Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 12/1 kur. 14-22
  • Tengenezo la Yehova Linasonga Mbele—Je! Wewe Unasonga Pamoja Nalo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tengenezo la Yehova Linasonga Mbele—Je! Wewe Unasonga Pamoja Nalo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIPINDI CHA WAKF CHAKAZIA UPANUZI
  • FRANZ ATOA HOTUBA YA WAKF
  • SIKU NZIMA YA BARAKA ZA KIROHO
  • KULIUNGA MKONO TENGENEZO LA YEHOVA LINALOSONGA MBELE
  • Kufanya Utumishi wa Wakati Wote Uwe Kazi-Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Tendo Lililounganishwa kwa Umoja Kufanya Ujenzi Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 12/1 kur. 14-22

Tengenezo la Yehova Linasonga Mbele​—Je! Wewe Unasonga Pamoja Nalo?

HUWEZI kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na ukose kuvutwa na namna Wakristo walivyopangwa kitengenezo kwa ajili ya ibada. Sana-sana, wao walipangwa kitengenezo ili wahubiri, wazieneze habari njema za ufalme wa Mungu.

H. G. Wells mwanahistoria wa kisasa alisema hivi juu ya Ukristo wa kwanza: “Tengenezo lake la pekee lilikuwa tengenezo la wahubiri, na kazi kubwa yake ilikuwa mahubiri.” Ndiyo, ni kama vile mtume Petro alivyosema: “Yeye [Yesu Kristo] alituagiza tuwahubiri watu na kutoa ushuhuda wa kutosha kabisa.”​— Matendo 10:42, NW; Mathayo 28:18, 19.

Lakini namna gani kuhubiri kwa siku zetu—hizi “siku za mwisho” za huu mfumo wa mambo? (2 Timotheo 3:1-5) Yesu Kristo alitabiri hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Basi, kabla mwisho wa huu mfumo wa mambo haujaja, ni lazima kazi kubwa sana ya kuhubiri ulimwenguni pote ifanywe. Ni tengenezo gani linaloifanya?

Kusema kweli, kuna kundi moja tu la watu ambalo limepangwa kitengenezo ulimwenguni pote kwa kusudi la kufanya kazi hiyo ya kuhubiri ufalme. Kundi hilo ni Mashahidi wa Yehova. Utendaji wao wa kuhubiri unaendelea kupanuka katika dunia yote, katika nchi 206. Mwaka wa 1981 kulikuwako Mashahidi 2,361,896 wenye kuishiriki kazi hiyo. Hiyo ni hesabu inayozidi robo tatu za milioni moja ya watangazaji zaidi wa ufalme kuliko wale waliokuwako miaka kumi tu kabla ya hapo!

Ili wasiachwe nyuma na mwendo wa utendaji wa kuhubiri unaoendelea kupanuka, Mashahidi wa Yehova, katika muda wa miaka miwili tu iliyopita, ama wamemaliza ama wameanza ujenzi wa viwanda vipya vipatavyo 20 vya kuchapia vitabu vya Biblia. Pia, ukuzi wenye kwenda haraka sana unatukia kwenye makao makuu ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova. Katika karne ya kwanza, Yerusalemu ndipo palipokuwa mahali ambapo tengenezo la Kikristo lilipelekewa mwongozo. (Matendo 15:1, 2) Lakini leo mwongozo huo unatoka Brooklyn, New York.

Jioni ya Machi 15 mwaka huu upanuzi wa karibuni zaidi kwenye mijengo ya makao makuu katika Brooklyn ulifanywa wakf. Upanuzi huo ni lile Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights, linaloonekana katika ukurasa unaofuata. Upanuzi huo una mjengo uliofanywa kwa namna tofauti na pia mwingine uliofanywa hivi karibuni, na mijengo miwili hiyo imeunganishwa pamoja kuwa jengo moja.

Washiriki zaidi ya elfu mbili wa jamaa ya makao makuu ya Brooklyn walihudhuria programu ya wakf, ambayo ilifanywa katika jumba la jamaa la makusanyiko la makao ya jamaa saa 12:45 ya jioni. Lakini programu hiyo ilienezwa pia kwa mfumo wa televisheni ikaingia ndani ya Jumba la Ufalme na vyumba mbalimbali vya kulia ili kufaidi washiriki wa jamaa waliokusanyika humo. Zaidi ya hilo, washiriki wengine zaidi ya mia sita wa jamaa hiyo wanaokaa huko Watchtower Farms (Mashamba ya Sosaiti), kilometa zapata 144 upande wa kaskazini wa New York, waliweza kusikiliza yaliyokuwa yakiendelea kwa kupitishiwa habari hizo na kamba za kupokeza habari.

KIPINDI CHA WAKF CHAKAZIA UPANUZI

Baada ya sala kutolewa na Carey W. Barber, programu ya wakf ilianza kwa muhtasari wa funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hiyo uliofanywa na John E. Barr. Kwa kufaa, habari za funzo hilo zilihusu wakf pia. Milton G. Henschel, mwenyekiti wa jioni hiyo, ndipo alipomkaribisha Grant Suiter arudie kueleza “matukio ya kihistoria” ya tengenezo la Mungu tangu mwaka wa 1919 mpaka wa 1935.

“Hatuyazungumzi mambo haya kwa kiburi, bila ya kumfikiria Yehova,” akaanza kusema Ndugu Suiter, “lakini, badala yake, tunamfikiria yeye na kukitambua kile ambacho yeye amependezwa kukitumia muda wa miongo yote hii ya miaka, yaani, jamaa hii.” Wakati Mashahidi wa Yehova walipohamia Brooklyn mara ya kwanza mwaka wa 1909, jamaa ya makao makuu ilikuwa na watu wapatao 30 tu.

Suiter alieleza kwamba Oktoba wa mwaka 1919 ndipo tengenezo lilipoanza kuchapisha gazeti jipya lililoitwa The Golden Age, ambalo sasa ni Amkeni! Halafu mwaka uliofuata, jamaa ya makao makuu ikaanza kuchapa vitabu vya Biblia katika mashine zao wenyewe, wakiwa mahali padogo kwenye Barabara ya Myrtle. Hivyo, Suiter akasema, kufikia mwaka wa 1921 jamaa ilikuwa imeongezeka ikawa na washiriki 107. Akasema mwaka wa 1923 walikuwa wakitokeza vitabu elfu tano kwa siku.

Mwendo huo wa kusonga mbele wa tengenezo la Mungu ukafanya sehemu kubwa za kufanyia kazi zihitajiwe. Kwa hiyo, kama Suiter alivyosimulia, mwaka wa 1927 makao mapya yaliyopanuliwa yalijengwa kwa ajili ya jamaa ya makao makuu huko Columbia Heights, kisha kiwanda chenye orofa nane kikajengwa mwendo mfupi kutoka hapo, huko 117 Adams Street.

Akiendelea kusimulia “matukio ya kihistoria,” naye Lyman A. Swingle alieleza habari za kusonga mbele kwa tengenezo la Yehova tangu mwaka wa 1936 mpaka wa 1950. “Mwaka wa 1936 mateso yalikuwa yakiongezeka ulimwenguni pote,” akasema. “Kambi za mateso za Hitler zilikuwa zimejengwa wakati huo.” Kisha, akiinamisha kichwa kuelekea mahali mume na mke walipokuwa wameketi, akasema: “Ndugu Poetzinger na mkewe walikamatwa mwaka huo, wakatupwa ndani ya kambi hizo, wakabaki humo muda wa miaka tisa.” Wajapoteswa hivyo, wao na maelfu ya wengine wameendelea kusonga mbele pamoja na tengenezo la Mungu.

“Hiyo ilikuwa miaka yenye majaribu makali,” Swingle akaendelea kusema. “Septemba 1, 1939, Hitler aliingiza askari wake Poland, basi Vita ya Ulimwengu ya Pili ikaanza.” Matata yaliongezeka United States pia. “Kukawa na ghasia-ghasia nchini pote,” akasimulia. “Majumba ya Ufalme kadha yetu yaliteketezwa kwa moto yakalazwa chini. Mengi ya magari yetu yaliharibiwa. . . . Lakini, yajapokuwapo matatizo hayo yote, mwaka wa 1940 tulikuwa na ongezeko la wahubiri kwa asilimia 40!” Akaonyesha kwamba wakati wa vita yenyewe ukubwa wa tengenezo ulikuja kuwa maradufu—kutoka wahubiri wa ufalme 71,500 kufikia zaidi ya 141,000.

“Mwaka wa 1946,” akazidi kusema Swingle, “kusanyiko la kwanza la baada ya vita lilifanywa huko Cleveland, Ohio​—watu elfu 80 wakahudhuria.” Huko ikatangazwa kwamba ujenzi zaidi ungefanywa Columbia Heights na kwamba akina ndugu wangeweza kuiunga mkono programu ya ujenzi kwa michango yao. “Ndipo tulipojenga jengo lenye orofa kumi [hiyo ikiwa ni ziada kwa makao yaliyokuwapo tayari], nalo lilikuwa kubwa sana,” kasema Swingle, “hata tukadhani hakuna siku tungejenga tena katika Brooklyn. Vilevile tulijenga ziada ya jengo lenye orofa tisa la kuongezea kiwanda cha 117 Adams Street. Majengo hayo yaliwekwa wakf mwaka wa 1950.”

Akimalizia, Ndugu Swingle alihadithia kwamba: “Mwaka wa 1950—Kusanyiko la Yankee Stadium la kwanza—siku nane. Ndugu walikuja kutoka nchi 67. Hudhurio lilikuwa 123,707.” Lo! kipindi cha upanuzi mkubwa kweli kweli! “Kutoka mwaka wa 1936 mpaka wa 1950 tulipanda juu tukaacha kuwa wahubiri wapatao 50,000 na kufika 373,430—lo! tukaongezeka mara saba na nusu muda wa hiyo miaka kumi na mitano!” Lakini ni nani ambaye kwa kufaa anastahili kupokea sifa kwa hayo? Akitamka maneno ya mwisho Swingle alitumia maneno ya Nehemia: “Waliitambua kazi hiyo ilivyotendwa na Mungu wetu.”​—Nehemia 6:15, 16.

Halafu, Ndugu Henschel mwenyewe akazungumza “matukio ya kihistoria​—mwaka wa 1951 mpaka wa 1981.” Akifanya utangulizi wa maneno yake, alisema: “Yehova hufanya mambo yatukie. Yehova hufanya vitu vikue.” Kisha akitumia maneno ya mtume Paulo, “Sisi ni wafanya kazi wenzi wa Mungu,” akauliza: “Je! hilo si wazo lenye kutia sana moyo, kuweza kufanya kazi pamoja na Mungu katika kazi yake na kuona matokeo ambayo Yehova hutokeza?”​—1 Wakorintho 3:6-9, NW.

“Ushuhuda upo,” Henschel akaendelea kusema, “matukio ya kihistoria yanaonyesha Yehova ndiye mwenye kusimamia kazi. . . . Ilikuwa lazima tuwe na wahubiri wa kuzijulisha habari njema hizi ulimwenguni pote. Huo ndio mgawo wetu—‘kuzihubiri habari njema za ufalme.’” Ndipo alipoutaja ukuzi mkubwa ajabu: “Wahubiri 798,000 mwaka wa 1958. Halafu, kufikia mwaka wa 1968, kukawa wafanya kazi 1,221,000. Kufikia wa 1978, kukawa 2,182,000, na kufikia wa 1981, kukawa 2,361,000.”

“Ili kazi ya kuhubiri iweze kufanywa na hawa wafanya kazi zaidi ya 2,000,000,” kasema Henschel, “ilikuwa lazima vifaa viwepo.” Ni nani ambaye angetokeza vifaa hivyo? Ni washiriki wa jamaa ya makao makuu! “Huko nyuma mwaka wa 1950,” Henschel akasema, “walikuwako washiriki 355 wa jamaa.” Lakini, akaonyesha kwamba watu walipozidi kutaka vitabu vya Biblia ndivyo jamaa ya makao makuu ilivyozidi kuongezeka—ikafikia hesabu ya 512 mwaka wa 1960, 678 mwaka wa 1965, washiriki 1,228 mwaka wa 1970, na leo ni karibu 2,600.

Ili kuwapa makao wafanya kazi hao wote, nafasi zaidi ilihitajiwa. Henschel akaeleza namna mpanuko ulivyotokea: Makao mapya yenye orofa kumi na mbili yaliwekwa wakf Oktoba 1960. Makao mengine mapya yalijengwa huko 119 Columbia Heights kisha yakawekwa wakf Mei 2, 1969. Ndipo Towers Hotel iliponunuliwa mwaka wa 1975 likiwa ni jengo kubwa. Lilifanyiwa marekebisho likawa makao ya washiriki wapatao mia tisa wa jamaa. Na huko juu kwenye Watchtower Farms majengo mapya ya kukaliwa yakamalizwa mwaka wa 1968, 1971 na 1973.

Henschel alieleza kwamba ili watu waweze kutimiziwa matakwa yao yenye kuongezeka ya vitabu vya Biblia viwanda vilijengwa na vingine vikanunuliwa. Mwaka wa 1956 jengo lenye orofa kumi na tatu lilijengwa huko 77 Sands Street. Halafu hapo karibu tu ng’ambo nyingine ya barabara hiyo jengo jingine (lenye orofa kumi) likanunuliwa mwaka wa 1958. Mwaka wa 1968 kiwanda kipya cha kuchapia vitabu chenye orofa kumi na moja kilimalizwa kikiwa kimeungana na jengo hilo. Majengo hayo yakijumlishwa na kile kiwanda cha 117 Adams Street, yanakuwa majengo makubwa manne ya viwanda ambavyo vimeunganishwa pamoja na madaraja yaliyojengwa huko juu kwenye orofa za majengo hayo. Halafu, Novemba wa mwaka 1969, mfumo wa majengo yanayoitwa Squibb, ulio umbali mdogo tu kutoka hapo, ulinunuliwa. Na, kama vile Henschel alivyosema, majengo hayo ni ya maana sana wakati wa programu hiyo ya wakf, kwa maana Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights ni sehemu ya mfumo huo.

Wakati huo, mpanuko zaidi ulikuwa ukiendelea huko Watchtower Farms, hayo yakiwa ni mashamba yaliyonunuliwa mwaka wa 1963. Henschel alisimulia namna, mwaka wa 1973, kiwanda cha kwanza kilivyomalizwa huko. Halafu mwaka wa 1975 kingine cha pili kilicho kikubwa zaidi kikaanza kujengwa.

Baada ya kueleza matukio mengine ya kihistoria ya miaka 30 iliyopita, kutia na kusanyiko lililofanywa kwenye Wanja za Yankee na Polo safari ile ile moja mwaka wa 1958, ambako watu 253,922 walihudhuria, Ndugu Henschel alimkaribisha Max H. Larson na habari yake yenye kusema “Sehemu-Sehemu za Ujenzi.” Ndugu Larson alionyesha picha 40 zisizo za mwendo, zikaonyesha ubomoaji wa visehemu vya mfumo wa majengo yaliyokuwa yakiitwa Squibb na ujenzi wa jengo jipya la afisi. Wenye kutazama picha hizo waliona namna jengo jipya hilo lilivyounganishwa na kiwanda kilichokuwa kimekuwapo, ambacho kilirekebishwa kikawa jengo la kisasa lenye afisi.

Larson alieleza hivi: “Katikati ya mwaka wa 1978 kazi ilianza ya kugeuza jengo la 25 Columbia Heights liache kuwa bohari liwe jengo la kisasa lenye afisi. Ili kutimiza kazi hiyo kilihitajiwa kikundi cha ndugu na dada wafanya kazi kuanzia 180 mpaka 200.” Wakati huo, mwezi Septemba wa mwaka 1979 ubomoaji uliotangulia kutajwa ulianza, halafu Desemba mwaka wa 1979 ujenzi ukaanza upande wa mashariki wa upanuzi mpya wa 25 Columbia Heights.

FRANZ ATOA HOTUBA YA WAKF

Kumalizia programu hii ya jioni yenye kutia sana moyo, Ndugu Henschel alimkaribisha msimamizi wa Sosaiti, Fred W. Franz. Ndugu Franz alianza kazi ya kuhubiri wakati wote huko nyuma mwaka wa 1914, naye ametumikia akiwa mshiriki wa jamaa ya makao makuu tangu mwaka wa 1920. Kwa hiyo aliweza kusimulia mambo mengi ya kupendeza aliyojionea mwenyewe kuhusu kusonga mbele kwa tengenezo la Yehova.

Ingawa majengo yaliyomalizwa hivi juzi huko 25 Columbia Heights ndiyo mazuri kupita yote, Ndugu Franz alikazia kwamba hayakujengwa kwa kusudi lo lote la kichoyo. Alielekeza fikira kwenye masimulizi ya Biblia katika Marko 7:11-13, ambapo anatajwa mtu aliyekuwa na mali, lakini badala ya kuitumia aheshimu wazazi wake kama ingalivyompasa kufanya, yeye alitaka iwe ya matumizi yake mwenyewe ya kichoyo. Kwa hiyo mtu huyo akaitangaza mali hiyo kuwa “korbani, yaani, kipaji kilichowekwa wakf kwa Mungu.” (NW)

Tofauti na hivyo, Ndugu Franz akasema: “Ndugu na dada zetu walio katika hizi afisi mpya tunazoziweka wakf kwa Yehova hawako hivyo. Bali, wao wanatumia majengo mapya haya ili kumpa Yehova Mungu kilicho bora zaidi. Wanatia bidii, si kwa kusudi la kupata raha ya kichoyo kwa sababu ya kuwa katika makao mazuri kabisa, bali kwa kusudi la kufanya kazi nyingi zaidi na kwa njia nzuri zaidi.”

Ijapokuwa majengo mapya hayo ni bora kabisa na yamejengwa kwa njia ya kudumu, Ndugu Franz alisema kwamba tunahitaji ulinzi wa Yehova, sawa na inavyosema Biblia katika Zaburi 127:1: “[Yehova] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure.” Ndivyo ilivyo kwa habari ya majengo haya, akaeleza Franz. Yehova asipokuwa anayalinda na kubariki kazi tunazofanya humo tunatia jitihada za bure. Lakini, akasema, historia ya watu wa Mungu wa miaka yote inaonyesha kwamba Yehova anawabariki na kuwalinda watu wake.

Akimalizia hotuba yake, Ndugu Franz akatumia maneno haya ya Mfalme Daudi: “Mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kutoa kwa hiari hivi? kwani vitu vyote vyatoka kwako, na katika vitu vyako mwenyewe tumekutolea.” (1 Mambo ya Nyakati 29:14) Kwa hiyo, kwa kuwa Yehova ndiye Mwenyeji wa kila kitu na sisi tumezipata mali hizi kutoka kwake, akasema Franz, tunalofanya tu ni kumrudishia tena Yehova vitu hivyo kwa kuviweka wakf kwake. Hivyo, kwa kuimalizia siku na jioni iliyo ya kupendeza zaidi, yenye kuinua sana hali ya kiroho, akatangaza hivi: “Sasa mimi ningependa kutangaza kwamba afisi mpya hizi zabaki zikiwa zimewekwa wakf kabisa kwa Yehova Mungu.”

SIKU NZIMA YA BARAKA ZA KIROHO

Programu ya jioni ya wakf ilikuwa imekuwa umalizio tu wa siku ya pekee sana ya utendaji mbalimbali. Asubuhi ya siku hiyo ilianza kama siku zile nyingine za kawaida za kazi kwenye makao makuu ya Brooklyn. Kulikuwa na mazungumzo ya andiko la Biblia kuanzia saa 1 ya asubuhi, kisha wakala kiamsha-kinywa. Lakini, saa 2 ya asubuhi, washiriki wengi wa jamaa​—wale wanaofanya kazi ndani ya makao na kwenye viwanda—walianza matembezi ya kuona utendaji wenye kuendelea katika Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights. Walakini, wale wanaofanya kazi katika afisi mbalimbali walienda kufanya migawo yao ya kazi zile za kawaida. Kijitabu cha kurasa 20 kilikuwa kimepigwa chapa kikiwa na orodha ya mipango ya siku hiyo na namna ya kufanya matembezi. Wenye kufanya matembezi waliona nini?

Walifuata maelekezo, wakaingia ndani ya sebule lenye kupendeza sana la jengo jipya la 25 Columbia Heights kisha wakafikia Idara ya Utumishi kwenye orofa iyo hiyo ya tatu. Hapo ripoti zipatazo 325 za waangalizi wa mizunguko hupokewa kila juma kwenye dawati za utumishi kumi. Kwenye orofa ya pili, waliiona Idara ya Maeneo na dawati ya mapainia. Kwenye dawati hiyo walielezwa kwamba mapainia wapya 5,578 waliwekwa mwaka wa 1981.

Wenye kutembelea sehemu hiyo walipandishwa na kiinuaji mpaka orofa ya kumi na mbili, kisha wakafikia afisi za wenye kushughulika na utunzaji wa fedha za Sosaiti. Kwenye orofa ya kumi na moja wakaona Idara ya Kuhesabu Gharama, na hapo ndipo penye kuhakikisha gharama zinazotumiwa kuendesha shughuli za Sosaiti, kwa mfano gharama za kutengeneza vitabu na kuvisafirisha. Chini kwenye orofa ya kumi walitembelea Afisi za Utekelezaji, na vilevile chumba cha mikutano ya Baraza Inayoongoza. Idara ya Ufundi wa Kuchora Picha ilionekana kwenye orofa ya tisa, na hapo ni penye mifano ya namna mbalimbali za uchoraji unaofanywa na wachoraji kutayarisha picha zitakazotumiwa katika vitabu vya Sosaiti.

Kituo kilichofuata ni Idara ya Uandikaji kwenye orofa ya nane, ambapo magazeti, vitabu na maandishi mengine ya Sosaiti huandikwa. Badala ya kutumia taipuraita, sasa waandikaji wengi wanaingiza nakala yenye maandishi moja kwa moja kwenye kompyuta. Maandishi hayo yanashikamanishwa na kichapaji ambacho, kikipashwa amri ya kufanya kazi, kitachapa maneno kama 700 kwa dakika moja kati ya yale maneno yaliyoingizwa ndani. Baada ya siku chache, jengo lote hilo litakuwa na kompyuta 149 za namna hiyo kwa ajili ya kazi mbalimbali za kiafisi. Kisha vichapaji vitakuwa 20.

Baada ya hayo watembeaji wakaenda kwenye orofa ya saba na kwenye Idara ya Kupanga Maneno kwa Mashine ya Kunakili. Hapo wakaonyeshwa namna maandishi yanayotoka kwenye Idara ya Uandikaji yanavyopangwa kwenye kituo cha kazi ya kupanga picha na maandishi ziwe kama zitakavyokuwa kwenye kurasa za magazeti au vitabu vinavyotokea. Halafu, hapo karibu katika Idara ya Upangaji wa Picha na Maandishi, wakaona namna maandishi yaliyoandikwa, na pia picha zilizochorwa, yanavyogeuzwa kuwa utepe kwa kutumia njia mbalimbali za upigaji wa picha. Tepe zinazofanyizwa kwa njia hiyo zinakusanywa pamoja na kupelekwa kiwandani ili mabamba ya upigaji wa chapa za mashine ya ofseti yakatayarishwe. Pia kwenye hii orofa ya saba jamaa ilitembelea Idara ya Kispania na Idara ya Usahihishaji wa Maandishi. Halafu, waliposhuka kwenye orofa ya sita na kuiingia Idara ya Kukusanya na Kupanga Habari Mbalimbali kwa Kompyuta, wakaona mifumo ile mikubwa-mikubwa ya kompyuta zinazoweka na kupitisha habari zinazozifikia kutoka mitambo yote ya jengo lote lenye afisi hizo.

Ingawa walikuwa wameona mengi sana, bado yalibaki mengine mengi kabla ya kutua nyumbani wapate chakula cha mchana saa 5:45 asubuhi kikiwa kwa namna ya kafeteria. Ndipo walipoenda kwenye Idara ya Barua na Idara ya Invoisi na Kutunza Hesabu kwenye orofa ya tano. Halafu wakapita kwenye daraja (linaweza kuonekana kwenye picha iliyo katika ukurasa wa 15) linalounganisha Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights na majengo yaliyoko ng’ambo ya pili ya barabara. Katika sehemu hiyo wakatembelea Afisi ya Ujenzi, Shule ya Gileadi, Idara ya Kutengeneza Vibweta vya Vitabu, pia Idara ya Rangi na Majukwaa ya Kujengea, Duka la Kutengeneza Vifaa Vilivyoharibika, Mahali pa Kuunganisha Vitabu kwa Mikono na Mahali pa Udumishaji wa Mashine.

Wengi walipendezwa sana na Vyumba vya Kunasia Sauti, ambamo michezo ya kuigizwa makusanyikoni, usomaji wa Biblia na muziki vinatiwa katika tepe. Halafu wakasisimuka kuiona Idara ya Kunakilia Tepe. Kila siku tepe za kaseti elfu kumi na tano zinatengenezwa—tepe zaidi ya milioni tisa tangu idara hiyo ianzwe mwaka wa 1978! Lakini kabla ya chakula cha mchana walipaswa kuona Duka la Vifaa vya Umeme, Idara ya Vitabu vya Vipofu, Afisi ya Kujenga, Afisi ya Michoro, Afisi ya Mambo ya Makusanyiko, Idara ya Upigaji wa Picha, Afisi ya Uangalizi wa Wafanya Kazi wa Betheli, Mahali pa Kutengenezea Magari na Idara ya Usafirishaji wa Vitabu.

Lo! matembezi yenye kuteremesha namna gani muda wa saa tatu na nusu! Wote waliona kwamba kwa uhakika tengenezo la Yehova linasonga mbele. Jamaa ilipokwisha kula, wakaondoka tena kutembelea kiwanda. Wafanya kazi wa kiwandani walikuwa wamekwisha kufika kwenye migawo yao ya kazi saa 6:30 alasiri ili kuionyesha sehemu ile nyingine yote ya jamaa matumizi ya vifaa vinavyohusika katika kuchapa na kufunga vitabu vya Biblia. Zenye kupendeza zaidi ni zile mashine kubwa sana za ofseti zilizo mpya​—wakati wa matembezi, mashine tano zilikuwako na nyingine tatu zitaletwa mwaka huu. Mashine iliyo kubwa zaidi ya zote, yaani ile ya kuchapia Biblia, ina urefu wa futi 109 (meta 33)!

Baada ya kutembelea kiwanda kwa muda wa saa tatu, jamaa ilielekea nyumbani, wakiwa wamechoka lakini wamesisimuliwa sana na baraka ya Yehova waliyoiona wazi ikiwa juu ya mpanuko huo. Saa 10 ya jioni wote walikusanyika pamoja kwenye mahali pao mbalimbali katika vyumba sita vya kulia chakula ili wajifurahishe kiliwaji cha pekee. Halafu, baada ya pumziko fupi, wote wakaifurahia programu ya wakf yenye kutia moyo zaidi sana.

KULIUNGA MKONO TENGENEZO LA YEHOVA LINALOSONGA MBELE

Katika nchi nyingine nyingi, watu wa Yehova wanaipata roho ii hii ya kuwa na furaha na shauku wanapouona ushuhuda wa kwamba Yehova anazibariki jitihada zao za kupanua majengo yao ya kuenezea habari njema za ufalme wake. Katika nchi baada ya nchi majengo mapya ya tawi ama yamemalizwa hivi majuzi ama yangali yanaendelea kujengwa.

Bila shaka, ujenzi wote huo na mpanuko unaofanyika ulimwenguni pote unahitaji pesa. Ingawa Mashahidi wa Yehova hawajapata kuomba-omba misaada ya pesa, wale wanaopendezwa kushiriki kifedha kupanua faida za ufalme wa Yehova wanaweza kufanya hivyo kwa kupeleka michango yao kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti iliyo katika nchi yao. Upaji wa namna hiyo unapigiwa asante za kuthamini.

Watu wa Yehova wanalo agizo lililo wazi kabisa la kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu katika dunia yote inayokaliwa na watu kabla mwisho haujaja. (Mathayo 24:14) Sisi hatujui ni mpaka kadiri gani Mungu anakusudia kazi hii izidi kufanywa. Lakini unaweza kuwa na uhakika kwamba, hata kuwe na mambo gani wakati ujao, tengenezo la Yehova litasonga mbele likifanya yale aamuruyo Yeye.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Haya ni yale majengo yaliyokuwa yakiitwa Squibb ambayo sasa ni mali ya Mashahidi wa Yehova. Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights liko upande wa kulia

[Picha katika ukurasa wa 16]

Makao ya 124 Columbia Heights mwaka wa 1950

Kiwanda cha 117 Adams Street mwaka wa 1950

[Picha katika ukurasa wa 17]

107 Columbia Heights

Jengo “Towers”

119 Columbia Heights

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kiwanda chenye majengo manne katika Brooklyn

Mashamba ya Sosaiti yanayoitwa Watchtower Farms yakiwa na viwanda vya uchapaji na makao

[Picha katika ukurasa wa 19]

Fred Franz akitoa hotuba ya wakf

[Picha katika ukurasa wa 21]

Jengo la Afisi za 25 Columbia Heights, likiwa na wonyesho wa utendaji mbalimbali

1. Kuliingia Jengo la 25 Columbia Heights

2. Kutembelea chumba cha Baraza Inayoongoza

3. Kukitazama chumba cha kompyuta

4. Kuzuru Afisi ya Msimamizi

5. Kuchunguza picha chache za Idara ya Uchoraji wa Picha

6. Kuona mtambo wa kompyuta katika Idara ya Uandikaji

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki