Upweke-Teso Kubwa Lililofichika
JE! WAWEZA kuwatambua katika umati? Je! upweke waweza kutambulika kwenye nyuso zao? Wanapokusalimu, je, tabasamu zao zitaufunika? Je! waweza kutambua kwa jinsi wanavyotembea, na kwa hali yao ya kukaa? Ona yule mtu mzee-mzee anayeketi peke yake kwenye benchi ya bustani au yule mwanamke mchanga aliye peke yake katika jumba la hifadhi la sanaa—je, wao wanateseka kwa sababu ya upweke? Chunguza vizazi vitatu vya mama, binti, na mjukuu wanaotembea madukani. Wanaonekana wenye furaha vya kutosha, lakini, je, waweza kuwa na hakika? Wafikirie wafanyakazi wenzako. Huenda ukawajua kuwa watu wenye furaha wenye familia nzuri na mapato ya kutosha kuwategemeza vizuri. Lakini, je, yawezekana mmoja wao aseme kikweli, “mimi ni mpweke”? Na kuna uwezekano gani kwamba yule kijana mwenye furaha na uchangamfu ni mpweke? Majibu ya maswali hayo yaweza kukushangaza.
Neno “upweke” linafasiliwa na Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary kuwa “kutokeza hali ya ukiwa na utupu.” Ni hisia ya kukosa kitu fulani, ya kuwa na utupu ndani yako, na haitambuliwi nyakati zote kwa sura ya nje ya mtu. Mtafiti mmoja asema hivi: “Katika jamii yetu, upweke ni siri ambayo hatufunui—nyakati nyingine hatukiri kwetu wenyewe kwamba tuna upweke. Kuna ubaya fulani unaoshikamanishwa na upweke. Kule nje kuna dhana kwamba ukiwa mpweke, ni lazima liwe kosa lako. Ama sivyo, kwa hakika ungekuwa na marafiki wengi, sivyo?” Nyakati nyingine hilo laweza kuwa kosa letu kweli, hasa tukitarajia au kudai mengi kupita kiasi kutoka kwa wengine.
Wanawake Wapweke
Inaonekana wastadi wanakubaliana kwamba wanawake—hasa wanawake walioolewa—wa umri wote hutazamia kupata mengi kutoka maishani kuliko wanaume. Inaeleweka kwamba wajane, wanawake waliotalikiwa, na wanawake waseja wenye umri mkubwa nyakati nyingine huhisi upweke. Lakini vipi juu ya wanawake walioolewa wanaoonekana kuwa na furaha ambao wana familia? Kwa kielelezo, fikiria lalamiko hili kutoka kwa mwalimu mwenye umri wa miaka 40: “Sina wakati wa kuwa na marafiki; ninakosa jambo hilo sana. Lakini nahisi wasiwasi hata kwa kusema hivyo. Naweza kulalamikaje juu ya kuwa mpweke . . . ? Ukiangalia hali yangu, nina ndoa nzuri sana, watoto wazuri, makao mazuri, kazi ninayofurahia. Najivunia yale ambayo nimetimiza. Lakini kuna kasoro fulani.”
Ingawa wanawake kwa kweli waweza kuwapenda waume zao na wajitolee kwao na kutendewa vivyo hivyo na waume zao, si lazima upendo huo ujazie mahitaji yao yote ya kuwa na mwenzi. Yule mwalimu wa shule aliyenukuliwa hapo juu aeleza hivi: “Hata ingawa mume wangu ni rafiki yangu wa karibu zaidi, urafiki huo hauchukui mahali pa marafiki wazuri wanawake. Huenda wanaume wakasikia, lakini wanawake husikiliza. Mume wangu hataki kujua jinsi nimelemewa. Ataka tu kurukia uamuzi mara hiyo na kutatua tatizo hilo. Lakini marafiki wangu wanawake watanipatia nafasi niongee juu ya tatizo hilo. Na nyakati nyingine mimi huhitaji tu kuongea.”
Mwanamke anapopoteza mpendwa wake katika kifo au talaka, mfadhaiko wake wa kihisia-moyo waweza kuwa mkubwa sana. Basi upweke waanza. Ni lazima mwanamke mwenye majonzi au aliyetaliki ategemee familia yake na marafiki wake ili kupata utegemezo lakini vilevile ni lazima ategemee nguvu zake mwenyewe na kujaribu kupatana na hali hiyo mpya. Ingawa msiba huo utabaki nyakati zote kuwa sehemu ya maisha yake, ni lazima ang’amue kwamba hauwezi kuruhusiwa uwe kizuizi kwa maisha yake ya kawaida. Wastadi wamepata kwamba watu wenye uthabiti mara nyingi waweza kuushinda upweke wao haraka kuliko watu wengine.
Kuna maoni yenye kutofautiana juu ya ni nani ana uchungu zaidi—mjane au mtu aliyetalikiwa. Gazeti 50 Plus liliripoti hivi: “Wakati wowote tunapowaalika watu waliotalikiwa kwenye vikundi vyetu vya kuwategemeza wajane, pande hizo mbili humalizia kwa mabishano juu ya ni nani mwenye uchungu mwingi zaidi. Mjane asema, ‘Alaa, angalau mwenzi wako yungali hai,’ ilhali mtu aliyetalikiwa atasema, ‘Alaa, wewe binafsi hujapata kukataliwa jinsi nilivyokataliwa. Huna ile hisi ya kushindwa.’”
Wanaume Wapweke
Kwa habari ya upweke, wanaume hawawezi kujivuna kuwa thabiti kuliko wanawake. “Wanaume hushughulikia mambo kimatendo kuliko kihisia-moyo,” akasema Anne Studner, mstadi wa programu ya Huduma ya Wajane ya AARP (Shirika la Amerika la Watu Waliostaafu). “Wanawake watasimulia uchungu wao mara trilioni 10, lakini wanaume watajaribu kuoa tena badala ya kushughulikia majonzi yao.” Washauri wanaume waweza kutumia wakati mwingi na wanaume waliofiwa kabla ya wao kuanza polepole kuzungumzia hisia zao za moyoni.
Wastadi wamepata kwamba, tofauti na wanawake, wanaume hutafuta mwenzi wa kike ili waeleze matatizo yao badala ya kutafuta mwanamume. Dakt. Ladd Wheeler, mstadi wa upweke katika Chuo Kikuu cha Rochester, afunua kwamba wanaume huwa hawazungumziani kindani vya kutosha ili wahisi ushikamano wa kihisia. “Uhitaji wa kuepuka hali ya kutengwa sana kihisia-moyo baada ya kupoteza mke, na kufuatia kujaribu kuwasiliana na rafiki mwanamke, waweza kusaidia pia kueleza sababu inayofanya wanaume kwa kawaida waoe tena haraka zaidi baada ya ujane au talaka kuliko wanawake.”—Gazeti 50 Plus.
Vijana Wapweke
Kuna sababu nyingi zinazofanya watoto na watu wazima wachanga wawe wapweke—mara nyingi zikifanana na zile za watu wenye umri mkubwa zaidi. Kuhamia mahali papya na kuacha marafiki; kutopendwa na wanadarasa wenzi katika shule mpya; malezi ya kidini na kikabila; talaka nyumbani; hisia ya kutopendwa na wazazi; kukataliwa na watu wa jinsia tofauti—hayo huwa mambo ya kusababisha sana upweke.
Wale wachanga zaidi huhitaji mtu wa kushiriki nao michezo yao. Wao huhitaji utegemezo wa kihisia-moyo na uelewevu. Wao huhitaji kuonyeshwa shauku na uthibitisho wa kustahili kwao. Ni lazima wajue kwamba wengine watakuwa waaminifu-washikamanifu na wenye ku-tumainika. Wanapopendwa, wao huhisi salama na pia hujifunza kuwapenda wengine. Mategemeo hayo ya kijamii yaweza kutoka kwa vyanzo tofauti-tofauti—familia, marika, na hata wanyama vipenzi.
Wanafunzi wa kiume na pia wa kike, kutoka darasa la chini zaidi hadi chuo, mara nyingi huteseka kwa kiasi kilekile cha upweke, mara nyingi ukisababishwa na kutokubaliwa na marika wao. “Nahisi vibaya kwa sababu niko peke yangu na siongei,” akaomboleza mwanafunzi mmoja wa kike wa shule ya sekondari. “Namsikiliza tu mwalimu, nafanya kazi yangu na basi. Kukiwa na wakati, mimi huketi tu na kuchora au kufanya jambo lolote lile. Kila mtu anaongea na mwingine, lakini hakuna mtu anayeongea na mimi. . . . Najua siwezi kunyamaza milele. Kwa sasa, ni upweke tu.”
Hata hivyo, haipasi nyakati zote lawama iwekwe kwa kufaa juu ya kujitenga au kujipendekeza kwa watu wengine. Huenda mtu akawa na matatizo ya tabia au ya kijamii, kama vile kuwa mwenye haya mno, mwenye hasira kali, na mwenye kujipendekeza zaidi na kupata matatizo katika uhusiano na marika. Ulemavu waweza pia kuchangia kwa kadiri kubwa sana katika kufanya vijana wa umri wote wapatwe na upweke ila tu vijana hao wawe thabiti na wenye urafiki.
Uhitaji wa Kujisaidia Mwenyewe
Mfunzi wa mambo ya afya Dolores Delcoma wa Chuo Kikuu cha Kalifornia katika Fullerton, alitambua kweli muhimu alipotoa maelezo juu ya jitihada za mtu za kupambana na upweke: “Jitihada yapaswa kutoka ndani yake mwenyewe. Hatimaye apaswa kung’amua tatizo lake kwa sababu hata watu wengine wajaribu kusaidia kadiri gani, mtu pekee anayeweza kumsaidia atatue tatizo lake ni yeye mwenyewe.”
Wale wanaofanya kubadilika kwao kuwe kugumu watambuliwa na Dakt. Warren Jones kuwa watu wenye mwelekeo wa upweke: “Bila kukusudia watu hao hufanya mambo yanayowazuia wasihisi ukaribiano na wengine. Wengine hawajui jinsi ya kusikiliza, na wanatawala mazungumzo. Wana mwelekeo wa kuwachambua wengine na kujichambua; wanauliza maswali machache zaidi, na mara nyingi huharibu urafiki kwa kusema mambo ya kuonyesha madharau au yenye kuchukiza.”
Kwa kuongezea watu kama hao, ambao kwa msingi huwa hawajistahi, kuna wengine wanaokosa stadi za kijamii zinazohitajika ili kuwa na uhusiano na wengine. Kuhusu watu kama hao, tabibu Evelyn Moschetta asema hivi: “Watu wapweke huwa hawahisi vizuri sana juu yao wenyewe. Wakitazamia kukataliwa, wao hawashughuliki kuwa wenye urafiki.”
Hata hivyo, kinyume cha hekima ya kawaida, wastadi wamepata kwamba wanawake na wanaume wazee-wazee hupatwa na upweke kwa kiwango kidogo kuliko wenye umri mdogo zaidi. Hawajui kwa uhakika sababu ya jambo hilo. Pia wamepata kwamba wazee-wazee wanapopatwa na upweke, sababu huwa ni kukosa marafiki badala ya kukosa mtu wa ukoo. “Si kwamba wazee-wazee hawajali mahusiano ya familia. Wao hutegemea familia kwa ajili ya msaada. Lakini wanaweza kuwa na familia nyingi za kuwasaidia, na bado wahisi wapweke sana ikiwa hawana marafiki.”
Uhitaji wa Marafiki wa Karibu
Kwa watu wa umri wote, nyakati nyingine marafiki wa karibu hujazia uhitaji ambao familia na watu wa ukoo hawawezi kujaza. Watu huhitaji rafiki, rafiki wa karibu, ambaye wao waweza kumwambia mambo yao au kufunulia mambo bila woga wa kuumizwa hisia. Bila rafiki kama huyo, upweke waweza kuongezeka. Ni juu ya rafiki kama huyo ambaye mwanainsha Mwamerika Ralph Waldo Emerson aliandika hivi: ‘Rafiki ni yule ambaye ninaweza kufikiri kwa sauti kubwa mbele yake.’ Mtu kama huyo ni msiri wako ambaye unaweza kumfunulia kitu chochote bila woga wa kusalitiwa au bila kuwa na wasiwasi kwamba mambo yako ya siri yatatumiwa kukushusha au kutumiwa na wengine kukucheka. Wengine ambao huenda ulifikiria kuwa waaminifu-washikamanifu huenda wamevunja tumaini lako nyakati fulani, lakini kuna “rafiki” ambaye ‘hafunui siri ya mtu mwingine,’ ambaye ‘huambatana na mtu kuliko ndugu.’—Mithali 18:24; 25:9.
Kuna wale ambao hutaka waonwe kuwa thabiti na kutohitaji mtu. Wanadai kuwa wenye kujitegemea na wenye kujitimizia mambo yao. Hata hivyo, mara nyingi wao hujikusanya katika vikundi vinavyoitwa mashujaa. Watoto huwa na vilabu, hujenga majumba ya vilabu, hufanyiza magenge; vijana wakubwa zaidi huwa na magenge ya kuendesha pikipiki; wahalifu wana marafiki wao ambao hawawezi kuwatambulisha; wale wenye matatizo ya unywaji hujiunga na Shirika la Kusaidia Wazoea Vileo Washinde Uzoevu wao; wale wanaopambana na unene wa kupita kiasi hujiunga na Shirika la Kusaidia Wanene Wapunguze Unene. Watu hupenda kushirikiana na wengine; wao hujiweka katika vikundi ili kupata utegemezo. Hata katika majonzi yao, wao hupenda ushirika. Na kwa ujumla wote huchukia upweke. Ni nini kinachoweza kufanywa juu ya upweke?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Watu wapweke huwa hawahisi vizuri sana juu yao wenyewe”