Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 7/15 kur. 15-21
  • Tendo Lililounganishwa kwa Umoja Kufanya Ujenzi Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tendo Lililounganishwa kwa Umoja Kufanya Ujenzi Ulimwenguni Pote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UMOJA KATIKA MAHALI PA UJENZI
  • SEHEMU ILIYOTIMIZWA NA ROHO YA MUNGU
  • WACHOCHEWA WAJIFUNZE
  • KUUNGWA MKONO KWA NJIA YENYE UMOJA NA WALE WALIO SHAMBANI
  • “WAFANYA KAZI WA MIISHO YA JUMA” WENYE NIA
  • “DHABIHU YA SIFA”
  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Ujenzi Unaotusaidia Kuhubiri
    Jinsi Michango Yako Inavyotumiwa
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-Mwaka 1994
    1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 7/15 kur. 15-21

Tendo Lililounganishwa kwa Umoja Kufanya Ujenzi Ulimwenguni Pote

KUANZIA Sweden mpaka Korea, kuanzia Australia mpaka Ivory Coast, Mashahidi wa Yehova wanajenga. Katika makorija ya nchi mbalimbali kuna shughuli kubwa zinazoendelea, kuanzia kufanya marekebisho ya majengo ya zamani mpaka kujenga majengo mapya makubwa ya viwanda na afisi. Kwa nini ujenzi wote huu unaendelea?

Mashahidi wa Yehova wanaichukua kwa uzito amri ya Yesu ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19, NW) Je! wewe umepata kufikiria ni kazi nyingi namna gani inayohusika katika agizo hilo? Mwaka wa 1981 peke yake, Mashahidi wenye juhudi ulimwenguni pote walieneza vitabu na Biblia zaidi ya milioni 31 na vilevile magazeti zaidi ya milioni 234​—vyote vikiwa na ujumbe wenye kuokoa maisha wa ufalme wa Mungu. Vitabu, magazeti na Biblia hizo zilitoka wapi? Zilichapwa katika viwanda vilivyojengwa na vyenye kuendeshwa na Mashahidi wa Yehova. Wafanya kazi wenye kuendesha viwanda hivyo wamepewa makao wakiwa jamaa kubwa inayoitwa Betheli, yaani “nyumba ya Mungu.”

Mashahidi wanaoeneza vitabu hivi hukutana kwa ukawaida katika makundi 43,870, nayo yanapatikana katika karibu kila nchi ya dunia hii. Makundi hayo yanatunzwa na afisi za matawi, na kila moja inatunza eneo lake. Wakati makundi yanapoendelea kukua (mwaka 1981 makundi mapya 689 yalianzishwa), afisi za matawi zinakuwa na nafasi ndogo ya kufanyia kazi na basi inakuwa lazima zipanuliwe au nyingine mpya zitafutwe mahali pengine. Ni nani anayefanya ujenzi? Ni Mashahidi wa eneo linalohusika, nyakati zote inapowezekana. Juhudi ile ile inayowachochea kuuhubiri Ufalme na kutolea watu vitabu ndiyo inayotumika mahali pa ujenzi.

UMOJA KATIKA MAHALI PA UJENZI

“Kwa nini ninyi hamgombani?” ndivyo alivyouliza seremala asiye Shahidi katika Abidjan, Ivory Coast. “Mahali pengine pa kazi za ujenzi inakuwa vigumu sana kufanya kazi.” Maneno yake yamenenwa mara nyingi na watu wasio Mashahidi wanaosaidia kujenga makao yenye ukubwa wa kadiri ya Betheli na afisi ya tawi ya Sosaiti katika Ivory Coast, ambako hesabu ya makundi imeongezeka mara nne kwa muda wa miaka 10.

Umoja huo haupasi kushangaza mashahidi wa Kikristo wa Yehova kulingana na sala aliyotoa Yesu kwamba wafuasi wake wawe wameungana kwa umoja. (Yohana 17:23; linganisha Zaburi 133.) Ni kama alivyoeleza Shahidi mmoja katika Abidjan: “Hapa ni mahali pa ujenzi pa Yehova.”

Katika bara nyingine, Amerika ya Kusini, makao makubwa na kiwanda kikubwa cha Betheli vinaendelea kumalizika. Majengo hayo mapya yaliyo makubwa sana katika Brazil yana nafasi ya sakafuni iliyo karibu mara sita zaidi ya nafasi iliyokuwako kwanza. Hesabu ya Mashahidi katika nchi hiyo ndiyo ya pili kwa wingi ikilinganishwa na ya nchi yo yote ulimwenguni, nayo inaongezeka upesi-upesi. Mwaka 1980 ongezeko lilikuwa asilimia 6 (%). Gazeti la Cesario Lange lilipaita mahali pa ujenzi pa sehemu hiyo “jiji lililo ndani ya jiji jingine,” kisha likaendelea kusema: “Huko hakuna fujo wala kubishana-bishana kama inavyokuwa kawaida kati ya watu wanaojenga majengo makubwa. . . . Hali hiyo ya Kikristo inapafanya mahali hapo pawe tofauti na vile mahali pa ujenzi huwa kati ya raia za Brazil.” Nao umekuwa ujenzi mkubwa kama nini​—wenye kuhitaji kokoto nyingi ya kuweza kujaza gari kubwa mara 10,000, kuhitaji mawe na mchanga, na kokoto nyingi ambayo ikimwagwa iende juu inaweza kuwa na urefu ulio mara mbili za Mlima Everest (mlima ulio mrefu zaidi ulimwenguni)!

Kundi jingine la Mashahidi wanaojenga wakiwa kama shirika la nyuki linapatikana katika Australia, ambako gazeti News la Campbelltown Ingleburn lilisema kwamba, “Wengine walikuwa wakisema jengo jipya la Mashahidi wa Yehova wa Australia huko Ingleburn ni ndoto kwa fundi wa ujenzi.” Kwa nini? “Wao hawana magombano ya aina yo yote wanapoendesha kazi.” Kundi lote la wafanya kazi 220 ni Mashahidi wa Yehova. Litakapokuwa limemalizika mwaka huu wa 1982, jengo hilo litausaidia sana utendaji wa kuuhubiri Ufalme wa Mashahidi 31,898 waliotapakaa katika nchi kubwa sana ya Australia.

SEHEMU ILIYOTIMIZWA NA ROHO YA MUNGU

Maelezo hayo ya waandikaji wa magazeti na watazamaji wengine ni mfano mdogo tu wa mambo yanayoonekana ulimwenguni pote. Mashahidi wa Yehova huwa na roho yenye kuonekana wazi sana ya kuwa na umoja na kusudi wakati wanapofanya kazi. Inatokana na nini? Inatokana na roho takatifu ya Mungu, au nguvu ya utendaji, inayoendeleza umoja na amani.​—Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 4:3.

Uwezo wenye kuwachochea wa roho ya Mungu unaonekana wazi katika maelezo ya wale ambao wamejitoa wafanye kazi sehemu mbalimbali za ujenzi ulimwenguni pote. Kwa mfano, katika Denmark tawi la sasa lilijengwa mwaka 1957 na sasa wanaokaa humo wamesongamana sana. Yale makao mapya ya Betheli yenye vyumba 50 ambayo yanaendelea kujengwa yatakuwa na nafasi ya kukaliwa na wafanya kazi wengi zaidi, halafu itawezekana kuchapa magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yakiwa na jumla ya kurasa 32 katika lugha ya taifa la Denmark, badala ya kuwa na kurasa zile za sasa 24. Jengo jipya hilo litakuwa na afisi ya tawi na kiwanda kikubwa. “Tukiwa na majengo mapya hayo ya tawi tutaweza kutumikia kina ndugu na watu wa eneo tunalotunza kwa njia nzuri zaidi,” ndivyo linavyosema tawi la huko. Eneo hilo ni pamoja na sehemu zilizotapakaa za Greenland, lceland na Visiwa Faroe.

Shahidi Mdenmark ambaye ni stadi wa kutengeneza mabomba ya maji na ambaye pia ni mwanamume mwenye jamaa alifanya uamuzi ufuatao asaidie katika ujenzi: “Ujenzi ulipokaribia kuanza, mimi nilitoa taarifa [ya kuacha kazi ya kimwili] nasi tukauza vifaa vya nyumba yetu Tuliamini sana kwamba baada ya kuumaliza ujenzi mimi ningetafuta kazi ya kuajiriwa na nyumba tena. Tutafikiria hilo kazi ikimalizika. Sisi tumejionea jinsi Yehova anavyotulisha wakati tunapomtia jaribuni na kuutafuta ufalme wake kwanza.” Hakika huo ni wonyesho mzuri sana wa kufuata maoni ya Yesu kwenye Mathayo 6:​25-33!

Roho kama iyo hiyo imeonekana huko Kanada ambako Mashahidi wa nchi kubwa hiyo wametoka sehemu zote wakajitoa kusaidia ujenzi wa ofisi mpya na kiwanda kipya cha tawi karibu na Toronto. Kiwanda kipya hicho ni kirefu tena kama nusu ya uwanja wa mpira na ni chenye upana wa futi 240 (metre 73), nayo makao mapya yatakuwa na nafasi ya washiriki wa jamaa ya Betheli 250. Katika Kanada kilele kisichopata kuwapo hapo zamani kilifikiwa mwaka 1981 kikiwa cha wahubiri wa Ufalme 67,328.

Shahidi mmoja wa Kanada alifunga biashara yake kisha ukaenda maili 2,200 (kilomita 3,540) akasimamie kuwekwa kwa mfumo wa paa refu kwenye lile jengo jipya. Mwishowe mkewe na wanawe wawili wakamfuata. Shahidi huyo anasema: “Hali yetu ya kiroho imeinuliwa juu na utendaji huu. Umefanya jamaa yetu ifikirie upainia, nasi tunakusudia kuanza upainia [utendaji wa kuhubiri wakati wote] baada ya kuondoka kwenye ujenzi. Utendaji huu umetupa sisi roho ya upainia ambayo hapo kwanza hatukuwa nayo.”

Maelezo ya Shahidi wa Australia yanapendeza sana. Yeye ana mke na watoto wawili. Alifunga biashara yake ya kufanya mikataba ya ujenzi na kuuza nyumba yake kisha akahamishia jamaa maili 930 (kilomita 1,500) kwenye uwanja wa Betheli mpya ya Australia ili wakajenge. “Tulipokwisha kuamua kuja ndipo tulipotambua kwamba tulikuwa tumeingilia sana biashara ya kimwili na kwamba ingetuchukua muda mrefu kujiondoa kwenye shughuli hizo za kilimwengu.” Alisema hivyo waziwazi kabisa. “Sasa tumeridhika sana na ‘vitu tunavyovihitaji kikweli’ na tumekaza nia tuendelee kuwa na uhuru wa kushiriki zaidi katika ‘utumishi mtakatifu.’ “​—Warumi 12:1, NW; Waebrania 13:5.

WACHOCHEWA WAJIFUNZE

Bila shaka, si wafanya kazi wote wenye kusaidia katika ujenzi wa makao mapya na viwanda vipya vya Betheli walio na ujuzi wa ujenzi. Sawa na vile roho ya Yehova imewachochea mafundi hodari wajitoe kujenga Betheli, ndivyo imechochea vijana na watu wasio na ujuzi waje, nayo imewasaidia kujifunza kazi ambazo hawakuwa wakizijua.

Katika Sweden Mashahidi wa Yehova ni kama 17,770. Elfu tano kati yao walijitoa wasaidie kuijenga Betheli mpya ya Sweden! Hiyo ni zaidi ya mmoja kati ya kila wahubiri wanne wa Ufalme walio katika nchi hiyo. Jengo jipya hilo lina kiasi kinachozidi ekari moja cha nafasi ya sakafuni, na hiyo ni nafasi ya idara ya uchapaji tu. Basi sasa utumishi mzuri zaidi unaweza kutolewa kwa ajili ya shamba la Sweden. Ingawa asilimia 85 (%) ya wenye kujitoa ilikuwa ya watu wasio na ujuzi, walifanya kazi nzuri. Dada mmoja, ambaye kazi yake ni kupamba nywele za watu, alijifunza upimaji na uchoraji wa maeneo ya ardhi kwa njia nzuri sana mpaka akaandikwa kazi na shirika la ujenzi moja kwa moja alipokwisha kurudi nyumbani.

Katika Brazil, madirisha ya madini nzuri ya aluminiamu yalipokuwa hayawezi kununuliwa, Mashahidi 20 ambao hawakuwa na ujuzi walitengeneza madirisha ya namna hiyo zaidi ya 700 bada ya kupewa mazoezi ya muda mfupi. Na katika Italia, ambako kiwanda kipya kilimalizwa hivi majuzi, Mashahidi vijana walijifunza kuendesha winchi kubwa (kreni), kutumia tingatinga la Katapila, kutengeneza kokoto, kuendesha mashini ya kupigia lipu (plasta) na kutumia simiti kuunganisha matofali katika ujenzi wa kuta. Kiwanda kipya hicho kinahitajiwa sana katika Italia. Katika nchi hiyo watangazaji wa Ufalme 90,553 wa Italia walifurahi sana kupata hudhurio la watu 187,165 katika Ukumbusho wa mwaka jana!

Shahidi kijana katika Australia alikuwa karibu kurudia chuo kikuu wakati aliposikia mambo yaliyoonwa yakamfanya asaidie ujenzi katika nchi hiyo. “Mwaka mmoja ulipokwisha nikaamua kuanza kazi ya kuhubiri wakati wote badala ya kurudia chuo kikuu,” asema yeye. “Sasa nikitazama nyuma, naweza kuona namna shughuli hiyo ya ujenzi ilivyonipa ujuzi wa kiroho na kunichochea niache maisha ya chuo kikuu niliyokuwa nikifurahia lakini yakawa yakinielekeza upande usiofaa.”

KUUNGWA MKONO KWA NJIA YENYE UMOJA NA WALE WALIO SHAMBANI

Si wote kati ya Mashahidi wa Yehova wanaoweza kutumia wakati wote wakisaidia ujenzi wa matawi, lakini wote wanaweza kuiunga mkono kazi hiyo​—na ndivyo wafanyavyo! Katika nchi ya Spania, kwa mfano, ambako hesabu ya Mashahidi imeongezeka kutoka 10,000 kufika zaidi ya 47,906 muda wa kumi moja la miaka iliyopita, tawi jipya linahitajiwa upesi. Uwanja mzuri sana ulipatikana, nao tayari ulikuwa na jengo lisilokamilika kabisa la ukubwa uliotakiwa. Tatizo likawa kwamba mwenye mahali hapo alitaka alipwe fedha taslimu, fedha nyingi weee!

Hakukuwa na wakati wa kutosha kuchangisha fedha. Je! Mashahidi Waspania wangesaidia? Wao walijibu kwa kuitikia Ndiyo, tena kwa haraka na kwa moyo kamili! Wengine “walijitokeza wakiwa na pete zao za dhahabu na za fedha, vikuku na mikufu,” lasema tawi la huko.“Watoto wadogo walituma fedha chache walizokuwa wamejiwekea akiba. Mapainia wa pekee walisema kiasi fulani cha alawansi zao za mavazi na tiba kitumiwe kwenye ujenzi wa Betheli. Ndugu wengi walijinyima malikizo yao wakayatumia kusaidia kazi. Kundi moja lililo katika Huelva huenda kwa wingi kwenye ua wa ndugu mmoja wenye vitu vilivyoharibika-haribika kuchagua vifaa vinavyoweza kutumika, na kikundi cha vijana katika Barcelona husaidia shirika lenye kutengeneza maziwa ya mgando kuyafunga katika vifuko. Katika hali zote hizo, fedha zipatikanazo hupelekwa kila mwezi ziwe za ujenzi wa Betheli.”

Je! si roho ya Mungu inayofanya kazi hiyo? Jambo hilo linatukumbusha sana namna Waisraeli walivyoitikia walipopewa nafasi ya kuchangia ujenzi wa hema takatifu!​—Kutoka 35:4-9, 21, 22; 36:7.

Ndivyo mambo yanavyoendelea ulimwenguni pote. Katika nchi ya Netherlands, ambako wahubiri wapya wa Ufalme 763 walibatizwa mwaka wa 1981, Betheli mpya na mahali pa uchapaji panaendelea kujengwa. Licha ya watu 80 wanaokuwa na zamu mbalimbali za kusaidia nyakati za miisho ya juma, ndugu wa hapo wamesaidia kwa njia nyingine nyingi. Wametoa misaada ya vyombo vya kazi na mavazi ya kazi, na wengine wao wamefanya hivyo kwa njia yenye kugutusha moyo sana. “Dada mmoja,” lasema tawi la huko, “akiwa mgonjwa mahututi na akijua kifo chake kilikuwa kimekaribia, alianza kufuma (kushona) stokingi (soksi) za sufu (manyoya ya wanyama) za kuvaliwa na kila mfanya kazi yafikapo majira ya baridi nyingi.”

Katika Afrika Kusini, ambako gazeti Mnara wa Mlinzi huchapwa katika lugha 13, nafasi zaidi inahitajiwa ya watafsiri na ya kuwekea vifaa vya uchapaji. Kwa hiyo kazi imeanza ya jengo jipya.Tawi la huko linatuambia “kina ndugu wametuunga mkono kwa njia ya kutuchangamsha sana. Kundi moja lilipanga kuchuma matunda ya mkulima mmoja naye akawapa theluthi mbili za fedha zilizopatikana ili ziwe za ujenzi. Dada wengi waliuza mavazi yaliyotumika . . . mume na mke wazee-wazee wakatoa fungu zima la vikombe vya chai na visahani liuzwe.”

Vijana wanaonyesha roho iyo hiyo. Katika Jamhuri ya Mwungano wa Ujeremani, ambako vitabu vya nchi nyingi za Ulaya vinachapiwa, lile tawi la kwanza katika Wiesbaden limepanuliwa mara tano, na uchunguzi umekwisha kufanywa juu ya uwezekano wa upanuzi zaidi. Kwa hiyo sasa majengo mapya kabisa katika Selters, zapata maili 25 (kilomita 40) kutoka hapo yanaendelea kujengwa yasaidie kutimiza mahitaji ya shamba la Ulaya kwa kuchapa vitabu katika lugha 14. Jengo jipya la kiwanda litakuwa na nafasi zaidi ya sakafuni iliyo kubwa mara nne kuliko uwanja wa mpira. Jengo hilo litafanya kazi nzuri sana ya kuunganisha utendaji mbalimbali. Limekusudiwa kutimiza mahitaji mbalimbali ya wenye kutumia majengo yale mengine, ambako watakuwa na Mashahidi 450 wenye kufanya kazi kwa hiari. Mtoto mdogo aitwaye Matthias, mwenye umri wa miaka sita tu, ‘alifagia’ akiba yake yote ya fedha iwe ya ujenzi, akatoa fedha zinazolingana na shilingi 250!

Wakati tawi la Visiwa vya Uingereza lilipowekwa wakf mwaka 1959 lilikuwa na nafasi kubwa sana, lakini sasa mambo yamekuwa mengine. Hesabu ya watangazaji wa Ufalme imekuwa zaidi ya maradufu langu wakati huo, kwa hiyo makao ya Betheli yanapanuliwa ili nafasi iwepo ya wafanya kazi zaidi. Pia, maili kadha kutoka hapo kiwanda kimenunuliwa cha kuwekea mashini ya ofseti ya uchapaji wa kutumia rangi nne. Nyakati inapojulikana vitu fulani vinahitajiwa, roho ya Yehova husukuma kina ndugu wasaidie. Ndugu mmoja aliombwa akaangalie bei ya kofia ngumu za kukinga vichwa vya wafanya kazi. Siku mbili baadaye akaja kusema: “Mimi sikuja niwajulishe bei. Nimekuja niwaletee kofia mlizohitaji.”

“WAFANYA KAZI WA MIISHO YA JUMA” WENYE NIA

Katika nchi nyingi “wafanya kazi wa miisho ya juma” wanasaidia sana ujenzi wa tawi. Katika Ivory Coast, manne kati ya makundi 16 ya Abidjan huombwa yasaidie ujenzi wa tawi kila Jumapili, na kufikia Oktoba mwaka jana kina ndugu walikuwa wametumia saa zaidi ya 10,000 katika kazi hiyo. Katika Italia, kati ya ndugu 30 na 50 wanasaidia kila juma na kuwatia nguvu wafanya kazi wa kila siku. Wao wametoka sehemu zote za Italia na vilevile kwenye visiwa ya Sicily na Sardnia. “Kwa njia hiyo,” lasema tawi la huko, “ndugu wote wa Italia wanahusika katika ujenzi huu.”

Mwaka wa 1971 Mashahidi walikuwa 10,711 katika Japan, lakini kufikia Juni 1981, hesabu yao ikawa imepanda na kuwa 62,381, au ongezeko la asilimia (%) 482! Basi si ajabu kwamba makao ya Betheli na kiwanda cha uchapaji vilivyojengwa miaka ya kwanza-kwanza ya 1970 kiliishiwa na nafasi baada ya muda mfupi! Jengo jipya linaloendelea kujengwa kule Ebina ni moja la majengo makubwa zaidi yaliyopata kujengwa na Mashahidi wa Yehova mahali po pote ulimwenguni. Sehemu iliyo kubwa ya jengo hilo ina nafasi ya ekari tisa za ardhi na humo mna nafasi ya kuwekea mashine mbili kubwa za ofseti zinazopiga chapa kwa kutumia rangi. Kazi ya kujenga makao mapya ya Betheli na kiwanda ilianza mwaka wa 1978, na wengi sana wamejitoa kusaidia. Jumamosi ya kwanza na ya tatu ya kila mwezi zinaitwa siku za utumishi wa kujitolea ujenzi wa tawi katika Japan, na watu wa makundi ya karibu na ya mbali wanasafiri kwa motakaa, gari-moshi au bas za kukodi ili washiriki kazini. Jumamosi moja kulikuwa na wafanya kazi 1,000, nao walikuja wakiwa na chakula cha mchana ili washinde kazini. Kwa sababu ya kuwa na mamia ya wenye hiari ya kusaidia, hata kung’oa misumari kunafurahisha.

Katika Australia, ambako makao mapya ya Betheli yatakuwa na nafasi ya watu 135, wafanya kazi wa muda wametumiwa kwa njia nzuri sana. Katika mwezi Agosti wa 1980 programu ya pekee ya juma mbili ilianzishwa kwa ajili ya wafanya kazi waliotaka kusaidia lakini wakawa wanashindwa kuhamia huko kwa muda mrefu wakiwa pamoja na jamaa zao. Mwangalizi wa programu hiyo anasema kwamba “kati ya muda wa miezi sita ya kwanza, karibu ndugu 500 wamesafiri wakaja kukaa nasi. Wengi wao wamefunga safari ya kuja na kurudi ya kilomita zisizopungua 2,000 [maili 1,240], na wengine wakafunga safari ya kurudi ya umbali wa kilomita 8,500 [maili 5,270].”

Wafanya kazi hawa wenye hiari, ‘wenye kuwaka kwa roho ya Mungu,’ wanafurahi kujilipia gharama ya kufika kwenye ujenzi, na vilevile kupata hasara ya kutokulipwa mshahara muda wa juma mbili. (Warumi 12:11, NW”) “Kikundi chenye jumla ya ndugu tisa hujilipia nauli za kusafiri kwa ndege kutoka Gold Coast kuja Sydney, na huo ni umbali wa karibu kilomita 1,000 (maili 620), kila wakati wanapohitajiwa kuja kumwaga saruji kwa wingi,” lasema tawi la huko, na kuongeza hivi: “Na kila wakati wanang’aa kwa furaha kwa sababu wameweza kushiriki kazini. Mshahara wa pekee wanaoomba walipwe ni kukaribishwa tena.”

Wengine katika Australia wanasaidia pia. Wanafanya hivyo kwa ukaribishaji wao wa Kikristo. “Kwa kuwa ni kawaida yetu kujaribu kupanga safari ya bas za mikoa mbalimbali, makundi yaliyo katika njia tunayopitia yanatutolea chakula na kushirikiana nasi kwenye kila kituo cha mapumziko,” aeleza mwangalizi wa programu. “Inapendeza sana kuona namna kila kundi limekuwa na nia ya kutusaidia! Kikundi kimoja chenye wahubiri 30 kilikuwa tayari kutulipia gharama za kula kiamsha-kinywa kwenye mkahawa. Walitaka kutulipia sisi sote tuliojaa ndani ya bas moja. Sababu ni kwamba bas yetu ingepitia mji wao wakiwa wamekwenda kuhudhuria kusanyiko la mzunguko katika eneo jingine.” Kwa kweli, Mashahidi hawa wa Australia wanafanya ‘kazi ya uaminifu’ kwa ‘kuwasafirisha ndugu zao kama ipasavyo kwa Mungu.’​—3 Yohana 5, 6.

“DHABIHU YA SIFA”

Ndiyo, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kutumia kwa hiari wakati wao, nguvu zao na fedha zao katika ujenzi ulimwenguni pote. Vifaa vya uchapaji vitasimamishwa, au vimekwisha kusimamishwa, katika majengo mapya huko Kanada, Australia, Denmark, Netherlands, Italia, Spania, Sweden, Jamhuri ya Mwungano wa Ujeremani, Uingereza, Ghana, Zambia, Afrika kusini, Nigeria, Brazil na Japan. Na Kila wakati nchi nyingine nyingi zinazidi kuanza ujenzi.

Dhabihu ya kweli inayotolewa katika nchi zote ni ‘dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina la Yehova.’ (Waebrania 13:15) Mashahidi wa Yehova wanahitaji kujenga afisi na viwanda, kusimamia kazi ya kuhubiri na kuchapa magazeti na kutayarisha vitabu kwa ajili ya utangazaji wao wenye juhudi wanaofanya mbele ya watu wote ili kuwajulisha jina la Yehova. Kwa hiyo isionekane kuwa ajabu kwamba roho ya Mungu yenye kuunganisha watu kwa umoja inawasaidia watu wake wafanye kazi kwa upendo na umoja kwenye shughuli hizo za ujenzi, kwa maana wao wanatenda kupatana na mapenzi yake yanayosema “habari njema” zihubiriwe ulimwenguni pote katika hizi “siku za mwisho.” ​—⁠Mathayo 24:14; Matendo 2:​17-21.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kati ya wafanya kazi 175 wenye kujitoa kwa hiari wajenge tawi jipya la Denmark kuna jamaa mbalimbali 46. Ili wajitoe, jamaa ya kina Jensen iliuza makao na biashara yao

[Picha katika ukurasa wa 18]

Makao mapya ya Betheli huko Kanada. Utendaji wa Mashahidi wa Kanada zaidi ya 67,000 unasimamiwa na makao haya

[Picha katika ukurasa wa 19]

Katika Ujeremani, mamia ya wanaume na wanawake wenye kujitoa husaidia nyakati za miisho ya juma katika ujenzi wa makao ya Betheli na kiwanda cha uchapaji huko Selters

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ili wasaidie ujenzi wa kiwanda kipya cha uchapaji huko Australia, Mashahidi wengi, kama Peter na Raelynn Johnson, walisafiri mamia ya maili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki