Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 5/15 kur. 10-15
  • Wazazi, Watoto Wenu Wahitaji Uangalifu wa Pekee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazazi, Watoto Wenu Wahitaji Uangalifu wa Pekee
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uangalifu wa Kila Siku Tangu Utoto
  • Uangalifu wa Pekee Unaohitajika
  • Thamini Wakati Mnaotumia Pamoja
  • Thawabu Bora
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Wazazi Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu Kutoka Utoto Mchanga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Wazazi, Pendezweni na Watoto Wenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 5/15 kur. 10-15

Wazazi, Watoto Wenu Wahitaji Uangalifu wa Pekee

“Wanao [watakuwa] kama miche ya mizeituni wakiizunguka meza yako.”—ZABURI 128:3.

1. Kukuza mimea na kulea watoto kwaweza kulinganishwaje?

KWA njia nyingi, watoto hukua na kusitawi kama mimea. Basi, haishangazi kwamba Biblia inazungumzia mke wa mtu kuwa “mzabibu uzaao” na kufananisha watoto wake na “miche ya mizeituni wakiizunguka meza [yake].” (Zaburi 128:3) Mkulima atakuambia kwamba kukuza miche si rahisi, hasa wakati hali ya hewa na udongo si mzuri. Vilevile, katika ‘siku hizi za mwisho’ zilizo hatari, ni vigumu sana kulea watoto wawe watu wazima wenye kufikiri vizuri, na wenye kumhofu Mungu.—2 Timotheo 3:1-5.

2. Ni nini ambacho mara nyingi huhitajika ili kuvuna mazao mazuri?

2 Ili kuvuna mazao mazuri, mkulima ahitaji udongo wenye rutuba, ujoto wa jua, na maji. Kwa kuongezea kulima na kupalilia, ni lazima adhibiti vidudu na kuandaa utunzi mwingineo. Nyakati zilizo ngumu zaweza kuwapo wakati wa ukuzi, kufikia wakati wa mavuno. Lasikitisha sana kama nini mazao yakiharibika! Lakini, mlimaji aweza kuridhika kama nini avunapo mazao bora baada ya kazi nyingi ya jasho!—Isaya 60:20-22; 61:3.

3. Umuhimu wa mimea na ule wa watoto walinganaje, na watoto wapaswa kupewa uangalifu wa aina gani?

3 Maisha ya binadamu yenye mafanikio na matokeo kwa hakika ni yenye thamani kushinda mavuno ya mkulima. Kwa hiyo haishangazi kwamba kulea watoto kwa mafanikio kwaweza kuchukua hata muda mrefu zaidi na jitihada zaidi kuliko kukuza mazao mengi. (Kumbukumbu la Torati 11:18-21) Mtoto mdogo aliyepandwa katika shamba la uhai, akitiwa maji na kutunzwa kwa upendo na kupewa mipaka ifaayo, aweza kukua na kusitawi kiroho hata akiwa katika ulimwengu uliojaa maadili mabaya. Lakini akitendwa vibaya, au kunyanyaswa, mtoto huyo atanyauka kindani na labda afe kiroho. (Wakolosai 3:21; linganisha Yeremia 2:21; 12:2.) Kwa kweli, watoto wote wahitaji uangalifu wa pekee!

Uangalifu wa Kila Siku Tangu Utoto

4. Watoto wanahitaji uangalifu wa aina gani “tangu utoto”?

4 Ni lazima wazazi watoe uangalifu wa karibu kila wakati kwa mtoto aliyetoka kuzaliwa. Lakini, je, mtoto anahitaji uangalifu wa kimwili tu kila siku? Mtume Paulo alimwandikia mtumishi wa Mungu Timotheo hivi: “Tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu.” (2 Timotheo 3:15) Kwa hiyo uangalifu wa wazazi ambao Timotheo alipokea, hata tangu utoto, ulikuwa wa kiroho pia. Lakini utoto unaanza wakati gani?

5, 6. (a) Biblia yasema nini juu ya kitoto ambacho hakijazaliwa? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba wazazi wanahitaji kuhangaikia hali-njema ya kitoto ambacho hakijazaliwa?

5 Neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia hapo (breʹphos) latumika pia kwa kitoto ambacho hakijazaliwa bado. Elisabeti, mama ya Yohana Mbatizaji, alimweleza mtu wa ukoo wake Mariamu hivi: “Sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga [breʹphos] kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu.” (Luka 1:44) Hivyo, hata wale ambao hawajazaliwa wanaitwa vitoto, na Biblia yaonyesha kwamba wao waweza kuitikia utendaji ulio nje ya tumbo. Basi, je, utunzi wa kabla ya kuzaliwa, ambao hupendekezwa sana leo, utie ndani uangalifu wa hali njema ya kiroho ya kitoto ambacho hakijazaliwa?

6 Hilo ni jambo la kufikiriwa kwa sababu uthibitisho waonyesha kwamba kitoto ambacho hakijazaliwa chaweza ama kunufaika na kile kinachosikia ama kuathiriwa vibaya nacho. Mkurugenzi mmoja wa muziki aligundua kwamba kwa njia fulani alifahamu muziki mbalimbali aliokuwa akijizoeza, hasa ule mtungo wa selo. Alipomtajia mama yake majina ya muziki huo, ambaye alikuwa mstadi wa kucheza mtungo wa selo, mama yake alisema kwamba hiyo ilikuwa ndiyo mitungo ya muziki ambayo hasa alikuwa akijizoeza alipokuwa na mimba yake. Vivyo hivyo, vitoto ambavyo havijazaliwa vyaweza kuathiriwa vibaya mama watazamapo sana vipindi mfululizo vya televisheni. Hivyo, jarida moja la kitiba lilisema juu ya “uzoelevu wa vijusi wa kutazama vipindi vya mfululizo.”

7. (a) Wazazi wengi wametoaje uangalifu kwa hali-njema ya vitoto vyao ambavyo havijazaliwa? (b) Mtoto ana uwezo gani?

7 Wakitambua manufaa ya kichocheo kifaacho kwa vitoto, wazazi wengi huanza kusoma, kusema, na kuimbia mtoto wao hata kabla hajazaliwa. Waweza kufanya vivyo hivyo. Ingawa huenda kitoto chako kisielewe maneno hayo, yaelekea kitanufaika na sauti yako yenye kutuliza na hali yayo ya upendo. Baada ya kuzaliwa, mtoto huyo ataanza kuelewa maneno yako, labda kwa haraka kuliko ufikirivyo. Kwa miaka miwili au mitatu tu, mtoto hujifunza lugha ngumu kwa kuwa katika mazingira yayo tu. Mtoto aweza pia kuanza kujifunza “lugha iliyo safi” ya kweli ya Biblia.—Sefania 3:9.

8. (a) Kwa wazi Biblia yamaanisha nini inaposema kwamba Timotheo aliyajua maandiko matakatifu “tangu utoto”? (b) Ni nini kilichokuwa kweli kwa upande wa Timotheo?

8 Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba Timotheo alikuwa ‘ameyajua maandiko matakatifu tangu utoto’? Kwa wazi alimaanisha kwamba Timotheo alikuwa amepokea mazoezi ya kiroho tangu awe kitoto kichanga, bali si tu tangu awe mtoto mkubwa. Jambo hilo lapatana na maana ya neno la Kigiriki breʹphos, ambalo kwa kawaida hurejezea mtoto aliyetoka tu kuzaliwa. (Luka 2:12, 16; Matendo 7:19) Timotheo alifundishwa kiroho na mama yake Eunike na nyanyake Loisi tangu awezapo kukumbuka. (2 Timotheo 1:5) Kwa hakika ule msemo, ‘Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo’ ulitumika kwa Timotheo. Alikuwa ‘amelelewa katika njia impasayo,’ na matokeo yakawa kwamba alikuwa mtumishi mzuri wa Mungu.—Mithali 22:6; Wafilipi 2:19-22.

Uangalifu wa Pekee Unaohitajika

9. (a) Wazazi wapaswa kuepuka kufanya nini, na kwa nini? (b) Mtoto akuapo, wazazi wanahitaji kufanya nini, nao wapaswa kufuata kielelezo gani?

9 Watoto pia wako kama mimea kwa sababu si watoto wote wanaofanana, wala wote hawaitikii njia zilezile za utunzi. Wazazi wenye hekima watatambua tofauti zilizopo na kuepuka kulinganisha mtoto mmoja na mwingine. (Linganisha Wagalatia 6:4.) Ikiwa watoto wako watasitawi kuwa watu wazima walio wema, unahitaji kuangalia vitabia vya nyutu zao tofauti-tofauti, ukikuza vile vizuri na kung’oa vile vibaya. Vipi ukitambua udhaifu fulani au mwenendo fulani usiofaa, labda kuelekea ukosefu wa kufuatia haki, kupenda vitu vya kimwili, au uchoyo? Rekebisha hilo kwa fadhili, kwa njia ambayo Yesu alirekebisha udhaifu mbalimbali wa mitume wake. (Marko 9:33-37) Hasa pongeza kila mtoto kwa ukawaida kwa ajili ya mambo afanyayo vizuri na vitabia vyake vizuri.

10. Watoto wahitaji nini hasa, na msaada huo waweza kuandaliwaje?

10 Watoto huhitaji hasa uangalifu wa pekee wenye upendo. Yesu alichukua wakati wa kuandalia watoto wadogo uangalifu wa pekee kama huo, hata katika kipindi chenye shughuli nyingi cha siku za mwisho wa huduma yake. (Marko 10:13-16, 32) Wazazi, fuateni kielelezo hicho! Tafuteni wakati bila ubinafsi wa kuwa na watoto wenu. Na msiaibike kuwaonyesha upendo wa kweli. Wekeni mikono yenu juu yao, kama Yesu alivyofanya. Mwakumbatie kwa shauku na kwa busu nyingi. Wazazi wa vijana wema walipoulizwa ni shauri jipi wangepatia wazazi wengine, machache ya majibu yaliyotajwa sana yalikuwa: ‘Uwapende sana,’ ‘tumieni wakati pamoja,’ ‘sitawisheni hali ya kustahiana,’ ‘uwasikilize kwelikweli,’ ‘toa mwongozo badala ya hotuba,’ na ‘chukua mambo kihalisi.’

11. (a) Wazazi wapaswa kuonaje habari ya kuandalia watoto wao uangalifu wa pekee? (b) Ni wakati gani wazazi waweza kufurahia mawasiliano yenye thamani na watoto wao?

11 Kuandaa uangalifu wa pekee kama huo kwaweza kuwa shangwe. Mzazi mmoja aliyefanikiwa aliandika hivi: “Wavulana wetu wawili walipokuwa wachanga, kule kuwatayarisha ili walale, kuwasomea vitabu, kuwafunika, na kutoa sala pamoja nao kulifurahisha sana.” Kutumia pindi kama hizo pamoja kwaandaa fursa za kuwasiliana zinazoweza kutia moyo mzazi na mtoto pia. (Linganisha Warumi 1:11, 12.) Mume na mke mmoja walisikiliza wakati mtoto wao wa miaka mitatu akiomba Mungu abariki “Wally.” Alisali kwa ajili ya “Wally” katika usiku kadhaa uliofuata, na wazazi walitiwa moyo sana walipotambua kwamba alimaaanisha akina ndugu katika Malawi, ambao wakati huo walikuwa wananyanyaswa. Mwanamke mmoja alisema hivi: ‘Nilipokuwa na miaka minne tu, mama yangu alinisaidia kukariri maandiko na kuimba nyimbo za Ufalme huku nikiwa nimesimama kwenye kiti nikikausha vyombo alipokuwa akiviosha.’ Je! waweza kuwazia nyakati ambapo unaweza kufurahia mawasiliano yenye thamani pamoja na watoto wako?

12. Wazazi wa Kikristo watawaandalia watoto wao nini kwa hekima, na ni njia zipi ziwezazo kutumiwa?

12 Wazazi ambao ni Wakristo wenye hekima waweza kupanga kuwe na programu ya funzo la kawaida. Ingawa unaweza kutumia njia rasmi ya maswali kwa majibu, je, unaweza kuchangia mawasiliano yenye kupendeza zaidi kwa kufanya vipindi vya funzo vifae hasa watoto wachanga zaidi? Unaweza kutia ndani kuchora picha za mandhari za Biblia, au kusimulia hadithi za Biblia, kusikiliza ripoti ulizouliza mtoto atayarishe. Fanya Neno la Mungu liwapendeze watoto wako kwa kadiri iwezekanavyo ili wasitawishe tamaa yalo. (1 Petro 2:2, 3) Baba mmoja alisema hivi: ‘Watoto walipokuwa wachanga, tulitambaa pamoja nao sakafuni na kuiga matukio fulani makubwa yaliyotia ndani watu fulani mashuhuri katika Biblia. Watoto walipenda sana jambo hilo.’

13. Manufaa ya vipindi vya mazoezi ni nini, na mnaweza kujizoeza nini katika pindi hizo?

13 Vipindi vya mazoezi pia hutokeza mawasiliano yenye thamani kwa sababu vipindi hivyo husaidia watoto wajitayarishe kwa ajili ya hali halisi maishani. Mmoja wa watoto wa Kusserow—wote wakiwa 11 waliodumisha uaminifu wao kwa Mungu wakati wa mnyanyaso wa Nazi—alisema hivi juu ya wazazi wake: “Walituonyesha jinsi ya kutenda na kujitetea kwa kutumia Biblia. [1 Petro 3:15] Mara nyingi tulikuwa na vipindi vya mazoezi, vya maswali na majibu.” Mbona msifanye vivyo hivyo? Mnaweza kufanya mazoezi ya utoaji mbalimbali kwa ajili ya huduma, mzazi akijifanya kuwa mwenye nyumba. Au kipindi cha mazoezi chaweza kushughulikia vishawishi vinavyotokea halisi maishani. (Mithali 1:10-15) “Kujizoeza kwa ajili ya hali zilizo ngumu kwaweza kujenga ustadi na uhakika wa mtoto,” kasema mwanamke mmoja. “Mazoezi hayo yaweza kutia ndani kujifanya kuwa rafiki anayetolea mtoto wako sigareti, kinywaji au dawa ya kulevya.” Vipindi hivyo vyaweza kukusaidia utambue jinsi mtoto wako atakavyoitikia akiwa katika hali kama hizo.

14. Ni kwa nini mazungumzo yenye upendo na huruma pamoja na watoto wako ni yenye maana sana?

14 Katika vipindi vya mawasiliano na mtoto wako, msihi kwa njia iyo hiyo yenye huruma kama vile mwandikaji wa maneno haya alivyofanya: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani.” (Mithali 3:1, 2) Je! halingegusa moyo wa mtoto wako kama ungemweleza kwa upendo kwamba unataka utiifu kwa sababu kufanya hivyo kutamtokezea amani na wingi wa siku—kwa hakika, uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye amani? Fikiria utu wa mtoto wako unaposababu kwa kutumia Neno la Mungu. Fanya hivyo kupitia sala, na Yehova atabariki jitihada zako. Mazungumzo kama hayo yanayotegemea Biblia yaliyo na upendo na huruma yaelekea yatakuwa na matokeo mazuri na kuleta baraka za kudumu.—Mithali 22:6.

15. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kutatua matatizo?

15 Hata kama mawasiliano kama hayo hayatokei katika wakati uliopangwa wa funzo, usikengeushwe na mambo mengine. Sikiliza kwa uangalifu yale ambayo mtoto anasema na vilevile jinsi ayasemavyo. “Mtazame mtoto wako,” akasema mstadi mmoja. “Mpe uangalifu wako wote. Unahitaji kuelewa, si kusikia tu. Wazazi ambao hutia jitihada hiyo ya ziada waweza kufanya kuwe na tofauti kubwa maishani mwa watoto wao.” Leo watoto hukabili matatizo mazito shuleni na kwingineko. Ukiwa mzazi, mfanye mtoto aeleze, na umsaidie aone mambo kwa maoni ya Mungu. Kama huna hakika ya jinsi ya kulitatua tatizo hilo, fanya utafiti katika Maandiko na vichapo vilivyoandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45) Kwa vyovyote vile, mpe mtoto wako uangalifu wote wa pekee unaohitajika ili atatue tatizo hilo.

Thamini Wakati Mnaotumia Pamoja

16, 17. (a) Ni kwa nini vijana hasa wanahitaji uangalifu na mafunzo ya pekee leo? (b) Watoto wanahitaji kujua nini wanapotiwa nidhamu na wazazi wao?

16 Leo vijana wahitaji uangalifu mwingi zaidi wa pekee kuliko wakati mwingine wowote kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho,” nazo ni “nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3-14) Wazazi pamoja na watoto wahitaji ulinzi unaoandaliwa na hekima ya kweli ‘inayohifadhi yeye aliye nayo.’ (Mhubiri 7:12) Kwa kuwa hekima ya kimungu yatia ndani kutumia vizuri ujuzi unaotokana na Biblia, watoto wahitaji kufundishwa Neno la Mungu kwa ukawaida. Kwa hiyo jifunze Maandiko pamoja na watoto wako. Uwaeleze juu ya Yehova, ukieleza kwa uangalifu juu ya matakwa yake, na kuweka tazamio lenye furaha la kutimizwa kwa ahadi zake tukufu. Sema juu ya mambo kama hayo ukiwa nyumbani, utembeapo pamoja na watoto wako—kwa kweli katika kila fursa ifaayo.—Kumbukumbu la Torati 6:4-7.

17 Wakulima wajua kwamba si mimea yote inayositawi ikiwa katika hali zilezile. Mimea huhitaji utunzi wa pekee. Vivyo hivyo, kila mtoto ni tofauti na ahitaji uangalifu, mafunzo, na nidhamu za pekee. Mathalani, mtazamo wa mzazi usiopendelea kitendo cha mtoto waweza kutosha kukomesha mwendo mbaya wa mtoto mmoja, ilhali mtoto mwingine huenda akahitaji nidhamu kali zaidi. Lakini watoto wako wote wahitaji kujua ni kwa nini hujafurahia maneno fulani ama vitendo fulani, na wazazi wote wapaswa kushirikiana ili nidhamu ipatane. (Waefeso 6:4) Ni muhimu hasa kwa wazazi Wakristo kutoa mwongozo ulio wazi unaopatana na Maandiko.

18, 19. Wazazi Wakristo wana daraka gani kuelekea watoto wao, na matokeo yaelekea kuwa nini kazi hiyo ikifanywa vizuri?

18 Ni lazima mkulima afanye kazi ya kupanda na kulima kwa wakati ufaao. Akichelewa au akipuuza mazao yake, atavuna kidogo sana au hatavuna chochote. Naam, watoto wenu wachanga ni “mimea” inayokua inayohitaji uangalifu wa pekee sasa hivi, si mwezi ujao ama mwaka ujao. Usiachilie fursa hizo zenye thamani sana zipite bila kuendeleza ukuzi wao wa kiroho kwa kupatana na Neno la Mungu na kung’oa mawazo ya kilimwengu yanayoweza kuwafanya wanyauke na kufa kiroho. Thamini sana zile saa na siku ambazo una pendeleo la kuwa pamoja na watoto wako, kwa kuwa nyakati hizo hupita kwa kasi. Fanya kazi kwa bidii ukuze katika watoto wako sifa za kimungu zinazohitajika kwa ajili ya maisha yenye furaha wakiwa watumishi waaminifu wa Yehova. (Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:12-14) Hiyo si kazi ya mtu mwingine; ni kazi yako, na Mungu aweza kukusaidia kuifanya.

19 Uwape watoto wako urithi mzuri wa kiroho. Jifunze Neno la Mungu pamoja nao, na kufurahia tafrija nzuri pamoja nao. Peleka watoto wako kwenye mikutano ya Kikristo, na uwe pamoja nao katika kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme. Jenga katika watoto wako wapendwa aina ya utu inayompendeza Yehova, na yaelekea sana kwamba watakuletea shangwe nyingi baadaye maishani. Kwa kweli, “baba yake mwenye haki atashangilia; naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia. Na wafurahi baba yako na mama yako; na afurahi aliyekuzaa.”—Mithali 23:24, 25.

Thawabu Bora

20. Ni nini ufunguo wa kuwa mzazi wa matineja mwenye mafanikio?

20 Kulea watoto ni mgawo mgumu wa muda mrefu. Kukuza ‘miche hiyo ya mizeituni kuzunguka meza yako’ wawe watu wazima wanaomhofu Mungu na wanaozaa matunda ya Ufalme kumeitwa mradi wa miaka 20. (Zaburi 128:3; Yohana 15:8) Mara nyingi mradi huo huwa mgumu zaidi watoto wafikapo umri wa utineja, wakati mibano yao mara nyingi huongezeka na wazazi waona uhitaji wa kuongeza jitihada zao. Lakini ufunguo wa mafanikio hubaki uleule—kuwa mwenye kusikiliza, mchangamfu, na mwenye kuelewa mambo. Kumbukeni kwamba kwa kweli vijana wenu wahitaji uangalifu wa pekee. Mwaweza kuwapa uangalifu kama huo kwa kuwaonyesha hangaiko la kweli lenye upendo kwa ajili ya hali-njema yao. Ili kuwasaidia, ni lazima ujitoe kabisa kwa kuwaandalia wakati, upendo, na hangaiko wanazohitaji sana.

21. Thawabu ya kuwapa watoto uangalifu wa pekee yaweza kuwa nini?

21 Thawabu ya jitihada zako za kutunza matunda yenye thamani ambayo Yehova amewapa yaweza kuwa yenye kuridhisha sana kuliko mavuno mengi yoyote ya mkulima. (Zaburi 127:3-5) Kwa hiyo wazazi, endeleeni kuwapa watoto wenu uangalifu wa pekee. Fanyeni hivyo kwa manufaa yao na kwa utukufu wa Baba yetu wa kimbingu, Yehova.

[Ungejibuje?

◻ Kukuza mimea na kulea watoto kwaweza kulinganishwaje?

◻ Mtoto ahitaji uangalifu wa aina gani tangu utoto?

◻ Watoto wahitaji utunzi gani wa pekee, nao waweza kuandaliwaje?

◻ Kwa nini uwape watoto wako uangalifu wa pekee?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki