Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Mungu
Kama ilivyosimuliwa Grant Suiter
MWAKA wa 1922, nilipokuwa mwenye miaka 14, baba yangu alihamisha jamaa yetu kutoka Chicago, Illinois, mpaka Kalifornia. Tulipokuwa safarini tulitembelea marafiki wa zamani katika Idaho. Walituarifu kwamba katika Kalifornia kulikuwako watu waliokuwa wakisema kwamba, kulingana na Biblia, mamilioni ya watu waliokuwa wakiishi wakati huo hawangekufa kamwe.
Muda mfupi baada ya kufika Kalifornia tuliona katika gazeti moja tangazo “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Hicho kilikuwa kichwa cha hotuba ya watu wote ambayo ingetolewa katika San Jose. Kwa njia hiyo baba yangu akawapata Wanafunzi wa Biblia (kama ambavyo Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakijulikana wakati huo), na yeye akaanza kutupeleka kwenye mikutano yao ya watu wote.
Mama alitaka mimi nijihusishe na Sunday school ya kanisa fulani. Ingawa baba yangu alikuwa mwenye kulaumu wahubiri wa madhehebu yote, alikubali kwamba huenda jambo hilo likawa la faida kwangu. Kwa hiyo nikawa mhudhuriaji wa kawaida wa Sunday school ya Methodisti. Mwishowe nikawa mweka-hazina wa shule hiyo na mchezaji wa timu yake ya mpira wa vikapu. Wakati uo huo, jamaa yetu ilihudhuria hotuba za watu wote zilizofanywa na Wanafunzi wa Biblia katika San Jose, maili chache tu kutoka nyumbani mwetu katika Santa Clara.
Baba yangu alitaka kuona hali zikifanywa nafuu na kwa sababu hiyo alifanya kampeni kwa ajili ya wagombea uchaguzi wa kisiasa mbalimbali, hata akaandika jina la mmoja wao kwenye kioo cha mbele cha motokaa yetu aina ya Model T Ford. Kwenye mikutano Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakimwambia kwa fadhili kwamba tumaini halisi la wanadamu halikuwa katika jitihada za kisiasa bali katika Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo Yesu. Baba alikuwa akikubali kidogo lakini akisema kwamba, ingawa hiyo ilikuwa ni sawa kwa wakati ujao, kwa wakati huu angependa kufanya mambo yawe mazuri iwezekanavyo kupitia njia za kisiasa. Muda si muda, hata hivyo jamaa yetu yote—mama, baba, dada na mimi—tukaanza kuthamini zaidi kweli ya Biblia na matakwa ya Neno la Mungu.
Ukuzi wa Kiroho
Mwishowe singeweza kuendelea kwa dhamiri safi katika Sunday school ya Methodisti, na kwa hiyo nikajiuzulu. Kufikia mwaka 1923 jamaa yetu ilikuwa imehamia Oakland kilomita chache mbele, ambako baba yangu aliendesha duka dogo la mboga nami nikahudhuria shule ya sekondari. Nilipojifunza kwamba Wanafunzi wa Biblia hawakuvuta sigara, nilijaribu kumbembeleza Baba aache kuuza sigara katika duka lake. Hakukubaliana na mimi lakini alizungumza juu ya hilo na mmoja wa Wanafunzi wa Biblia, Robert Craig.
Baada ya mazungumzo hayo baba yangu aliamua kuuza biashara yote na kuhama Oakland. Uamuzi wake pia ulichochewa na jitihada za kikundi kimoja za kumwingiza katika biashara ya kutengeneza pombe ya haramu, jambo ambalo alijua halikupatana na aliyokuwa akijifunza kupitia Eklesia ya Oakland (Kundi) ya Wanafunzi wa Biblia. Karibu wakati uo huo, kwa ruhusa ya wazazi wangu, niliacha shule ya sekondari baada ya mwaka mmoja na nusu tu wa kuihudhuria kwa sababu ya uvutano wa kukosa adili katika shule.
