Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 6/15 kur. 8-11
  • Je! Wewe Hufurahia Funzo la Kibinafsi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Hufurahia Funzo la Kibinafsi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Walifanya Upya Nguvu Zao Kupitia Funzo la Kibinafsi
  • Huduma na Iwe Kichocheo
  • Jilishe Neno la Mungu kwa Ukawaida
  • Mawazo Fulani ya Busara
  • Uwe na Hamu ya Kujifunza Nyakati Zote
  • Fuata Kielelezo cha Wafalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kupata Upendezi Katika Neno la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Boresha Mazoea Yako ya Kujifunza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Kunufaika kwa Usomaji wa Biblia Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 6/15 kur. 8-11

Je! Wewe Hufurahia Funzo la Kibinafsi?

MTUMISHI yeyote wa Mungu mwenye moyo mweupe angefurahi kutumia wakati wa kutosha katika funzo la Biblia la kibinafsi. (Zaburi 1:1, 2) Lakini, wengi huona vigumu kutumia wakati na nishati nyingi kadiri ambavyo wangependa, kwa sababu wanahisi kuwa kuna mambo mengi ya kufanywa yanayohitaji nguvu zao na wakati wao.

Hata hivyo, ili kuendelea wakiwa watumishi wa Mungu wenye utendaji, wote wanahitaji kuimarisha shangwe yao na nguvu zao kila siku kwa kupata mambo mapya au yenye kina zaidi ya kweli ya Neno la Mungu. Kweli za Biblia zilizokusukuma kwa kina kirefu miaka iliyopita huenda hazikusukumi kwa kadiri hiyo sasa. Hivyo, ni vema, na muhimu, kwamba tufanye jitihada yenye kudhamiria na yenye kuendelea kupata ufahamu wa ndani ulio mpya katika kweli ili tuendelee kuwa wenye kuchochewa kiroho.

Wanaume wa kale wenye imani walijiimarishaje kiroho kupitia funzo la kibinafsi la Neno la Mungu? Baadhi ya watumishi wa Yehova wa kisasa hufanyaje funzo lao liwe lenye kufurahisha zaidi na pia lenye matokeo zaidi? Wao wamethawabishwaje kwa ajili ya jitihada zao?

Walifanya Upya Nguvu Zao Kupitia Funzo la Kibinafsi

Mfalme Yosia wa Yuda alianza kampeni yake dhidi ya ibada ya sanamu kwa bidii hata zaidi baada ya yeye kusomewa ‘kitabu cha torati ya Yehova iliyotolewa kwa mkono wa Musa.’ Hakuna shaka kwamba hiyo haikuwa mara yake ya kwanza kusoma sehemu hiyo ya Neno la Mungu; lakini kusikia ujumbe huo moja kwa moja kutoka kwa hati-mkono ya awali kulimchochea katika pigano lake kwa ajili ya ibada safi.—2 Mambo ya Nyakati 34:14-19.

Nabii Danieli alifahamu ‘hesabu ya miaka ya kuutimiza ukiwa wa Yerusalemu’ na uhakika wa jambo hilo si kutokana na kitabu cha Yeremia tu, bali pia kutoka kwa vile “vitabu.” Yaelekea sana kwamba hivyo vilitia ndani vitabu kama vile Mambo ya Walawi (26:34, 35), Isaya (44:26-28), Hosea (14:4-7), na Amosi (9:13-15). Yale aliyothibitisha kupitia funzo lake la bidii la vitabu vya Biblia yalimwongoza mwanamume huyo mchaji amtafute Mungu kwa sala ya bidii. Maombi yake ya bidii yalijibiwa kwa ufunuo zaidi na uhakikishio kuhusiana na jiji la Yerusalemu kutia na watu wake.—Danieli, sura 9.

Yosia, aliyefanya ‘yaliyo mema machoni pa Yehova,’ na Danieli, aliyekuwa ‘mtu wa kupendeza sana’ machoni pa Mungu, hawakuwa tofauti nasi leo kwa msingi. (2 Wafalme 22:2; Danieli 9:23) Jitihada zao za kibinafsi zilizotolewa katika funzo la bidii sana la Maandiko yaliyopatikana wakati huo ziliwaongoza kuwa na hali ya kiroho iliyo bora zaidi na kuwasaidia kuwa na uhusiano wenye nguvu zaidi na Mungu. Jambo ilo hilo laweza kusemwa juu ya watumishi wa Yehova wengine wengi, kama vile Yeftha, mtunga-zaburi wa nyumba ya Asafu, Nehemia, na Stefano. Wote hao walitoa ithibati ya funzo la kibinafsi lenye uangalifu wa sehemu ya Biblia iliyopatikana wakati huo.—Waamuzi 11:14-27; Zaburi 79, 80; Nehemia 1:8-10; 8:9-12; 13:29-31; Matendo 6:15–7:53.

Huduma na Iwe Kichocheo

Watumishi wengi wa Yehova leo ambao wamemtumikia kwa miaka mingi wana ratiba ya funzo la Biblia la kibinafsi. Wameona hilo kuwa jambo muhimu ili kuendelea kuwa macho na kutimiza kikamili madaraka yao ya Kikristo. Hata hivyo, wengi wao wakiri kwamba si rahisi sikuzote kusawazisha utumizi wao wa wakati na nishati kati ya funzo na mambo mengine yasiyopaswa kupuuzwa.

Bado, kuendelea kuwa macho kiroho kupitia funzo la kibinafsi lenye bidii ni jambo muhimu katika kushughulika na mahitaji ya huduma ya Kikristo kwenye hatua hii iliyosonga sana ya kazi ya kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote. Wale wanaosisimuliwa na ufahamu mpya wa ndani zaidi na wenye kina zaidi wa Neno la Mungu waweza kushinda ugumu wa kufikia mioyo yenye kuona njaa. Na ndivyo ilivyo, iwe mtu amegawiwa mahali ambapo uvuvi mkubwa katika maana ya uvuvi wa kiroho waweza kutazamiwa au mtu anavumilia katika maeneo yaliyohubiriwa mara nyingi ambapo ubaridi wa kawaida waenea.

Jilishe Neno la Mungu kwa Ukawaida

Yale ambayo wengine wanafanya yaweza kukupa mawazo fulani juu ya jinsi unavyoweza kufurahia zaidi kawaida yako ya funzo au jinsi wewe na familia yako mwaweza kutumia wakati wa funzo kwa matokeo zaidi. Miongoni mwa mambo ambayo mtumishi wa Mungu hatapenda kukosa ni kusoma Neno la Mungu lenyewe kwa ukawaida. Wengi wameufanya uwe mradi wao kusoma angalau sura tatu hadi nne za Biblia kila juma. Je! wataka kusoma Biblia nzima katika mwaka mmoja? Basi utafurahia kutumia wakati mwingi zaidi kuisoma, labda nusu saa kila siku.

Je! umeisoma Biblia nzima zaidi ya mara moja? Kwa nini wakati huo mwingine usiweke mradi mpya? Ili kubadilisha, mwanamke mmoja Mkristo alisoma vitabu vya Biblia kulingana na mpangilio ambao viliandikwa. Yeye alipata kufahamu mambo mengi, yanayotegemea kronolojia, aliyokuwa amekosa kufahamu hapo kwanza. Mwanamke mwingine Mkristo ameisoma Biblia nzima mara tano katika muda wa miaka mitano iliyopita, kila wakati kutoka upande tofauti. Wakati wa kwanza, aliisoma yote. Wakati wa kusoma mara ya pili, alifanya muhtasari wa yaliyomo katika kila sura katika mstari mmoja au miwili katika kitabu cha kuandikia (daftari). Kuanzia mwaka wa tatu kuendelea, alianza kutumia Biblia ya marejezo ya chapa kubwa, kwanza akichunguza kwa uteuzi marejezo-mlinganisho yaliyo pambizoni na kisha kutoa uangalifu zaidi kwa vielezi-chini kutia na habari ya nyongeza. Mara ya tano, alitumia ramani za Biblia ili kuongeza uelewevu wa kijiografia. Yeye asema: “Kwangu mimi, kusoma Biblia kukawa jambo la kufurahisha kama kula mlo.”

Baadhi ya wanafunzi wa Biblia wenye hamu wamepata kwamba inanufaisha kuwa na nakala ya Biblia inayotumiwa kwa ajili ya funzo la kibinafsi tu, wakiandika kifupi katika mapambizo yayo maelezo yenye kupendeza, vielezi vyenye kuvuta fikira, au nambari za kurasa za vichapo vingine ambavyo waweza kurejezea baadaye. Mhudumu mmoja wa wakati wote huliona kuwa jambo la kufurahisha mwishoni mwa kila mwezi kuandika katika nakala yake ya funzo, mambo mapya ambayo amejifunza wakati wa mwezi huo. “Kutazamia mbele kwenye saa hizi zangu zenye thamani,” yeye asema, “hunisaidia nitimize miradi mingine ya mwezi upesi zaidi.”

Mawazo Fulani ya Busara

Je! wahisi kwamba ratiba yako imejaa mambo ya lazima ya kila siku na kila juma na kwamba unahitaji madokezo fulani ili utumie vizuri zaidi wakati wako mchache? Basi, chukua kile unachohitaji kusoma, na utumie kikamili pindi zako za starehe. Nyumbani, au mahali unapojifunza kwa kawaida, kwa kadiri iwezekanavyo panga vitabu na visaidizi vingine vya funzo ili viwe rahisi kufikiwa. Fanya mahali pako pa kujifunzia pawe penye starehe lakini si penye starehe mno hata usinzie. Je! una mgawo wa hotuba? Soma habari hiyo mapema iwezekanavyo, halafu uache mawazo yakujie unapostarehe au kufanya kazi mbalimbali.

Huenda wengine wakashirikiana nawe katika kutumia wakati vizuri zaidi kwa manufaa ya wote wawili. Kwa kielelezo, huenda ukamwomba mtu akusomee kwa sauti habari iliyo rahisi kuelewa unapofanya kazi mbalimbali au unapomwandalia chai msomaji wako mwenye fadhili. Vipi wote nyumbani wakikubaliana kuwa na wakati wa ukimya kwa ajili ya funzo la kibinafsi? “Umefurahia kusoma nini karibuni?” Nyakati nyingine huenda ukaweza kujua yale ambayo marafiki wako wamejifunza kwa kuanzisha mazungumzo kwa njia hiyo.

Je! unapendezwa kuanzisha mawazo mapya katika programu yako ya funzo? Waweza kuweka mradi wa wakati kwa ajili ya funzo kwa njia ileile ambayo wengi huweka mradi wa wakati wa kuzungumza juu ya Biblia na wengine. Mhubiri mmoja wa wakati wote (painia) huweka mradi wa kiwango kidogo wa saa wa kila mwezi wa funzo naye hufurahi kuona akitimiza mpangilio wa mradi wake. Wengine hupunguza wakati wanaotazama televisheni na kwa njia hiyo wanapata wakati wa funzo. Wengi huchagua kichwa cha funzo wanachofuatia kwa wakati fulani, kama vile matunda ya roho, maelezo ya vitabu vya Biblia, au ustadi wa kufundisha. Wengine hufurahia kufanyiza chati za kronolojia, kama zile zinazoonyesha uhusiano kati ya wafalme na manabii Waisraelia au Matendo ya Mitume na barua za Paulo.

Vijana, je! mwataka kuwa na imani yenye nguvu zaidi? Kwa nini msichague kichapo kwa ajili ya funzo la bidii wakati wa likizo yenu ya shule inayokuja? Mwanafunzi mmoja aliyebatizwa wa shule ya sekondari alichagua kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kilichochapishwa na Watch Tower Society. Sura baada ya sura, alifanya mihtasari mifupi katika kitabu cha kuandikia juu ya yale aliyojifunza. Lilikuwa jambo gumu na alichukua muda mrefu kuliko vile alivyokuwa amefikiri. Hata hivyo, alipomaliza kitabu kizima, alivutiwa sana na ukweli wa ujumbe wa Biblia.

Uwe na Hamu ya Kujifunza Nyakati Zote

Watumishi wengi wa Yehova wa kisasa walio waaminifu tayari wana “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58, NW) Hata ukiwa na ratiba iliyorekebishwa na jitihada za moyo mweupe, huenda ratiba unayofuata katika juma fulani isibadilike sana. Lakini, hamu yenye kuendelea kwa upande wako kupata uelewevu wenye kina zaidi juu ya kweli na kuendelea kujipatanisha na kule kufunuliwa kwa makusudi ya Yehova huleta mafanikio.

Ni jambo la kutia moyo kusikia juu ya thawabu za wale ambao wameboresha njia zao za kujifunza. Mwanamume mmoja Mkristo, aking’amua kwamba alikuwa akipoteza mtazamo ufaao kuelekea kutafuta uelewevu wa kweli wenye kina zaidi, alipanga maisha yake ili aweze kutoa wasaa wake mwingi zaidi katika funzo la kibinafsi. “Kumeniletea furaha ambayo sikuwa nayo hapo awali,” yeye asema. “Nikiwa na uhakika wenye kuendelea kukua juu ya utungaji wa kimungu wa Biblia, ninapata kwamba ninaweza kusema na wengine juu ya imani yangu nikiwa na idili halisi. Nahisi nikiwa nimelishwa vyema, mwenye afya kiroho, na mwenye uradhi mwishoni mwa kila siku.”

Mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova, anayezuru makutaniko mengi, alieleza manufaa mengine kwa njia hii: “Wale wenye bidii katika funzo la kibinafsi kwa kawaida huwa wachangamfu na wenye idili katika maelezo yao. Wao wana uhusiano mwema pamoja na wengine, na hawayumbishwi kwa urahisi na maneno yasiyofaa ya wengine. Wanapokuwa katika huduma ya shambani, wao huwa wenye kubadilikana na pia huwa macho kuona mahitaji ya watu wanaokutana nao.”

Yeye aongeza jambo ambalo wengine huenda wakataka kukumbuka wanapochanganua kawaida yao ya kujifunza. “Kwenye mikutano ya mazungumzo ya Kimaandiko, wengi huelekea kusoma maelezo yao kutoka kwenye ukurasa uliochapishwa. Wao wangeweza kunufaika zaidi ikiwa wangetafakari juu ya jinsi habari hiyo inavyohusiana na yale ambayo wametangulia kujifunza au na maisha yao wenyewe.” Je! wafikiri ungeweza kufanyia jambo hilo maendeleo?

Baada ya miaka zaidi ya 90 ya kuishi, nabii Danieli, hakuhisi kwamba alielewa mambo ya kutosha juu ya njia za Yehova. Katika miaka yake ya kumalizia, yeye aliuliza hivi kuhusu mambo ambayo yeye hangeweza kuelewa kikamili: “Ee Bwana wangu, mwisho wa mambo haya utakuwaje?” (Danieli 12:8) Hakuna shaka kwamba hamu hiyo isiyobadilika ya kujifunza mengi zaidi juu ya kweli ya Mungu ndiyo iliyomfanya akawa na uaminifu-maadili wenye kutokeza katika mwendo wake wote wa maisha wenye matukio mengi.—Danieli 7:8, 16, 19, 20.

Kila mmoja wa watumishi wa Yehova ana daraka lilelile la kusimama imara akiwa mmoja wa Mashahidi Wake. Nyakati zote uwe na hamu ya kujifunza ili uwe mwenye nguvu kiroho. Jaribu kutia jambo moja au mawili mapya katika ratiba yako ya kujifunza kibinafsi kila juma, kila mwezi, au kila mwaka. Ona jinsi Mungu atakavyobariki jitihada yoyote ndogo utakayofanya. Ndiyo, furahia funzo lako la Biblia la kibinafsi na matokeo linayoleta.—Zaburi 107:43.

[Maelezo ya Chini]

a Ukiwa msingi wa funzo lako lililopanuliwa, huenda ukapenda kutumia chati inayopatikana katika “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa” kurasa 294-297.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki