Kwa Nini Ni Wakati wa Kuamua?
KATIKA karne ya 16 K.W.K., Mungu alichagua Waisraeli wawe ‘tunu kwake kuliko makabila yote ya watu, taifa takatifu.’ (Kutoka 19:5, 6) Upesi walipoteza utakatifu wao, usafi wao wa kidini, wakijiruhusu kuchafuliwa kwa ibada ya sanamu na mazoea ya ufisadi ya mataifa jirani. Hivyo walijionyesha kuwa “taifa lenye shingo ngumu.” (Kumbukumbu la Torati 9:6, 13; 10:16; 1 Wakorintho 10:7-11) Katika kipindi cha zaidi ya miaka mia tatu baada ya kifo cha Yoshua, Yehova aliwainua waamuzi, viongozi waaminifu waliopaswa kuongoza Waisraeli kurudia ibada ya kweli. Hata hivyo, watu hao, “hawakuacha matendo yao, wala njia zao za ukaidi.”—Waamuzi 2:17-19.
Baada ya hayo, Mungu aliwainua wafalme na manabii waaminifu ili kuchochea watu warudie ibada ya kweli. Nabii Azaria alimtia moyo Mfalme Asa na wananchi wenzake kumtafuta Yehova: “Mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi.” Asa alifanya marekebisho ya kidini katika ufalme wa Yuda. (2 Mambo ya Nyakati 15:1-16) Baadaye, ilibidi Mungu afanye upya ukaribishaji huo kupitia nabii Yoeli. (Yoeli 2:12, 13) Na hata baadaye, Sefania aliwasihi wakaaji wa Yuda ‘wamtafute BWANA.’ mfalme Yosia aliyekuwa mchanga alifanya hivyo katika kampeni ya marekebisho ili kuondoa ibada ya sanamu na uovu.—Sefania 2:3; 2 Mambo ya Nyakati 34:3-7.
Yajapokuwa matukio kama hayo ya toba, hali ya kidini ya watu ilikuwa mbaya zaidi na zaidi. (Yeremia 2:13; 44:4, 5) Yeremia alishutumu mfumo wa kidini uliochafuliwa na mazoea ya ibada ya sanamu, akiyafafanua kuwa yasiyoweza kurekebika: “Je! Mkushi aweza kuibadili ngozi yake, au chui madoa-doa yake? Kama aweza, ndipo na ninyi mwaweza kutenda mema, ninyi mliozoea kutenda mabaya.” (Yeremia 13:23) Kwa sababu hii, Mungu alitoa hukumu kali kwa ufalme wa Yuda. Yerusalemu na hekalu lalo liliharibiwa katika 607 K.W.K., na waokokaji walihamishwa wakiwa watumwa Babiloni, ambako walikaa kwa miaka 70.
Kipindi hicho kilipopita, Mungu alionyesha rehema. Alimwelekeza Mfalme Sairasi kuwaacha huru Waisraeli, mabaki ambao walirudi Yerusalemu ili kujenga upya hekalu. Badala ya kujifunza somo kutokana na yote haya, walikengeuka kwa mara nyingine tena kutoka kwa ibada ya kweli, wakimfanya Yehova Mungu awakaribishe tena: “Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi.”—Malaki 3:7.
Sababu Iliyofanya Waisraeli Wakataliwe
Hali ya kidini ya Waisraeli katika wakati wa Yesu ilikuwaje? Viongozi wa kidini wanafiki walikuwa “viongozi vipofu” waliofundisha “mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” ‘Walikuwa wanaihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yao.’ Watu walimheshimu Mungu ‘kwa midomo yao,’ lakini mioyo yao ilikuwa imeondoshwa mbali naye. (Mathayo 15:3, 4, 8, 9, 14) Je, wao wakiwa taifa wangalipokea nafasi nyingine tena ya kutubu? La. Yesu alisema hivi: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa tai[f]a lingine lenye kuzaa matunda yake.” Naye akaongezea hivi: “Nyumba yenu,” yaani hekalu katika Yerusalemu, “mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 21:43; 23:38) Makosa yao yalikuwa makubwa mno. Walimkataa Yesu akiwa Mesiya na kumfanya auawe, wakichagua Kaisari Mroma mwenye kudhulumu kuwa mfalme wao.—Mathayo 27:25; Yohana 19:15.
Waisraeli hawakutaka kuelewa kwamba kipindi ambacho Yesu alikuwa akihubiri kilikuwa wakati wa hukumu. Kwa wakaaji wa Yerusalemu wasio waaminifu, Yesu alisema hivi: “Hukutambua majira ya kujiliwa kwako.”—Luka 19:44.
Katika Pentekoste 33 W.K., Mungu alifanyiza taifa jipya, au watu, wale wanafunzi watiwa-mafuta kwa roho wa Mwanaye, Yesu Kristo, ambao wangechaguliwa kutoka kila kabila na taifa. (Matendo 10:34, 35; 15:14) Je, kulikuwako tumaini lolote kwamba mfumo wa kidini wa Kiyahudi mwishowe ungerekebishwa? Majeshi ya Waroma yalitoa jibu katika mwaka wa 70 W.K., yakiharibu Yerusalemu kabisa. Mungu alikuwa amekataa kabisa mfumo huo wa kidini.—Luka 21:5, 6.
Uasi-Imani Mkubwa wa Jumuiya ya Wakristo
Wakristo watiwa-mafuta kwa roho pia walifanyiza “taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.” (1 Petro 2:9; Wagalatia 6:16) Lakini hata kutaniko la Kikristo la kale halikuhifadhi usafi walo wa kidini kwa muda mrefu.
Maandiko yalitabiri uasi-imani mkubwa, au kuacha imani ya kweli. Yale magugu ya ufananisho ya mfano wa Yesu, yaani, Wakristo bandia, wangejaribu kukaba ngano ya ufananisho, au Wakristo wa kweli, wale waliotiwa mafuta kwa roho ya Mungu. Mfano huo wafunua kwamba kuenea kwa Ukristo bandia, ulioendelezwa na adui mkuu wa Mungu, Ibilisi, ulikuwa karibu kuanza, “watu walipolala.” Haya yalitokea baada ya kifo cha mitume waaminifu wa Kristo, wakati wa kipindi cha usingizi wa kiroho uliofuata. (Mathayo 13:24-30, 36-43; 2 Wathesalonike 2:6-8) Kama mitume walivyotabiri, Wakristo wengi bandia walijipenyeza ndani ya kundi. (Matendo 20:29, 30; 1 Timotheo 4:1-3; 2 Timotheo 2:16-18; 2 Petro 2:1-3) Yohana alikuwa wa mwisho wa mitume kufa. Karibu na mwaka wa 98 W.K., yeye aliandika kwamba “wakati wa mwisho,” sehemu ya mwisho ya kipindi cha mitume, kilikuwa tayari kimeanza.—1 Yohana 2:18, 19.
Huku muungano wa kidini na mamlaka ya kisiasa ukiidhinishwa na maliki Mroma Konstantino, hali ya kiroho, mafundisho ya kidini, na ya maadili ya Jumuiya ya Wakristo iliharibika sana. Wanahistoria wengi hukubali kwamba “kule kushinda kwa Kanisa wakati wa karne ya nne” kulikuwa, “msiba” tukiona mambo kwa njia ya Kikristo. ‘Jumuiya ya Wakristo ilipoteza kanuni zayo za maadili za hali ya juu’ na kukubali mazoea mengi na falsafa kutoka kwa upagani, kama vile “ibada ya Mariamu” na ile ibada ya “watakatifu,” na vilevile wazo la Utatu.
Baada ya ushindi wayo bandia, hali ya Jumuiya ya Wakristo ikaharibika. Amri nyingi na mafafanuo ya mafundisho yaliyofanywa na mapapa na mabaraza, na pia Baraza la Kuhukumu Wazushi, Krusedi, na vita “vitakatifu” kati ya Wakatoliki na Waprotestanti, yalitokeza mfumo wa kidini usioweza kurekebika.
Katika kitabu chake A World Lit Only by Fire, William Manchester aandika hivi: “Mapapa katika karne za kumi na tano na kumi na sita waliishi kama maliki wa Waroma. Walikuwa ndio matajiri zaidi ulimwenguni, nao na makardinali wao walijitajirisha zaidi kwa kuuza vyeo vitakatifu.” Wakati huo wa uasi-imani mkubwa, vikundi vidogo au watu mmoja-mmoja walijaribu kutafuta tena Ukristo wa kweli, wakionyesha sifa za ngano ya ufananisho. Mara nyingi walinyanyaswa sana. Kitabu hichohicho chasema hivi: “Nyakati nyingine ilionekana kwamba watakatifu wa kweli wa Ukristo, Waprotestanti na Wakatoliki vilevile, walikuwa wamefia imani.” Wengine, waitwao eti Warekebishaji kama vile Martin Luther na John Calvin, waliweza kuunda mifumo ya kidini yenye kudumu iliyokuwa imejitenga na Kanisa Katoliki lakini iliyoshiriki mafundisho yalo ya msingi. Walikuwa pia wamejiingiza sana katika mambo ya kisiasa.
Katika eneo la Waprotestanti, jitihada zilifanywa ili kufanya kile kiitwacho eti kuamka tena kwa kidini kiwezekane. Kwa mfano, wakati wa karne za 18 na 19, jitihada hizi zilileta tokeo la wamishonari wenye bidii wa kigeni. Hata hivyo, kwa maneno ya wachungaji wenyewe, leo hali ya kiroho ya kundi la Waprotestanti haitii moyo hata kidogo. Mwanatheolojia Mprotestanti Oscar Cullmann hivi karibuni alikubali kwamba “ndani ya makanisa yenyewe, mna tatizo la imani.”
Marekebisho ya kwanza na yale ya baadaye pia yametokea katika Kanisa Katoliki. Kutoka karne za 11 hadi 13 W.K., wakati wa kuongezeka kwa upotovu na utajiri mwingi wa makasisi, kikundi cha watawa kilichofuata sana kiapo cha umaskini kilifanyizwa. Lakini walichunguzwa sana, na kulingana na wasomi, wao walikandamizwa na jamii ya makasisi. Halafu karne ya 16 kukaja Marekebisho Mengine yaliyoendelezwa na Baraza la Trent ambayo yalielekezwa kuyakabili Marekebisho ya Kidini ya Waprotestanti.
Katika nusu ya kwanza ya karne ya 19, wakati wa kipindi cha kurudishwa kwa jamii ya makasisi, Kanisa Katoliki lilichukua msimamo wa kutawala kiimla na kukubali mabadiliko. Hata hivyo, haiwezi kusemwa kwamba marekebisho halisi yoyote yalifanywa ili kurudisha Ukristo wa kweli. Badala ya hivyo, hizi zilikuwa jitihada tu za kuimarisha mamlaka ya makasisi dhidi ya mabadiliko ya ulimwengu ya kidini, kisiasa, na kijamii.
Hivi karibuni, katika miaka ya 1960, ilionekana kwamba Kanisa Katoliki lilitaka kuanzisha badiliko kubwa sana katika baraza la makanisa la Vatican 2. Hata hivyo, kusimamishwa kwa ghafula kwa kile kilichoitwa baraza la kufanya upya kuliamrishwa na papa ili kuondoa mwelekeo wa washiriki wa kanisa wenye kutaka mabadiliko. Jambo hili, ambalo wengine huliita urudisho wa Wojtyła, limefafanuliwa na kikundi kimoja cha Kikatoliki kuwa “aina mpya ya Ukonstantino.” Kama ilivyoelezwa katika gazeti la Kiyesuiti La Civiltà Cattolica, Kanisa Katoliki, kama vile dini nyinginezo, linakabili “tatizo kubwa sana la ulimwenguni pote: kwa sababu lahusu mizizi yenyewe ya imani na maisha ya Kikristo; la ulimwenguni pote kwa sababu unahusu hali zote za Ukristo.”
Kwa kweli dini za Jumuiya ya Wakristo hazijarekebika hasa, wala hazingeweza, kwa sababu Ukristo wa kweli ungerudishwa tu wakati wa “mavuno,” kwa kukusanywa kwa ngano ya ufananisho katika kutaniko moja safi. (Mathayo 13:30, 39) Orodha ndefu ya jeuri na mambo mabaya yaliyofanyika kwa jina la dini, yawe yanadaiwa kuwa ya Kikristo au sivyo, yanatokeza swali hili, Je, ni halisi kutazamia marekebisho ya kweli kutoka kwa Jumuiya ya Wakristo?
Marekebisho Hayawezekani?
Kitabu cha Ufunuo, au Apokalipsi, husema juu ya kahaba mkuu wa ufananisho mwenye jina la kifumbo “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:1, 5, New World Translation) Kwa karne nyingi wasomaji wa Biblia wametafuta kufafanua lile fumbo la ufananisho huu. Wengi walichukizwa na utajiri na upotovu wa makasisi. Wengine walifikiri kwamba Babiloni Mkubwa aliwakilisha utawala wa jamii ya makasisi. Miongoni mwao walikuwa Jan Hus, Mbohemia kasisi Mkatoliki aliyechomwa akiwa hai katika 1415, na Aonio Paleario, mtetea mambo ya binadamu Mwitalia aliyenyongwa na kuchomwa katika 1570. Wote wawili walijaribu bila kufanikiwa kurekebisha Kanisa Katoliki wakiwa na tumaini la kwamba litarudia “heshima yalo ya kale.”
Kinyume cha hayo, sura za 17 na 18 za Ufunuo zaonyesha kwamba Babiloni Mkubwa anawakilisha milki ya ulimwengu ya dini zote bandia.a “Kahaba mkuu” huyu wa ufananishi ahusishaye mengi hawezi kurekebika kwa sababu “dhambi zake zimefika hata mbinguni.” Kwa kweli, katika karne hii ya 20, karibu dini zote, si zile tu za Jumuiya ya Wakristo, zalaumiwa kwa ajili ya vita vinavyoendelea kumwaga damu nyingi na kwa ajili ya maadili yaliyoshuka sana yanayopata wanadamu. Kwa hiyo, Mungu amemhukumu “Babiloni” uharibifu.—Ufunuo 18:5, 8.
Sasa Ndio Wakati wa ‘Kutoka Kwake’
Utimizo wa unabii mwingi wa Biblia hufunua kwamba wakati wetu unalingana na “umalizio” wa huu “mfumo wa mambo” ulio mwovu. (Mathayo 24:3, NW) Yeyote anayetaka kumwabudu Mungu kwa moyo mweupe hapaswi kufuata maoni na mapendezi yake mwenyewe. Ni lazima ‘amtafute BWANA maadamu anapatikana,’ ndiyo, hivi sasa, kwa sababu ‘dhiki kubwa’ iliyotabiriwa na Yesu i karibu. (Isaya 55:6; Mathayo 24:21, NW) Kama ilivyokuwa katika kisa cha Waisraeli, Mungu hataruhusu ufisadi wa dini eti kwa sababu inajidai juu ya ukale wayo. Badala ya kujaribu kurekebisha merikebu inayoelekea kuzama, wale wote wanaotamani kibali cha Mungu na wokovu lazima watii bila kukawia amri iliyopuliziwa na Mungu ya Ufunuo 18:4: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa], enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”
Lakini ‘watoke’ waende wapi? Ni wapi kwingineko wokovu wapatikana? Je, hakuna hatari ya kutafuta kimbilio mahali pasipofaa? Dini pekee iliyo na kibali cha Mungu yaweza kutambuliwaje? Majibu ya pekee ya kutumainiwa yaweza kupatikana katika Neno la Mungu. (2 Timotheo 3:16, 17) Mashahidi wa Yehova wanakualika uchunguze Biblia kwa undani zaidi. Utaweza kuelewa ni akina nani Mungu amechagua “[watu] kwa ajili ya jina lake,” atakaowalinda wakati wa siku ya hasira yake inayokaribia.—Matendo 15:14, Sefania 2:3; Ufunuo 16:14-16.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kutambua Babiloni Mkubwa wa ufananisho Kimaandiko kwa njia sahihi, ona sura za 33 hadi 37 za kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichotangazwa katika mwaka wa 1988 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ikiwa merikebu yako ya kidini inazama, nenda kwenye merikebu ya kuokokea ya Ukristo wa kweli