Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 8/1 kur. 21-26
  • Kutumikia Katika Tengenezo Lenye Kuendelea Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumikia Katika Tengenezo Lenye Kuendelea Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Siku za Mapema
  • Maisha Mapya Katika Betheli
  • Ushirika Pamoja na Ndugu Rutherford
  • Nyakati Zilizo Ngumu Kifedha
  • Kufanya Kazi kwa Redio
  • Kinanda
  • Kazi Yenye Shangwe Shambani
  • Mwongozo wa Kimungu
  • Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Maisha Yangu Katika Tengenezo la Yehova Lenye Kuelekezwa kwa Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Maisha Yenye Kuthawabisha Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Mbinu za Kuhubiri​—Kutumia Kila Njia Ili Kuwafikia Watu
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 8/1 kur. 21-26

Kutumikia Katika Tengenezo Lenye Kuendelea Zaidi

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ROBERT HATZFELD

Watu wengi sana leo huwasha televisheni kwa kutumia kidude cha kushikiliwa mkononi ili kutazama taarifa za habari za jioni katika rangi kamili, bila kuona hilo kuwa jambo la ajabu sana. Lakini yaonekana tu ni kama jana nilipokuwa kijana mwenye miaka 12 mwenye mshangao nikitazama sinema yenye picha kubwa sana ya mtu, naye alikuwa akiongea!

LABDA waweza kuwazia kwamba hiyo si habari ya maana sana. Lakini hakika hilo lililoonekana kwangu kama muujiza wa kisasa huko nyuma katika 1915, katika siku za mapema za sinema zisizotoa sauti na zilizo na rangi nyeusi na nyeupe tu. Mtu mmoja mwenye fahari aliye na kidevu alitokea kwenye kiwambo na kusema: “Photo-Drama of Creation imetokezwa na I.B.S.A., International Bible Students Association.” Kwa muda wa saa mbili zilizofuata, simulizi la Biblia lilisimuliwa mbele ya macho yetu. Ujumbe walo wa Kimaandiko ulikuwa safi na wenye kuburudisha. Lakini, ni sinema hiyo yenye picha za kusonga, ikiwa na picha zenye rangi katika visehemu, na sauti iliyopatana na picha iliyoninasa akili sana.

Sikutambua jambo hilo wakati huo, lakini shauku yangu ya ujana kwa ufundi huo ilikuwa mwanzo wa kazi-maisha katika tengenezo lenye kuendelea zaidi duniani.

Siku za Mapema

Mnamo 1891 baba yangu alitoka Dillenburg, Ujerumani, na kuja katika jumuiya ya Wajerumani katika Allegheny, Pennsylvania, Marekani. Baadaye alikutana na msichana mmoja wa familia ya Kijerumani huko, nao wakaoana. Nilizaliwa mnamo Julai 7, 1903, na nililelewa nikisema Kijerumani na Kiingereza. Kabla tu Vita ya Ulimwengu 1 kuanza katika 1914, ugonjwa ulioenea sana wa kifua-kikuu ulisababisha vifo vya wazazi wangu wote wawili na kuniacha yatima. Babu yangu akafa kutokana na maradhi ya ghafula karibu na wakati uo huo.

Kwa fadhili shangazi yangu, Minna Boemer, alinichukua kwa familia yake. “Nina watoto watano,” yeye alisema. “Naweza kuongeza mwingine mmoja tena.” Ingawa nilihisi kuwakosa wazazi, Shangazi Minna alinipa makao mazuri.

Shangazi yangu alikuwa mshiriki wa muda mrefu wa Kutaniko la Allegheny la Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana siku hizo). Kabla ya 1909, Ndugu C. T. Russell, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Society, pia alikuwa akihudhuria kutaniko hilo. Shangazi Minna alikuwa akinipeleka kwenye mikutano. Ingawa familia yetu haikuwa na jitihada sana ya kujifunza au kuhubiri wakati huo, tulieleza kivivi-hivi watu tuliowajua yale yote tuliyoyasikia mikutanoni.

Ilikuwa ni pindi hiyo ambapo ile “Photo-Drama” iliponishangaza sana. Kwa kuwa nilikuwa na mwelekeo wa kiufundi, mbinu hizo mpya na hali ya kupatanisha sauti na picha zilinivutia sana, kama ilivyokuwa vilevile na picha zilizofanywa zisonge kwa kasi. Kuona kufumbuka kwa maua kwa kasi kulisisimua kama nini!

Tulihuzunishwa na kifo cha Ndugu Russell mnamo 1916. Kwa kuwa tuliishi papo hapo Allegheny, tulihudhuria mazishi yake katika Carnegie Hall. Hilo lilikuwa ndilo jumba ambalo Ndugu Russell alikuwa amejadiliana na E. L. Eaton katika 1903. Nilikuwa nimesikia habari kuhusu mhudumu huyo Mwepiskopali wa Methodisti aliyemtolea wito C. T. Russell wajadiliane kwa siku sita, akitumaini kushusha heshima ya usomi wa Biblia wa Ndugu Russell. Badala ya hivyo, ilisemwa, Russell ‘alizima helo kwa maji.’ Sara Kaelin, kolpota ajulikanaye sana katika Pittsburgh, aliwajua akina Russell kibinafsi. Katika maziko alimwona Maria Russell akiweka maua katika jeneza yenye taarifa isemayo, “Kwa Mume Wangu Mpendwa.” Ingawa Maria alikuwa amemwacha miaka kadhaa mapema, bado alimtambua kuwa mume wake.

Miaka ilipoendelea kupita, nilikuwa na fursa nyingi za kupata ujuzi mwingi wa kiufundi ambao ungenisaidia kwa kazi-maisha yangu ya wakati ujao. Mjomba wangu, ambaye alikuwa mlezi wangu alikuwa mwana-kondarati. Katika pindi za likizo ya shule, aliniruhusu nifanye kazi pamoja na mafundi wake wa umeme, tukiingiza umeme badala ya kutumia mafuta-taa katika nyumba kubwa za zamani. Mnamo 1918 wanafunzi katika shule yetu walijitengenezea chombo cha redio-telegrafu. Tulikuwa tukikutana pindi za jioni kujifunza na kufanya majaribio na umeme pamoja na sumaku. Mnamo 1926 rafiki yangu mmoja pamoja nami tuliamua kufuatia ndoto yetu ya ujana—kufanya kazi katika meli na kusafiri ulimwenguni kote. Tulijiandikisha katika shule ya Shirika la Redio la Marekani kujifunza kuwa waendeshaji wa redio-telegrafu.

Maisha Mapya Katika Betheli

Shule ya redio tuliyohudhuria ilikuwa katika New York City, kwa hiyo nilikuwa nikisafiri kuvuka mto kwenda Brooklyn kwa ajili ya mikutano ya Wanafunzi wa Biblia, iliyokuwa ikifanywa katika jumba la kale lilikodishwa la Masonic Temple. Wakati huo, kulikuwa na kutaniko moja tu kwa ajili ya New York na viunga vyalo vyote. Ndugu kutoka Betheli (kao la familia ya makao-makuu ya Wanafunzi wa Biblia) walipojua kwamba nilikuwa nikisoma ili nipate leseni ya redio ya kibiashara, wao walisema: “Kwa nini uende baharini? Tuna stesheni ya redio apa hapa na twahitaji mwendeshaji wa stesheni hiyo.” Wakaniambia niende ofisini nikahojiwe. Sikujua chochote kuhusu Betheli ila tu kwamba ilikuwa makao makuu ya Wanafunzi wa Biblia.

Akina ndugu walinihoji nao wakapendekeza kwamba nimalize masomo yangu, nipate leseni, kisha nije Betheli. Baada ya kuhitimu, badala ya kupanda meli inayoelekea bahari kuu, nilipakia nguo zangu chache na kupanda gari-moshi la chini ya ardhi nikielekea Betheli. Ingawa nilikuwa nimejiweka wakfu kwa Yehova na nilikuwa nimeshiriki katika kazi ya kuhubiri kwa miaka mingi, sikubatizwa mpaka Desemba 1926, majuma mawili baada ya kufika Betheli. Hilo lilikuwa jambo la kawaida wakati huo.

Kukiwa na washiriki 150, Betheli ilijaa sana wakati huo. Tulikuwa na ndugu wanne katika kila chumba. Upesi nilipata kufahamu wengi wao, maana sisi sote tulikula, kufanya kazi, na kulala katika jengo moja, na bila shaka, sisi sote tulihudhuria kutaniko moja pekee lililokuwa katika New York City. Makao mapya ya Betheli yalikamilika katika barabara ya 124 Columbia Heights mnamo 1927, na tuliweza kuishi wawili-wawili katika chumba kimoja.

Vilevile katika 1927 kiwanda kipya katika barabara ya 117 Adams Street kilifunguliwa. Nilisaidia kuhamisha vifaa kutoka kiwanda cha zamani katika barabara ya 55 Concord Street. Kwa kuongezea vifaa vya redio, nilirekebisha lifti, matbaa za uchapishaji, vifaa vya dobi, meko ya kutumia mafuta katika kiwanda hicho—kama zilikuwa na waya za umeme.

Hata hivyo, Betheli ilikuwa zaidi ya kuwa kiwanda tu. Katika kutokezwa kwa kila kitabu, trakti, kila gazeti, kulikuwa na watumishi wengi wanyenyekevu na wenye kufanya kazi kwa bidii. Wao hawakuwa na lengo la kutambuliwa na kupata umashuhuri ulimwenguni. Badala ya hivyo, wao walitaka tu kutimiza kazi ya Bwana—na kulikuwa na mengi kwelikweli ya kufanya!

Ushirika Pamoja na Ndugu Rutherford

Nilinufaika sana na pendeleo la kufanya kazi pamoja na Joseph F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Sosaiti. Alikuwa mtu mwenye umbo kubwa, akiwa zaidi ya futi sita [sentimeta 183] kwa urefu, asiye mnene, lakini mwenye nguvu. Wengi wa ndugu wachanga katika Betheli walimwogopa kwa njia fulani mpaka walipomjua vizuri. Alikuwa akisoma nyakati zote, akitayarisha habari za kuchapishwa.

Ndugu Rutherford alikuwa mcheshi sana. Kulikuwa na dada kadhaa wenye umri mkubwa katika familia ya Betheli waliokuwa wamekuwa hapo tangu wakati wa Ndugu Russell. Walikuwa hawaonyeshi hisia zao nao waliamini kwamba haikufaa kucheka kwa sauti hata kama kulikuwa na jambo la kuchekesha. Nyakati nyingine wakati wa mlo mkuu Ndugu Rutherford angesimulia kichekeshi ambacho kingechekesha kila mtu, na hilo liliudhi sana dada hao wawili. Hata hivyo, mara nyingi aliongoza pia mazungumzo mazito ya Biblia wakati wa mlo.

Ndugu Rutherford alikuwa mpishi bora naye alifurahia kutayarishia marafiki wake mlo. Pindi moja wapishi wa Betheli walipasua mifupa fulani ya kuku walipokuwa wakikata kuku. Alienda jikoni na kuwaonyesha mara moja jinsi ya kukata kuku. Hakupenda vipande vya mifupa katika chakula chake!

Mara nyingi nilikuwa karibu na Ndugu Rutherford katika pindi zisizo rasmi, kama vile katika stesheni yetu ya redio, WBBR, au katika chumba chake cha kusoma katika Staten Island. Alikuwa mtu mwenye fadhili sana naye alitenda kulingana na yale aliyohubiri. Hakutarajia wengine wafanye yale ambayo yeye mwenyewe hangeweza kufanya. Akiwa tofauti na watu wengine wenye madaraka katika mashirika mengine mengi ya kidini, Ndugu Rutherford alikuwa na tabia ya hali ya juu sana ya kiroho na kiadili. Kwa wazi alijitoa kwa ajili ya Ufalme wa Yehova.

Nyakati Zilizo Ngumu Kifedha

Miaka michache baada yangu kwenda Betheli, ulimwengu ulitumbukia katika ule Mshuko Mkuu wa Kiuchumi. Masoko ya kifedha yakaanguka, na bei za bidhaa nazo zikaharibika. Kazi zilikuwa chache sana, na hakukuwa na fedha za kutosha. Betheli iliendelea kwa michango ya kifedha, na nyakati zote Yehova alihakikisha kwamba kulikuwa na fedha za kutosha za kushughulikia kazi. Hatukukosa chakula kamwe, ingawa huenda hakikuwa hasa kile ambacho kila mmoja angependa. Tuliishi kwa chakula kidogo kadiri ilivyowezekana, na ndugu nje ya Betheli walitusaidia kadiri walivyoweza.

Mnamo 1932, Ndugu Robert Martin, mwangalizi mwaminifu wa kiwanda chetu alikufa. Nathan Knorr mwenye umri wa miaka 27 aliwekwa rasmi kuchukua mahali pake. Alikuwa kijana mwenye uwezo mwingi sana. Sikumbuki kama kulikuwa na mtu aliyeona ugumu wa kumkubali kuwa mwangalizi wa kiwanda. Ndugu wengine waaminifu, miongoni mwao John Kurzen, George Kelly, Doug Galbraith, Ralph Lefller, na Ed Becker—wote wafanyakazi wenzangu wapenzi—kwa hiari walitia ufundi wao na ujuzi wao katika utumishi wa Ufalme.—Linganisha Kutoka 35:34, 35.

Kufanya Kazi kwa Redio

Tengenezo letu lilijitoa kabisa kueneza habari njema kwa njia yoyote iliyopatikana. Ulimwengu mzima ulihitaji kujua juu ya Ufalme, lakini tulikuwa maelfu machache tu. Ufundi wa Redio ulikuwa ndio unaanza baada ya Vita ya Ulimwengu 1. Hata hivyo, ndugu wenye utambuzi walihisi kwamba njia hiyo ya kuwasiliana ilikuwa ndiyo andalio la Yehova kwa wakati huo. Kwa hiyo mnamo 1923 walianza kujenga stesheni ya redio ya WBBR katika Staten Island, mojapo wilaya tano za New York City.

Nyakati nyingine nilikuwa nikiendesha stesheni yetu peke yangu. Niliishi hapo katika Staten Island lakini nilikuwa nikisafiri kwa muda wa saa tatu kwa feri na gari-moshi kwenda na kurudi kutoka kiwanda kilichokuwa Brooklyn ili kufanya kazi za umeme na za kiufundi. Ili kufanya stesheni yetu ya redio ijitegemee kabisa, tuliweka mtambo wa genereta wenye kutumia dizeli. Pia tulikuwa na visima vyetu wenyewe vya maji katika Staten Island pamoja na shamba la mboga lililotoa chakula kwa wafanyakazi wachache huko, na vilevile pamoja na familia ya Betheli iliyoko Brooklyn.

Mpaka nilipopata msaada baadaye, madaraka yangu ya kazi ya redio yalipunguza sana kuhudhuria kwangu mikutano na utumishi wangu wa shambani. Hakukuwa na wakati wowote kwa ajili ya mambo ya kijamii au ziara za miisho-juma ila tu kwa ajili ya likizo ya kila mwaka. Mtu mmoja alipata kuniuliza hivi: “Ukiwa na ratiba yenye kudai mno hivi, je, hukufikiria kuacha Betheli?” Kwa unyoofu, ilikuwa lazima niseme: “La.” Limekuwa pendeleo na shangwe kuishi na kufanya kazi pamoja na ndugu na dada wengi waliojitoa. Na nyakati zote kulikuwa na kazi ya kufanywa, mradi mpya wa kuanzishwa.

Tulitokeza na kutangaza drama za redio zenye kuchochea sana. Bila vyombo vya kutokeza sauti za kipekee katika kurekodi, tulilazimika kubuni mbinu zetu wenyewe. Tulitengeneza mashine ambayo ingefanyiza sauti ya upepo mwanana au dhoruba inayokumba. Sauti ya vipande viwili vya vifuvu (vifuniko vya nazi) vikipiga ubao uliofunikwa ilitokeza sauti ya nyayo za farasi wakikimbia kwenye barabara za mawe. Kila drama ilikuwa kazi ya kustaajabisha sana. Na watu walisikiliza. Katika siku hizo zenye vikengeusha-fikira vichache, watu wengi waliketi na kusikiliza kwa makini.

Katika miaka ya 1920 na mapema katika miaka ya 1930, Sosaiti ilifanyiza historia, ikiunganisha mara kwa mara hesabu kubwa sana za stesheni kwa programu moja tu. Kwa njia hiyo habari za Ufalme zilifikia mamilioni ulimwenguni pote.

Kinanda

Katika miaka ya kati ya 1930 na miaka ya mapema ya 1940, tulibuni na kutengeneza mashine za santuri, vinanda, na vifaa vingine vya sauti. Kwa kutumia kikatio cha kipekee, tulikata rekodi za kunakiliwa kutoka kwa diski zenye ulaini kama kioo na zinazotokana na nta ya nyuki. Kisha tulichunguza kila rekodi ya kunakiliwa kwa uangalifu kwa kutumia darubini ili kuhakikisha kwamba haikuwa na kasoro yoyote. Kama kulikuwa na kasoro yoyote, ilikuwa lazima kipindi cha kurekodi kirudiwe na rekodi nyingine ikatwe na kikatio. Kisha tulipeleka rekodi hiyo ya nta ya nyuki kwa kampuni ya kurekodi, iliyotokeza kinanda na santuri.

Tukio moja lenye kusisimua sana ninalokumbuka vizuri sana lilikuwa hotuba ya Ndugu Rutherford katika 1933 yenye kichwa “Matokeo ya Mwaka Mtakatifu kwa Amani na Ufanisi.” Papa alikuwa ametangaza mwaka huo kuwa “mwaka mtakatifu,” na kwa matangazo ya redio na kinanda, tulifichua jambo hilo nasi tukaonyesha kwamba hakuna kitu kitakatifu kingetokana nalo. Kama ilivyotokea, Hitler alichukua mamlaka mwaka huo akiungwa mkono na Kanisa Katoliki, kwa hiyo tumaini lolote la amani likapotea.

Kule Marekani, Kikundi cha Katoliki kilifanyizwa ili kutekeleza kile ambacho kanisa lilitaka. Waliweka watu wao wenyewe katika kamati za wahariri wa magazeti ya habari yaliyo mashuhuri, na za wachapishaji wa vitabu. Walijiingiza katika siasa na kutisha kususia stesheni yoyote ya redio inayotangaza hotuba za Biblia. Mashahidi wengi walifanyiwa ghasia na vikundi vya Kikundi cha Katoliki, hasa katika sehemu iliyokuwa karibu ya New Jersey. Hizo zilikuwa siku zenye misisimuko kama nini!

Kazi Yenye Shangwe Shambani

Kufikia miaka ya kati ya 1950, wahubiri wa Ufalme waliokuwa wakiongezeka walikuwa wakifikia watu wengi zaidi milangoni pao wenyewe. Hilo lilikuwa na matokeo zaidi kuliko redio katika kusaidia watu kuelewa kweli ya Biblia. Kwa hiyo katika 1957 iliamuliwa kwamba WBBR iuzwe na tutumie mali katika kupanua kazi ya umishonari katika nchi nyinginezo.

Katika 1955, nilipewa mgawo wa kwenda Kutaniko la Bedford katika Brooklyn, ambako nilikuwa nikiongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida. Sosaiti pia ilinituma nje kuwa msemaji anayezuru kwenda kaskazini mwa New York, Pennsylvania, Connecticut, na New Jersey. Nilipopewa mgawo wa kwenda Kutaniko la Bedford, nilijiambia hivi, ‘Ninazidi miaka 50 kwa umri. Ni afadhali nishiriki kwa kadiri niwezavyo katika utumishi wa shambani sasa. Baadaye naweza kupata maumivu ya viunoni na nisifurahie utumishi kadiri hiyo.’

Baada ya kufanya kazi miaka hiyo yote kwa upande wa kiufundi wa kutangaza mbegu ya Ufalme kupitia redio, nilifurahia sana kupanda na kutia maji mbegu za kweli ya Biblia moja kwa moja kwa watu mmoja-mmoja. Nilifurahia sana kufanya kazi pamoja na kutaniko. Watu tofauti-tofauti walinifanya kuwa sehemu ya familia zao, wakinifanya nijihisi nyumbani. Baadhi ya watoto hao wachanga, sasa wakiwa wamekua, wangali wakiniita babu. Kwa miaka 30 tulikuwa na pindi zenye kufurahisha pamoja katika huduma ya shambani, mpaka matatizo ya mikono na miguu yangu yaliponifanya nisiweze kupanda ngazi wala kusafiri katika gari-moshi ya chini ya ardhi. Mnamo 1985, nilihamia Kutaniko la Brooklyn Heights, linalokutana papo hapo Betheli.

Tengenezo la Yehova lilipoendelea kupanuka sana, mimi binafsi nilipata pendeleo la kuona baraka zake katika mashamba ya kigeni nilipohudhuria mikusanyiko mikubwa ya Mashahidi wa Yehova katika nchi za mbali. Hata niliweza kusafiri ulimwenguni! Kuanzia miaka ya 1950, baadhi yetu sisi Wanabetheli tuliweza kuona London, Paris, Rome, Nuremberg, na Copenhagen. Tulisafiri kwa ndege za kijeshi zilizobadilishwa kuwa za abiria, mashua, na gari-moshi. Bila shaka, safari hizo zilikuwa na mandhari zenye kuvutia lakini mwono wenye kusisimua kuliko wote ulikuwa umati mkubwa wa ndugu wachangamfu wenye ukaribishaji. Miongo ya miaka baadaye nilizuru sehemu ya Mashariki, Ulaya Magharibi tena, na karibuni zaidi Ulaya Mashariki. Mikusanyiko ya ajabu katika Poland, Ujerumani, na Chekoslovakia ilifana sana. Familia yetu ya kitheokrasi imekua kama nini tangu niwe mshiriki wayo kwa mara ya kwanza!

Mwongozo wa Kimungu

Jambo lililoonekana kuwa hatua ndogo-ndogo zilizokuwa zikichukuliwa na tengenezo baadaye likawa hatua kubwa-kubwa. Tulipokuwa tukishughulikia miradi mipya, vyombo vya kutusaidia tu kuhubiri, ni nani angeweza kuona kimbele ukuzi huo mkubwa? Tumesonga mbele kwa imani, tukiitikia mwongozo wa Yehova.

Tengenezo hili lenye kuendelea halijasita kutumia ufundi wa kisasa unaopatikana au kujifanyizia ufundi walo lenyewe ili kutunza shamba la ulimwenguni pote. Miongoni mwa njia zitumiwazo kuendeleza utangazaji wa Ufalme zimekuwa mahubiri ya nyumba kwa nyumba, matumizi ya stesheni za redio zilizounganishwa, ushahidi wa kinanda, na programu ya kuongoza mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu. Kuanzisha uchapishaji wetu wenyewe katika siku hizo za mapema na sasa kutumia uchapishaji wa kutumia kompyuta wa phototypesetting na offset katika lugha nyingi si matimizo madogo. Watchtower Bible School of Gilead, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na mikusanyiko ya kawaida yote imechangia kumletea Yehova Mungu na Mwana wake utukufu. Limekuwa pendeleo langu kuyaona binafsi matukio hayo yote na hata kuyashiriki.

Ni wazi kwangu kwamba tengenezo la Yehova lililo duniani lenye kuongozwa na roho huongozwa kwa mambo yale yatakayofanywa na jinsi ya kuyafanya. Tengenezo lake lote la ulimwengu wote mzima, lionekanalo na lisiloonekana, lafanya kazi pamoja.

Sijapata kamwe kusikitika kwa sababu ya kuachilia mbali mipango yangu ya kuabiri zile bahari kuu. Kwani, maendeleo yenye kusisimua zaidi na yenye maana zaidi ulimwenguni yanatendeka katika tengenezo la Yehova! Kwa hiyo safari yangu njiani kuelekea “mwito wa kwenda juu” imekuwa yenye shangwe nyingi sana na baraka bila masikitiko.—Wafilipi 3:13, 14, NW.

Nyakati zote mimi hueleza vijana wakumbuke 1914—yaani Zaburi 19:14, lisemalo: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA, mwamba wangu, na mwokozi wangu.” Twataka kumpendeza Yehova kwa kila kitu na kusali kama Daudi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu, nakungoja Wewe mchana kutwa.” (Zaburi 25:4, 5) Kuna umaana mwingi katika maneno hayo. Kuyakumbuka kwaweza kutusaidia kubaki katika njia ya kweli, kwenda upande ufaao, sambamba na tengenezo lenye kuendelea la Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ndugu Rutherford alifurahia kutayarishia marafiki mlo

[Picha katika ukurasa wa 25]

Robert Hatzfeld akiwa kwenye mitambo ya stesheni ya redio ya WBBR

[Picha katika ukurasa wa 26]

Picha ya karibuni ya Ndugu Hatzfeld

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki