Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 10/1 kur. 15-20
  • Kuchunga Kundi la Mungu kwa Upendo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuchunga Kundi la Mungu kwa Upendo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kielelezo cha Mchungaji Mwema
  • Wachungaji Wakatili Katika Israeli
  • Wachungaji Wenye Upendo Katika Kutaniko la Kikristo
  • Stahi Matumizi ya Hiari
  • Wazee, Chukueni kwa Uzito Madaraka Yenu ya Uchungaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Wachungaji, Waigeni Wale Wachungaji Wakuu Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Tii Wachungaji Waliowekwa na Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Kuchunga kwa Wororo Kondoo za Yehova Wenye Thamani Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 10/1 kur. 15-20

Kuchunga Kundi la Mungu kwa Upendo

“Lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu.”—1 PETRO 5:2.

1, 2. Sifa kuu ya Yehova ni nini, nayo inajionyeshaje?

KOTEKOTE katika Maandiko Matakatifu, imeonyeshwa wazi kwamba upendo ni sifa kuu ya Mungu. “Mungu ni upendo,” yataarifu 1 Yohana 4:8. Kwa kuwa upendo wake waonyeshwa kwa matendo, 1 Petro 5:7, NW, yasema kwamba Mungu “huwajali nyinyi.” Katika Biblia njia ambayo Yehova hushughulikia watu wake hufananishwa na njia ambayo mchungaji mwenye upendo hushughulikia kondoo zake kwa wororo: “Tazameni, Bwana Mungu . . . atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake, nao wanyonyeshao atawaongoza polepole.” (Isaya 40:10, 11) Daudi alifarijika kama nini kuweza kusema kwamba: “Bwana ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu”!—Zaburi 23:1.

2 Yafaa kwamba Biblia yalinganisha watu wanaopendelewa na Mungu na kondoo, kwa kuwa kondoo ni wenye amani, unyenyekeo, na watiifu kwa mchungaji wao mwenye kuwajali. Akiwa Mchungaji mwenye upendo, Yehova hujali sana watu wake wenye mfano wa kondoo. Yeye aonyesha hivyo kwa kuwaandalia kimwili na kiroho na kwa kuwaongoza kupitia “siku za mwisho” zilizo ngumu za ulimwengu huu mwovu kuelekea ulimwengu wake mpya wenye uadilifu.—2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 6:31-34; 10:28-31; 2 Petro 3:13.

3. Mtunga-zaburi alifafanuaje njia ambayo Yehova hutunza kondoo zake?

3 Ona utunzi wenye upendo wa Yehova kwa kondoo zake: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. . . . Walilia, naye BWANA akasikia, akawaponya taabu zao zote. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA humponya nayo yote.” (Zaburi 34:15-19) Ni faraja kuu kama nini aandaye Mchungaji wa Ulimwengu Wote Mzima kwa watu wake wenye mfano wa kondoo!

Kielelezo cha Mchungaji Mwema

4. Yesu ana fungu gani katika kutunza kundi la Mungu?

4 Mwana wa Mungu, Yesu, alijifunza vema kutoka kwa Baba yake, kwa kuwa Biblia yamwita Yesu “mchungaji mwema.” (Yohana 10:11-16) Utumishi wake muhimu kwa kundi la Mungu watajwa kwenye Ufunuo sura ya 7. Katika mstari wa 9, watumishi wa Mungu wa siku yetu waitwa “mkutano mkubwa . . . wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Kisha mstari wa 17 wasema: “Mwana-Kondoo [Yesu] . . . atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.” Yesu aongoza kondoo za Mungu kwenye maji ya kweli iongozayo kwenye uzima wa milele. (Yohana 17:3) Ona kwamba Yesu anaitwa “Mwana-Kondoo,” jambo lionyeshalo sifa zake kama za kondoo, yeye akiwa kielelezo kikuu cha unyenyekeo kwa Mungu.

5. Yesu alihisije juu ya watu?

5 Akiwa duniani Yesu aliishi miongoni mwa watu naye aliona hali zao zilizokuwa mbaya sana. Yeye aliitikiaje hali zao? “Aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Kondoo wasio na mchungaji huumizwa sana na wanyama-wawindaji, kama ilivyo vilevile na kondoo wenye wachungaji wasiojali. Lakini Yesu alijali sana, kwa kuwa alisema: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

6. Yesu alionyesha ufikirio upi kwa watu waliodharauliwa?

6 Unabii wa Biblia ulitabiri kwamba Yesu angeshughulika na watu kwa njia ya upendo: “BWANA amenitia mafuta . . . kuwaganga waliovunjika moyo, . . . kuwafariji wote waliao.” (Isaya 61:1, 2; Luka 4:17-21) Yesu hakuwadharau maskini na wale ambao hawakufanikiwa. Badala ya hivyo, yeye alitimiza Isaya 42:3: “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima.” (Linganisha Mathayo 12:17-21.) Watu waliopatwa na pigo walikuwa kama mianzi iliyopondeka, kama tambi za taa zielekeazo kuzimika kwa kukosa mafuta. Akitambua hali yao yenye kuhurumiwa sana, Yesu aliwaonyesha huruma na kuwapa nguvu na tumaini, akiwaponya kiroho na kimwili.—Mathayo 4:23.

7. Yesu aliwaelekeza watu waliomwitikia wapi?

7 Watu wenye mfano wa kondoo walimwitikia Yesu sana. Mafundisho yake yalikuwa yenye kuvutia hivi kwamba maofisa waliotumwa kumkamata waliripoti hivi: “Hajanena kamwe mtu ye yote kama huyu anavyonena.” (Yohana 7:46) Kwani, viongozi wa kidini wenye unafiki walilalamika hivi: “Ulimwengu umekwenda nyuma yake”! (Yohana 12:19) Lakini Yesu hakujitakia mwenyewe staha wala utukufu. Yeye alielekeza watu kwa Baba yake. Aliwafundisha kumtumikia Yehova kwa sababu ya upendo kwa sifa Zake zenye kuvutia: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote.”—Luka 10:27, 28.

8. Utii ambao watu wa Mungu humpa watofautianaje na ule ambao wengine huwapa watawala wa kilimwengu?

8 Yehova hushangilia kwamba enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima inategemezwa na watu wake wenye mfano wa kondoo, kwa kutegemea upendo wao kwake. Wao huchagua kwa hiari kumtumikia kwa sababu ya kujua kwao sifa zake zenye kupendeleka. Hilo ni tofauti kama nini na viongozi wa kilimwengu ambao raia zao hutii kwa sababu ya hofu, au kwa shingo upande, au kwa sababu ya kusudi fulani! Haiwezi kusemwa juu ya Yehova au Yesu yale yaliyosemwa juu ya papa mmoja wa Kanisa Katoliki la Roma: “Yeye alivutia wengi, aliogopwa na wote, naye hakupendwa na wowote.”—Vicars of Christ—The Dark Side of the Papacy cha Peter De Rosa.

Wachungaji Wakatili Katika Israeli

9, 10. Fafanua juu ya viongozi wa Israeli la kale na wale wa karne ya kwanza.

9 Kinyume cha Yesu, viongozi wa kidini wa Israeli katika siku yake hawakuwapenda kondoo. Wao walikuwa kama watawala wa awali katika Israeli ambao Yehova alisema hivi juu yao: “Ole wao wachungaji wa Israeli, wanaojilisha wenyewe; je! haiwapasi wachungaji kuwalisha kondoo? . . . Wagonjwa hamkuwatia nguvu, wala hamkuwaponya wenye maradhi, wala hamkuwafunga waliovunjika, wala hamkuwarudisha waliofukuzwa, wala hamkuwatafuta waliopotea; bali kwa nguvu na kwa ukali mmewatawala.”—Ezekieli 34:2-4.

10 Kama wachungaji hao wa kisiasa, viongozi wa kidini wa Kiyahudi wa karne ya kwanza walikuwa wenye mioyo migumu. (Luka 11:47-52) Ili kutoa kielezi cha jambo hilo, Yesu alisimulia juu ya Myahudi aliyekuwa amenyang’anywa vitu, kupigwa na kuachwa mahututi kando ya barabara. Kuhani Mwisraeli alikuja, lakini alipomwona Myahudi huyo, alivuka njia kwenye upande mwingine wa barabara. Mlawi akafanya vivyo hivyo. Kisha mtu asiye Mwisraeli, Msamaria anayedharauliwa, akaja akamwonea huruma mtu huyo aliyepigwa. Alifunga majeraha yake, akambeba kwenye mnyama na kumpeleka katika nyumba ya wageni, akamtunza. Akamlipa mwenye nyumba ya wageni na kusema kwamba angerudi kulipa gharama za ziada.—Luka 10:30-37.

11, 12. (a) Uovu wa viongozi wa kidini ulifikiaje upeo katika siku ya Yesu? (b) Waroma walifanya nini hatimaye kwa viongozi wa kidini?

11 Viongozi wa kidini wa siku ya Yesu walikuwa wafisadi sana hivi kwamba Yesu alipomfufua Lazaro kutoka kwa wafu, wakuu wa makuhani na Mafarisayo waliita Sanhedrini pamoja na kusema: “Tunafanya nini? Maana mtu huyu [Yesu] afanya ishara nyingi. Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu.” (Yohana 11:47, 48) Wao hawakujali juu ya mema ambayo Yesu alikuwa amefanyia mfu huyo. Wao walihangaikia vyeo vyao. Kwa hiyo “tangu siku ile walifanya shauri la kumwua [Yesu].”—Yohana 11:53.

12 Na kuzidisha uovu wao, wakuu wa makuhani nao “wakafanya shauri la kumwua Lazaro naye, maana kwa ajili yake wengi katika Wayahudi walijitenga, wakamwamini Yesu.” (Yohana 12:10, 11) Jitihada za ubinafsi za kulinda vyeo vyao hazikufua dafu, kwa kuwa Yesu alikuwa amewaambia: “Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38) Kwa kupatana na maneno hayo, katika kizazi hicho, Waroma walikuja na kuwaondolea ‘mahali pao na taifa lao,’ na uhai wao vilevile.

Wachungaji Wenye Upendo Katika Kutaniko la Kikristo

13. Yehova aliahidi kumtuma nani kulichunga kundi lake?

13 Badala ya wachungaji wakatili wenye ubinafsi, Yehova angetokeza Mchungaji Mwema, Yesu, kulitunza kundi Lake. Yeye pia aliahidi kutokeza wachungaji wa chini wa kutunza kondoo zake: “Nami nitaweka juu yao wachungaji watakaowalisha watu wangu; wala hawataona hofu tena.” (Yeremia 23:4) Kwa hiyo, kama ilivyokuwa katika makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza ndivyo ilivyo leo, ‘kuwekwa kwa wazee katika kila mji’ hufanywa. (Tito 1:5) Hao wazee wa kiroho wanaotimiza sifa zinazotajwa katika Maandiko ni lazima ‘walichunge kundi la Mungu.’—1 Petro 5:2; 1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:7-9.

14, 15. (a) Wafuasi walipata ugumu wa kusitawisha mwelekeo gani? (b) Yesu alifanya nini ili kuwaonyesha kwamba wazee wapaswa kuwa watumishi wanyenyekevu?

14 Katika kutunza kondoo, “zaidi ya yote” ni lazima wazee ‘wawe na upendo mwingi kwao.’ (1 Petro 4:8) Lakini wafuasi wa Yesu, wakishughulikia mno umashuhuri na cheo, walilazimika kujifunza hilo. Kwa hiyo wakati mama ya wale wanafunzi wawili alipomwambia Yesu: “Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako,” wale wanafunzi wengine wakakasirika. Yesu akawaambia: “Wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu.”—Mathayo 20:20-28.

15 Katika pindi nyingine, baada ya wanafunzi ‘kubishana wao kwa wao ni nani aliye mkubwa,’ Yesu akawaeleza: “Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote.” (Marko 9:34, 35) Unyenyekevu wa akilini na utayari wa kutumika ulikuwa lazima uwe sehemu ya utu wao. Na bado wanafunzi walikuwa wanaendelea kuwa na matatizo ya mawazo hayo, kwa kuwa usiku huo tu kabla ya kifo cha Yesu, kwenye mlo wake wa mwisho wa jioni, “mashindano” yalitokea miongoni mwao juu ya ni nani alikuwa mkuu zaidi! Hilo lilitukia Yesu ajapowaonyesha jinsi mzee apaswa kutumikia kundi; yeye alikuwa amejinyenyekeza na kuosha miguu yao. Yeye alisema hivi: “Ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.”—Luka 22:24; Yohana 13:14, 15.

16. Katika 1899, Mnara wa Mlinzi la Kiingereza lilitoa maelezo gani juu ya sifa muhimu zaidi ya wazee?

16 Sikuzote Mashahidi wa Yehova wamefundisha kwamba ni lazima wazee wawe hivyo. Karibu karne moja iliyopita, Aprili 1, 1899, Mnara wa Mlinzi la Kiingereza lilitaja maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:1-8 kisha likasema: “Mitume wasema wazi kwamba ujuzi na uwezo wa kusema kwa ufasaha si mambo muhimu zaidi, bali upendo utokao moyoni na kuenea katika mwendo wote wa maisha, unaotendesha na kutenda katika miili yetu inayokufa, ndiyo muhimu zaidi—uthibitisho kamili wa uhusiano wetu wa kimungu. . . . Sifa ya kwanza kuchunguzwa katika kila mtu akubaliwaye kuwa mtumishi wa kanisa, wa kuhudumia mambo matakatifu, kwanza kabisa yapasa kuwa roho ya upendo.” Lilisema kwamba wanaume ambao hawangetumika kwa unyenyekevu kwa sababu ya upendo “walikuwa walimu wasio salama, na waelekea kudhuru zaidi kuliko kutoa mema.”—1 Wakorintho 8:1.

17. Biblia yakaziaje sifa ambazo ni lazima wazee wawe nazo?

17 Kwa hiyo, ni lazima wazee ‘wasifanye ubwana’ juu ya kondoo. (1 Petro 5:3) Badala ya hivyo, wao wapaswa kuongoza katika kuwa ‘wafadhili wao kwa wao, wenye huruma.’ (Waefeso 4:32) Paulo alikazia hivi: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu. . . . Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”—Wakolosai 3:12-14.

18. (a) Paulo aliweka kielelezo gani chema katika kushughulika na kondoo? (b) Kwa nini ni lazima wazee wasipuuze mahitaji ya kondoo?

18 Paulo alijifunza kufanya hivyo, akisema: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 Wathesalonike 2:7, 8) Kwa kupatana na hayo, yeye alisema: “Watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote.” (1 Wathesalonike 5:14) Bila kujali aina ya tatizo ambalo huenda kondoo wakawaletea, wazee wapaswa kukumbuka Mithali 21:13: “Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini, yeye naye atalia, lakini hatasikiwa.”

19. Kwa nini wazee wenye upendo ni baraka, nao kondoo huitikiaje upendo huo?

19 Wazee wanaochunga kundi kwa upendo ni baraka kwa kondoo. Isaya 32:2 ilitabiri: “Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Tunafurahi kujua kwamba wengi wa wazee wetu wanapatana na maelezo hayo mazuri yafarijiyo. Wao wamejifunza kutumia kanuni hii ifuatayo: “Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu.” (Warumi 12:10) Wazee waonyeshapo aina hii ya upendo na unyenyekevu, kondoo huitikia kwa kuwapa ‘ustahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi yao.’—1 Wathesalonike 5:12, 13.

Stahi Matumizi ya Hiari

20. Kwa nini ni lazima wazee wastahi hiari?

20 Yehova aliumba wanadamu wakiwa na hiari ya kujifanyia maamuzi. Ingawa wazee wapaswa kushauri na hata kutoa nidhamu, wao hawapaswi kudhibiti maisha au imani ya mwingine. Paulo alisema: “Si kwamba tunatawala imani yenu; bali tu wasaidizi wa furaha yenu; maana kwa imani yenu mnasimama.” (2 Wakorintho 1:24) Ndiyo, “kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Yehova ametupa uhuru mwingi katika sheria na kanuni zake. Kwa hiyo wazee wapaswa kuepuka kuweka sheria katika hali ambapo hakuna kanuni za Kimaandiko zinazovunjwa. Nao wapaswa kuepuka mwelekeo wa kutoa maoni yao binafsi kuwa sheria au kuacha kijitutumua kwao kuwashinde iwapo mtu fulani akataa kukubali maoni hayo.—2 Wakorintho 3:17; 1 Petro 2:16.

21. Twaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo wa Paulo kuelekea Filemoni?

21 Ona jinsi Paulo, akiwa amefungwa katika Roma, alivyoshughulika na Filemoni, Mkristo katika Kolosai katika Asia Ndogo aliye na mtumwa. Mtumwa wa Filemoni aliyeitwa Onesimo alikimbilia Roma, akawa Mkristo, naye alikuwa akisaidia Paulo. Paulo aliandikia Filemoni: “Nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili. Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari.” (Filemoni 13, 14) Paulo alimrudisha Onesimo, akimwomba Filemoni amtendee kama ndugu Mkristo. Paulo alijua kwamba kundi halikuwa lake; lilikuwa la Mungu. Yeye hakuwa bwana mkubwa walo bali mtumishi walo. Paulo hakumshurutisha Filemoni; yeye alistahi hiari yake.

22. (a) Wazee wapaswa kuelewa vyeo vyao kuwa nini? (b) Yehova anasitawisha tengenezo la aina gani?

22 Kadiri tengenezo la Mungu likuavyo, wazee zaidi huwekwa rasmi. Wao, pamoja na wazee wenye ujuzi zaidi wa muda mrefu, wapaswa kuelewa kwamba cheo chao ni cha utumishi mnyenyekevu. Katika njia hii, Mungu aongozapo tengenezo lake kuelekea ulimwengu mpya, litaendelea kukua kama atakavyo—lililopangwa vizuri kitengenezo bila kudhabihu upendo na huruma kwa ajili ya ubora wa kazi. Kwa njia hiyo, tengenezo lake litaendelea kupendeza zaidi watu wenye mfano wa kondoo ambao wataona ndani yalo uthibitisho kwamba “Mungu hufanya kazi zake zote zipatane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wampendao Mungu.” Hilo ndilo jambo litarajiwalo kwa tengenezo linalotegemezwa kwa upendo, kwa sababu “upendo haupungui.”—Warumi 8:28, NW; 1 Wakorintho 13:8.

ngejibuje?

◻ Biblia yafafanuaje utunzi wa Yehova kwa watu wake?

◻ Yesu anatimiza fungu gani katika kutunza kundi la Mungu?

◻ Ni lazima wazee wawe na sifa gani kuu?

◻ Kwa nini ni lazima wazee wafikirie hiari ya kondoo?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu, yule “mchungaji mwema,” alionyesha huruma

[Picha katika ukurasa wa 17]

Viongozi wa kidini wafisadi walifanya njama za kumwua Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki