Mpiganaji Mshikamanifu Apita na Kusonga Mbele
MNARA WA MLINZI huu, katika makala yenye kichwa “Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Mungu,” una hadithi ya maisha ya mpiganaji hodari kwa ajili ya Ufalme wa Mungu—Grant Suiter. Ndugu Suiter alikuwa ameumizwa vibaya sana uti wake wa mgongo. Hiyo ilikuwa Mei 30, 1983. Ingawa alikuwa karibu amelemaa kabisa, Ndugu Suiter aling’ang’ana kuishi kwa miezi karibu sita. Ajapolemazwa vibaya sana, na akiwa hawezi kusema, yeye aliendelea kuonyesha kupendezwa kwingi na mwendo wa kusonga mbele wa tengenezo la Yehova duniani, ambalo alikuwa amelitumikia akiwa mwandishi-mweka-hazina wa shirika kwa miaka karibu 36. Lakini, alimaliza mwendo wake wa kidunia asubuhi ya Novemba 22, 1983 na tangazo la jambo hilo lilitolewa kwa jamaa ya Betheli katika Brooklyn na Watchtower Farms baada ya ibada ya asubuhi na kiamsha-kinywa asubuhi hiyo.
Jumatano jioni, Novemba 23, hotuba ya ukumbusho ilifanyiwa kwenye Jumba la UfaIme la Brooklyn Bethel, na ikatawanywa kwa njia zetu za televisheni kwenye vyumba vya kulia chakula na kwa kuunganisha simu na Watchtower Farms. Kwa hiyo sehemu kubwa ya jamaa ya Betheli ya washiriki 3,123, kutia na wanafunzi wa Gileadi, na pia wageni wengi, waliweza kusikia hotuba zilizotolewa na washiriki kadha wa jamaa. Hazikuwa za kutaja sifa. Badala yake zilitia moyo wote waliokuwapo wafaidike na mwendo wa maisha wa ushikamanifu wa Ndugu Suiter, ambaye kweli kweli alikuwa amejithibitisha kuwa ‘mti mkubwa wa uadilifu’ na mshindi katika kupigania faida za Ufalme. (Isaya 61:3, NW; Ufunuo 14:13) Shukrani pia zilitolewa kwa ajili ya uungaji-mkono wa ushikamanifu aliopewa na mkeye, Edith, wakati wa siku za mwisho-mwisho za utumishi wake wa kujitoa duniani.