Usiache upweke uathiri vibaya maisha yako
UPWEKE waweza kuathiri maisha za wote vijana kwa wazee. Asema mwandikaji Judith Viorst katika gazeti Redbook: “Upweke hulemea kama jiwe katika moyo. . . . Upweke hutufanya tuhisi utupu na hali ya kutamauka. Upweke hutufanya tuhisi kama mtoto asiye na mama, kama mwana-kondoo aliyepotea, akiwa mdogo sana na kupotea katika ulimwengu mkubwa sana usiojali.”—Septemba 1991.
Kuwa mbali na marafiki, mazingira mageni, talaka, kufiwa, au kuvunjika kwa uwasiliano—mambo ya aina nyingi yaweza kukufanya uhisi upweke. Hata wakiwa katikati ya watu wengine, watu fulani ni wapweke sana.
Unaweza Kufanya Nini?
Ukipatwa na upweke, je, uwe tu mtesekaji asiyejiweza? Je, kuna jambo uwezalo kufanya ili kuzuia upweke usikuharibu hatua kwa hatua au kudhoofisha tamaa yako ya kuishi? Kwa kweli unaweza. Kuna mashauri mengi yenye mafaa. Na mashauri mengi mazuri yanatolewa katika Neno la Mungu lenye pumzi yake, Biblia. Kitia moyo kama hicho chaweza kuwa ndicho unachohitaji kukabili upweke.—Mathayo 11:28, 29.
Kwa kielelezo, waweza kupata kitia moyo katika kusoma juu ya Ruthu, mwanamke mchanga aliyeishi katika Mashariki ya Kati miaka ipatayo 3,000 iliyopita. Yeye alielekea zaidi kupatwa na upweke. Mume wake alipokufa, alienda pamoja na mama-mkwe wake kuishi katika mazingira mageni ya Israeli. (Ruthu 2:11) Ingawa hakuwa na familia yake na marafiki wake wa zamani naye alikuwa mgeni katika nchi geni, hakuna mahali popote katika Biblia ionyeshapo kwamba yeye aliacha upweke umshinde. Waweza kusoma masimulizi yake katika kitabu cha Biblia cha Ruthu.
Kama Ruthu, wahitaji kudumisha mtazamo mzuri. Jinsi unavyofikiria mambo na matukio yaweza kukuza upweke. Ann, ambaye kwa miaka minne alimtunza baba yake aliyekuwa akiugua ungonjwa wa kudhoofisha, athibitisha jambo hilo. Baba yake alipokufa alikuja kuwa mpweke sana. “Nilihisi kana kwamba nilikuwa katika utupu fulani, nikiwa mtu asiyefaa kabisa—kana kwamba hakuna mtu aliyenihitaji tena,” yeye asema. “Lakini nilikabili uhakika wa kwamba maisha yangu yalikuwa yamebadilika sasa, na nikang’amua kwamba ili nishinde upweke wangu ilikuwa ni lazima nitumie kwa njia bora zaidi hali zangu za sasa.” Nyakati nyingine huwezi kubadili hali zako, lakini yawezekana kwamba waweza kubadili mtazamo wako kuzielekea.
Ingawa kwasaidia, kujishughulisha katika utendaji wenye kuthawabisha hakuandai msaada wote katika kukabili upweke. Irene, aliyekuwa mjane baada tu ya miezi sita ya ndoa, aliona ukweli wa jambo hili katika hali yake. “Niliona kwamba upweke ulinipata sana nilipokuwa na shughuli kidogo zaidi,” yeye asema, “kwa hiyo nilikazia fikira kujishughulisha na wengine na kuwasaidia kukabili matatizo yao.” Kusaidia wengine huleta furaha, na Wakristo wapweke waweza kupata mambo mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.—Matendo 20:35; 1 Wakorintho 15:58.
Acha Marafiki Wasaidie
The New York Times Magazine laeleza juu ya watoto wapweke kuwa wameumizwa na “majeraha ya urafiki.” (Aprili 28, 1991) Watu wengi wapweke, vijana kwa wazee-wazee, huhisi urafiki. Kwa hiyo ni mafaa makubwa kuwa na ule urafiki wa kweli ambao kutaniko la Kikristo lenye kujali huandaa. Jitahidi kupata marafiki wengi zaidi katika kutaniko, nao wakusaidie katika hali zozote wawezazo. Hiyo ni sababu moja ya kuwa na marafiki—ili kukutegemeza katika nyakati za matatizo.—Mithali 17:17; 18:24.
Lakini, ujue kwamba kwa sababu ya maumivu yako ya kihisia, hasa unaweza kufanya iwe vigumu kwa marafiki kukusaidia. Kwa njia gani? Mwandikaji Jeffrey Young aeleza: “Watu fulani wapweke. . . hupoteza wale waelekeao kuwa marafiki, ama kwa kudhibiti sana mazungumzo ama kwa kusema mambo yachukizayo au yasiyofaa. Kwa njia moja au nyingine, watu ambao daima ni wapweke huelekea kuharibu mahusiano ya karibu.”—U.S.News & World Report, Septemba 17, 1984.
Nyakati nyingine, waweza kuharibu mambo zaidi kwa kujitenga na watu wengine. Peter, mtu aliye katika miaka ya 50, alifanya hivyo. Baada ya mke wake kufa, yeye alijikuta akijitenga na wengine, hata ingawa moyoni mwake kabisa alitaka msaada wao. “Nyakati nyingine,” yeye asema, “Nilishindwa kabisa kukabili watu wengine, na baada ya muda nilijikuta nikijitenga na watu.” Kufanya hivyo kwaweza kuwa hatari. Ingawa pindi za kuwa peke yako ni zenye mafaa, kujitenga kunadhuru. (Mithali 18:1) Peter alitambua jambo hilo. Yeye asema: “Hatimaye nilishinda hali hiyo, nikaikabili hali yangu, na kwa msaada wa marafiki wangu, niliweza tena kuanzisha maisha yangu upya.”
Lakini usidhanie kwamba wengine wana wajibu fulani wa kukusaidia. Jaribu kutokuwa mwenye kudai mno. Kubali kwa furaha fadhili yoyote ionyeshwayo, na uonyeshe uthamini kwayo. Lakini kumbuka pia shauri hili zuri lipatikanalo kwenye Mithali 25:17: “Mguu wako usiingie katika nyumba ya jirani yako ila kwa kiasi; asije akakukinai na kukuchukia.” Frances, aliyekabili upweke mwingi sana mume wake alipokufa baada ya miaka 35 ya ndoa, ahisi kwamba tahadhari kama hiyo ni muhimu. “Uwe mwenye kufikiri kuzuri kwa mataraji yako,” yeye asema, “na usidai mno kutoka kwa wengine. Usiwe daima mlangoni mwa mtu kutafuta msaada.”
Yehova Anajali
Hata kama marafiki wa kibinadamu hutuvunja moyo nyakati nyingine, bado unaweza kuwa na Yehova Mungu akiwa Rafiki yako. Uwe na hakika kwamba anakujali. Dumisha tumaini lako kwake likiwa na nguvu, na uendelee kutafuta kimbilio katika utunzi wake wenye ulinzi. (Zaburi 27:10; 91:1, 2; Mithali 3:5, 6) Yule Mmoabu Ruthu alifanya hivyo naye alithawabishwa sana. Kwani, hata alikuja kuwa nyanya ya Yesu Kristo!—Ruthu 2:12; 4:17; Mathayo 1:5, 16.
Sali kwa Yehova daima. (Zaburi 34:4; 62:7, 8) Margaret alipata kwamba sala ilimpa nguvu sana katika kukabili upweke. Yeye alishiriki katika huduma ya wakati wote pamoja na mume wake mpaka alipokufa akiwa angali kijana. “Sikuzote mimi huona ikiwa vizuri kusali kwa sauti na kumwambia Yehova kila kitu, hofu zangu na wasiwasi wangu,” yeye asema. “Jambo hilo lilinisaidia kuona mambo kwa njia ifaayo upweke uliponipata. Na kuona Yehova akijibu sala hizo kulinipa uhakika.” Yeye hufaidika sana kufuata shauri la mtume Petro: “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”—1 Petro 5:6, 7; Zaburi 55:22.
Uhusiano mzuri na Yehova utakusaidia kudumisha jambo ambalo watu wengi wapweke hupoteza—kujistahi. Mume wake alipokufa kwa kansa, mwandikaji-habari Jeannette Kupfermann aliandika juu ya “hisia ya kujishusha staha na kutofaa kitu.” Yeye alisema: “Ni hisia hii ya kutofaa kitu inayofanya wajane wengi wapatwe na mshuko wa moyo uwezao kusababisha kujiua.”
Kumbuka kwamba Yehova anakuthamini sana. Yeye hafikirii kwamba wewe hufai kitu. (Yohana 3:16) Mungu atakutegemeza jinsi alivyotegemeza watu wake Waisraeli katika nyakati zilizopita. Yeye aliwaambia: “Sikukutupa. Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”—Isaya 41:9, 10.
Usimlaumu Mungu
Jambo la maana zaidi, usimlaumu Mungu kwa sababu ya upweke wako. Yehova hausababishi. Kusudi lake sikuzote limekuwa kwamba wewe, na wanadamu wote, ufurahie uandamani mzuri, wenye kuridhisha. Mungu alipomwumba Adamu, alisema hivi: “Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.” (Mwanzo 2:18) Na hivyo ndivyo Mungu alivyofanya alipomwumba Hawa, mwanamke wa kwanza. Kama usingalikuwa ule uasi wa kishetani, mwanamume na mwanamke na ile familia waliyotokeza hawangalipatwa na upweke.
Hali ya Yehova ya kuruhusu uovu uwepo kwa muda bila shaka imefanya upweke uongezeke na mateseko mengine kutukia. Hata hivyo, kumbuka vizuri akilini kwamba hali hiyo ni ya muda tu. Majaribu ya upweke huonekana kuwa rahisi kidogo kushughulika nayo yaonwapo kwa mtazamo wa mambo ambayo Mungu atakuja kukufanyia katika ulimwengu wake mpya. Kwa wakati huu yeye atakutegemeza na kukufariji.—Zaburi 18:2; Wafilipi 4:6, 7.
Kujua jambo hili kwaweza kukupa nguvu. Frances (aliyetajwa mapema) alipofiwa na mume wake, alipata faraja sana katika maneno ya Zaburi 4:8, hasa wakati wa usiku: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana wewe, BWANA, peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” Tafakari maneno kama yale yapatikanayo katika kitabu cha Zaburi. Fikiria jinsi Mungu anavyokujali, kama ionyeshwavyo kwenye Zaburi 23:1-3.
Wapweke Waweza Kusaidiwaje?
Njia kuu ya kusaidia wapweke ni kuwaonyesha upendo. Kwa kurudia-rudia Biblia hutia moyo watu wa Mungu waonyeshane upendo, hasa katika nyakati za matatizo. “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi,” akaandika mtume Paulo. (Warumi 12:10) Kwa kweli, Neno la Mungu lenye pumzi yake lasema: “Upendo haupungui.” (1 Wakorintho 13:8) Unaweza kuonyeshaje upendo kwa wapweke?
Badala ya kukataa au kupuuza watu wenye upweke, watu mmoja mmoja wenye kuonyesha hangaiko waweza kuonyesha upendo wao wororo kwa kuwasaidia kwa subira wakati wowote uwezakanao. Wao waweza kuwa kama Ayubu, aliyesema hivi: “Kwa sababu nalimwokoa maskini aliyenililia; yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia. . . . Nikaufanya moyo wa mjane kuimba kwa furaha.” (Ayubu 29:12, 13) Wazee waliowekwa rasmi katika kutaniko la Kikristo na marafiki wenye huruma waweza kutenda kwa njia ya fadhili kama hiyo, kwa kuandaa mahitaji ya msingi ya binadamu kama kuelewa mambo, uchangamfu, na faraja. Wao waweza kuonyesha hisia-mwenzi, na nyakati nyingine wao waweza kujazia uhitaji wa kuwa msiri.—1 Petro 3:8.
Mara nyingi, ni mambo madogo-madogo ambayo marafiki hufanyia wapweke ndiyo yaliyo muhimu zaidi. Kwa kielelezo, mwamini mwenzako apotezapo mpendwa wake katika kifo, mambo mengi mazuri yaweza kutimizwa kupitia matendo ya fadhili ya urafiki wa kweli. Usipuuze zile fadhili ndogo-ndogo, kama mwaliko kwa mlo, kusikiliza kwa huruma, au mazungumzo yenye kutia moyo. Mambo haya yana matokeo sana katika kusaidia mtu kushinda upweke.—Waebrania 13:16.
Yaelekea kwamba sisi sote tutapatwa na vipindi vya upweke mara kwa mara. Lakini, si lazima upweke uwe pigo kubwa kwetu. Jaza maisha yako na utendaji mbalimbali ufaao wenye kujenga. Acha marafiki wasaidie wawezapo. Uwe na hakika katika Yehova Mungu. Kumbuka akilini ahadi yenye kutia moyo iliyoandikwa kwenye Zaburi 34:19: “Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA humponya nayo yote.” Mwendee Yehova kwa ajili ya msaada, na usiache upweke uathiri maisha yako.
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
NJIA FULANI ZA KUPIGANA NA UPWEKE
▪ Dumisha ukaribu na Yehova
▪ Tafuta faraja kwa kusoma Biblia
▪ Dumisha mtazamo mzuri wa Kikristo
▪ Jishughulishe na utendaji wenye maana
▪ Pata marafiki wengi zaidi
▪ Fanya iwe rahisi kwa marafiki kusaidia
▪ Usijitenge, bali sitawisha upendo wenye uchangamfu
▪ Uwe na uhakika kwamba Yehova anakujali
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
JINSI UWEZAVYO KUSAIDIA WAPWEKE
▪ Uwe mwenye kuelewa mambo, mchangamfu, na kuandaa faraja
▪ Jazia uhitaji wa kuwa msiri
▪ Vumilia katika kufanya mambo madogo-madogo yanayosaidia
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ajapopatwa na hali zilizo ngumu, hakuna jambo lolote lionyeshalo kwamba Ruthu aliacha upweke uathiri maisha yake