Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Tulifurahia kujifunza unabii mbalimbali wa Danieli kama ulivyotolewa katika “Mnara wa Mlinzi.” Lakini, kwa nini tarehe za nyakati tatu na nusu za Ufunuo 11:3 zatofautiana na za kitabu “Upeo wa Ufunuo”?
Ndiyo, Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1993, lilikuwa na badiliko dogo kwa habari ya tarehe ya kutimizwa kwa Ufunuo 11:3. Kwa nini?
Ebu kwanza tuangalie Ufunuo 11:2, ambalo mwisho walo wataja “miezi arobaini na miwili.” Twaendelea kusoma katika mstari wa 3: “Nitawaruhusu mashahidi wangu wawili, nao watatoa unabii siku elfu na mia mbili na sitini, hali wamevikwa magunia.” Hilo lahusu pindi gani?
Naam, kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wametambua kwamba unabii huo ulitimizwa kwa Wakristo watiwa-mafuta kwa roho baada ya mwisho wa “majira ya mataifa” (Nyakati za Mataifa) katika 1914. (Luka 21:24; 2 Wakorintho 1:21, 22) Kikieleza juu ya hilo, Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!a (1988) chasema hivi kwenye ukurasa 164: “Kulikuwako wakati uliotiwa alama wa miaka mitatu na nusu ambao magumu yaliyowapata watu wa Mungu yalilingana na matukio yaliyotolewa unabii hapa—kuanzia wakati wa kufyatuka kwa vita ya kwanza ya ulimwengu katika sehemu ya mwisho ya mwaka 1914 na kuendelea mpaka mapema mwa 1918.”
Ona kwamba tarehe iliyotajwa ilikuwa “kufyatuka kwa vita ya kwanza ya ulimwengu katika sehemu ya mwisho ya 1914 [hadi] mapema mwa 1918.” Hilo lapatana na tarehe ambayo hutolewa kwa kawaida, kama vile katika kitabu “Then Is Finished the Mystery of God,” kurasa 261-4, (1969).b
Hata hivyo, Mnara wa Mlinzi lilikazia akili unabii mbalimbali katika Danieli, kitabu kinachotaja mara mbili kipindi kinacholingana na kile kinachotajwa baadaye katika Ufunuo—miaka 3 1/2, au miezi 42. Kusema kihususa, Danieli 7:25 lasema kwamba watakatifu wa Mungu wangetaabishwa “kwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati,” au nyakati 3 1/2. Baadaye, Danieli 12:7 latabiri “wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati,” au nyakati 3 1/2, ambao ungefikia upeo kwa ‘kuvunjwa kwa nguvu za hao watu watakatifu.’
Kwa hiyo tuna unabii mbalimbali unaoshughulika na kipindi kinacholingana kwenye Danieli 7:25, Danieli 12:7, na Ufunuo 11:2, 3, na vilevile kwenye Ufunuo 13:5. Vichapo vyetu vimeonyesha kwamba huo wote ulitimizwa katika kipindi cha 1914 hadi 1918. Lakini katika kushughulikia kila mmoja wa unabii huo, tarehe za kuanza na kumalizika zatofautiana kidogo.
Lakini, Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1993, liliuliza hivi: “Unabii huo wote wenye kufanana ulitimizwaje?” Naam, unabii wa nyakati 3 1/2 unaotajwa kwenye Danieli 7:25, Danieli 12:7, na Ufunuo 11:3 ulitambuliwa kuwa ‘unabii wenye kufanana.’ Kwa hiyo, wote ungepatana kwa mwanzo wao na mwisho wao.
Kwa habari ya mwisho wao, gazeti lilionyesha kwamba kutaabishwa kwa watiwa-mafuta wa Mungu (Danieli 7:25) kulifikia upeo mnamo Juni 1918 wakati J. F. Rutherford na wakurugenzi wengine wa Watch Tower Bible and Tract Society ‘walihukumiwa kifungo cha muda mrefu gerezani kwa madai bandia.’ Kwa hakika tukio hilo lilikuwa “kuvunja nguvu za hao watu watakatifu,” kama itajwavyo kwenye Danieli 12:7.
Kuhesabu kuanzia Juni 1918 kurudi nyuma kwatufikisha Desemba 1914 kwa ajili ya nyakati 3 1/2. Katika mwezi huo wa kumalizia 1914, watiwa-mafuta wa Mungu walioko duniani walijifunza andiko la mwaka uliofuata: “Je! mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi?”—Mathayo 20:20-23. Makala iliyolitangaza lilionya hivi: “Nani ajuaye kwamba kwaweza kuwa jaribu la kipekee, kikombe cha kuteseka au cha kuaibishwa, kwa wafuasi waaminifu-washikamanifu wa Mwana-Kondoo katika 1915!” Kama Danieli 7:25 ilivyotabiri kwa kipindi hiki cha nyakati 3 1/2, ‘mnyanyaso ulitokea na kuendelea dhidi ya watakatifu hao wenyewe wa Aliye Mkuu Kabisa.’ Mataifa yalijiingiza katika Vita ya Ulimwengu 1, jambo lililofanya liwe rahisi kuwanyanyasa bila sababu. Mkataa ni huu: Unabii wote tatu unaofanana—Danieli 7:25, 12:7, na Ufunuo 11:3—ulitimizwa katika miaka 3 1/2, au miezi 42, kutokea Desemba 1914 hadi Juni 1918.
Hilo laeleza rekebisho dogo katika tarehe ya utimizo wa Ufunuo 11:3. Twaweza kukumbuka rekebisho hilo akilini tujifunzapo na kutumia kitabu Upeo wa Ufunuo katika wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.