Tulihamia maili chache mpaka Mountain View, karibu vya kutosha na San Jose kuweza kuhudhuria mikutano ya eklesia huko kwa mara nyingine. Baba yangu aliendesha duka jingine, nami nilifanya kazi humo wakati wote, bila kupokea mshahara wo wote lakini nikimsaida tu. Baba aliandikisha Mnara wa Mlinzi na The Golden Age (sasa linaitwa Amkeni!), nami nilifurahia hasa The Golden Age kama nini! Nilikuwa na maoni kwamba nilikuwa nikipata habari zaidi kutoka kwalo zaidi ya ambazo ningalipata kama ningaliendelea na shule ya sekondari.
Mikutano ya eklesia ilikuwa inakuwa yenye kupendeza zaidi na zaidi kwangu. Nilivutiwa hasa na makala katika toleo la Machi 1, 1925 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa.” Habari iliyokuwamo ilikuwa hatua kubwa ya kusonga mbele katika ufahamu wa Wanafunzi wa Biblia kuhusu Ufalme wa Yehova mikononi mwa Kristo Yesu, yaani, ulikuwa umekwisha kusimamishwa mbinguni mwaka wa 1914. Katika wakati huo jamaa yetu ilikuwa inakuwa yenye urafiki wa karibu na Wanafunzi wa Biblia katika Mountain View, ikitumia wakati mwingi pamoja nao katika nyumba zao.
Mwishowe tulijifunza kwamba sala haikuwa sehemu ya mikutano ya eklesia tu bali pia marafiki walisali katika nyumba zao za kibinafsi, kutia ndani kutoa shukrani wakati wa chakula. Jambo la kusifika ni kwamba baba yangu alitaka kuiona sala kwa maoni yanayofaa. Kwa ujumla yeye alikuwa ameiona kuwa ya unafiki. Nakumbuka nikiwapo wakati sala ilipokuwa ikizungumzwa na yeye na mmoja wa Wanafunzi wa Biblia aliyekuwa akitembelea duka lake. Mgeni huyo alitaja jinsi tunavyopaswa kumtolea Yehova Mungu shukrani kwa ajili ya baraka zetu. Lakini baba yangu alimuuliza ni kwa sababu gani tunapaswa kumshukuru Yehova kwa ajili ya baraka zetu zote na tusimlaumu kwa ajili ya matatizo yetu yote. Hata hivyo, mwishowe, tukiwa jamaa, tulielewa sala kwa njia nzuri na kutumia kabisa kwa faida uandalizi huo wa upendo.
Uandalizi wa eklesia ambao nilifaidika nao sana ilikuwa Shule ya Manabii. Huo ulikuwa mkutano wa wazee na watu wengine wa kiume kwa kusudi la kupokea mazoezi ya kuzungumza mbele ya watu wote. Mwanafunzi angetoa hotuba ambayo alikuwa ametayarisha juu ya habari fulani aliyogawiwa, na wale wengine wangempa mashauri ya kusaidia. Hata hivyo, kutolewa makosa kwa njia yenye kusaidia nilikopata kwenye shule hiyo hakukuwa kitu kukilinganishwa na kule ambako nilipata binafsi kutoka kwa baba yangu baada ya yeye kuhudhuria kipindi mojapo anisikilize nikijaribu kutoa hotuba.
Jamaa yetu na mimi tulisaidiwa sana na mapiligrimu, ambao walikuwa mawakili wa pekee wa Sosaiti. Maeklesia yalitoa maombi ya kila mwaka kwa Sosaiti ili watembelewe nao. J. A. Bohnet alinivutia hasa na alinisaidia kipekee. Yeye alikuwa mwanamume aliyekuwa na sifa ambazo zilimfanya apendeke sana kwa watu fulani lakini kwa wengine matokeo yalikuwa kinyume. Yeye alimpenda Yehova, na kwa wazi alikuwa mwenye kiasi, lakini kidogo alificha sifa hiyo kwa kuwa mkali-mkali.
