Mateseko ya Binadamu—Mbona Mungu Anayaruhusu?
KATIKA mwanzo wa historia ya mwanadamu, hakukuwa na machozi ya huzuni au ya maumivu. Mateseko ya binadamu hayakuwapo. Mwanadamu alipewa mwanzo mkamilifu. “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwanzo 1:31.
Lakini wengine hukataa wakisema, ‘Lile simulizi la Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni ni mambo ya kusikia tu.’ Kwa sikitiko, makasisi wengi wa Jumuiya ya Wakristo husema hivyo. Hata hivyo, hakuna mtu mwingine ila Yesu Kristo aliyethibitisha kwamba matukio katika Edeni kuwa yalikuwa ya kihistoria. (Mathayo 19:4-6) Zaidi ya hayo, njia pekee ya kufahamu kwa nini Mungu ameruhusu mateseko ya binadamu ni kuchunguza matukio haya ya historia ya mapema ya mwanadamu.
Yule mwanadamu wa kwanza, Adamu, alipewa kazi yenye kuridhisha ya kutunza bustani ya Edeni. Pia, Mungu alimwekea mradi wa kupanua makao yake ya Kiedeni yawe bustani ya raha ya ulimwenguni pote. (Mwanzo 1:28; 2:15) Ili kusaidia Adamu atimize kazi hii ngumu, Mungu alimpa mwenzi wa ndoa, Hawa, naye akawaambia wazae, waongezeke na kuijaza dunia. Walakini kitu kingine kilihitajiwa ili kuhakikisha kufanikiwa kwa kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu. Wakiwa wameumbwa kwa mfano wa Mungu, mwanadamu alipewa hiari; kwa hiyo, ilikuwa lazima kwamba mapenzi ya mwanadamu yasipingane na mapenzi ya Mungu. Ama sivyo, kungekuwapo mvurugo katika ulimwengu wote mzima, na kusudi la Mungu la kujaza dunia na familia ya wanadamu wenye amani halingetimizwa.
Utii kwa utawala wa Mungu haukuwa jambo la kujitokeza lenyewe tu. Ulikuwa wonyesho wa upendo wa hiari ya mwanadamu. Kwa kielelezo, tunasoma kwamba wakati Yesu Kristo alipokabili jaribu kali sana, aliomba, “Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.
Vivyo hivyo, ilikuwa juu ya Adamu na Hawa kuthibitisha kama walitaka kujitiisha chini ya utawala wa Mungu. Kuhakikisha hili, Yehova Mungu alifanya mpango wa jaribio rahisi. Mmoja kati ya miti katika bustani uliitwa “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Uliwakilisha haki ya Mungu ya kuamua viwango sahihi vya mwenendo. Kwa lugha iliyo wazi, Mungu alikataza kula tunda kutoka kwa mti huu hususa. Ikiwa Adamu na Hawa walikosa kutii, matokeo yangekuwa kifo kwao.—Mwanzo 2:9, 16, 17.
Mwanzo wa Mateseko ya Binadamu
Siku moja mwana wa roho wa Mungu alitilia shaka njia ya Mungu ya kutawala. Akitumia nyoka kama msemaji, alimwuliza Hawa: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 3:1) Hivyo mbegu moja ya shaka ilipandwa ndani ya akili ya Hawa kama njia ya Mungu ya kutawala ilikuwa sahihi.a Katika kujibu Hawa alitoa jibu sahihi, alilokuwa amejifunza kutoka kwa mumeye. Hata hivyo, kiumbe huyo wa roho alimpinga Mungu na kudanganya kuhusu matokeo ya kutotii, akisema: “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:4, 5.
Kwa huzuni, Hawa alidanganyika katika kufikiri kwamba kutotii kungeleta tokeo, si la mateseko ya binadamu, bali la maisha mazuri zaidi. Kadiri alivyotazama lile tunda, ndivyo lilivyozidi kuonekana kuwa lenye kutamanika, naye akaanza kulila. Baadaye, alimshawishi Adamu ale pia. Kwa huzuni, Adamu alichagua kuwa na upendeleo wa mkeye badala ya wa Mungu.—Mwanzo 3:6; 1 Timotheo 2:13, 14.
Kwa kuanzisha uasi huu, kiumbe huyo wa roho alijigeuza kuwa mpingaji wa Mungu. Hivyo, akaja kuitwa Shetani, kutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “mpingaji.” Pia alisema uongo kuhusu Mungu, akawa mchongezi. Hivyo, pia anaitwa Ibilisi, kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “mchongezi.”—Ufunuo 12:9.
Hivyo, mateseko ya binadamu yakaanza. Watatu wa viumbe wa Mungu walikuwa wametumia vibaya hiari yao, wakichagua njia ya maisha ya ubinafsi kwa kumpinga Muumba wao. Swali sasa likazuka, Mungu angeshughulikiaje uasi huu katika njia ya haki ambayo ingetoa uhakikisho kwa viumbe wale wengine wenye akili, kutia na malaika waaminifu mbinguni na wazao wa baadaye wa Adamu na Hawa?
Itikio la Mungu la Hekima
Wengine waweza kudai kwamba lingalikuwa jambo bora zaidi kama Mungu angewaharibu Shetani, Adamu, na Hawa mara hiyo. Lakini hilo halingesuluhisha masuala yaliyotokezwa na ule uasi. Shetani alikuwa ametilia shaka njia ya Mungu ya kutawala, akidokeza kwamba binadamu wangekuwa bora zaidi bila utawala wa Mungu. Pia, kufanikiwa kwake katika kugeuza wanadamu wawili wa kwanza dhidi ya utawala wa Mungu kulitokeza maswali mengine. Kwa kuwa Adamu na Hawa walifanya dhambi, je, hili lilimaanisha kwamba kulikuwa na kasoro katika njia ambayo Mungu alikuwa amemuumba mwanadamu? Je, Mungu angekuwa na mtu yeyote duniani ambaye angeweza kubaki akiwa mwaminifu kwake? Na vipi kuhusu wana wa kimalaika wa Yehova walioshuhudia uasi wa Shetani? Je, wangetegemeza haki ya enzi kuu Yake? Bila shaka, wakati wa kutosha ulihitajiwa kujibu masuala haya. Hiyo ndiyo sababu Mungu ameruhusu Shetani kuwapo hadi siku yetu.
Kuhusu Adamu na Hawa, siku walipokataa kutii, Mungu aliwahukumia kifo. Hivyo kifo kikaanza. Wazao wao, waliozaliwa baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, walirithi dhambi na kifo kutoka kwa wazazi wao wasiokamilika.—Warumi 5:14.
Shetani alianza na wanadamu wawili wa kwanza wakiwa upande wake wa lile suala. Ametumia wakati alioruhusiwa ajaribu kuweka wazao wote wa Adamu chini ya utawala wake. Yeye pia alifaulu katika kushawishi idadi fulani ya malaika kuungana naye katika uasi wake. Hata hivyo, wengi wa wana wa kimalaika wa Mungu kwa uaminifu mshikamanifu wameitegemeza haki ya utawala wa Yehova.—Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6; Ufunuo 12:3, 9.
Utawala wa Mungu dhidi ya ule wa Shetani ulikuwa suala kuu nalo lilitokea sana katika siku za Ayubu. Mwanamume huyu mwaminifu alithibitisha kwa mwenendo wake kwamba alichagua utawala wa uadilifu wa Mungu badala ya uhuru wa kishetani, kama vile wanaume wenye kumhofu Mungu kama Abeli, Enoki, Noa, Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yusufu walivyokuwa tayari wamefanya. Ayubu akawa kichwa cha mazungumzo yaliyofanyika mbinguni mbele ya malaika waaminifu wa Mungu. Kwa kutegemeza utawala Wake wa uadilifu, Mungu alimwambia Shetani: “Je, umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na uelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu?”—Ayubu 1:6-8.
Akikataa kukubali kushindwa, Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo tu, kwa maana Mungu alikuwa amembariki Ayubu sana kwa ufanisi wa kimwili. Hivyo ndivyo Shetani alisisitiza: “Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.” (Ayubu 1:11) Shetani hata aliendelea zaidi, akitilia shaka ushikamanifu wa viumbe vyote vya Mungu. “Yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake,” akasema. (Ayubu 2:4) Ushambulizi huu wenye uchongezi ulihusu si Ayubu tu lakini waabudu waaminifu wote wa Mungu mbinguni na duniani. Shetani alidokeza kwamba wangeachilia uhusiano wao pamoja na Yehova ikiwa uhai wao ungekuwa hatarini.
Yehova Mungu alikuwa na uhakika kamili katika ushikamanifu wa Ayubu. Akithibitisha hilo, alimruhusu Shetani kuleta mateseko ya binadamu juu ya Ayubu. Kwa uaminifu wake Ayubu hakuliondolea lawama jina lake tu bali la maana zaidi, alitetea uadilifu wa enzi kuu ya Yehova. Ibilisi alithibitishwa kuwa mwongo.—Ayubu 2:10; 42:7.
Hata hivyo, kielelezo bora zaidi cha uaminifu chini ya jaribu kilikuwa Yesu Kristo. Mungu alikuwa ameuhamisha uhai wa Mwanaye wa kimalaika ndani ya tumbo la uzazi la bikira. Hivyo basi Yesu hakurithi dhambi na kutokamilika. Badala yake alikua akawa mwanadamu mkamilifu, ulinganifu sahihi wa mwanadamu wa kwanza kabla ya huyo kupoteza ukamilifu wake. Shetani alimfanya Yesu shabaha ya pekee, akileta ushawishi na majaribu mengi juu yake, na kumalizia kwa kumwaibisha kwa kifo. Lakini Shetani alishindwa kuharibu ushikamanifu wa Yesu. Kwa njia kamili, Yesu alitegemeza uadilifu wa utawala wa Baba yake. Pia alithibitisha kwamba mtu mkamilifu Adamu hakuwa na sababu ya kujiunga na uasi wa Shetani. Adamu angalikuwa mwaminifu chini ya mtihani wake mdogo.
Ni Nini Jingine Limethibitishwa?
Karibu miaka 6,000 ya mateseko ya binadamu imekwisha kupita tangu uasi wa Adamu na Hawa. Katika wakati huu Mungu ameruhusu wanadamu kufanya majaribio ya aina tofauti-tofauti za serikali. Rekodi ya mateseko mabaya sana ya binadamu yathibitisha kwamba mwanadamu hana uwezo wa kujitawala mwenyewe. Kwa kweli, michafuko ya kisiasa sasa imeenea katika sehemu nyingi za dunia. Uhuru kutokana na Mungu, kama Shetani alivyodai, ni yenye msiba.
Yehova hajalazimika kujithibitishia chochote. Anajua kwamba njia yake ya kutawala ni ya uadilifu na ya kuwatakia mema viumbe vyake. Hata hivyo, ili kujibu maswali yote yaliyotokezwa na uasi wa Shetani kwa njia ya kuridhisha amewapa viumbe vyake vyenye hekima fursa ya kuonyesha uchaguzi wao wa utawala wake wa uadilifu.
Thawabu ya kumpenda Mungu na ya kuwa mwaminifu yapita muda mfupi wa mateseko mkononi mwa Ibilisi. Kisa cha Ayubu chatoa kielezi juu ya hili. Yehova Mungu alimponya Ayubu kutokana na ugonjwa ambao Ibilisi alikuwa amemletea. Zaidi ya hayo, Mungu “akaubariki huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake.” Mwishowe, baada ya miaka 140 ya ziada ya maisha, “Ayubu akafa, mzee sana mwenye kujawa na siku.”—Ayubu 42:10-17.
Mwandikaji wa Biblia Mkristo Yakobo aelekeza uangalifu huu akisema: “Mmesikia juu ya uvumilivu wa [Ayubu] na mmeona tokeo alilotoa Yehova, kwamba Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye huruma.”—Yakobo 5:11, kielezi-chini cha New World Translation.
Wakati sasa umekwisha wa Shetani na ulimwengu wake. Karibuni, Mungu atayaondoa mateseko yote ambayo uasi wa Shetani umeletea wanadamu. Hata wafu watafufuliwa. (Yohana 11:25) Halafu, wanaume waaminifu kama Ayubu watapata fursa ya kupata uhai wa milele katika dunia paradiso. Hizi baraka za wakati ujao ambazo Mungu atawamwagia watumishi wake zitamtetea milele na milele akiwa Mwenye Enzi Kuu mwadilifu ambaye kwelikweli “ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye huruma.”
[Maelezo ya Chini]
a Mwanasheria mmoja na mtungaji wa mapema katika karne ya 20, Philip Mauro, aliyechunguza swali hili katika mazungumzo yake ya “Chanzo cha Uovu,” alimalizia kwamba hii ilikuwa “sababu ya matatizo yote ya mwanadamu.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
MIUNGU MIKATILI YA WANADAMU
MIUNGU ya kale mara nyingi ilionyeshwa kuwa yenye tamaa ya kumwaga damu na yenye uchu. Ili kuwaridhisha, wazazi hata walichoma watoto wao wakiwa hai motoni. (Kumbukumbu la Torati 12:31) Kwa upande mwingine wenye kupita kiasi, wanafalsafa wapagani walifundisha kwamba Mungu hana hisia kama hasira au sikitiko.
Maoni ya wanafalsafa yenye uvuvio wa mashetani yalikuwa na uvutano kwa watu waliodai kuwa wa Mungu, Wayahudi. Mwanafalsafa Myahudi Filo, aliyeishi wakati wa Yesu, alisisitiza kwamba Mungu “hana hisia kamwe.”
Hata dhehebu la Wayahudi la Mafarisayo lenye kufuata sheria sana halikuepuka uvutano wa falsafa za Kigiriki. Wao walikubali mafundisho ya Plato kwamba mwanadamu amefanyizwa kwa nafsi isiyoweza kufa iliyokwama ndani ya mwili wa binadamu. Isitoshe, kulingana na mwanahistoria wa karne ya kwanza Yosefo, Mafarisayo waliamini kwamba nafsi za watu waovu “hupatwa na adhabu ya milele.” Hata hivyo, Biblia haitoi msingi wowote kwa maoni hayo.—Mwanzo 2:7; 3:19; Mhubiri 9:5; Ezekieli 18:4.
Vipi juu ya wafuasi wa Yesu? Je, walijiruhusu kuvutiwa na falsafa za kipagani? Wakitambua hatari hiyo, mtume Paulo alionya Wakristo wenzake hivi: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”—Wakolosai 2:8; ona pia 1 Timotheo 6:20.
Yasikitisha kwamba idadi fulani ya wale waliodai kuwa waangalizi wa Kikristo wa karne za pili na tatu walipuuza onyo hilo na kufundisha kwamba Mungu hana hisia. The Encyclopedia of Religion chaeleza hivi: “Kwa ujumla, sifa za Mungu zilieleweka sana kama zilivyothibitishwa katika mawazo ya Kiyahudi na ya kifalsafa ya wakati huo . . . Wazo la kwamba Mungu Baba angeweza kuwa na hisia kama sikitiko . . . limeonwa kwa ujumla kuwa lisilokubalika angalau hadi karne ya ishirini.”
Kwa hiyo, Jumuiya ya Wakristo imekubali fundisho la uwongo la mungu mkatili aadhibuye watenda dhambi kwa kuwafanya wateseke milele wakiwa macho. Kwa upande mwingine, Yehova Mungu asema waziwazi katika Neno lake, Biblia, kwamba “mshahara wa dhambi ni mauti,” si mateso ya milele ukiwa macho.—Warumi 6:23.
[Hisani]
Juu: Acropolis Museum, Ugiriki
Kwa hisani ya The British Museum
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kusudi la Mungu la kugeuza dunia iwe paradiso ya Kiedeni lazima litimizwe!