Kufanya Utumishi wa Wakati Wote Uwe Kazi-Maisha
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MAX LARSON
KATIKA 1910 mama yangu, ambaye wazazi wake wote wawili walikuwa wamekufa, aliondoka Denmark na kuchukua meli mpaka United States. Yeye alikuwa na miaka 18 tu, hakusema Kiingereza, na hakujua hata mtu mmoja katika nchi hiyo.
Alipowasili Jiji la New York, alichukua gari-moshi ya kwenda Dakota Kusini, mwendo wa zaidi ya kilometa 2,400. Katika Dakota Kusini, ambako kulikuwa na makazi ya Wadani wahamiaji, alikutana na mwanamume ambaye angekuwa baba yangu. Walifunga ndoa katika Septemba 20, 1911.
Mapema katika 1913 Baba alifunga safari peke yake kwa gari kubwa lenye kufunikwa juu kuelekea Montana ili akafanye makao katika shamba lililopatikana. Huko alijenga nyumba yenye chumba kimoja cha magogo. Kilipomalizika wakati wa kiangazi, mama yangu alienda kwa gari-moshi akaungane naye akiwa pamoja na ndugu yangu Norman aliyekuwa na umri wa miezi michache tu.
Miaka miwili baadaye mtoto wa pili alikuwa njiani. Nimekuwa nikisema kwa ucheshi kwamba mimi “nilimsaidia” mama aezeke paa, kwa kuwa alikuwa akiezeka nyongeza fulani ya nyumba ile siku moja kabla sijazaliwa. Siku iliyofuata, Aprili 29, 1915, Baba alipokuja toka shambani ili apate chakula cha mchana, Mama alisema: “Nafikiri nitampata mtoto.” Mimi nilizaliwa alasiri hiyo. Hata hivyo kufikia jioni, Baba aliporudi nyumbani tena Mama alikuwa ameamka na alikuwa amemtayarishia chakula cha jioni!
Miaka mitatu baadaye dada yangu Jean alizaliwa mahali hapo hapo. Mwaka uliofuata jamaa yetu ilihamia Montana ya mashariki, ambako Baba alikodisha shamba. Katika 1921 dada yangu wa pili, Laverna, alizaliwa, nasi watoto wanne tulikulia katika nyanda wazi za Montana.
Kutengeneza Maisha Yangu
Wazazi wangu walikuwa Walutheri, na kila Jumapili sisi sote watu sita tulienda kanisani. Lakini upesi jirani mmoja, Mwanafunzi wa Kimataifa wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa wakati huo, alianza kutembelea Mama na kujifunza Biblia pamoja naye. Baada ya miaka kadhaa, Mama alikubali kweli za Biblia ambazo alikuwa akijifunza, na katika 1925 alibatizwa katika kihori cha kuwekea farasi maji. Wala Baba wala sisi watoto hatukukubali imani yake mpya, lakini sisi sote tulifurahia kuacha kwenda kwenye Kanisa Lutheri. Sikuzote Mama alituambia: “Hamtaki kumtumikia Yehova, lakini msivunje sheria zake kamwe.” Shauri hili lilitusaidia tusiingie matatani.
Jamaa yetu ya watu sita ilikuwa ikilima shamba lenye hektari 320 kwa farasi 14 na trakta moja. Hatukuwa na stima wala mabomba ya kuingiza maji nyumbani, na maji yetu yote yalivutwa kutoka kisima kilichokuwa umbali wa kilometa 4. Kwa sababu ya ukame uliokuwako mapema katika miaka ya 1930 na ukosefu wa kuvuna mazao kwa miaka minne, tuliamua kuhamia Mkoa wa Washington. Kwa kujitayarishia mhamo huo, tulihitaji kuhamisha vifaa fulani vya shambani na vya nyumbani kutoka Montana mpaka Washington. Kwa hiyo mgawo wangu ulikuwa kuandamana na gari la reli na kuhakikisha kwamba farasi zetu walilishwa na kunyweshwa maji safarini. Baada ya siku sita, niliwasili hatimaye katika pwani ya magharibi ya Washington.
Nilimsaidia Baba kuanzisha na kuendesha shamba la uuzaji maziwa huko. Baada ya mwaka mmoja hivi, nikiwa na umri wa 20, nilijasiria kwenda peke yangu, nikiendesha malori ya kubeba magogo katika milima na pia kukaa Alaska miezi sita nikiwa mhandisi wa meli. Katika 1938 dada yangu Jean na mimi tulikuwa na kazi katika Seattle na tulikuwa tunaishi katika nyumba ya mashua katika Ziwa Union. Katika kiangazi hicho, Mama, aliyekuwa akiishi umbali wa kilometa 80, alihudhuria mkusanyiko wa kila mwaka wa Mashahidi wa Yehova katika Seattle. Kwa kuwa mahali mkusanyiko ulipokuwa palikuwa mwendo wa kutembea tu kutoka nyumba yetu ya mashua, tulimwalika aishi nasi. Naye alifanya hivyo, nasi tukakubali kuhudhuria mkusanyiko.
Kuamua Kazi-Maisha Yangu
Jumamosi jioni, Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti wakati huo, alizungumzia kichwa “Wapenda Uadilifu.” Hotuba yake ilishughulikia huduma ya wakati wote, au utumishi wa painia. Baadaye Bill Griffith, aliyekuwa akiketi kando yangu, alisema: “Max, yafaa tufanye hivyo. Twende tukapainie!”
“Haya,” nikajibu. “Na tupainie basi.”
“Unacheza, sivyo?” Bill akauliza.
“La,” nikajibu. “Baada ya kusikiliza hotuba hiyo, nimesadikishwa kwamba ndilo jambo zuri la kufanya.”
“Lakini wewe hata si mhubiri. Hujabatizwa.”
“Kweli, lakini wametangaza sasa tu kwamba kutakuwa na ubatizo kesho. Nitabatizwa wakati huo.”
Kwa hiyo, tukiwa tumesisimuka sana, tukaenda kwenye Idara ya Utumishi wa Shambani kuchukua maombi yetu ya upainia. Tulikutana na Ndugu Van Amburgh huko, mwandishi-mtunza-hazina wa Sosaiti. Tulipomwambia tulichokuwa tukifanya, alituchukua kando kisha akazungumza nasi kama baba. “Sasa msifanye jambo hili kana kwamba ni jaribio au utendaji wa kufurahisha tu,” akasema. “Mnafanya jambo zuri, lakini ingieni katika jambo hili kana kwamba ni kazi-maisha yenu.” Na sikuzote shauri hilo limenisaidia sana. Kwa hiyo tukapeleka maombi yetu, na siku iliyofuata, Juni 5, 1938, nikabatizwa.
Mgawo wa Kwanza wa Upainia
Siku iliyofuata, Jumatatu, nilimjulisha mwajiri kazi wangu kwamba nilikuwa ninaacha kazi yangu ili niwe mhudumu. Nilitumia juma hilo la kwanza katika funzo la makini la kitabu cha karibuni cha Sosaiti, chenye kichwa Enemies, na kuhudhuria mikutano yote. Juma la pili, nilijifunza kitabu kilichofuata ambacho kilikuwa kipya, Riches. Na juma la tatu, nikapokea mgawo wangu wa upainia, ambao ulikuwa Raymond, Washington.
Bill nami tulipata kikundi cha watu 27 huko wakiongoza mikutano katika nyumba ya mmoja wa Mashahidi. Maagizo yetu yalikuwa kuongoza mikutano yote na kuwasaidia wahubiri na kuwazoeza waongoze mafunzo ya Biblia, ambayo ilikuwa kazi mpya wakati huo.
Kwenye Mkutano wa Utumishi wa Kwanza, Alhamisi, nilimwuliza mtumishi wa shirika, kama mwangalizi-msimamizi alivyoitwa wakati huo, aende nami jioni iliyofuata ili tujaribu kuanzisha funzo la Biblia. Alisema kwamba alikuwa na shughuli. Kwa hiyo Bill nami tuliondoka peke yetu. Tulipokuwa tunarudi, tulitua kwenye mkingamo wa njia ili turuhusu gwaride ya Lejioni ya Amerika ipite. Kwa mshangao wetu, mtumishi wa shirika alikuwa ndiye kiongozi wa gwaride hiyo.
Jumapili hiyo ya kwanza, nilianzisha funzo langu la kwanza la nyumbani la Biblia pamoja na mwanamume mmoja. Baadaye, niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi la kundi likiwa ndilo langu la kwanza. Na ajabu ni kwamba, lilikuwa katika toleo la Juni 1, 1938, lililoanzisha usimamizi wa kitheokrasi ndani ya makundi. Kati ya wale 27 waliokuwa wakishiriki, 3 tu ndio waliokubali mpango mpya wa kitheokrasi.
Jamaa ya Mapainia
Mara tu baada ya kuanza kupainia, dada zangu na ndugu yangu, Norman, walichukua huduma ya wakati wote pia. Norman na mke wake waliuza shamba lao, wakanunua gari la kukokotwa lenye meta 3.7, na wakiwa pamoja na binti yao Joan mwenye umri wa miaka mitatu, wakaenda kuhubiri. Ilitukia kwamba walipokuwa wakiendesha kazi Raymond katika 1941, Norman aliniandikia kwamba wale 24 waliokataa mpango wa kitheokrasi walikuwa wameacha na kujiunga na kikundi cha waasi-imani. Hata hivyo, yule funzo wangu wa kwanza wa Biblia alikuwa wakati huo ndiye mtumishi wa shirika!
Binti wa Norman Joan na mume wake, Maurice O’Callaghan, wamezuru makundi katika kazi ya mzunguko kwa miaka 24 sasa. Dada yangu mdogo, Laverna, alihudhuria darasa la 12 la shule ya misionari ya Gileadi katika 1949 na akapewa mgawo wa kwenda Italia. Kufaulu kwa kazi ya kimisionari huko mapema kulitokeza kuhamishwa kwake mpaka Switzerland, ambako angali anaishi pamoja na mume wake.
Tamaa ya Utumishi Uliopanuliwa
Baada ya kutumikia nikiwa painia wa kawaida kwa miezi miwili, nilipewa mgawo wa kufanya kazi ya painia wa pekee. Aliyejiunga na Bill pamoja nami wakati huo alikuwa Warren Henschel, ndugu mkubwa wa Milton Henschel. Sasa Milton ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.
Ilikuwa katika mwezi wa kwanza wa kufanya upainia wa pekee niliposimama jioni moja ili nimtembelee Albert Hoffman. Yeye alikuwa mwangalizi wa jimbo au asafiriye, na alikuwa akikaa katika gari la kukokotwa pamoja na mke wake, Zola, upande ule mwingi, wa barabara kutoka kwenye Jumba la Ufalme. Wakati wa miaka hiyo ya Mshuko wa Thamani ya Pesa, mara nyingi tulibadilisha fasihi na vyakula. Siku hiyo nilikuwa nimebadilisha kikapu kikubwa cha matunda ya pea, kwa hiyo nikamtembelea Ndugu Hoffman na kumwuliza kama angependa kupata mengine. Alifurahia sana kisha akanialika niingie ndani.
Ilikuwa saa tatu usiku alipoendelea kuniambia juu ya Bible House (sasa huitwa Betheli), makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York. Hatimaye, mke wake akasema: “Je! mnajua ni saa ngapi? Ni saa 10:30.” Tulikuwa tumeongea usiku kucha! Kabla ya kwenda kulala katika orofa ya juu kabisa ya Jumba la Ufalme, niliandika barua nikiomba ombi la Betheli, nikaenda mara moja kupeleka ombi langu kwa posta.
Kila siku niliweka jambo hilo mbele ya Yehova katika sala, na miezi mitatu baadaye nilishangilia kupokea barua ikinialika kwenye Betheli ya Brooklyn. Kwa kujitayarishia safari hiyo, nilimpa gari langu Jean dada yangu, ambaye sasa alikuwa painia wa pekee pia. Kwa pindi sita za mchana na usiku, nilisafiri kwa basi kupitia pepo kali mbili za theluji katika Montana na zile sehemu za Dakota mpaka nikawasili Jiji la New York, Januari 14, 1939.
Utumishi wa Betheli
Niliandikishwa na mtumishi wa Betheli, Grant Suiter, kisha nikapelekwa kwenye kiwanda ili nikapige ripoti kwa Nathan Knorr, aliyekuwa mtumishi wa kiwanda. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa kufunga katoni za vitabu katika Idara ya Upakizi. Juma la pili, nilipewa mgawo wa kufanya kazi katika orofa ya mashine-rotari ya uchapaji. Ndugu Knorr alisema: “Ikiwa unaweza kujifunza kuendesha mashine hii kwa miezi sita, unaweza kuwa mwendeshaji wayo, kwa kuwa anayeiendesha sasa atapelekwa kwenye mashine nyingine mpya.” Nilijifunza na nikashangilia sana kuendesha mashine hiyo.
Baada ya kuwa katika chumba kile cha mashine kwa mwaka mmoja na nusu, Ndugu Knorr alipita kwenye mashine ile siku moja akasema: “Max, unaonaje kama ungefanya kazi katika ofisi?”
“Oh, Ndugu Knorr, hiyo ndiyo kazi ya mwisho ambayo ningechagua kufanya. Lakini ikiwa ni mgawo wangu, nitaifanya iwe upendezi wangu wa kwanza.”
“Piga ripoti katika ofisi yangu Jumatatu asubuhi,” akajibu.
Nimekuwa huko tangu wakati huo. Kwanza, nilifanya kazi nikiwa msaidizi wa ndugu Knorr, halafu Ndugu Rutherford alipokufa katika Januari 8, 1942, Ndugu Knorr akawa msimamizi, nami nikawekwa rasmi niwe mwangalizi wa kiwanda. Nilikuwa na umri wa miaka 26 na nilikuwa na ujuzi wa Betheli kwa miaka mitatu tu. Kwa hiyo nilihisi uzito wa daraka.
Hata hivyo, waangalizi wapakwa-mafuta wa idara mbalimbali za kiwanda walinipa usaidizi wa upendo. Mtazamo wao wa kujinyenyekeza na wa kutoa msaada uliongeza sana upendo wangu na uthamini kwao. Chanzo kikubwa cha msaada na mazoezi yangu alikuwa Ndugu Knorr. Kwa miaka zaidi ya 35, mpaka kifo chake katika 1977, nilikuwa na pendeleo la kufanya kazi pamoja naye katika kuendesha shughuli za uchapaji na utendaji wa ujenzi wa Sosaiti. Yeye alikuwa na uwezo mkubwa ajabu wa kusimamia mambo, naye alinisaidia sana ili nitimize mgawo wangu.
Mbele ya Maofisa wa Serikali
Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, kulikuwa na upungufu mkubwa wa mali ghafi ambayo tulihitaji ili kuendeleza kazi yetu ya uchapaji. Kwa hiyo, mimi nilifanya ziara kadhaa kwa mwaka kwenda Washington, D.C., ili nikutane na Mabaraza ya Kufanyiza Vifaa vya Vita na pamoja na halmashauri za Seneti. Niliwasihi wanipe karatasi na vifaa vingine, na Yehova akabariki sana jitihada hizo.
Katika pindi moja nilifanya utoaji wangu kwa kuonyesha kurasa mbalimbali kutoka karatasi-habari mashuhuri ambazo zilitangaza habari zisizo za lazima. Nikionyesha tangazo moja lililochukua ukurasa mzima kuhusu koti moja la manyoya katika karatasi kuu ya New York, nilisema: “Kiasi cha karatasi ambacho kimetumiwa kwa tangazo hilo katika toleo moja la Jumapili kinalingana na jumla ya shehena ya ziada tunayoomba kwa mwaka mzima.”
“Umeelewesha habari yako vizuri,” akajibu mzee mmoja. Kutokana na baraka ya Yehova juu ya safari hizi, hatukusimamisha mashine zetu kamwe wakati wa vita kwa sababu ya kukosa karatasi au vifaa vingine. Lakini kwa uwazi, hatukuhitaji akiba kubwa ya karatasi kama tunavyohitaji leo.
