Kaburi la Petro—Je, Liko Vatikani?
“KABURI la Mwana-Mfalme wa Mitume limepatikana.” Tangazo hilo la ushindi la Papa Pius 12 lilitangazwa na redio ya Vatikani. Ulikuwa mwisho wa 1950, uchimbuzi mwingi mgumu chini ya Basilika ya St. Peter ulikuwa umetoka tu kukamilishwa. Kulingana na watu fulani, matokeo ya utafiti huo wa akiolojia ulithibitisha kwamba kwa kweli Petro alizikwa Vatikani. Lakini, si kila mtu alikubali.
Kwa Wakatoliki, Kanisa la St. Peter lililoko Vatikani lina umaana wa kipekee. “Kusudi kuu la kuhiji Roma ni kukutana na mwandamani wa Petro na kupokea baraka yake,” chasema kitabu fulani cha mambo ya Kikatoliki, “kwa sababu Petro alikuja Roma naye alizikwa huko.” Lakini kweli Petro alizikwa Roma? Je, kaburi lake liko Vatikani? Je, mifupa yake imepatikana?
Fumbo la Kiakiolojia
Uchimbuzi mwingi, ulioanza karibu 1940 na kuendelea kwa karibu miaka kumi, umekuwa suala lenye mzozo mwingi sana. Waakiolojia walioteuliwa na papa walipata nini? Kwanza, mahali pa maziko pa wapagani penye makaburi mengi. Katikati yayo, chini ya altare ya sasa ya papa, walitambua aedicula, yaani nguzo iliyowekwa katika pengo la ukutani, iliyokusudiwa kubeba sanamu, na kuwekwa katika ukuta uliopigwa plasta nyekundu na kufungwa kwa kuta mbili. Hatimaye, na kwa kushangaza sana, mabaki fulani ya binadamu yalipatikana, ambayo yasemekana yalitoka katika zile kuta mbili.
Hapa ndipo mafasiri yalipoanza. Kulingana na wasomi kadhaa Wakatoliki, magunduo hayo yathibitisha pokeo la kwamba Petro aliishi na kufia-imani katika Roma wakati wa utawala wa Nero, labda wakati wa mnyanyaso wa 64 W.K. Hata imesemwa kwamba mabaki hayo ni masalio ya mtume huyo na yaweza kutambulishwa hivyo kwa mwandiko ambao, kulingana na fasiri moja, yasema, “Petro yu hapa.” Yaonekana kwamba Papa Paulo 6 alikuwa akitegemeza wazo lake wakati ambapo katika 1968 alitangaza ugunduzi wa “miili mifu ya M[takatifu] Petro, yastahiliyo ujitoaji wetu na kicho chetu.”
Hata hivyo, pamoja na mafasiri hayo kulikuwa na mabishano pia. Mwaakiolojia Mkatoliki Antonio Ferrua, ambaye ni Myesuiti aliyeshiriki katika uchimbuzi wa Vatikani, amethibitisha zaidi ya mara moja kwamba ‘hakuruhusiwa kuchapisha’ kila kitu anachojua juu ya suala hilo, mambo ambayo yaonekana yangepinga dai la kwamba masalio ya Petro yametambuliwa. Isitoshe, kitabu fulani cha mambo ya Roma, kilichohaririwa na Kardinali wa Katoliki Poupard na kuchapishwa katika 1991, kilisema kwamba “uchunguzi wa kisayansi wa mifupa ya kibinadamu iliyopatikana chini ya misingi ya Ukuta Mwekundu inaonekana haikuwa na uhusiano wowote na mtume Petro.” Na kwa kushangaza, katika chapa iliyofuata (baadaye katika 1991), fungu hilo la maneno lilipotea, na sura mpya, yenye kichwa “Jambo la Hakika: Petro Katika St. Peter,” iliongezwa.
Fasiri ya Masalio
Ni wazi kwamba magunduzi hayo yangeweza kufasiriwa na kwamba hayo hufasiriwa kuwa mambo tofauti kwa watu tofauti-tofauti. Kwa kweli, wanahistoria wa Katoliki wenye mamlaka zaidi watambua kwamba “matatizo ya kihistoria ya kufia-imani kwa Petro katika Roma, na mahali alipozikwa, yanatiliwa shaka.” Magunduzi hayo yafunua nini?
Ile nguzo ya aedicula, kulingana na wale wanaotaka kushikilia mapokeo ya Katoliki, ndiyo “kumbukumbu” lirejezewalo na Gayo fulani, kasisi mmoja aliyeishi mwanzoni mwa karne ya tatu. Kulingana na Eusebio wa Kaisaria, ambaye alikuwa mwanahistoria wa karne ya nne, Gayo alisema kwamba ‘angeonyesha kumbukumbu la Petro katika Kilima cha Vatikani.’ Waungaji-mkono wa mapokeo wadai kwamba mtume huyo alizikwa hapo, chini ya nguzo iliyokuja kuitwa “kumbukumbu la Gayo.” Hata hivyo, wengine hufasiri matokeo ya uchimbuzi huo kwa njia tofauti sana, wakisema kwamba Wakristo wa kwanza hawakushughulika kupita kiasi juu ya kuzika wafu wao na kwamba hata kama Petro aliuawa huko, hakungewezekana kupata mwili wake. (Ona sanduku, ukurasa 29.)
Kuna wale ambao hawakubali kwamba “kumbukumbu la Gayo” (kama hilo ndilo limepatikana) ni kaburi. Wao wasisitiza kwamba hiyo ni nguzo iliyojengwa kwa heshima ya Petro karibu na mwisho wa karne ya pili na kwamba baadaye ilikuja “kuonwa kuwa nguzo la kaburi.” Hata hivyo, kulingana na mwanatheolojia Oscar Cullmann, “uchimbuzi mwingi wa Vatikani hautambui kamwe kaburi la Petro.”
Vipi juu ya mifupa? Yaweza kusemwa kwamba bado haijulikani mahali mifupa hiyo ilipotoka hasa. Kwa kuwa makaburini makubwa ya karne ya kwanza ya wapagani yalikuwa mahali ambapo sasa ni Kilima cha Vatikani, masalio mengi ya binadamu yalizikwa katika eneo hilo, na mengi tayari yamepatikana. Maandishi yasiyokamilika (labda ya karne ya nne) ambayo wengine wasema yanatambua mahali ambapo masalio hayo yalipatikana kuwa kaburi la mtume huyo, huenda, yakarejezea “ile idhaniwayo kuwa kuwapo kwa mifupa ya Petro.” Isitoshe, wastadi wengi wa maandiko wanaonelea kwamba mwandiko huo waweza hata kumaanisha kwamba “Petro hayupo hapa.”
‘Mapokeo Yasiyotegemeka’
“Vyanzo vya awali na vyenye kutegemeka havitaji mahali pa kufia-imani [kwa Petro], lakini miongoni mwa vyanzo vya habari vya baadaye na visivyotegemeka kuna upatano kwa vyote kwamba palikuwa katika eneo la Vatikani,” asema mwanahistoria D. W. O’Connor. Kwa hiyo, utafutaji wa kaburi la Petro katika Vatikani ulitegemea mapokeo yasiyotegemeka. “Masalio yalipokuja kuwa yenye umaana sana,” athibitisha O’Connor, “Wakristo walikuja kuamini kwa moyo mweupe kwamba lile [kumbukumbu] la Petro kwa kweli lilionyesha mahali hasa pa kaburi lenyewe.”
Mapokeo hayo yalisitawi pamoja na kutoa kicho kusiko kimaandiko kwa masalio. Kutokea karne za tatu na nne na kuendelea, vituo kadhaa vya kikanisa vilitumia, kikweli au kibandia—na bila kukosa kupata faida ya kifedha—katika jitihada ya kupata ukuu kabisa wa “kiroho” na kuendeleza mamlaka yao wenyewe. Hivyo, wakiwa na hakika kwamba mabaki ya Petro yalikuwa na nguvu za kimwujiza, wahiji walisafiri kuona hilo lidhaniwalo kuwa kaburi lake. Mwishoni mwa karne ya sita, waamini walikuwa na mazoea ya kutupa vipande vyenye uzito fulani vya nguo katika “kaburi.” “Ajabu,” likasema simulizi moja la wakati huo, “kama imani ya mwombaji ni thabiti, nguo itolewapo kutoka ndani ya kaburi, hiyo itajawa na sifa za kimungu nayo itakuwa na uzito kuliko ilivyokuwa awali.” Jambo hilo laonyesha utayari wa watu kuamini mambo wakati huo.
Kwa karne zilizopita, hekaya kama hii na mapokeo yasiyo na msingi wowote ulichangia sana kukua kwa umashuhuri wa Basilika ya Vatikani. Hata hivyo, hoja zenye kupinga zilitolewa. Katika karne za 12 na 13, Wawaldense walishutumu mambo hayo yanayopita kiasi na, kwa kutumia Biblia, wakaeleza kwamba Petro hakuwahi kuwa Roma. Karne kadhaa baadaye, wateteaji wa Mabadiliko ya Kiprotestanti walibisha kwa njia iyo hiyo. Katika karne ya 18, wanafalsafa mashuhuri waliona mapokeo hayo kuwa hayana msingi, kihistoria na Kimaandiko. Wasomi, Wakatoliki na watu wengine wote walio mashuhuri wana maoni ayo hayo mpaka leo hii.
Je, Petro Alikufa Roma?
Petro, mvuvi mnyenyekevu wa Galilaya, hakuwazia kamwe wazo lolote la ukuu juu ya wazee katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Badala ya hivyo, yeye alijieleza kuwa “mzee mwenzi.” (1 Petro 5:1-6, Revised Standard Version) Unyenyekevu wa Petro watofautiana sana na umashuhuri unaopewa lile lidhaniwalo kuwa kaburi lake, kama iwezavyo kuonekana na mtu yeyote azuruye Basilika ya Vatikani.
Ili lisisitize ukuu walo juu ya dini nyingine za Kikristo, Kanisa Katoliki limetumia mapokeo ‘ya baadaye na yasiyotegemeka sana’ yasemayo kwamba Petro aliishi kwa muda fulani katika Roma. Lakini yashangaza kwamba mapokeo ya kale yaona mahali alipozikwa kuwa mahali pengine katika Roma bali si katika Vatikani. Hata hivyo, kwa nini tusishikilie mambo ya hakika yaliyoandikwa katika Biblia, ambayo ndiyo chanzo cha habari kamili za Petro? Kutokana na Neno la Mungu ni wazi kwamba, kwa kutii mielekezo aliyopokea kutoka baraza linaloongoza la kutaniko la Kikristo katika Yerusalemu, Petro alifanya kazi yake katika sehemu za mashariki mwa ulimwengu wa kale, kutia ndani Babiloni.—Wagalatia 2:1-9; 1 Petro 5:13; linganisha Matendo 8:14.
Alipowaandikia Wakristo katika Roma, karibu 56 W.K., mtume Paulo alisalimu washiriki wapatao 30 wa kutaniko hilo bila hata kutaja Petro. (Warumi 1:1, 7; 16:3-23) Kisha, kati ya miaka 60 na 65 W.K., Paulo aliandika barua sita kutoka Roma, lakini Petro hatajwi—uthibitisho wa hali hiyo wenye nguvu sana kwamba Petro hakuwa huko.a (Linganisha 2 Timotheo 1:15-17; 4:11.) Utendaji wa Paulo katika Roma waelezwa kwenye mwisho wa kitabu cha Matendo, na mara nyingine tena, bila mtajo wowote wa Petro. (Matendo 28:16, 30, 31) Na basi, uchunguzi mzuri wa uthibitisho wa Biblia, bila kuwa mawazo yaliyotungwa awali, waweza kuongoza tu kwenye mkataa kwamba Petro hakuhubiri katika Roma.b
“Ukuu” wa papa wategemea mapokeo yasiyotegemeka na matumizi mabaya ya maandiko. Ni Yesu, wala si Petro, ndiye msingi wa Ukristo. ‘Kristo ni kichwa cha kutaniko,’ asema Paulo. (Waefeso 2:20-22; 5:23, NW) Ni Yesu Kristo ambaye Yehova alimtuma kubariki na kuokoa watu wote wenye imani.—Yohana 3:16; Matendo 4:12; Warumi 15:29; ona pia 1 Petro 2:4-8.
Kwa hiyo, wale wote ambao husafiri kuona kile wanachoamini kuwa kaburi la Petro ili ‘kukutana na mwandamani wake’ wanakabiliwa na tatizo la kukubali ‘mapokeo yasiyotegemeka’ au kuamini Neno la Mungu lenye uaminifu. Kwa kuwa Wakristo wanataka ibada yao ikubalike na Mungu, ‘wamkaziapo macho Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu,’ na kile kielelezo kikamilifu ambacho yeye alituachia tufuate.—Waebrania 12:2; 1 Petro 2:21.
[Maelezo ya Chini]
a Karibu na miaka 60-61 W.K., Paulo aliandika barua zake kwa Waefeso, Wafilipi, Wakolosai, Filemoni, na kwa Waebrania; karibu 65 W.K., akaandika barua yake ya pili kwa Timotheo.
b Swali “Je, Petro Alipata Kuwa Katika Roma?” lilishughulikiwa katika Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1972, kurasa 669-71 la Kingereza.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
“Uchimbuzi mwingi haujagundua ishara yoyote ya kaburi chini ya Aedicula; wala kwa kweli hakuna uhakika wowote kwamba mwili wa M[takatifu] Petro uliweza kupatikana kutoka kwa wafishaji ili uzikwe na jamii ya Wakristo. Katika hali za kawaida, mwili wa mtu aliyeonwa kuwa mgeni (peregrinus), na machoni pa sheria mhalifu wa kawaida, sanasana ungetupwa katika Tiber. . . . Na zaidi, hakungekuwa na upendezi mwingi wa kuhifadhi masalio ya mwili katika tarehe hiyo ya mapema kama ilivyokuwa baadaye, wakati ambapo imani katika mwisho uliokaribia sana wa ulimwengu ilipokwisha na vidhehebu vya wafia-imani kuanza kutokea. Basi, kuna uwezekano mkubwa halisi kwamba mwili wa M[takatifu] Petro kwa kweli haukupatikana ili uzikwe.”—The Shrine of St. Peter and the Vatican Excavations, cha Jocelyn Toynbee na John Ward Perkins.