Vijana—Mnatii Mafundisho ya Nani?
“Wengine watajitenga na imani, wakisikiliza . . . mafundisho ya mashetani.”—1 TIMOTHEO 4:1.
1. (a) Vijana wana uchaguzi gani? (b) Yehova hufundishaje?
SWALI ambalo vijana wanaulizwa hapa ni hili, Mnatii mafundisho ya nani? Jambo hilo ladokeza kwamba nyinyi vijana mna uchaguzi wa kufanya. Uchaguzi huo ni kuitikia ifaavyo mafundisho ya kimungu ama kufuata mafundisho ya mashetani. Yehova hufundisha kupitia Neno lake, Biblia, na vilevile kupitia huduma ya wale anaowatumia kuwa wawakilishi wake duniani. (Isaya 54:13; Matendo 8:26-39; Mathayo 24:45-47) Lakini, je, mnashangaa kwamba hata mashetani hufundisha pia?
2. Kwa nini ni muhimu kujihadhari na mafundisho ya mashetani hasa katika wakati huu?
2 Mtume Paulo aliandika hivi: “Nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani.” (1 Timotheo 4:1) Kwa kuwa tunaishi katika “siku za mwisho” wakati Shetani na mashetani wake hasa wana utendaji mwingi, je, mwaona ni kwa nini twauliza swali hili, Mnatii mafundisho ya nani? (2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 12:7-12) Kwa sababu Shetani na mashetani wake ni werevu sana, na ni wenye kushawishi sana katika njia zao za utendaji, ni muhimu sana kufikiria kwa uangalifu swali hilo.—2 Wakorintho 11:14, 15.
Mashetani na Mafundisho Yao
3. Mashetani ni akina nani, kusudi lao ni nini, na wanajaribu kutimizaje kusudi lao?
3 Pindi moja mashetani walikuwa malaika wa Yehova, lakini waliasi dhidi ya Muumba wao na hivyo wakawa waungaji mkono wa Shetani. (Mathayo 12:24) Kusudi lao ni kufisidi watu na kuwageuza wasimtumikie Mungu. Ili kutimiza kusudi hilo, mashetani hutumia walimu wa kibinadamu kuendeleza njia yao ya maisha yenye ubinafsi, na iliyopotoka kiadili na inayoshutumiwa na Yehova. (Linganisha 2 Petro 2:1, 12-15.) Pitio la jinsi malaika waliokuwa waaminifu walivyokuja kuwa mashetani kutawasaidia mtambue mafundisho yao na njia ya maisha inayoendelezwa na mafundisho hayo.
4. (a) Mbona malaika wasiotii walikuja duniani katika siku ya Noa? (b) Ni nini kilichopata malaika waovu na wazao wao wakati wa Furiko?
4 Katika siku za Noa, malaika fulani walivutiwa sana na binti za watu waliokuwa warembo hivi kwamba wakaacha makao yao mbinguni kuja duniani. Muungano wao wa kingono na wanawake hao ulitokeza wana-mivyauso walioitwa Wanefili. Kwa kuwa si jambo la asili kwa viumbe-roho kuishi pamoja na wanadamu, mambo ambayo malaika hao wasiotii walifanya na wanawake hao yalikuwa mabaya kama tu vile vitendo vya ugoni wa jinsia-moja vilivyofanywa baadaye na wanaume na wavulana wa Sodoma. (Mwanzo 6:1-4; 19:4-11; Yuda 6, 7) Ingawa wake za malaika hao walikufa katika maji ya furiko pamoja na watoto wao mivyauso, malaika hao waovu walivua miili yao ya kibinadamu na kurudi mbinguni na ambako walikuja kuwa wenzi wa Shetani Ibilisi.—2 Petro 2:4.
5. Mashetani ni viumbe vya aina gani, na wanajaribuje kuvunja sheria za Mungu?
5 Kwa kutazama historia hiyo ya nyuma, je, mwaona mashetani ni viumbe vya aina gani hasa? Wao ni wapotovu wa ngono wanaodhibiti ulimwengu huu wenye kichaa cha ngono bila kuonekana na wanadamu. Ingawa wamezuiwa wasivae tena miili ya kibinadamu, wao wanapata raha kutokana na upotovu wa kingono wa wale wanaoweza kufisidi duniani. (Waefeso 6:11, 12) Mashetani hujaribu kuvunja sheria za Yehova za usafi wa kiadili na maadili kwa kufanya sheria hizo zionekane kuwa zenye kuzuia isivyofaa. Malaika hao waovu hutetea ukosefu wa adili kingono kuwa njia ya maisha ya kawaida na yenye kufurahisha.
Kuendeleza Mafundisho ya Mashetani
6. Ni kwa nini tusishangae kwamba mashetani wanaendeleza mafundisho yao kwa njia ya hila?
6 Hatupaswi kushangaa kwamba mashetani wangeendeleza mafundisho yao kwa njia ya hila kwa sababu hiyo ndiyo mbinu ambayo kiongozi wao, Shetani Ibilisi, alitumia katika kudanganya Hawa. Kumbuka kwamba alisema na Hawa kana kwamba alitaka kumsaidia. “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” Shetani akauliza. Kisha kwa ujanja akajaribu kupinga mafundisho ya Mungu kwa kumwambia Hawa kwamba angenufaika kwa kula kutoka kwenye mti ule uliokatazwa. “Siku mtakayokula matunda ya mti huo,” Ibilisi akaahidi, “mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:1-5) Hivyo Hawa alivutiwa, naam akashawishwa, akose kumtii Mungu.—2 Wakorintho 11:3; 1 Timotheo 2:13, 14.
7. Matokeo ya mafundisho ya hila ya mashetani yamekuwa nini, na jambo hilo linatupa onyo gani?
7 Katika nyakati za karibuni vilevile, watu wengi wameshawishwa. Mashetani wameendeleza kwa ujanja sana ukosefu wa adili kingono hivi kwamba umekuja kukubaliwa na watu wengi ambao zamani waliushutumu. Kwa kielelezo, wakati mtoa-shauri mmoja wa gazeti kule Marekani alipojibu barua moja iliyohusu watu wasiooana kufanya ngono, yeye aliandika hivi: “Sikudhani kwamba ningebadili maoni yangu juu ya suala hilo, lakini sasa naamini kwamba wale ambao wanafikiria kwa uzito juu ya kuoana wapaswa kufunga safari za mwisho-juma pamoja ili waone kama wanapatana.” Kisha akaongezea hivi: “Siamini kwamba niliandika maneno hayo!” Hata yeye hakuamini kwamba alikuwa amependekeza uasherati, lakini alikuwa amefanya hivyo! Kwa wazi, ni lazima tuwe waangalifu mafundisho ya mashetani yasije yakaathiri maoni yetu juu ya matendo yanayokatazwa na Mungu.—Warumi 1:26, 27; Waefeso 5:5, 10-12.
8. (a) Neno “ulimwengu” latumiwaje katika Biblia? (b) Ni nani anayetawala ulimwengu, na wafuasi wa Yesu wapaswa waonaje ulimwengu?
8 Tusisahau kamwe kwamba Shetani ndiye “mkuu wa ulimwengu huu.” Kwa kweli, mtume Yohana alisema kwamba “dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Ni kweli kwamba nyakati nyingine Yesu alitumia neno “ulimwengu” kurejezea jamii yote ya wanadamu. (Mathayo 26:13; Yohana 3:16; 12:46) Hata hivyo, mara nyingi zaidi alitumia neno “ulimwengu” kurejezea jamii yote ya wanadamu ambayo haimo katika kutaniko la kweli la Kikristo. Mathalani, Yesu alisema kwamba ni lazima wafuasi wake wasiwe “sehemu ya ulimwengu” (jamii ya wanadamu ambao si waadilifu) na kwamba ulimwengu ungewachukia kwa sababu hawangekuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 15:19; 17:14-16, New World Translation) Biblia ilionya zaidi kwamba tuepuke kuwa marafiki wa ulimwengu huu unaotawalwa na Shetani.—Yakobo 4:4.
9, 10. (a) Ni vitu gani vya kilimwengu huchochea tamaa mbaya ya kingono? (b) Inawezekanaje kutambua ni nani anayeendeleza mambo yanayofundishwa na vitumbuizo vya ulimwengu?
9 Mtume Yohana alihimiza hivi: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama mambo katika ulimwengu.” Yeye alisema hivi pia: “Kila jambo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu kujivunia njia yake ya kutegemeza uhai—halitokani na Baba.” (1 Yohana 2:15, 16, NW) Ebu fikirieni jambo hilo. Ni nini kilichomo ulimwenguni leo kinachochochea tamaa mbaya, kama vile tamaa ya ngono haramu? (1 Wathesalonike 4:3-5) Vipi juu ya muziki mwingi wa ulimwengu? Polisi mmoja wa kuchunguza wafungwa wa nje katika California alisema hivi: “Kwa msingi, muziki wafundisha kwamba si lazima uwasikilize wazazi wako, na kwamba unapaswa kuendesha maisha yako utakavyo.” Je! mwatambua chanzo cha mafundisho yanayotolewa na muziki huo?
10 Kumbuka kwamba Shetani alimaanisha hivi kwa Hawa: ‘Unakosa kitu chenye maana. Ishi maisha yako utakavyo. Jiamulie mwenyewe mema na mabaya. Huhitaji kumsikiliza Mungu.’ (Mwanzo 3:1-5) Je! ujumbe kama huo haupatikani katika muziki mwingi wa ulimwengu? Lakini mashetani hawafundishi kupitia muziki pekee. Wao pia hutumia vipindi vya kibiashara vya televisheni, sinema, na vidio kufundisha. Kwa njia gani? Njia za mawasiliano za ulimwengu huleta vitumbuizo vinavyofanya mafundisho ya kiadili ya Mungu yaonekane kuwa yenye vizuizi. Hizo hutetea uasherati kwa kuukazia na kuuonyesha kuwa kitendo chenye kufaa.
11. Tukisema kiadili, mara nyingi televisheni hufundisha nini?
11 Gazeti U.S.News & World Report lilisema hivi: “Katika 1991, stesheni tatu [za televisheni za U.S.] zilionyesha zaidi ya visa 10,000 vya ngono wakati watu wengi zaidi hutazama televisheni; kwa kila wonyesho mmoja wa ngono kati ya watu waliooana, stesheni hizo zilionyesha maonyesho 14 ya ngono nje ya ndoa.” Kwa kuonyesha visa zaidi ya 9,000 vya ngono haramu kwa mwaka mmoja wakati watu wengi zaidi hutazama televisheni, mwaweza kusema televisheni inafundisha nini? Barry S. Sapolsky, aliyesaidia kuandika ripoti iliyoitwa “Ngono Wakati Watu Wengi Zaidi Hutazama Televisheni: 1979 Kwa Kulinganisha na 1989,” asema hivi: “Kijana akitumia miaka mingi akitazama vipindi vya televisheni vinavyoonyesha watu wakijiingiza katika tabia ya michezo ya kingono au ngono halisi, maelfu ya picha hizo kwa muda wa miaka hiyo yatamfundisha kwamba ngono inafurahisha—bila madhara yoyote.” Hakuna shaka juu ya jambo hilo: Vitumbuizo vya ulimwengu hufundisha vijana kwamba hakuna sheria, kwamba uasherati unakubalika, na kwamba hakuna madhara katika kuishi maisha anayokataa Mungu.—1 Wakorintho 6:18; Waefeso 5:3-5.
12. Kwa nini vitumbuizo vya ulimwengu ni vyenye hatari sana hasa kwa vijana Wakristo?
12 Muziki wa ulimwengu, sinema, vidio, na televisheni zimekusudiwa zivutie vijana. Hizo zaendeleza mafundisho yenye ufisadi ya mashetani! Lakini, je, jambo hilo litushangaze? Fikirieni jambo hilo. Kama dini bandia na siasa ni sehemu ya ulimwengu wa Shetani—na kwa wazi ziko hivyo—je, lapatana na akili kufikiri kwamba vitumbuizo vinavyoendelezwa na ulimwengu havina uvutano wa mashetani? Hasa nyinyi vijana mnahitaji kujihadhari ‘msiache ulimwengu unaowazunguka uwafinyange kwa njia yao.’—Warumi 12:2, The New Testament in Modern English, cha J. B. Phillips.
Jichunguze
13. Ni kujichunguza kupi kunakopaswa kufanywa?
13 Suala la kwamba unatii mafundisho ya nani haliamuliwi na usemi wako pekee bali huamuliwa pia na matendo yako. (Warumi 6:16) Basi jiulize hivi, ‘Je! mtazamo wangu na njia yangu ya maisha zinaathiriwa vibaya na yale ninayojifunza kupitia njia za ulimwengu za kueneza propaganda? Je! yawezekana kwamba mafundisho ya mashetani yanaingia katika maisha yangu?’ Ili kukusaidia ujibu maswali kama hayo, mbona usiangalie kadiri ya wakati na jitihada unazotumia kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kusema na wengine juu ya Ufalme wa Mungu na ulinganishe na wakati unaotumia kutazama televisheni, kusikiliza muziki, kushiriki katika mchezo upendao, au unaotumia katika utendaji mwingine kama huo? Kwa kuwa kuna mengi sana—kwa kweli, uhai wako mwenyewe—yaliyo hatarini, jichunguze kwa unyoofu.—2 Wakorintho 13:5.
14. Ni nini kitakachoathiri afya yetu ya kiroho, na twapaswa kukumbuka jambo gani kwa uzito?
14 Unajua vema kwamba chakula halisi unachokula kitaathiri afya yako ya kimwili. Vilevile, afya yako ya kiroho inaathiriwa na chakula unacholisha akili yako na moyo wako. (1 Petro 2:1, 2) Ingawa unaweza kujidanganya kuhusu mapendezi yako halisi, huwezi kumdanganya Hakimu wetu, Yesu Kristo. (Yohana 5:30) Kwa hiyo jiulize, ‘Kama Yesu angekuwa duniani, je, ningeaibika kama angeingia chumbani mwangu na kusikia au kuona kile ninachotazama kwenye televisheni?’ Jambo la kufikiria kwa uzito ni kwamba Yesu anatuona na anajua matendo yetu.—Ufunuo 3:15.
Kataa Mafundisho ya Mashetani
15. Ni kwa nini Wakristo wanahitaji kupigana kwa bidii ili kukinza mafundisho ya mashetani?
15 Ule mbano ambao mashetani wanaweka juu ya vijana ili wasikilize mafundisho yao ni mkubwa mno. Mashetani hao huonekana kuwa wenye kuandaa maisha ya kujiridhisha papo hapo—maisha ya raha na anasa. Ili ampendeze Mungu, Musa wa kale alikataa “kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo” akiwa mshiriki mashuhuri wa nyumba ya Farao. (Waebrania 11:24-27) Si rahisi kukataa mambo wanayotutolea mashetani, kwa hiyo ni lazima ujitahidi kufanya yaliyo mema. Na jambo hilo ni kweli hasa kwa sababu tumerithi dhambi na mioyo yetu hutamani kufanya yaliyo mabaya. (Mwanzo 8:21; Warumi 5:12) Kwa sababu ya mwelekeo wetu wa kufanya dhambi, hata mtume Paulo alihitaji kuwa mgumu na mwili wake asije akaruhusu tamaa za kimwili zimshinde.—1 Wakorintho 9:27; Warumi 7:21-23.
16. Vijana wawezaje kukinza mibano ya kujiingiza katika mwenendo usio wa adili?
16 Ingawa unaweza kushawishwa ‘kuandamana na mkutano ili kutenda maovu,’ Mungu anaweza kukusaidia kukinza mbano kutoka kwa marika wako wa kufuata mwendo wao mbaya. (Kutoka 23:2; 1 Wakorintho 10:13) Lakini ni lazima usikilize mielekezo ya Mungu, ukiikumbuka misemo yake moyoni mwako. (Zaburi 119:9, 11) Unahitaji kung’amua kwamba vijana wanapojitenga, tamaa ya kingono yaweza kupanda na kufanya sheria ya Mungu ivunjwe. “Tunapokuwa peke yetu na mvulana rafiki yangu, mwili wangu waniambia nifanye jambo fulani na ubongo wangu waniambia nifanye jambo jingine,” akakiri msichana mmoja. Kwa hiyo tambua mipaka yako na ung’amue kwamba moyo wako ni mdanganyifu. (Yeremia 17:9) Usijitenge. (Mithali 18:1) Wekeni mipaka ya maonyesho yenu ya mapenzi. Na jambo muhimu zaidi, kuwa karibu sana na watu wanaompenda Yehova na walio na staha ya ndani kwa ajili ya sheria zake.—Zaburi 119:63; Mithali 13:20; 1 Wakorintho 15:33.
17. Ni nini kinachoweza kusaidia vijana Wakristo wapate nguvu ya kukinza mafundisho ya mashetani?
17 Funzo la uangalifu la vichapo vya Kikristo vilivyotayarishwa kwa ajili ya kukuimarisha kiroho litakusaidia. Mathalani, fikiria kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na ile sura “Vile Vita vya Kufanya Yaliyo Mema” katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Acha maagizo ya Kimaandiko yaliyoandaliwa yaingie ndani sana akilini na moyoni mwako, na yatakuimarisha. Jambo ambalo hupaswi kusahau kamwe ni kwamba si rahisi kufanya yaliyo sawa katika ulimwengu huu unaotawalwa na mashetani. Kwa hiyo jitahidi. (Luka 13:24) Jenga nguvu zako za kiroho. Usiige wanyonge na wenye hofu wanaofuata umati wa watu.
Nufaika na Mafundisho ya Kimungu
18. Baadhi ya manufaa za kutii mafundisho ya kimungu ni yapi?
18 Kumbuka pia kwamba hutakosa kitu chochote kifaacho kwa kutii mafundisho ya Yehova. Yeye akupenda kwelikweli, na hiyo ndiyo sababu ‘anakufundisha ili upate faida.’ (Isaya 48:17) Kwa hiyo tii mafundisho ya Yehova, na uepuke maumivu ya dhamiri iliyoharibika, kutojistahi, mimba zisizotakiwa, maradhi yanayopitishwa kingono, au misiba kama hiyo. Yehova hufurahi watumishi wake wanapompa jibu kwa ushindani wa Shetani kwamba wanadamu hawatadumisha uaminifu kwa Mungu wakijaribiwa. (Ayubu 1:6-12) Ukifurahisha moyo wa Yehova kwa kuwa mwaminifu kwake, utaokoka atakapotekeleza hukumu kali dhidi ya ulimwengu huu, wakati ambapo wote wanaokiuka sheria zake wataangamizwa.—Mithali 27:11; 1 Wakorintho 6:9, 10; 1 Yohana 2:17.
19. Kuna umuhimu gani wa kushirikiana na watu wanaothamini manufaa za mafundisho ya Yehova?
19 Ukishirikiana kwa ukaribu na wale wanaothamini mambo ambayo Yehova amewafanyia, unaweza kujifunza kutokana na maono yao. Mwanamke mmoja ambaye zamani alikuwa mzoelevu wa dawa za kulevya na aliyezoea maisha ya ukosefu wa adili alieleza hivi: “Kama nisingalimsikiliza Yehova, ningalikufa. Mtu yule ambaye angenioa alikufa kutokana na UKIMWI. Wale wote waliokuwa marafiki wangu wa karibu wa kilimwengu ama wamekufa kutokana na UKIMWI ama wanaelekea kufa. Mara nyingi mimi huwaona barabarani, nami humshukuru Yehova kila siku kwa ajili ya sheria zake zinazoongoza watu wake na zitakazotudumisha tukiwa watakatifu maadamu tuzitumie. Sijapata kuwa mwenye furaha, mwenye kuridhika, na mwenye usalama maishani mwangu mwote kuliko nilivyo sasa.” Kwa kweli, kutii mafundisho ya Yehova hutunufaisha nyakati zote!
Chagueni Vizuri
20, 21. (a) Vijana wana mambo gani mawili ya kuchagua? (b) Kutakuwa na manufaa gani ya kudumu tukitii mafundisho ya kimungu?
20 Twawahimiza hivi vijana: Chagueni vizuri kwa kumtumikia Yehova. Kisha azimieni kushikamana na uamuzi huo. (Yoshua 24:15) Kwa hakika, mnaweza kuchagua njia moja tu kati ya mbili. Yesu alisema kwamba kuna njia pana—iliyo rahisi ya mtu kufanya atakavyo. Njia hiyo yaelekea ukingoni, kwenye uharibifu. Njia ile nyingine imesongamana. Ni njia ngumu kusafiri katika ulimwengu huu usio na adili na unaotawalwa na mashetani. Lakini hatimaye njia hiyo itapeleka wale wanaoisafiri kwenye ulimwengu mpya wa Mungu ulio mzuri ajabu. (Mathayo 7:13, 14) Mtachagua njia gani? Mtatii mafundisho ya nani?
21 Yehova amewapa uhuru wa kuchagua wenyewe. Yeye hajaribu kuwalazimisha mumtumikie. “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti,” akasema nabii wa Mungu Musa, akihimiza hivi: “Chagua uzima.” Uchaguzi huo unafanywa kwa “kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 29:2; 30:19, 20) Na mchague kwa hekima kutii mafundisho ya kimungu na mfurahie uhai wa milele katika ulimwengu mpya mtukufu wa Mungu.
Ungejibuje?
◻ Mashetani ni akina nani, nao hufundisha nini?
◻ Mashetani huendelezaje mafundisho yao leo?
◻ Inawezekanaje kukinza mafundisho ya mashetani?
◻ Kuna manufaa gani za kutii mafundisho ya Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kabla ya Furiko, malaika wasiotii na wazao wao waliendeleza jeuri na ufisadi
[Picha katika ukurasa wa 18]
Je! ungeaibika kama Yesu angesikia muziki upendao?