Ubatizo na Huduma ya Kikristo
Ilikuwa hotuba iliyotolewa na Ndugu Bohnet katika nyumba ya mmoja wa Wanafunzi wa Biblia ndiyo iliyokuwa na matokeo mazuri maishani mwangu. Nilipokuwa nikimsikiliza akisema juu ya mapendeleo ya kumtumikia Yehova na daraka la kufanya hivyo, nikatambua ninayopaswa kufanya na ambayo nilitaka kufanya. Kwa hiyo nikajiweka wakf binafsi kwa Yehova, na karibu wakati uo huo wale washiriki wengine wa jamaa yetu wakafanya hiyo. Katika Octoba 10, 1926, katika San Jose, Kalifornia, sisi sote pamoja tulionyesha wakf wetu kwa Yehova Mungu kwa kuzamishwa katika maji.
Ubatizo wakati huo ulikuwa ukifanywa tofauti kidogo na leo. Mzee aliyekuwa akiufanya ubatizo aliniambia hivi: “Ndugu Grant, katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, sasa nakubatiza wewe katika Kristo.” Kila mmoja wetu aliyekuwa akibatizwa tulivaa kanzu fupi nyeusi zenye kutoka shingoni mpaka kwenye vifundo vya miguu, za mikono mifupi. Ili kuhakikisha kwamba kanzu hiyo haingeruka juu na ili imfunike mwenye kubatizwa kwa kiasi, katika sehemu ya chini iliwekwa uzito mkubwa kwa vyuma vya risasi.
Baada ya ubatizo, na baada ya kuvaa nguo, baba yangu alimwambia mzee aliyekuwa akisimamia ubatizo: “Ninyi huenda nje na vitabu, sivyo? Sisi pia twataka kufanya hivyo, sasa.” Kwa hivyo jamaa yetu ikaanza kwenda nje kwenye huduma ya shambani.
Mara yangu ya kwanza katika utumishi wa shambani ilikuwa wakati mzee mmoja, H. O. Lawrence, alipopanga kunipeleka. Alinipa vijitabu fulani halafu akaendesha motokaa mpaka kwenye eneo katika San Jose. Nilifikiri angefanya kazi pamoja na mimi nyumba kwa nyumba, lakini aliniambia nitoke ndani ya motokaa akasema, “Sasa wewe fanya upande huu wa nyumba hizi.” Kisha akaendesha motokaa akaenda zake. Kwa hiyo nikafanya upande huo wa nyumba hizo nikaangusha vijitabu vitatu kwa mchango wa senti 25 (za Kiamerika) nikawa mwenye furaha sana. Kama matokeo ya kushiriki hivyo katika huduma ya Kikristo, nikajisikia kweli kweli kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu.
Karibu na wakati huu tukapokea maagizo katika mwelekezo wetu wa kila mwezi wa utumishi The Bulletin (sasa inaitwa Huduma ya Ufalme Yetu) tumweleze mwenye nyumba jambo fulani kuhusu tengenezo la Shetani. Kwa hiyo watu walipotaka niende zangu kwa kuniambia hawakupendezwa kwa kusisitiza kidogo niliendelea kuwaambia juu ya kuwapo kwa tengenezo la Ibilisi na uharibifu walo unaokuja. Hiyo ilikuwa tofauti kubwa na mahubiri yetu ya kawaida juu ya taraja la kuishi milele juu ya dunia-Paradiso bila kuwa na lazima ya kufa kamwe.
Eklesia ya San Jose ilikuwa ikisafiri miendo mirefu ili kufikia watu kwa ujumbe wa Ufalme. Vilivyokuwa vikiitwa vikundi vya kutembelea watu vilienda nje kwa ukawaida katika Santa Clara Valley na vilima vilivyokuwa karibu-karibu. Naweza kukumbuka ardhi kwa umbali wote ambao macho yangeweza kuona ikiwa imefunikwa na miti ya matunda iliyochanua. Tulikuwa tukichukua chakula na kutumia siku nzima, nyakati nyingine tukasafiri kilomita 121 au zaidi ili tufike kwenye sehemu ambayo tungetoa ushuhuda.
Kituo cha Radio cha KFWM katika Oakland kilitumiwa kwa miaka mingi kuutangaza ujumbe wa Ufalme, na maeklesia mbalimbali katika eneo la ujirani yalipokezana zamu kutoa programu kwa kituo hicho mwishoni mwa juma. Nilikuwa na pendeleo la kusoma hotuba za Biblia kwenye vyombo vya kutangazia vya KFWM, kama ile ya Julai 24, 1927. Herufi za kutaja kituo hicho cha redio zilionekana kuwa zenye kufaa kuwa herufi zenye kusimamia ‘Kingdom For World of Mankind’ (‘Ufalme Kwa Ajili ya Ulimwengu wa Wanadamu’).
Kupanua Utumishi Wangu
Siku moja tulipokuwa tukiendesha motokaa kurudi nyumbani kutoka kwenye mkutano mmoja, Ndugu Lawrence, ambaye ndiye kwa mara ya kwanza alikuwa amenipeleka kwenye utumishi wa shambani, alinipa karatasi ya maombi ya kutumikia katika makao makuu ya Brooklyn, New York. Wakati fulani kabla ya hapo, muda mfupi baada ya ubatizo wetu, nilikuwa nimesikia baba yangu akimwambia mama kwamba kama angalikuwa mimi angefanya utumishi wa Yehova kuwa kazi ya maishani mwake. Mimi, pia, nilitaka hivyo, na mimi nilikuwa na maoni kwamba kwa kutoa maombi ya Betheli nafasi ilitolewa kwangu kufanya hivyo.
Toleo la Mei 15, 1928 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilitangaza kwamba tangu Julai 30 mpaka Agosti 6 kungekuwako kusanyiko la mataifa yote la Wanafunzi wa Biblia katika Detroit, Michigan. Nilikuwa nataka sana kuhudhuria, na jamaa yetu na marafiki walifanya iwezekane kwangu kufanya hivyo. Wakati wa kusanyiko hili Donald Haslett, mwandishi wa J. F. Rutherford, msimamizi wa Sosaiti, alitangaza kutoka jukwaani kwamba akina ndugu walikuwa wakihitajiwa kwa ajili ya utumishi wa Betheli. Yeye alisema kwamba wale waliokuwa wakitaka kufanya maombi wangeweza kuhojiwa na Ndugu Rutherford. Nilikubali, nikajaza maombi mengine ya Betheli, na Ndugu Rutherford akaniambia niripoti katika Betheli Agosti 13, 1928.
Kwa ujumla, tulioripoti kwa ajili ya utumishi wa Betheli katika Agosti 13 tulikuwa 13. Hiyo ilikuwa juma moja tu baada ya kusanyiko la Detroit. Wakati huo washiriki 95 wa jamaa ya Betheli walikuwa wakifanya kazi katika utengenezaji na utumaji wa vitabu vya Biblia kwenye kiwanda kilichokuwa kimetoka tu kumalizwa cha 117 Adams Street, na wachache kidogo walikuwa wakifanya kazi katika makao ya Betheli na afisi mbalimbali za Sosaiti. Kazi yangu ya kwanza katika Betheli ilikuwa ni kuondoa vijitabu katika mashine iliyotumiwa kukunja vitabu baada ya kushikanishwa na majalada kwa viunganishaji vya waya. Nilifanya kazi katika matbaa kwa muda unaopungua juma mbili nilipohamishwa kwenye afisi, Idara ya Utumishi. Kushiriki katika utendaji huo kweli kweli kulinipa wazo la kusonga mbele pamoja na tengenezo la Mungu.
Kwa kuwa sikuwa na mahali pa kwenda wakati wa likizo yangu ya kwanza, mwaka wa 1929, niliitumia nikiwa Betheli. Kwa hiyo nilikuwapo Ndugu Rutherford alipotoa hotuba yake ya kwanza katika Masonic Temple huko Brooklyn juu ya Yehova kuruhusu uovu na kuondolewa lawama kwa jina Lake. Kabla ya wakati huo hatukufahamu jambo hilo, na kwa hiyo hotuba ya Ndugu Rutherford ilikuwa maelezo yenye kusisimua juu ya habari hiyo ya msingi yenye maana.
Kusonga Mbele Katika Miaka ya Kuanzia 1930
Jambo kubwa kweli kweli la mwaka 1931 lilikuwa ni kupokea jina Mashahidi wa Yehova, kwa njia hiyo kutoa jina lenye kuunganisha watu wote wa Mungu. Mwaka uliofuata neno la kutambulisha kundi la watu wa Mungu lilibadilishwa kutoka “eklesia” likawa “kampuni,” badiliko ambalo msingi wake ulikuwa kufikiria Zaburi 68:11 (Authorized Version). Kwa hiyo ulimwenguni pote tulikuwa na “makampuni” ya Mashahidi wa Yehova wala si “madarasa,” wala “maeklesia.”
Mwaka wa 1932 baba yangu aliacha biashara yake katika Kalifornia, na yeye, mama yangu na dada yangu tukaingia utumishi wa painia. Walijijengea motokaa-nyumba, na kwa miaka 20 iliyofuata ilitumika ikiwa nyumba ya painia kwa wazazi wangu. Dada yangu, Grace, alitumikia pamoja nao mpaka 1939 alipoalikwa awe mshiriki wa jamaa ya Betheli ya Brooklyn. Aliendelea kutumikia huko, na tangu 1959 ni mke wa Simon Kraker.
Msimamizi wa kiwanda, Robert J. Martin, alikufa Septemba 23, 1932, na Nathan H. Knorr akawekwa na Ndugu Rutherford mahali pake. Ndugu Knorr hapo mbele alikuwa katika meza ya kushughulikia upelekaji-haraka wa vichapo.
Mwaka uliofuata taabu zenyewe zikaanza kwa watu wa Mungu. Katika Januari 30, 1933, Adolf Hitler akawa mtawala wa Ujeremani, na katika Juni 28, 1933, tawi la Ujeremani la Sosaiti katika Magdeburg likatwaliwa na kufungwa. Papa Pius wa 11 alitangaza mwaka 1933 kuwa “Mwaka Mtakatifu,” na Ndugu Rutherford upesi baada ya hapo akazungumza kwa njia ya vituo vya radio zaidi ya 55 kuhusu “Matokeo ya Mwaka Mtakatifu juu ya Amani na Fanaka.” Lilikuwa pendeleo langu kuwa mtangazaji wake wa radio katika programu hiyo.
Katika miaka ya kwanza-kwanza ya 1930 upinzani mkubwa juu ya kazi yetu ulisitawi na kulikuwako mateso yenye kuenea sana. Mashahidi wa Yehova walipangwa katika “vikundi-vikundi” kwa ajili ya kusudi la kutoa ushahidi kamili katika maeneo ya matata. Katika Ujeremani mateso yaliongezeka sana hata kwamba katika Oktoba 7, 1934, makampuni ya watu wa Mungu katika nchi nyingi yakampelekea Hitler simu za barua zenye kumwonya aache jambo hilo.
Katika wakati huo kulikuwako mazungumzo mengi kati ya watu wa Mungu kuhusu ni nani “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9. Kwa ujumla ilikuwa ikiaminiwa wakati huo kwamba wao walikuwa jamii ya pili, ya kimbingu, yenye uaminifu kidogo. Katika funzo la Betheli moja, lililoongozwa na Ndugu T. J. Sullivan, niliuliza: “Kwa kuwa mkutano mkubwa utapata uzima wa milele, je, wale ambao ni washiriki wa kikundi hicho wanadumisha ukamilifu?” Kulikuwako maelezo mengi lakini hakukuwa jibu kamili. Nilipoulizwa nitoe maelezo yangu mwenyewe nilisema kwamba nilikuwa nikitaka tu kupata jibu ndiyo au hapana.
Katika Mei 31, 1935, kwenye kusanyiko la Washington, D.C., Ndugu Rutherford alizungumza juu ya habari iyo hiyo. Nilikuwa nimeketi juu nikitazama chini ambako kulikuwa umati, na ilisisimua kama nini hotuba yake ilipokuwa ikiendelea kufunua! Mkutano mkubwa ulitambulishwa waziwazi Kimaandiko kuwa ni wale watakaookoka Har–Magedoni wakiwa na taraja la kuishi milele duniani. Ndiyo, hayo yalikuwa maelezo zaidi juu ya “mamilioni wanaoishi sasa ambao hawatakufa kamwe.’
Katika Julai 12, 1937, niliwekwa na Ndugu Rutherford niwe mtumishi wa Betheli. Katika ile miaka minne na nusu ya mwisho ya maisha ya Rutherford nilikuwa na pendeleo la kufanya kazi karibu-karibu na yeye. Mwishoni-mwishoni mwa 1937 jina la The Golden Age lilibadilishwa likawa Consolation (Faraja), jambo hilo likafanya Ndugu Rutherford aseme jambo la kuchekesha nilipokuwa nikimwendesha kwa motokaa huko Scranton, Pennsylvania, karibu na mji wa nyumbani kwa C. J. Woodworth, mhariri wa gazeti hilo. Ilikuwa vigumu kupitia Scranton kwa motokaa katika siku hizo, na akimtaja Ndugu Woodworth kama “Woody,” Rutherford alisema: “Si ajabu Woody anataka faraja, kwani anaishi mahali kama hapa.”
Vita ya Ulimwengu ya Pili—Kipindi cha Majaribu
Katika Septemba 1939 Vita ya Ulimwengu ya Pili ilitokea. Katika Oktoba afisi ya tawi yetu ya Paris ilifungwa na kazi yetu ikapigwa marufuku katika Ufaransa. Mwaka uliofuata Kanada ikapiga marufuku kazi yetu. Katika kiangazi hicho cha mwaka 1940 Ndugu Rutherford alikuwa mgonjwa, na sisi hatukujua kama angeweza kuhudhuria kusanyiko lililopangwa katika Detroit, Michigan. Alihudhuria, lakini hotuba ya watu wote ilipokuwa ikiendelea aliniletea ujumbe kwamba angerudi mara moja Betheli na nifanye mipango ya jambo hilo.
Kiangazi kilichofuata kilikuwa na lile kusanyiko kubwa katika St. Louis, Missouri, kusanyiko kubwa zaidi lililokuwa limepata kufanywa na Mashahidi wa Yehova kufikia wakati huo. Nilipewa mgawo wa kupokea vifaa vya kafeteria na niliingia katika jumba kuu wakati tu wa kipindi cha siku ya mwisho wakati kitabu Children kilipotolewa. Katika kusanyiko hilo pia kijitabu Jehovah’s Servants Defended kilitolewa, chenye habari ya kutusaidia kupambana na utendaji wenye kuchochewa kidini wa polisi dhidi ya huduma yetu ya nyumba kwa nyumba.
Kichapo hicho kilikuja kwa wakati wake kabisa. Baadaye katika mwaka huo baba yangu alikamatwa na kufungwa gerezani kwa ajili ya kushiriki katika huduma. Mama, ambaye kwa sababu hiyo aliachwa peke yake katika motokaa-nyumba alishambuliwa na wafanya-ghasia. Ingawa hakuumizwa kimwili, wafanya-ghasia hiyo waling’oa vitu katika motokaa-nyumba hiyo, na kwa hiyo mama yangu akalazimika kufanya makao pamoja na Mashahidi katika eneo hilo.
Katika Oktoba 1, 1941, lilikuwa pendeleo langu kusimamia mkutano wa kila mwaka wa Sosaiti ya Pennsylvania Ndugu Rutherford alipokuwa hayupo. Ni kwenye mkutano huo nilipochaguliwa kuwa kiongozi mojapo wa shirika la Pennsylvania la Sosaiti.
Miezi miwili baadaye, Jumapili, Desemba 7, 1941, N. H. Knorr, G. E. Hanan na mimi tulikuwa tukirudi kwa motokaa kutoka utumishi wa shambani katika kisehemu cha karibu cha Long Island. Tulikuwa tukisikiliza radio ya motokaa tukasikia tangazo lenye kushtua kwamba Wajapani walikuwa wamepiga kwa makombora Pearl Harbor. Mambo yenye kuelekea kutokea yalikuwa makubwa sana kwa watu wa Yehova—United States ilikuwa katika hali ya vita, msimamizi wa Sosaiti alikuwa mgonjwa mahututi na kulikuwako maadui wenye kutoka pande zote wenye kutaka kusimamisha utendaji wetu wa kuhubiri.
Ingawa Ndugu Rutherford alikufa mwezi mmoja na siku moja tu baadaye, kazi ya Ufalme iliendelea kwa nguvu. Ndugu Knorr alichaguliwa awe msimamizi, na mwaka mmoja baadaye katika Februari 1, 1943, alitangaza kufunguliwa kwa Shule ya Gileadi, ya kuzoeza wamisionari.
Katika Mei 8, 1945, Rais wa U.S. Harry S. Truman alitangaza Ujeremani ilikuwa imekubali kushindwa. Katika Agosti United States ilitupa makombora ya atomu juu ya miji ya Wajapani ya Hiroshima na Nagasaki, na kipindi cha baada ya vita kikawa kimetufikia.
Maendeleo ya Baada ya Vita
Taarifa ilitolewa na Mji wa New York kuwa wanachukua sehemu ya nyuma ya makao yetu ya Kolumbia Heights ambayo yalisambaa mpaka Furman Street ili wajenge kijia cha watu kutembelea na barabara kubwa. Hata hivyo, Sosaiti, iliweza kununua viwanja katika Kolumbia Heights ili kuongeza makao ya Betheli, na kibali ya serikali ilipokewa Oktoba 11, 1946, ya kuruhusu ujenzi. Kwa hiyo Januari 27, 1947, kazi ya kubomoa sehemu ya nyuma ya jengo letu katika Furman Street ikaanza, na wakati wa miaka 1948 na 1949 nyongeza mpya ya Betheli ilijengwa, nyongeza hiyo mpya nzuri iliwekwa wakfu mwaka wa 1950. Nyongeza kubwa ya orofa tisa kwenye kiwanda cha 117 Adams Street ilimalizwa pia karibu na wakati huo.
Mwandishi na mweka-hazina wa Sosaiti W. E. Van Amburgh, alikuwa amekuwa hajiwezi kwa ajili ya uzee na ugonjwa na kwa hiyo akajiuzulu cheo chake. Nilichaguliwa nichukue mahali pake Februari 6, 1947, na Ndugu Van Amburgh akafa siku iliyofuata.
Muda mfupi baadaye, katika masika ya 1947, nilitumwa na Sosaiti nikatembelee nchi kadha za Ulaya ambazo zilikuwa zimeharibiwa sana na Vita ya Ulimwengu ya Pili. Hakika lilikuwa pendeleo kushirikiana na watumishi waaminifu wa Yehova ambao karibuni walikuwa wamefunguliwa baada ya miaka mingi katika kambi za mateso za Nazi. Ilikuwa furaha kwangu kuwapa kitia-moyo cha kiroho nikiwa msemaji mkuu wakati wa makusanyiko yaliyofanywa wakati huo.
Tangu kuja Betheli mwaka wa 1928 sikuwa nimepata kurudi Kalifornia kamwe. Wazazi wangu walikuwa wakipainia sana-sana upande wa Mashariki, kwa hiyo niliweza kuwaona mara kwa mara, hasa kwenye makusanyiko makubwa. Lakini katika kiangazi cha 1947 nafasi ilijitoa kwangu kufanya ziara ya kurudia Kalifornia. Kusanyiko lilipangwa kufanywa Los Angeles, Agosti 13 mpaka 17, na Sosaiti iliwasafirisha wale ambao walikuwa wamekuwa washiriki wa jamaa ya Betheli kwa miaka 15 au zaidi. Ilikuwa safari na kusanyiko zuri lenye kupendeza kama nini!
Mapendeleo ya Pekee ya Utumishi
Katika miaka mingi iliyopita nimefurahia pia mapendeleo yasiyo ya kawaida kuhusiana na upanuzi wa tengenezo lionekanalo la Mungu. Ununuzi wa karibuni zaidi kati ya mwingi wa Sosaiti ambao nimesaidia kufanya mapatano ulikuwa ununuzi mapema mwaka huu (1983) wa viwanja vipya katika 175 Pearl Street and 360 Furman Street katika Brooklyn. Ni tumaini langu la moyoni kwamba majengo haya makubwa mapya yatatumiwa katika upanuzi mkubwa zaidi wa utangazaji wa Ufalme duniani pote.
Nimesafiri mamia ya maelfu ya maili si katika United States yote peke yake bali pia katika nchi nyingine nyingi, nikitoa hotuba kwa wasikilizaji wengi walio watu wa Mungu ili kuwatia moyo katika huduma yao ya Kikristo. Kwa mfano, wakati wa ziara ya ulimwengu wote ya “Habari Njema za Milele” kusanyiko mwaka wa 1963, nilitumika nikiwa mmoja wa wawakilishi rasmi wa Sosaiti, hilo likiwa ni moja tu la mapendeleo mengi ambayo ninamshukuru Yehova kwa ajili yayo. Pia lilikuwa pendeleo la pekee, kutumika nikiwa msemaji wakati wa makusanyiko mengi ya kihistoria ya Mashahidi wa Yehova katika Yankee Stadium, kama vile mwaka wa 1958 wakati kulikuwako watu zaidi ya robo milioni.
Tengenezo Lenye Kusonga Mbele
Katika maisha yetu ya kibinadamu miaka inaleta mabadiliko, nyakati nyingine kwa huzuni ikileta kifo, kama katika kisa cha kifo cha baba yangu Desemba 31,1954, katika Illinois, tarafa ya mwisho ya mgawo wa painia wake. Mwaka uliofuata dada yangu, Grace, na mimi tulimhamisha mama kutoka Illinois mpaka New York, ambako aliishi mpaka kifo chake Mei 6, 1962. Lakini badiliko la furaha sana kwangu lilikuwa wakati Edith Rettos, painia mwenye bidii, alipokuwa mke wangu katika Mei 12, 1956. Tangu wakati huo ametumika kwa uaminifu kando yangu hapa Betheli.
Ninapoendelea kuzeeka katika miaka ya utumishi hapa kwenye makao makuu ya tengenezo la Yehova linaloonekana, jambo linaloniletea furaha hasa ni ushuhuda wenye kuendelea wa baraka za Yehova juu ya kazi ambayo amegawia watu wake wafanye, yaani, kuhubiri habari njema hizi za Ufalme katika dunia yote kabla ya mwisho kuja. (Mathayo 24:14) Nilishuhudia kupanuliwa kwa Baraza Linaloongoza 1971, na kwa mara nyingine mwaka wa 1974, na tangu wakati huo nimeshiriki mengi ya maamuzi makubwa mazuri ambayo yamefanywa kuhusu matawi na kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Pia nimeona hesabu ya watangazaji wa Ufalme ikikua kutoka 44,080 ulimwenguni pote wakati nilipokuja Betheli mwaka wa 1928 mpaka kufikia karibu 2,500,000 wanaoshiriki katika kazi hiyo wakati huu. Kweli kweli tengenezo la Mungu limekuwa likisonga mbele, na mimi ninashukuru kwa ajili ya mapendeleo mengi ya utumishi ambayo nimeaminishwa nifanye kuhusiana na kutoa ushuhuda mkubwa wa mwisho.
Imani yangu katika ahadi za Biblia za serikali ya uadilifu ya Mungu na baraka ambazo italeta duniani ni yenye nguvu zaidi ya wakati mwingineo wote. Kama ningalikuwa na maisha ya kuishi tena, hakuna njia nyingineyo yote ambayo ningechagua kuishi, isipokuwa hii hii. Ni furaha na pendeleo kama nini kutumikia hapa Betheli miaka 55 ambayo imepita pamoja na jamaa ya Kikristo iliyo kubwa zaidi na iliyo nzuri ajabu duniani!
[Picha katika ukurasa wa 19]
J. A. Bohnet alivuta maisha yangu sana
[Picha katika ukurasa wa 20]
Pamoja na dada yangu na wazazi wangu
[Picha katika ukurasa wa 21]
Wazazi wangu walipainia kwa miaka 20 katika hii motokaa-nyumba
[Picha katika ukurasa wa 22]
W. E. Van Amburgh ambaye nilichukua mahali pake kuwa mwandishi-mweka-hazina wa Sosaiti mwaka wa 1947
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nilisema mara nyingi kwenye makusanyiko makubwa—kama hili katika Yankee Stadium mwaka wa 1958
[Picha katika ukurasa wa 24]
Edith amekuwa mwenzi wangu mwaminifu tangu mwaka wa 1956