Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 12/15 kur. 4-7
  • Krismasi—Je, Kweli Ni ya Kikristo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Krismasi—Je, Kweli Ni ya Kikristo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Asili ya Kipagani ya “Krismasi”
  • Tukio Lenye Shangwe
  • Zawadi za Krismasi
  • Mheshimu Kristo Akiwa Mfalme!
  • Je, Krismasi Ni ya Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Ukweli Kuhusu Krismasi
    Amkeni!—2010
  • Krismasi Mambo ya Kweli au Ngano?
    Amkeni!—1992
  • Kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 12/15 kur. 4-7

Krismasi—Je, Kweli Ni ya Kikristo?

KULINGANA na The World Book Encyclopedia, “Krismasi ni siku ambayo Wakristo husherehekea siku ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo.” Hata hivyo, ensaiklopedia hiyo pia husema hivi: “Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku ya kuzaliwa kwa [Yesu] kwa sababu waliiona sherehe ya kuzaliwa kwa mtu yeyote kuwa desturi ya wapagani.”

The Making of the Modern Christmas, cha Golby na Purdue, chakubali: “Wakristo wa mapema hawakusherehekea kuzaliwa kwa Kristo. Sherehe za siku zenyewe za kuzaliwa zilishirikishwa na mazoea ya kipagani; Gospeli hazisemi lolote kuhusu tarehe yenyewe ya kuzaliwa kwa Kristo.”

Ikiwa sherehe za siku ya kuzaliwa hazina chanzo cha Kikristo, siku ya kuzaliwa kwa Kristo ilikujaje kuwa sherehe maarufu ya “Kikristo”?

Asili ya Kipagani ya “Krismasi”

“Kila mtu alikula na kufurahi, kazi na biashara zilifungwa kabisa kwa kipindi fulani, nyumba zilipambwa kwa miti na kudumisha rangi ya kijani-kibichi, kutembelea marafiki na kuwapa zawadi, na matajiri waliwapa zawadi wateja wao. Kipindi hicho chote kilikuwa cha kufurahisha na kutakiana mema, na watu walijiingiza katika kila aina ya vitumbuizo.”—Paganism in Christian Festivals, cha J. M. Wheeler.

Je, maelezo haya yanapatana na sherehe za Krismasi ujuazo? Kwa kushangaza hii haikuwa Krismasi! Badala ya hivyo, hayo ni maelezo ya Saturnalia—sherehe ya juma zima ya Kiroma iliyoshirikishwa na masika ya kikomo cha jua (inaonyeshwa katika ukurasa wa nyuma). Siku ya kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa kulisherehekewa katika Desemba 25, siku ya pekee ya karamu kwa dini ya Mithra ya Roma.

Kulingana na The New Encyclopædia Britannica, “Desemba 25, siku ya kuzaliwa ya Mithra, mungu wa Iran wa mwangaza na . . . siku iliyotolewa kwa jua lisiloonekana, pamoja na siku baada ya Saturnalia, ilifanywa na kanisa kuwa Krismasi, kuzaliwa kwa Kristo, ili kukinza matokeo ya sherehe hizo.” Hivyo sherehe za kuzaliwa za wapagani ziliendelea kwa kubadilisha tu majina kwa urahisi, kutoka Mithra hadi Kristo!

Hata hivyo, waweza kuhisi kwamba kuzaliwa kwa Mwana wa Mungu, Yesu, kulikuwa jambo la pekee linalostahili kukumbukwa. Kutazama yale Biblia inaeleza juu ya jambo hili kutatupa ujuzi zaidi.

Tukio Lenye Shangwe

Sura ya 2 ya Gospeli ya Luka inaeleza juu ya mandhari hiyo. Luka anatueleza jinsi malaika mbinguni, wachungaji wa hali ya chini, watumishi wa Mungu waliojitoa, na Mariamu mwenyewe alivyotenda kuelekea tukio hili lenye kutokeza.

Fikiria kwanza ‘wachungaji waliokaa makondeni’ waliokuwa ‘wakilinda kundi lao kwa zamu usiku’ jambo ambalo hawangefanya wakati wa masika. Wakati ‘malaika wa Yehova’ alipotokea na utukufu wa Mungu kung’aa kuwazunguka, wachungaji waliogopa kwanza. Walitulizwa malaika aliposema: “Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; maana leo . . . amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana.” “Wingi wa jeshi la mbinguni” la malaika lilipotokea kwa ghafula, wachungaji walijua kwamba kuzaliwa huku ni tofauti na kwingine kote. Kwa kupendeza, malaika hawakuleta zawadi zozote kwa kitoto kilichozaliwa. Badala ya hivyo malaika walimsifu Yehova, wakisema: “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.”—Luka 2:8-14.

Kihalisi, wachungaji walitaka kujionea huyu mtoto, maana ni Yehova aliyekuwa ametangaza tukio hili la furaha. Walipokuta kitoto kimelala kwenye hori, waliwaambia wazazi wao yale ambayo malaika walikuwa wamesema. Halafu wachungaji wakaenda zao, ‘huku wakimtukuza Mungu na kumsifu,’ bali si mtoto.—Luka 2:15-18, 20.

Mariamu, mama ya Yesu, bila shaka alifurahia kujifungua mtoto wake wa kwanza kwa mafanikio. Lakini pia alikuwa ‘akiyakiri maneno moyoni mwake.’ Halafu akiandamana na mumeye, Yusufu, alisafiri kwenda Yerusalemu kwa kutii Sheria ya Kimusa. Hii haikuwa sherehe ya siku ya kuzaliwa. Badala ya hivyo ulikuwa wakati wa kukipeleka kitoto kwa Mungu, “kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana.”—Luka 2:19, 22-24.

Kwenye hekalu katika Yerusalemu, Mariamu na Yusufu walikutana na Simeoni, ambaye Luka amfafanua kuwa “mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli.” Akiwa amevuviwa, alikuwa ameambiwa kwamba hangekufa kabla ya kumwona “Kristo wa Bwana.” ‘Kilichotokea baadaye pia kiliongozwa na roho ya Mungu.’ Simeoni alikichukua kitoto mikononi mwake, si ili ampe zawadi, la, bali, kumbariki Mungu, akisema: “Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, kwa amani, kama ulivyosema; kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, uliouweka tayari machoni pa watu wote.”—Luka 2:25-32.

Kisha, Ana aliye nabii mke mzee-mzee akakaribia. Yeye pia “akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake [“huyo mtoto,” New World Translation].”—Luka 2:36-38.

Mariamu, Simeoni, Ana, wachungaji, pamoja na malaika wa mbinguni, wote walifurahia kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, tafadhali, angalia kwamba hawakujiingiza katika karamu zozote za siku ya kuzaliwa, wala kujiingiza katika kutoa zawadi. Bali, walimtukuza Yehova, Mwandaliaji wa kimbingu wa njia yao ya wokovu.

Bado, wengine waweza kusababu, ‘Kwa kweli kupeana zawadi wakati wa Krismasi si makosa, maana, je, wale “wanaume watatu wenye hekima” hawakumheshimu Yesu kwa zawadi?’

Zawadi za Krismasi

Acha tuchunguze maelezo ya Kibiblia tena. Utapata yakiwa yamerekodiwa katika Gospeli ya Mathayo sura ya 2. Hakuna mtajo wowote wa sherehe ya siku ya kuzaliwa, wala hakuna tarehe yoyote inayoonyeshwa, maana kwa wazi muda fulani ulikuwa umepita baada ya kuzaliwa kwa Yesu. Katika mstari wa 1, Mathayo awaita wageni hao “mamajusi [Kigiriki, maʹgoi] wa mashariki,” na hivyo wapagani wasiokuwa na ujuzi juu ya Yehova Mungu. Ile nyota waliyofuata hawa wanaume iliwaongoza, si moja kwa moja kuelekea Bethlehemu mahali Yesu alipozaliwa, bali katika Yerusalemu, ambapo Mfalme Herode alitawala.

Mtawala huyo mwovu alipowasikia wakiuliza juu ya “yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi,” aliwahoji makuhani ili ajue hasa ‘mahali ambapo Kristo angezaliwa’ ili mtoto auawe. Makuhani walijibu kwa kunukuu unabii wa Mika ulioonyesha mahali pa kuzaliwa pa Mesiya katika Bethlehemu. (Mika 5:2) Herode kwa unafiki aliwaagiza wageni wake hivi: “Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie.” Mamajusi wakaenda zao, na ile nyota “ikawatangulia, hata ikaenda ikasimama juu ya mahali alipokuwapo mtoto.” Ona kwamba anafafanuliwa kuwa “mtoto,” na si akiwa kitoto kilichozaliwa.—Mathayo 2:1-10.

Kama matajiri wa sehemu za Mashariki walivyokuwa wakifanya walipomtembelea mtawala, mamajusi hao wapagani walianguka chini “wakamtolea [yule mtoto] tunu; dhahabu na uvumba na manemane.” Mathayo aongeza hivi: “Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine.”—Mathayo 2:11, 12.

Kutokana na maelezo haya mafupi ya Kimaandiko, watu fulani waweza kujaribu kupata msingi wa kupeana zawadi wakati wa Krismasi. Hata hivyo, Discovering Christmas Customs and Folklore chaeleza kwamba desturi za karibuni za kupeana zawadi zinapata chanzo chazo katika zawadi za Saturnalia ambazo Waroma walitolea majirani zao maskini. “Kanisa la mapema . . . kwa werevu lilihamisha umaana wazo kuwa uadhimisho wa kawaida wa zawadi za Magi.” Hili ni tofauti kama nini na waabudu wa kweli—kama wale wachungaji wa hali ya chini—ambao walimsifu Mungu, Yesu alipozaliwa!

Mheshimu Kristo Akiwa Mfalme!

Leo Yesu si mtoto tena. Yeye ni Mtawala mwenye nguvu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu, naye anapaswa kuheshimiwa akiwa hivyo.—1 Timotheo 6:15, 16.

Ikiwa wewe sasa ni mtu mzima, umewahi kuona aibu wakati, ukiwapo, watu walionyesha picha zako ukiwa mtoto? Kwa kweli, picha kama hizo zinawakumbusha wazazi wako furaha yao ulipozaliwa. Lakini sasa ukiwa na utu wako mwenyewe, je, si kweli kwamba wewe hupendelea wengine wakuone kama ulivyo? Kutokana na hilo, fikiria lilivyo jambo la ukosefu wa heshima kuelekea Kristo Yesu wakati wale wanaodai kuwa wafuasi wake wanapojiingiza sana kila mwaka katika desturi za kipagani za Krismasi na kuheshimu kitoto huku wakikosa kumheshimu akiwa Mfalme. Hata katika karne ya kwanza, mtume Paulo Mkristo alisababu juu ya kufikiri kwa kufaa juu ya Kristo kama alivyo sasa—Mfalme mbinguni. Paulo aliandika hivi: “Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena”!—2 Wakorintho 5:16, italiki ni zetu.

Kristo, akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, atatimiza ile ahadi ya kiunabii ya kuondoa maumivu, mateseko, maradhi, na kifo, iwe kweli. Ni yeye atakayeandaa makao mazuri na kazi yenye uradhi kwa wote chini ya hali za Paradiso hapa duniani. (Isaya 65:21-23; Luka 23:43; 2 Wakorintho 1:20; Ufunuo 21:3, 4) Kwa kweli, hizi ni sababu za kutosha kuepuka kutomheshimu Yesu!

Kwa kufuata mfano wa Kristo mwenyewe, Wakristo wa kweli wanajitahidi kuwapa jirani zao moja ya zawadi kuu zaidi ambazo yeyote aweza kutoa—ufahamu wa kusudi la Mungu, unaoweza kuongoza kwenye uhai wa milele. (Yohana 17:3) Aina hii ya kutoa zawadi huwaletea furaha nyingi sana, kama vile Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW; Luka 11:27, 28.

Wakristo wanaopendana kwa kweli hawaoni ugumu wa kuonyeshana upendo kwa moyo wa hiari pindi yoyote katika mwaka. (Wafilipi 2:3, 4) Kwa kielelezo kilicho rahisi, ni jambo la kusisimua kama nini kupokea zawadi ya picha kutoka kwa Mkristo mchanga ambaye, baada ya kusikiliza hotuba ya Biblia, akaichora ikiwa wonyesho wa shukrani! Pia ni jambo lenye kutia moyo kupokea zawadi isiyotazamiwa kutoka kwa mtu wa ukoo kama ishara ya upendo wake kwetu. Vivyo hivyo, wazazi Wakristo hupata furaha nyingi wachaguapo pindi ifaayo kutoa zawadi kwa watoto wao mwaka mzima. Ukarimu wa Kikristo kama huu hauharibiwi na tazamio la zawadi wakati wa siku za sherehe au desturi za kipagani.

Kwa sababu hiyo, zaidi ya Wakristo milioni nne na nusu kutoka kwa mataifa yote hawasherehekei Krismasi. Hawa ni Mashahidi wa Yehova, ambao kwa kawaida hujishughulisha kuwapa jirani zao ushahidi kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Waweza kukutana nao wanapokutembelea nyumbani kwako, labda hivi karibuni. Ukaribishaji wako wa shauku kwa yale wanayokuletea na kuongoze familia yako kwenye furaha kuu, unapojifunza jinsi ya kumsifu Yehova Mungu kila siku mwakani.—Zaburi 145:1, 2.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo huwapa jirani zao mojapo zawadi kuu zaidi—ufahamu wa kusudi la Mungu unaoweza kuongoza kwenye uhai wa milele

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Culver Pictures

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki