale ambao huwasiliana nao wamekiri ukuu wa Yehova na ukweli wa Mashahidi wake. Je! Wakristo warudie hadithi za jinsi hiyo?

La, hawapaswi. Biblia husema kwamba roho wasio safi walipopaaza sauti kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, yeye “a[li]wakataza sana wasimdhihirishe.” (Marko 3:12) Vivyo hivyo, shetani wa uaguzi alipomchochea msichana mmoja awatambulishe Paulo na Barnaba kuwa “watumishi wa Mungu aliye juu” na wahubiri wa “njia ya wokovu,” Paulo alimwondosha roho huyo kutoka kwa msichana huyo. (Matendo 16:16-18) Wala Yesu, wala Paulo, wala yeyote kati ya waandishi wa Biblia hawakuruhusu mashetani washuhudie kusudi la Mungu au watumishi wake wateule.

Yastahili kuonwa pia kwamba Yesu Kristo alikuwa ameishi katika makao ya kiroho kabla ya yeye kuja duniani. Alikuwa amejua Shetani binafsi. Lakini, Yesu hakuwatumbuiza wanafunzi wake kwa hadithi juu ya utendaji mbalimbali wa Shetani, wala hakuandaa maelezo madogo-madogo juu ya yale ambayo Ibilisi angeweza kufanya na yale hakuweza kufanya. Shetani na mashetani wake hawakuwa marafiki wa Yesu. Walikuwa wahuni, waasi, wenye kuchukia mambo matakatifu, na maadui wa Mungu.

Biblia hutuambia yale tunayohitaji kujua. Hueleza mashetani ni nani, jinsi wanavyowaongoza watu vibaya, na jinsi tuwezavyo kuwaepuka. Hiyo huonyesha kwamba Yehova na Yesu ni wenye nguvu zaidi ya mashetani. Na hutufundisha kwamba tukimtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu, roho waovu hawawezi kutudhuru kwa njia ya kudumu.—Yakobo 4:7.

Basi Wakristo wana sababu nzuri ya kukataa hadithi zisizo za kweli, hadithi zinazochochea tu masilahi ya wale wampingao Mungu. Kama vile Yesu ‘alivyoishuhudia kweli,’ ndivyo wafuasi wake wafanyavyo leo. (Yohana 18:37) Wao hutii himizo hili la Biblia kwa hekima: “Mambo yo yote yaliyo ya kweli . . . yatafakarini hayo.”—Wafilipi 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Madhihirisho yote ya mafumbo ya kishetani yapaswa kuepukwa kabisa na Wakristo wa kweli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki