Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 10/1 kur. 21-25
  • Nchi Isiyozaa Yawa na Rutuba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nchi Isiyozaa Yawa na Rutuba
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Urithi wa Kiroho
  • Kushiriki Katika Kazi ya Kuhubiri
  • Kupanda Mbegu Kando ya Bahari
  • Kuendeleza Huduma Pamoja na Mwenzi
  • Kushinda Upinzani
  • Kuvumilia Matatizo Baharini
  • Marekebisho Zaidi
  • Nchi Imekuwa na Rutuba
  • Meli Inaharibika Katika Kisiwa
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kumtegemea Yehova Huleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Mashua ya Galilaya—Hazina ya Nyakati za Biblia
    Amkeni!—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 10/1 kur. 21-25

Nchi Isiyozaa Yawa na Rutuba

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ARTHUR MELIN

Ilikuwa siku nyangavu wakati wa masika katika 1930, nami nilikuwa nimesimama gatini katika Prince Rupert, British Columbia. Nikitazama mashua iliyosimama sakafuni mwa bahari, nilistaajabu, ‘Maji yote yameenda wapi?’ Huu ulikuwa wakati wangu wa kwanza kuona kupwa kwa maji ya Pwani ya Magharibi ya Pasifiki ambako usawa wa bahari waweza kupungua kwa meta saba kwa muda wa saa sita tu. Lakini kijana aliyekulia nyanda za mashambani alipataje kuwa katika fuo za Bahari ya Pasifiki?

NILIKUWA nimealikwa kupanua pendeleo langu la utumishi wa wakati wote kwa Yehova kwa kujiunga na watumishi katika mashua Charmian. Mgawo wetu ulikuwa kuanzisha kazi ya kuhubiri kwenye maeneo ya mbali yaliyo kando-kando ya pwani ya magharibi kutoka Vancouver hadi Alaska. Hiki kilikuwa kisehemu chenye maili nyingi za pwani za British Columbia ambacho hakikuwa na watendaji wenye kusifu Yehova. Ni mji wa Prince Rupert pekee uliokuwa na kikundi kidogo cha wahubiri wa Ufalme.

Nilikuwa na hamu nyingi ya kuanza kazi ya kuhubiri, hivyo baada ya kushuka gari la moshi, nilitembea moja kwa moja kuelekea gatini kuiona mashua Charmian na watu wayo, Arne na Christina Barstad. Hakuna yeyote aliyekuwa ndani, hivyo nikaondoka. Niliporudi baadaye siku hiyo, nilishangaa. Ilionekana kana kwamba bahari inakauka!

Lakini ni nini lililoongoza kwenye mgawo huu wenye kupendeza?

Urithi wa Kiroho

Uthamini wangu kwa mambo ya kiroho ulianza nyumbani katika nyanda za Alberta, Kanada. Baba yangu alikuwa amepata trakti iliyoandikwa na Charles Taze Russell wa Zion’s Watch Tower Tract Society iliyobadili maisha yake sana. Baba yangu akaanza kuwahubiri majirani wake, ijapokuwa kazi yake ya ukulima yenye kuchukua muda mwingi katika Calmar, Alberta. Hiyo ilikuwa miaka mia moja iliyopita, katika miaka ya mapema ya 1890.

Ni katika familia hii yenye kumhofu Mungu ndipo nilizaliwa katika Februari 20, 1905, nikiwa mtoto wa nane wa iliyokuja kuwa familia ya wavulana na wasichana kumi. Baba, pamoja na wengine katika jumuiya hiyo ya Wasweden, wakaanza kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa. Baada ya muda, wakajenga mahali pa kukutania, palipokuja kuitwa baadaye Jumba la Ufalme. Lilikuwa la kwanza katika Kanada.

Kazi ya shamba haikutuzuia kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ambayo mingine yayo ilikuwa na hotuba zilizotolewa na wasemaji wenye kuzuru waliotumwa na Watch Tower Society. Hotuba hizi zilijenga ndani yetu tamaa nyingi sana ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Kama tokeo, karibu wote wa familia yetu wametembea katika nuru ya kweli za Biblia kwa ushikamanifu.

Kushiriki Katika Kazi ya Kuhubiri

Mapema katika miaka ya 1920, nilipewa mgawo wangu wa kwanza wa kuhubiri. Nilikuwa nigawe mlango kwa mlango vikaratasi vya ukaribishaji kwenye hotuba ya watu wote katika jiji la Edmonton. Nilipokuwa nimesimama hapo peke yangu siku hiyo, nilijifunza somo la maana: Tumaini katika Yehova. (Mithali 3:5, 6, NW) Nilifurahi kama nini kutimiza mgawo huo wa kwanza kwa msaada wa Yehova!

Uhakika wangu kwa tengenezo lionekanalo la Yehova na kwa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye busara wake uliendelea kukua nilipoendelea kupata ufahamu zaidi wa Neno lake la kweli. Desturi nyingi za Jumuiya ya Wakristo, kama vile kusherehekea Krismasi na siku za kuzaliwa, zilitupiliwa mbali. Wokovu wa kibinafsi haukuwa tena jambo la maana sana; badala yake, kuhubiri juu ya Ufalme kulianza kuchukua umuhimu unaofaa. Yote haya yaliathiri sana maisha yangu. Hivyo baada ya muda mfupi baada ya kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova katika Aprili 23, 1923, nilifanya utumishi wa wakati wote kuwa mradi wangu.

Wakati wa halijoto ya kipupwe ipunguayo Selsiasi 18 chini ya sufuri katika nyanda hizo tulitoa ushahidi katika sehemu za mashambani tukiwa tumepanda kigari cha kukokotwa na farasi. Wakati mmoja nilitumia pamoja na kikundi fulani majuma mawili ndani ya ile iliyoitwa kazi ya gari-nyumba. Magari haya ya pekee yalithibitika kuwa ya kufaa kwa kuhubiri kwenye sehemu kubwa za nyanda za Kanada. Yajapokuwa matatizo ya kifedha, hali mbaya za hewa, na sehemu kubwa ya kusafiri, niliweza kuvumilia katika huduma ya upainia katika Alberta kwa kuacha na kuendelea kwa karibu miaka mitatu hadi ile siku ya kukumbukwa katika 1930 nilipoalikwa kutumika kwenye Pwani ya Magharibi ya Pasifiki. Niliduwazwa na mwaliko huo, kwani sikujua chochote kuhusu bahari au mashua.

Basi, upesi baada ya kufika Prince Rupert nilijihisi nyumbani pamoja na wafanya kazi wenzangu wapya kwenye mashua. Ndugu Barstad alikuwa baharia mwenye ujuzi, akiwa amefanya biashara ya uvuvi kwa miaka mingi. Miaka sita iliyofuata kilikuwa kipindi cha kuhubiri sana, tukiabiri katika pwani ya British Columbia kutoka Vancouver mpaka Alaska. Somo jingine nililojifunza: Sikuzote kubali mgawo kutoka kwa Yehova, na usisite kamwe.

Kupanda Mbegu Kando ya Bahari

Bandari yetu ya kwanza kuzuru katika masika hayo ya 1930 ilikuwa Ketchikan, Alaska, tulipopakia katoni 60 za fasihi za Biblia. Kwa majuma kadhaa, tulizuru nyumba zote katika Ketchikan, Wrangell, Petersburg, Juneau, Skagway, Haines, Sitka, na vijiji vingine vilivyotawanyika. Halafu tukahubiri pwani yote ya British Columbia, na kuimaliza kabla ya mwisho wa kiangazi. Kambi pweke za kukata mti, kambi za kutayarisha samaki, vijiji vya Wahindi wa wenyeji, miji midogo, pamoja na wakaaji na wawindaji walio peke yao, walitembelewa. Nyakati nyingine ilikuwa vigumu kuwaacha watunza minara yenye taa ya kuonya meli, waliokaribisha mtu wa kusema nao.

Baadaye, Sosaiti ilituandalia vinanda vyenye kubebeka na hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Tulizibeba hizi, pamoja na vitabu, Biblia, na magazeti. Mara nyingi ilibidi tuzibebe kwa shida tukitembea juu ya mawe ya pwani. Wakati wa kupwa kwa maji, ilitubidi kuzikokota juu kwa ngazi zisizo imara za kupanda kwenye gati. Nilifurahi kwa mazoezi ya kimwili niliyokuwa nimepata ujanani nikifanya kazi kwenye mbuga nyumbani.

Kikuza-sauti katika mashua yetu kilitumika kama kifaa chenye nguvu cha kueneza habari za Ufalme. Mwangwi wa hotuba zilizorekodiwa uliporudishwa, hotuba hizo zilisikiwa kwa umbali sana. Pindi moja tukiwa tumetia nanga katika ghuba moja ya pweke kwenye Kisiwa cha Vancouver, tulicheza moja ya hizi hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Siku iliyofuata watu walioishi nchi kavu walituambia kwa kusisimuka: “Jana tulisikia mahubiri moja kwa moja kutoka mbinguni!”

Katika pindi nyingine wenzi fulani wa ndoa walio wazee-wazee walisema kwamba walisikia muziki ukiingia ndani kupitia dohani lakini walipotoka nje, hawakusikia chochote. Kurudi ndani, wakasikia sauti. Kwa nini ilikuwa hivyo? Walipokuwa nje, tulikuwa tukibadili rekodi. Tungecheza muziki kwanza ili kuvuta fikira za watu, halafu kuchezesha hotuba za Biblia.

Katika pindi nyingine tena, tulipokuwa tumetia nanga karibu na kisiwa chenye kijiji cha Wahindi wenyeji, vijana wawili wenyeji walikuja kwenye mashua kuona ni wapi sauti zilikuwa zikitoka. Wengine kwenye kisiwa walifikiri zilikuwa sauti za wafu wao waliokuwa wamepata uhai!

Lilikuwa jambo la kawaida kuangusha mamia ya vitabu kwa siku kwa wafanya kazi wa viwanda vya samaki vilivyo mbali. Bila vikengeusha fikira vingi, walikuwa na wakati wa kufikiri juu ya mambo ya kiroho. Mwishowe wengi wa hawa walio mbali wakawa Mashahidi. Safari zilizofuata, tulitazamia mbele kuwatembelea ili “tufarijiane.”—Warumi 1:12.

Kuendeleza Huduma Pamoja na Mwenzi

Katika 1931, nilimuoa Anna, dada wa Christina Barstad. Baadaye tuliendeleza upainia wetu pamoja kwenye mashua na kufurahia maono mengi yenye kuthawabisha kwa miaka mingi iliyofuata. Nyangumi, simba wa baharini, sili, pomboo, kulungu, dubu, na tai walikuwa washiriki wenzetu katika mandhari ya milima yenye fahari, viingilio vya maji vilivyo peke yavyo na ghuba zenye utulivu, misitu ya mierezi, misonobari na Douglas fir mikubwa mno. Mara kadhaa tulisaidia kulungu wachovu na watoto wao walipojaribu kuogelea kuvuka milango-bahari yenye maji ya kwenda kasi wakitoroka wawindaji.

Alasiri moja tulimwona aina ya tai akipaa chinichini kuvuka bahari, kucha zake zikishika kwa thabiti aina ya samaki ya salmoni mkubwa. Samaki huyo alikuwa mkubwa sana asiweze kumwinua juu kabisa nje ya maji, hivyo tai alielekea ufuoni mwa bahari akifungasha samaki salmoni. Frank Franske, mshiriki mwenzetu, aliona uwezekano wa mlo naye akakimbia ufuoni mwa bahari kukutana na tai huyo mchovu na kumshawishi ampe mawindo yake. Kundi letu la mapainia likawa na chakula kitamu cha jioni cha salmoni, na tai akajifunza kutoa bila kupenda.

Kwenye kisiwa kidogo kimoja katika ukingo wa Kisiwa cha Vancouver, wenzi wa ndoa walioitwa Thuot walikubali kweli za Biblia. Mume hakujua kusoma, mwenye kushikilia maoni sana, anayefuata maoni yake mwenyewe aliyekuwa katika umri wa miaka ya kati ya 90, na mkeye alikuwa katika umri wa miaka ya kati ya 80. Hata hivyo, mume alipendezwa sana na kweli hivi kwamba alijinyenyekeza na kumruhusu mkeye kumfundisha kusoma. Muda si muda aliweza kujifunza Biblia na vichapo vya Sosaiti mwenyewe. Chini ya miaka mitatu baadaye, nilikuwa na furaha ya kubatiza wote wawili nyumbani kwenye kisiwa chao kilicho mbali, tukitumia mashua yetu ya makasia kuwa kidimbwi cha kubatiza!

Pia tulikuwa na furaha ya kuona familia ya Sallis katika Mto Powell wakiitikia ujumbe wa Ufalme. Walter alikisoma kijitabu War or Peace—Which? na kutambua kweli zilizokuwamo mara moja. Baada ya muda mfupi familia nzima ikaungana na Walter katika upainia katika Vancouver, mahali tulikuwa tukifunga Charmian katika kipindi cha kipupwe. Alithibitika kuwa mwenye bidii sana, na kwa miaka mingi alipendwa sana na ushirika mzima wa ndugu katika eneo la Vancouver. Alimaliza mwendo wake wa kidunia katika 1976, akiacha familia kubwa ya Mashahidi.

Kushinda Upinzani

Makasisi katika vijiji vya Wahindi wenyeji mara nyingi hawakupenda kazi yetu, wakitudhania kuwa wezi wa makao yao ya kiroho. Katika Port Simpson kasisi wa mahali pale aliamuru kwamba chifu wa kijiji atukataze kutembelea nyumba za watu. Tulikutana na chifu na kumwuliza ikiwa alifikiri kasisi kwa kufaa aliwaona watu kuwa wajinga wasiweze kutumia akili zao wenyewe. Tulidokeza kuwa watu wake wapewe fursa ya kusikia Neno la Mungu na kujiamulia wenyewe wanachotaka kuamini. Tokeo: Alituruhusu kuendelea kuhubiri katika kijiji.

Chifu mwingine wa kijiji kwa miongo mingi alizuia jitihada zote kupitia kwa washiriki wa baraza na vikundi vya kidini kuzuia Mashahidi wasikutane na watu wake. “Maadamu mimi ni chifu,” akasema, “Mashahidi wa Yehova wanakaribishwa hapa.” Kweli, hatukukaribishwa kila mahali, lakini hatukulazimishwa kamwe kuondoka kwenye eneo ujapokuwa upinzani. Hivyo tuliweza kutimiza huduma yetu kila mara tulipotia nanga.

Kuvumilia Matatizo Baharini

Kwa miaka mingi, tulitatizwa na dhoruba, kujaa na kupwa kwa maji, mawe yasiyoonyeshwa katika ramani, na wakati mwingine matatizo ya mtambo wa mashua. Wakati mmoja tulipeperushwa karibu sana na Kisiwa cha Lasqueti, karibu kilometa 160 kaskazini mwa Vancouver. Tulikwama kwenye miamba tukiachwa hapo na kupwa kwa maji, na usalama wetu ukitegemea hali ya hewa. Ikiwa hali ya hewa ingebadilika kuwa mbaya, mashua ingalivunjwa vipande-vipande kwenye mawe. Sote tulitambaa kwenye miamba na kufanya yote tuliyoweza katika hali hiyo mbaya. Tulikula chakula cha mchana, tukasoma, na kungoja kujaa kwa maji tena.

Zijapokuwa hatari nyingi na mambo yaliyotusumbua, hayo yalikuwa maisha yenye afya na furaha. Hata hivyo, kuzaliwa kwa wana wetu wawili kulileta badiliko kubwa. Tuliendelea kuishi kwenye mashua, lakini wakati wowote ambapo tungesafiri mbali kaskazini kufikia Mto Oona, Anna na vivulana hao walibaki hapo na wazazi wake wakati sisi wengine tuliendelea zaidi kaskazini kuelekea Alaska. Halafu tuliporudi kusini, Anna na watoto walijiunga nasi tena.

Siwezi kukumbuka watoto wakilalamika au wakiwa wagonjwa. Walivalia mishipi ya kinga-uhai wakati wote, na wakati mwingine tulifunga kamba kuwazungushia. Ndiyo, kulikuwa na pindi zenye mkazo.

Marekebisho Zaidi

Katika 1936 ilitubidi kuacha Charmian, na nilipata kazi ya kimwili. Baadaye tulipata mwana wa tatu. Baada ya muda, nikanunua mashua ya uvuvi, ambayo haikutumika tu kwa mahitaji ya maisha lakini pia ilituwezesha kuendelea katika kazi ya kuhubiri katika pwani.

Tulianzisha makao katika Kisiwa cha Digby, upande wa pili wa ghuba kutoka Prince Rupert, na muda si muda kutaniko dogo likaanzishwa. Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2 kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilipopigwa marufuku katika Kanada, tungechukua mashua kwenda upande wa Prince Rupert baada ya usiku wa manane kuvamia eneo haraka haraka, tukiacha fasihi kwa kila nyumba. Hakuna yeyote aliyepata kuhusianisha pitapita zetu katika usiku wa manane na ugawanyaji wa fasihi zilizopigwa marufuku!

Nchi Imekuwa na Rutuba

Pole pole watu wengi zaidi wakaanza kushiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova, na katika 1948 uhitaji wa Jumba la Ufalme katika Prince Rupert ulionekana. Baada ya kununua jengo la kijeshi lililokuwa upande mwingine wa bandari, tulilibomoa, tukalicheleza upande mwingine, halafu kulipeleka mahali pa ujenzi. Yehova akabariki kazi yetu ngumu, na tukawa na Jumba la Ufalme letu.

Katika 1956, nilirudia upainia, na Anna alijiunga nami katika 1964. Tulihubiri kwa mashua kando ya Pwani ya Pasifiki. Kwa muda tulishiriki katika kazi ya mzunguko pia, tukizungukia makutaniko kutoka Visiwa vya Queen Charlotte upande wa mashariki hadi upande mwingine wa milima kufika Ziwa Fraser, na baadaye mpaka Prince George na mji wa Mackenzie. Kwa miaka mingi, tulisafiri maelfu ya maili kwa gari, mashua, na ndege Kaskazini–Magharibi mwa Pasifiki kote.

Katika Prince Rupert tumeendelea kufurahia maono mazuri katika huduma. Anna na mimi tumejifunza na watu mmoja-mmoja waliohudhuria Watchtower Bible School of Gilead na baadaye kutumika wakiwa wamishonari katika nchi za kigeni. Ni furaha iliyoje kuona watoto wetu wa kiroho wakipeleka ujumbe wa Ufalme wenye thamani katika nchi za mbali!

Sasa sote wawili tuna umri uzidio miaka 80 na tunakabiliana na afya inayodhoofika, lakini bado tuna furaha katika utumishi wa Yehova. Umaridadi wa maumbile tulioona katika Alaska na British Columbia huamsha kumbukumbu nzuri sana. Na bado ni furaha iliyoje inayoletwa kwa kuona nchi iliyokuwa jangwa isiyozaa kiroho katika eneo hili kubwa sasa ikisitawi na makutaniko mengi ya wamsifuo Yehova.

Na hasa tunapowaona watoto wetu wenyewe pamoja na watoto wetu wa kiroho wakikua na kubariki Yehova, jambo hili linafanya mioyo yetu kuwa na furaha. Twafurahi kwamba tumeshiriki sehemu ndogo ya ukuzi wa kiroho katika eneo hili la dunia. Kwa mfano, Alaska sasa ina ofisi yake ya tawi ambayo huratibu kazi ya zaidi ya makutaniko 25.

Hapa Prince Rupert katikati kabisa ya jiji, tulikuwa na pendeleo la kuweka wakfu Jumba la Ufalme jipya lenye kupendeza katika 1988. Ndiyo, twashangilia, kama vile Isaya, katika kusema: “Umeliongeza hilo taifa, BWANA, . .  wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii.”—Isaya 26:15.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikitumika katika kazi ya mzunguko 1964-67

[Picha katika ukurasa wa 24]

Aina ya mashua iliyotumiwa katika kutoa ushahidi kandokando ya pwani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki