‘Tumefanya Lile Tulilopaswa Kufanya’
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GEORGE COUCH
Baada ya kuwa katika huduma ya nyumba hadi nyumba asubuhi, mwenzangu alitoa vipande viwili vya mkate. tulipomaliza kula, nilitoa sigareti ili nivute. “Umekuwa katika kweli kwa muda gani?” akaniuliza. “Nilihudhuria mkutano wa kwanza usiku uliopita,” Nikamjibu.
NILIZALIWA Machi 3, 1917, katika shamba lililokuwa kilometa 50 mashariki mwa Pittsburgh, Pennsylvania, Marekani, karibu na mji mdogo wa Avonmore. Huko ndiko wazazi wangu walikolelea ndugu zangu wanne, dada mmoja, nami.
Hatukupata mazoezi mengi ya kidini. Kuna pindi fulani ambapo wazazi wangu walikuwa wakienda kanisani, lakini tulipokuwa bado wachanga, wazazi wangu waliacha kwenda. Ingawa hivyo, tulikuwa na imani katika Muumba, na katika maisha yetu ya familia tulifuata kanuni za msingi zipatikanazo katika Biblia.
Wazazi wangu walinizoeza vizuri zaidi kuhusiana na daraka—jinsi ya kukubali daraka na kulitimiza. Hayo ndiyo yaliyokuwa maisha ya shambani. Lakini hatukufanya kazi wakati wote. Tulifurahia tafrija ifaayo, kama vile kucheza mpira wa kikapu na besiboli, kuendesha farasi, na kuogelea. Siku hizo pesa zilikuwa haba, lakini maisha ya shambani yalipendeza. Tulisomea shule ya msingi yenye chumba kimoja kisha tukajiunga na shule ya sekondari iliyokuwa mjini.
Usiku mmoja nilikuwa nikitembea mjini pamoja na rafiki yangu. Msichana mrembo akatoka nyumbani mwake kuja kusalimia rafiki yangu. Rafiki huyo alinijulisha kwa msichana huyo aliyeitwa Fern Prugh. Kwa kufaa, yeye aliishi kwenye mtaa ambapo hiyo shule ya sekondari ilikuwa. Mara nyingi nilipopita karibu na nyumba yake, Fern alikuwa nje akifanya kazi. Ni wazi kwamba, alifanya kazi kwa bidii, jambo lililonivutia. Tulisitawisha urafiki wa karibu na upendo, tukaoana katika Aprili 1936.
Kupata Kujua Kweli ya Biblia
Kabla sijazaliwa, kulikuwa na mwanamke mmoja mzee-mzee ambaye watu mjini walikuwa wakimtenda vibaya kwa sababu ya dini yake. Mama yangu alimtembelea kila Jumamosi alipokuwa akienda mjini kununua vitu. Mama alisafisha nyumba yake na kumsaidia kwa kwenda hapa na pale kwa niaba yake, akifanya hivyo hadi huyo mwanamke alipokufa. Ninaamini kwamba Yehova alimbariki Mama kwa sababu alimwonyesha fadhili nyingi mwanamke huyo aliyekuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.
Baada ya muda fulani, binti mchanga wa shangazi yangu alikufa ghafula. Kanisa halikumfariji sana shangazi yangu, lakini jirani fulani aliyekuwa Mwanafunzi wa Biblia alifanya hivyo. Huyo Mwanafunzi wa Biblia alimfafanulia kile kimpatacho mtu anapokufa. (Ayubu 14:13-15; Mhubiri 9:5, 10) Ufafanuzi huo ulitokeza faraja kubwa. Shangazi yangu naye, alizungumza na Mama juu ya tumaini la ufufuo. Mazungumzo hayo yaliamsha upendezi wa Mama, kwa kuwa wazazi wake walikufa alipokuwa mchanga na alitamani sana kujua kile kimpatacho mtu anapokufa. Jambo hilo lilinikazia umuhimu wa kutumia vizuri sikuzote fursa za kutoa ushahidi wa kivivi hivi.
Katika miaka ya 1930, Mama alianza kusikiliza matangazo ya redio ya Jumapili ya Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society wakati huo. Katika miaka hiyo, Mashahidi pia walianza kuhubiri nyumba hadi nyumba huko tulikoishi. Wangeweka kinanda cha gramafoni chenye kuchukulika chini ya mti wenye kivuli na kupiga mirekodi ya mahubiri ya Ndugu Rutherford. Mirekodi hiyo na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Golden Age (ambalo sasa huitwa Amkeni!) yalitegemeza upendezi wa Mama.
Katika 1938, miaka michache baadaye, postikadi ilipelekewa wale waliokuwa wameandikisha gazeti la Mnara wa Mlinzi ikiwaalika wahudhurie mkutano wa pekee katika nyumba ya faragha iliyokuwa umbali wa kilometa 25 hivi. Mama alitaka kuhudhuria, kwa hiyo Fern nami na ndugu zangu wawili tuliandamana naye. Waangalizi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova, John Booth na Charles Hessler, walitutolea hotuba tukiwa watu 12 hivi. Baadaye, walianza kupanga ili kikundi fulani kishiriki katika huduma ya shambani asubuhi iliyofuata. Hakuna yeyote aliyejitolea kwenda nao, kwa hiyo Ndugu Hessler alinichagua na kuniuliza, “Kwa nini usiende nasi?” Sikujua kabisa walichokuwa wakienda kufanya, lakini sikuwa na sababu ya kutowasaidia.
Tulienda nyumba hadi nyumba hadi kipindi cha adhuhuri hivi, kisha Ndugu Hessler akatoa vipande viwili vya mkate. Tuliketi kwenye vipandio vya kanisa na kuanza kula. Ilikuwa baada ya kutoa sigara hiyo kwamba Ndugu Hessler alipata kujua kwamba nilikuwa nimehudhuria mkutano mara moja tu. Jioni hiyohiyo alijialika kwa chakula cha jioni na kutuomba tualike majirani zetu kwa mazungumzo ya Biblia. Baada ya chakula cha jioni, alijifunza Biblia pamoja nasi, kisha akakitolea hotuba kikundi cha watu kumi hivi ambao walikuwa wamekuja. Alituambia kwamba ilitupasa kuwa na funzo la Biblia kila juma. Ingawa majirani zetu hawakukubaliana na jambo hilo, Fern nami tulipanga kuwa na funzo la Biblia nyumbani kila juma.
Maendeleo Katika Kweli
Muda mfupi baadaye, Fern nami tulienda katika huduma ya shambani. Tulikuwa kwenye kiti cha nyuma cha gari, na tulikuwa tu tumewasha sigara wakati ndugu yangu alipotugeukia na kusema hivi: “Nimetoka tu kugundua kwamba Mashahidi hawavuti sigara.” Fern alitupa sigara yake mara moja kupitia dirishani lakini mimi nilimaliza kuvuta yangu. Hata ingawa tulifurahia kuvuta sigara, hatukugusa sigara tena kamwe.
Baada ya ubatizo wetu mwaka wa 1940, Fern nami tulikuwa katika mkutano ambako tulisoma makala fulani iliyotia watu moyo wapainie, kama vile kuhubiri wakati wote kuitwavyo. Tulipokuwa njiani kwenda nyumbani, ndugu fulani alituuliza hivi: “Kwa nini wewe na Fern hampainii? Hamna chochote cha kuwazuia.” Tulikubaliana naye, kwa hiyo tukajitolea. Nilitoa notisi ya siku 30 mahali nilipokuwa nikifanya kazi, na tukafanya mipango ya kupainia.
Tulishauriana na Watch Tower Society juu ya pale ambapo tungetumikia, kisha tukahamia Baltimore, Maryland. Huko kulikuwa na makao ya mapainia, na gharama ya chumba na chakula ilikuwa dola 10 kwa mwezi. Tulikuwa na akiba za benki ambazo tulifikiri zingetutegemeza hadi Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Kwa vyovyote, sikuzote tulifikiri kwamba Har–Magedoni ilikuwa karibu sana. Kwa hiyo tulipoanza kupainia, tuliacha makao yetu na kuachana na mambo yote tuliyokuwa tukifuatia hapo awali.
Tulipainia huko Baltimore kuanzia mwaka wa 1942 hadi 1947. Upinzani dhidi ya kazi ya Mashahidi wa Yehova ulikuwa mwingi sana miaka hiyo. Badala ya kutumia gari letu kwenda kwenye mafunzo yetu ya Biblia, nyakati nyingine tuliomba mtu fulani atupeleke. Kwa kufanya hivyo magurudumu ya gari letu hayangekatwakatwa. Hakuna apendaye upinzani wa namna hiyo, lakini naweza kusema kwamba tulifurahia huduma ya shambani siku zote. Kwa hakika, tulitazamia kusisimuliwa kidogo katika kufanya kazi ya Bwana.
Punde si punde tulikuwa tumetumia pesa zote tulizokuwa tumeweka akiba. Magurudumu ya gari letu, nguo na viatu vyetu vilikuwa vimechakaa. Tulikuwa wagonjwa mara mbili au tatu kwa vipindi virefu. Maisha hayakuwa rahisi, lakini hatukufikiria kamwe kuacha mgawo wetu. Hata hatukuzungumzia kamwe jambo hilo. Tulisahilisha mtindo wetu wa maisha ili tuweze kuendelea katika kazi ya upainia.
Mabadiliko ya Mgawo
Katika 1947 tulihudhuria mkusanyiko huko Los Angeles, California. Tukiwa huko, mimi na ndugu yangu William, tulipewa kila mmoja barua iliyokuwa na mgawo wa kazi ya kusafiri kwenda kuzuru na kusaidia makutaniko. Wakati huo hatukupata mazoezi yoyote ya pekee kwa ajili ya kazi hiyo. Tulienda tu. Katika miaka saba iliyofuata, Fern nami tulitumikia katika Ohio, Michigan, Indiana, Illinois, na New York. Katika 1954 tulialikwa kuhudhuria darasa la 24 la Gileadi, shule ya kuwazoeza wamishonari. Tukiwa huko, Fern alishikwa na ugonjwa wa polio. Kwa kufurahisha, alipona kabisa, na tulipewa mgawo wa kazi ya kusafiri katika New York na Connecticut.
Tulipokuwa tukitumikia huko Stamford, Connecticut, Nathan H. Knorr, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Society, alituomba tupishe mwisho-juma pamoja naye na mke wake, Audrey. Walitutayarishia mlo wa jioni wa nyama tamu na vipamba-chakula vyote. Tulikuwa tumejuana nao mapema kidogo, na nilimjua Ndugu Knorr vizuri vya kutosha kung’amua kwamba, mbali na ushirika wetu na mlo huo wa jioni, yeye alikuwa akifikiria jambo fulani. Baadaye jioni hiyo aliniuliza, “Je, ungependa kuja Betheli?”
“Sina hakika kabisa; sijui mengi kuhusu maisha ya Betheli,” nikajibu.
Baada ya kufikiria jambo hilo kwa majuma kadhaa, tulimwambia Ndugu Knorr kwamba tungekuja ikiwa alitaka tufanye hivyo. Juma lililofuata, tulipokea barua iliyotualika turipoti Betheli katika Aprili 27, 1957, siku ya ukumbusho wa arusi yetu ya 21.
Siku hiyo ya kwanza Betheli, Ndugu Knorr alinitolea maagizo dhahiri juu ya yale niliyotarajiwa kufanya. Aliniambia hivi: “Wewe si mtumishi wa mzunguko tena; uko hapa kufanya kazi Betheli. Hii ndiyo kazi muhimu zaidi upaswayo kufanya, nasi twataka utumie wakati na nishati zako katika kutumia mazoezi utakayopokea hapa Betheli. Tunataka ukae.”
Maisha Yenye Maana Betheli
Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa katika Idara ya Magazeti na Upelekaji Barua. Baadaye, baada ya miaka mitatu hivi, Ndugu Knorr aliniomba nipige ripoti ofisini mwake. Wakati huo alinijulisha kwamba sababu halisi iliyofanya nipelekwe Betheli ilikuwa kufanya kazi katika makao hayo. Maagizo yake yalikuwa ya moja kwa moja kabisa, “Uko hapa kusimamia Makao ya Betheli.”
Kusimamia Makao ya Betheli kulinikumbusha masomo ambayo wazazi wangu walikuwa wamenifundisha huko shambani nilipokuwa nikikua. Makao ya Betheli ni kama nyumba ya familia ya kawaida. Kuna nguo za kusafishwa, chakula cha kutayarishwa, vyombo vya kuoshwa, vitanda vya kutandikwa, na kadhalika. Huo utaratibu wa kinyumbani hujaribu kuifanya Betheli mahali penye kustarehesha kuishi, mahali ambapo mtu aweza kupaita nyumbani.
Ninaamini kwamba kuna masomo mengi ambayo familia zaweza kujifunza kutokana na vile ambavyo Betheli huendesha shughuli zake. Sisi huamka asubuhi na mapema na kuanza siku kwa mambo ya kiroho kwa kuchunguza andiko la Biblia la kila siku. Tunatarajiwa kufanya kazi kwa bidii na kuishi maisha yenye usawaziko lakini yenye shughuli nyingi. Betheli sio kama nyumba ya watawa, kama vile ambavyo wengine huenda wakafikiri. Tunatimiza mengi kwa sababu ya njia yetu ya maisha yenye utaratibu. Wengi wamesema kwamba mazoezi waliyopokea Betheli yaliwasaidia baadaye kukubali madaraka katika familia zao na katika kutaniko la Kikristo.
Huenda wanaume na wanawake vijana wanaokuja Betheli wakapewa mgawo wa kusafisha, udobi, au mgawo wa kufanya kazi katika kiwanda. Huenda ulimwengu ukataka tuamini kwamba kazi ngumu kama hiyo inatushushia heshima na hatustahili kuifanya. Hata hivyo, vijana katika Betheli huja kuthamini kwamba migawo hiyo ya kazi ni ya lazima ili familia yetu iendeshe shughuli zake ifaavyo na kwa furaha.
Huenda ulimwengu pia ukaendeleza wazo la kwamba unahitaji cheo na fahari ili kuwa mwenye furaha kikweli. Si sawa kuwaza hivyo. Tufanyapo kazi ambayo tumegawiwa, huwa ‘tunafanya tunalopaswa kufanya,’ nasi hupokea baraka za Yehova. (Luka 17:10) Tunaweza kuwa na uradhi na furaha halisi tukikumbuka tu kusudi la kazi yetu ambalo ni kufanya mapenzi ya Yehova na kuendeleza masilahi ya Ufalme. Tukikumbuka mambo hayo, mgawo wowote ule unaweza kuwa wenye kufurahisha na kuridhisha.
Pendeleo la Kushiriki Katika Upanuzi
Katika mkusanyiko huko Cleveland, Ohio, mwaka wa 1942, zaidi ya mwongo mmoja kabla ya sisi kuja Betheli, Ndugu Knorr alitoa hotuba “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Alielewesha wazi kwamba Vita ya Ulimwengu ya Pili, iliyokuwa ikiendelea wakati huo, ingeisha na kwamba kungekuwa na kipindi cha amani ambacho kingeandaa fursa ya kupanua kampeni ya kuhubiri. Shule ya Gileadi ya kuwazoeza wamishonari na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya kusitawisha uwezo wa akina ndugu wa kusema hadharani, ilianzishwa mwaka wa 1943. Mikusanyiko mikubwa ilipangwa pia. Yenye kutokeza hasa ni mikusanyiko iliyofanyiwa Stediamu ya Yankee, huko New York katika miaka ya 1950. Kuhusiana na mikusanyiko hiyo ya mwaka wa 1950 na 1953, nilikuwa na fursa ya kusaidia kutayarisha jumba liitwalo Trailer City lililokuwa na nafasi iliyotoshea kulala watu makumi ya maelfu kwa siku nane za kila mkusanyiko.
Baada ya mikusanyiko hiyo, kutia na ule wa mwaka wa 1958, uliokuwa mkubwa zaidi kupita yote, kulikuwa na ongezeko kubwa la wahubiri wa Ufalme. Ongezeko hilo liliathiri moja kwa moja kazi yetu Betheli. Mwishoni mwa miaka ya 1960 na mwanzoni mwa miaka ya 1970, tulikuwa na uhitaji mkubwa sana wa nafasi na vyumba vya kukaa wafanyakazi. Ili kuipa makao familia yetu iliyokuwa inazidi kuongezeka, ilitubidi kuwa na vyumba vingi zaidi vya kulala, jikoni, na vyumba vya kulia.
Ndugu Knorr alimwomba mwangalizi wa kiwanda, Ndugu Max Larson nami, tutafute uwanja ufaao kwa ajili ya upanuzi. Mwaka wa 1957, nilipokuja Betheli, familia yetu ya watu 500 hivi ilikuwa ikikaa katika jengo kubwa moja. Katika miaka iliyopita, Sosaiti ilinunua na kurekebisha upya hoteli kubwa tatu—ziitwazo Towers, Standish, na Bossert—na vilevile majengo mengine madogo ya kuishi. Katika 1986 Sosaiti ilinunua uwanja mwingine ambapo hoteli iitwayo Hotel Margaret ilikuwa imejengwa, na kugeuza jengo jipya zuri lililokuwa limejengwa hapo kuwa makao ya watu 250 hivi. Kisha mapema miaka ya 1990 makao yenye orofa 30 yalijengwa kwa ajili ya wafanyakazi 1,000 zaidi. Sasa Betheli ya Brooklyn inaweza kuandaa makao na chakula kwa washiriki zaidi ya 3,300 wa familia yetu.
Pia uwanja ulinunuliwa katika Wallkill, New York, kilometa 160 kutoka Betheli ya Brooklyn. Kwa miaka ambayo imepita, kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1960, majengo ya kuishi na matbaa kubwa ilijengwa hapo. Sasa, washiriki 1,200 hivi wa familia yetu ya Betheli huishi na kufanya kazi huko. Katika mwaka wa 1980 uwanja wenye ekari 600 hivi ulio karibu zaidi na New York City, na wenye njia ya kufikia barabara kuu, ulianza kutafutwa. Mwakilishi wa ununuzi wa mali alicheka na kusema hivi: “Mtapata wapi uwanja mkubwa hivyo? Haiwezekani kabisa.” Lakini asubuhi siku iliyofuata alipiga simu na kusema: “Nimepata uwanja wenu.” Leo hii, mahali hapo panaitwa Kitovu cha Kielimu cha Watchtower cha Patterson, New York. Shule mbalimbali hufanyiwa huko na kuna familia ya wahudumu zaidi ya 1,300.
Masomo Ambayo Nimejifunza
Nimejifunza kwamba mwangalizi mzuri ni yule awezaye kupata habari yenye thamani kutoka kwa wengine. Maoni yaliyo mengi ambayo nimependelewa kutumia nikiwa mwangalizi wa Betheli yametokana na wengine.
Nilipokuja Betheli, wengi walikuwa na umri mkubwa zaidi, kama nilivyo leo. Wengi sasa hawako. Ni nani ambaye huchukua mahali pa wanaozeeka na kufa? Sikuzote si wale wenye uwezo zaidi. Bali ni wale wanaopatikana, wanaofanya kazi kwa uaminifu na wanaojitoa.
Jambo jingine la maana kukumbukwa ni thamani ya mke mwema. Utegemezo wa Fern, mke wangu mpendwa, umenisaidia sana kutimiza migawo yangu ya kitheokrasi. Waume wana daraka la kuhakikisha kwamba wake zao wanafurahia migawo yao. Huwa ninajaribu kupanga jambo fulani ambalo Fern nami hupenda kufanya. Si lazima liwe jambo lenye gharama kubwa, bali ni jambo tofauti na yale sisi hufanya kila siku. Ni jukumu la mume kufanya mambo ili kumfurahisha mke wake. Wakati anaotumia pamoja naye ni wenye thamani na hupita haraka, kwa hiyo anahitaji kuutumia vizuri kabisa.
Ninafurahi kuishi katika siku za mwisho ambazo Yesu alizungumzia. Huu ndio wakati wenye kustaajabisha zaidi katika historia yote ya kibinadamu. Tunaweza kuangalia na kuona kwa macho yetu ya imani jinsi Bwana anavyolisitawisha tengenezo lake ili liwe tayari kwa ajili ya kufika kwa ulimwengu mpya ulioahidiwa. Nikumbukapo maisha yangu nikiwa katika utumishi wa Yehova, ninaweza kuona kwamba Yehova ndiye anayeongoza tengenezo hili—si wanadamu. Sisi ni watumishi wake tu. Na tukiwa watumishi wake, ni lazima sikuzote tumtegemee kupata mwongozo. Mara atuelezapo yale tupaswayo kufanya, twapaswa kuwa tayari kutii na kuwa wenye ushirikiano.
Shirikiana kikamili na tengenezo, na unahakikishiwa kuwa na maisha kamili yenye furaha. Lolote lile ufanyalo—liwe ni upainia, kazi ya kuzunguka, kutumikia kutanikoni ukiwa mhubiri, utumishi wa Betheli au kazi ya umishonari—fuata mwongozo unaotolewa, na thamini mgawo wako. Jaribu kadiri uwezavyo kufurahia kila mgawo na pia kila siku ufanyayo kazi katika utumishi wa Yehova. Utachoka, na huenda ukafanya kazi kupita kiasi au nyakati nyingine ukavunjika moyo. Huo ndio wakati ambapo inakubidi ukumbuke kusudi la kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova. Ni kufanya mapenzi yake, si yako mwenyewe.
Hakuna siku ambayo nimekuja kazini nisifurahie nilichofanya. Kwa nini? Kwa sababu tunapojitoa kwa Yehova kwa nafsi yote, tunapata uradhi wa kujua kwamba ‘tumefanya lile tulilopaswa kufanya.’
[Picha katika ukurasa wa 19]
Idara ya Magazeti
[Picha katika ukurasa wa 19]
Trailer City, mwaka wa 195
[Picha katika ukurasa wa 19]
Nikipainia huko Baltimore, mwaka wa 1946
[Picha katika ukurasa wa 19]
Nikiwa na Fern katika Trailer City mwaka wa 1950
[Picha katika ukurasa wa 22]
Tukiwa na Audrey na Nathan Knorr
[Picha katika ukurasa wa 23]
Kitovu cha Kielimu cha Watch Tower karibu na Patterson, New York
[Picha katika ukurasa wa 24]
Nikiwa na Fern leo