Vifaa vya Kiwanda Vilivyopanuliwa
Miaka kumi na miwili kabla ya kuja Betheli, Sosaiti ilijenga kiwanda chao cha kwanza chenye orofa nane katika 117 Adams Street, kikichukua nusu ya eneo la jengo moja la jiji. Lakini kufikia 1949 ikawa inahitajiwa kujenga kiwanda chenye orofa tisa na jengo la ofisi kwenye nusu ya sehemu iliyobaki ya jengo hilo la jiji. Hii ilijaza jengo hilo kwa kiwanda kimoja kikubwa cha meta za mraba zinazokaribia 15,000 za nafasi ya sakafu.
Wakati huo ndipo nilipopewa mgawo wa kusimamia kazi ya ujenzi wa Sosaiti hapa penye makao makuu. Tulikuwa na jengo moja tu kwa utendaji wa ofisi na kiwanda na jengo moja la kukaa katika Brooklyn. Lakini sasa, miaka 40 baadaye, tuna majengo 10 ya utendaji wa kiwanda na ofisi na majengo kama 20 ya kukaa hapa Brooklyn tu!
Katika miaka ya mapema ya 1950, tulijaribu kupata kiwanja kilichokuwa ng’ambo nyingine ya barabara kuelekea kaskazini mwa jengo letu katika 117 Adams Street, lakini mwenye kiwanja hicho hakukubali toleo letu. Kwa kweli, hakutaka makubaliano yoyote, kwa kuwa aliona kwamba Sosaiti ingeweza kulipa bei yake kubwa. Kwa hiyo tulielekeza fikira zetu kwenye eneo la jengo lililo mashariki mwa kiwanda chetu cha Adams Street, ng’ambo nyingine ya Pearl Street. Hili lilikuwa eneo lenye viwanja vinane vilivyo tofauti tofauti. Ilikuwa lazima kushughulika na kila mwenye kiwanja akiwa peke yake, lakini Yehova alifungua njia ili tupate viwanja vyote nane katika muda wa mwaka mmoja kwa bei ya wastani wa dola 97 kwa kila meta ya mraba!
Hapa Sosaiti ilijenga katika 1955 na 1956 jengo la kiwanda chenye orofa 13 lililo 77 Sands Street. Hiki kilikuwa kiwanda chetu cha pili, na kiliongeza nafasi ya sakafu yetu maradufu kwa meta za mraba kama 33,000 hivi. Hata hivyo, kwa kuwa tengenezo lilikuwa likikua sana, iling’amuliwa kwamba karibuni tungehitaji nafasi zaidi. Kwa hiyo katika 1958 tulinunua kiwanda kilichopo katika pembe ya Prospect na Pearl na tukaanza kukitumia kuwa mahali pa kuweka akiba.
Sasa eneo lililobaki tu ambalo tungeweza kuunganisha na majengo yetu mengine kwa daraja zilizopita juu ya barabara zilizopo lilikuwa lile la upande wa kaskazini ambalo tulikuwa tumejaribu kununua mapema. Tuling’amua kwamba mwenye kiwanja hicho huenda bado akajaribu kupata bei yake ya juu sana ikiwa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ingejaribu kukinunua. Kwa hiyo tuliomba mtu fulani aliye katika biashara ya kununua viwanja ajaribu kukinunua. Yeye alikadiria bei ya ununuzi iliyokuwa chini sana ya ile tuliyokuwa tumetaka kutoa. Pasipo uhitaji wa kusema, mwenye kiwanja hicho alifoka sana alipopata kujua kwamba hati ilibadilishwa baadaye ikapewa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi.
Katika 1966 na 1967, tulijenga kiwanda chenye nafasi ya sakafu yenye meta za mraba 21,000 penye kiwanja hiki. Sasa tulikuwa na majengo ya kiwanda yenye kukalia nafasi ya eneo la majengo manne ya jiji—yote yakiwa yameunganishwa na daraja zinazopita juu ya barabara. Baadaye, katika 1983 na 1986, tulinunua majengo mawili ya kiwanda ng’ambo nyingine kusini mwa barabara hizo, na tukaweza kujenga daraja lenye urefu wa meta 49 linalounganisha majengo haya na viwanda vingine vinne. Viwanda hivi sita vilivyounganishwa vina nafasi ya sakafu ya meta za mraba 95,000, au hektari 9 hivi. Katika 1983 tulinunua pia jengo kubwa lenye meta za mraba 93,000 katika Furman Street, upande wa bahari umbali wa majengo machache hivi, ambako vifaa vyetu vya upakizi viko sasa.
Kupata Jengo-Tata la Ofisi
Ono jingine lenye kupendeza katika kushughulika kwangu na ununuzi wa viwanja ni jengo-tata la Squibb Pharmaceuticals lenye majengo kumi yakiwa yameunganishwa ndani. Baada ya ununuzi wetu, manne ya majengo hayo yalibomolewa, na jengo jipya likaunganishwa na lile lililokuwapo ili kufanyiza 25 Columbia Heights, ambalo ndilo makao makuu ya sasa ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Hivi ndivyo kiwanja hiki kilivyonunuliwa.
Kufikia 1969 tulikuwa tunatafuta kupanua vifaa vyetu vya uchapishaji. Lakini hali ya kifedha ilikuwa nzuri, kwa hiyo, nilipokuwa nikiendea kila mtu mwenye uwanja katika eneo hilo, hakuna hata mmoja aliyetaka kuuza.
Wakati huu, nilifanya ziara ya kwenda Carolina ya Kaskazini, kilipo kiwanda cha karatasi ambacho hutupelekea karatasi zetu za Biblia. Nikiwa huko nilimtajia mmoja wa wale watu wa kiwanda uhitaji wetu wa kupata kiwanja katika Brooklyn. Ilitukia kwamba ndugu ya mwanamume huyu alikuwa rafiki wa kibinafsi wa mmoja wa wenye kiwanja cha majengo-tata ya Squibb. Yeye alifanya shughuli iliyohitajiwa kisha akanijulisha kwamba nikirudi Brooklyn, napaswa kumpigia simu mwanamume huyu.
Nilipompigia simu, mwanamume huyo akathibitisha kwamba Squibb ilikuwa ikifikiria kuuza viwanja vyayo katika Brooklyn na kuhama kutoka jiji, wakati ufikapo. Alisema kwamba wakiwa tayari, angetupigia simu, nasi tungesikilizana bei. Baada ya miezi kadhaa simu ikapigwa, nami nikaambiwa kwamba walikuwa tayari kuuza na kwamba twende kwenye ofisi yao kesho yake.
Ndugu Knorr nami tukakutana na kuamua bei ambayo tulifikiri tunaweza kulipa. Kwenye mkutano siku iliyofuata, tuliambiwa kwamba bei haiwezi kubadilika. “Tunataka dola milioni tatu taslimu,” wakasema. Tulijaribu tusionekane kana kwamba tumeshangaa kwa kuwa bei ilikuwa chini sana ya ile tuliyotaka kutoa. Ni wazi kwamba tulikinunua haraka. Wakati huo, tulikuwa tumekamilisha hivi karibuni ujenzi wa kiwanda chetu kipya kilichogharimu dola milioni nne, lakini watu wa Bwana walipojua tulikuwa na mahitaji zaidi ya kifedha, pesa zilipatikana upesi.
Majengo Zaidi ya Kukaliwa
Wakati wa miaka ya 1950, tulipata kiwanja ng’ambo nyingine ya barabara kutoka 124 Columbia Heights na katika 1959 na 1960 tukajenga jengo jipya kubwa la kukaliwa. Lakini tangu 1965 imekuwa vigumu zaidi kujenga majengo mapya ya kukaliwa. Mwaka huo serikali iliagiza eneo ambapo Betheli ipo liwe eneo la kihistoria na majengo ya eneo hilo yawe alama za kumbukumbu ya kihistoria. Jambo hili limetokeza uzuizi mwingi kuhusu kujenga na kutengeneza upya majengo. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova sikuzote tumeweza kujiandalia mahitaji yetu.
Kwa kielelezo, katika 1967, tulijaza ombi tukitaka jengo lenye kukaliwa la orofa sita katika 119 Columbia Heights. Kwa sababu ya kuhifadhi majengo yaliyo alama za kumbukumbu ya kihistoria, tayari tumepunguza jengo lililotazamiwa liwe lenye orofa 12 hapo awali kuwa lenye orofa 6. Hata hivyo, wenye mamlaka wa mahali hapo, walikuwa sasa wanajaribu kutufanya tupunguze angalau orofa nyingine.
Katika Juni, nilitembelea msimamizi wa mji wa Brooklyn, aliyesema kwamba tukiweza kuweka msingi kabla ya mkutano wa Septemba wa Baraza la Makadirio, ambalo ndilo baraza la juu zaidi katika serikali ya jiji, yeye angejaribu kudumisha jengo letu liwe lenye orofa sita. Tengenezo letu la ujenzi likaingia katika mwendo wa kasi, nasi tukaweza kuimwaga misingi kufikia Septemba.
Msimamizi wa mji aliniita siku moja kabla ya wakati ambapo kesi yetu ingesikilizwa peupe. Alituomba tufike kwenye Jumba la Jiji saa mbili kabla Baraza la Makadirio halijafungua mkutano wa watu wote na kwamba tukutane naye nyuma ya jukwaa. Kwa hiyo Ndugu Knorr na Ndugu Suiter, msimamizi-mweka-hazina wetu, na mimi tukafika kwenye Jumba la Jiji mapema sana asubuhi iliyofuata. Tulipokuwa tukizungumza njia iliyo bora ya kutoa kesi yetu mbele ya Baraza la Makadirio, kijambo kimoja cha maana kilionekana wazi kuhusu mambo ya ufundi ya Tume ya Mpangilio wa Majengo ya Jiji. Simu ilipigwa ili kuhakikisha jambo hilo. Mara moja kamishna wa mpangilio wa majengo ya jiji akasema angekuja kushughulikia jambo hilo yeye mwenyewe. “Kwa kuwa watu wengi watapinga kesi yenu,” akasema, “mimi nitajitoa ili niwakilishe Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi mbele ya Baraza.”
Kwa asili tulipendezwa na toleo lake. Sasa, mpango unaofuatwa mbele ya Baraza la Makadirio ni kwamba kesi zote zilizoandikwa siku hiyo katika kalenda yao huahirishwa, na ikiwa kuna makatao yoyote, basi kesi hiyo huahirishwa mpaka alasiri. Kesi yetu ilitajwa mapema asubuhi na kamishna wa mpangilio wa majengo ya jiji akainuka na kumwambia meya: “Ningependa kuzungumza kwa niaba ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi.”
“Unajua si mpango wetu kuruhusu mazungumzo wakati habari inapotajwa mara ya kwanza kwa kawaida [mazungumzo huahirishwa mpaka alasiri],” meya akajibu. “Hata hivyo, najua wewe una shughuli nyingi sana, Kamishna, ingawa si kawaida, nitakubali ombi lako.” Kamishna aliendelea kueleza kisa chetu, na Baraza la Makadirio likapiga kura huku wote wakikubali ombi letu. Tulipokuwa tukiondoka kwenye jumba la kusikilia kesi, wakili wa upande wenye kupinga alitufikilia akikimbia katika jumba na kupaaza sauti hivi: “Mimi nina ubishi utakaochukua muda wa saa moja dhidi ya kesi hii.” Lakini alikuwa amechelewa mno! Sisi tulipita tu, tukimshukuru Yehova kwa ushindi.
Lazima niseme kwamba limekuwa pendeleo lenye kuthawabisha sana kwa muda wa miaka mingi kuwakilisha Sosaiti katika mambo haya ya kibiashara. Na imekuwa shangwe kubwa kushuhudia ongezeko kubwa sana katika kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote ambayo ilifanya ununuzi wa majengo haya yote uhitajiwe kabisa. Msaada mkubwa katika mambo haya ya kibiashara ni kufanywa kwangu kuwa msimamizi-msaidizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ya New York, Inc., katika Januari 1, 1977.
Mwenye Furaha Katika Utumishi wa Betheli
Tangu nilipowasili katika Betheli katika 1939, jamaa ya Betheli imekua kutoka washiriki wa kawaida 185 kufika zaidi ya 2,800 katika Brooklyn na zaidi ya 900 katika Mashamba ya Watchtower! Mara nyingi mimi nimeulizwa: “Ni nini kimekusaidia ukae Betheli hiyo miaka 50?” Sikuzote jibu langu limekuwa: “Sijafikiria jambo jingine lolote isipokuwa utumishi wa Betheli.”
Pia, ombi la utumishi wa Betheli nililojaza na kutia sahihi liliuliza: “Je! unakubali kukaa Betheli mpaka Bwana akuondoe?” Yeye hajaniondoa, kwa hiyo bado nipo hapa nikishangilia utumishi kwa Yehova. Tangu siku niliyojiweka wakfu, nimepiga moyo konde kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi-maisha yangu.
Wakati wa miaka yangu ya mapema katika Betheli, mipango haikuruhusu kufunga ndoa, kwa hiyo, kama vile ilivyo kwa wengine wengi, niliridhika na useja na utumishi wa Betheli. Hata hivyo, wakati maongozi ya jamaa ya Betheli yalipobadilika, yakiruhusu kufunga ndoa, nilimwoa Helen Lapshanski katika Aprili 7, 1956. Yeye alikuwa amekuja Betheli katika 1951. Tumehazini sana uandamani wenye msaada ambao tumeandaliana mmoja na mwenzake.
Mapema katika ndoa yetu, Helen alipatwa na multiple sclerosis (ugonjwa wa kuwa na viraka-viraka vya tishu ngumu katika mishipa ya fahamu na unaohusianishwa na kupooza viungo vya mwili), na katika miaka ya karibuni ugonjwa huo umeendelea sana. Lakini kwa msaada wa kifaa cha kutembea na kigari kinachoendeshwa na makaa-mawe, anaweza kuendesha mambo vizuri. Yeye amedumisha roho nzuri ajabu ya kuonyesha shangwe, naye hushiriki kazi katika Betheli kila siku, akitumikia katika ofisi ya Makao ya Betheli.
Mapema katika miaka yetu ya ukuzi, dada yangu Jean na mimi tulikuwa na ukaribiano mwingi na tulifanya mambo pamoja. Kwa sababu hiyo, sikuzote yeye alipiga moyo konde ili anifuate, na katika 1943 alialikwa Betheli. Katika 1952 yeye na Russell Mock walioana, na wanatumikia hapa pamoja nasi wakiwa washiriki wa jamaa ya Betheli.
Mimi naamini kwa uthabiti kwamba Betheli ndipo mahali bora zaidi duniani upande huu wa Paradiso ya kidunia inayokuja. Sijapata kujuta hata kwa sekunde moja kwa kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi-maisha yangu. Lo, imekuwa shangwe kama nini kuona na kushiriki katika ukuzi mkubwa wa tengenezo la kidunia la Yehova! Nimepiga moyo konde ili, kwa msaada wa Yehova niendelee kufanya Betheli iwe makao yangu na kujitia mwenyewe kwa nafsi nzima katika kusogeza mbele masilahi ya Ufalme.
[Blabu katika ukurasa wa 30]
“Mimi naamini kwa uthabiti kwamba Betheli ndipo mahali bora zaidi duniani upande huu wa Paradiso ya kidunia inayokuja”
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Juu: Kiwanja kilicho katika 360 Furman Street, kilichonunuliwa katika 1983
Chini: Kiwanja kilicho katika Columbia Heights ambacho tulinunua kutoka Squibb Pharmaceuticals katika 1969
Kushoto: Chanzo kikubwa cha msaada na mazoezi yangu alikuwa Ndugu Knorr
Chini: Kufikia 1986 tulikuwa na majengo sita ya viwanda yaliyounganishwa kwa madaraja yanayopita juu ya barabara
Picha katika ukurasa wa 27]
Kiwanda baada ya kupanuliwa katika 1949
Picha katika ukurasa wa 30]
Siku yetu ya arusi