Jinsi Jumuiya ya Wakristo Ilivyokuja Kuwa Sehemu ya Ulimwengu Huu
BAADAYE Milki ya Roma, ambamo Ukristo wa mapema ulianza, ikaanguka. Wanahistoria wengi hudai kwamba anguko hilo lilitukia wakati uleule ambapo Ukristo ulikuwa umeushinda upagani kabisa. Akitoa maoni tofauti, askofu Mwanglikana E. W. Barnes aliandika hivi: “Ustaarabu wa [Kiroma] ulipoanguka, Ukristo uliacha kuwa ile imani bora ya Yesu Kristo: ulikuja kuwa dini iliyofaa kutumiwa kama imara ya kijamii ya ulimwengu uliokuwa ukiharibika.”—The Rise of Christianity.
Kabla ya anguko hilo, katika karne ya pili, ya tatu, na ya nne W.K., historia yarekodi kwamba kwa ujumla wale waliodai kumfuata Yesu walijitenga na ulimwengu wa Kiroma. Lakini inafunua pia mwanzo wa uasi-imani katika fundisho, mwenendo, na tengenezo, kama vile Yesu na mitume wake walivyokuwa wametabiri. (Mathayo 13:36-43; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3-12; 2 Timotheo 2:16-18; 2 Petro 2:1-3, 10-22) Hatimaye kuridhiana na ulimwengu wa Kigiriki na Kiroma kulianza, na wengine waliodai kuwa Wakristo wakaanza kufuata upagani wa ulimwengu (kama vile sikukuu zao na ibada yao ya mama mungu-mke na ya mungu wa utatu) falsafa yao (kama vile kuamini katika nafsi isiyoweza kufa), na kupangwa kwao kitengenezo (kunakoonwa katika kule kutokea kwa jamii ya makasisi). Hiyo ilikuwa namna ya Ukristo iliyofisidiwa ambayo iliwavutia misongamano ya wapagani ikawa kani ambayo wamaliki wa Roma walijaribu kukomesha mwanzoni lakini baadaye wakaikubali na wakajitahidi kuitumia ili kutimiza makusudi yao wenyewe.
Yashindwa na Ulimwengu
Mwanahistoria wa kanisa Augustus Neander alionyesha hatari zilizohusika katika uhusiano huo mpya kati ya “Ukristo” na ulimwengu. Ikiwa Wakristo wangedhabihu kujitenga kwao na ulimwengu, “tokeo lingekua mchafuko wa kanisa na ulimwengu . . . ambamo kanisa lingepoteza usafi walo, na, huku likionekana kana kwamba limeshinda, lenyewe lingekuwa limeshindwa,” akaandika.—General History of the Christian Religion and Church, Buku 2, ukurasa 161.
Hilo ndilo jambo lililotukia. Mapema katika karne ya nne, maliki Mroma Konstantino alijaribu kuitumia dini ya “Ukristo” ya siku yake ili kuimarisha milki yake iliyokuwa ikivunjika. Kutimiza hilo, aliwapa wale waliodai kuwa Wakristo uhuru wa kidini akawapa wale wa jamii yao ya makasisi baadhi ya mapendeleo ya ukuhani wa kipagani. The New Encyclopædia Britannica yasema hivi: “Konstantino alitoa kanisa kutoka katika kujitenga kwalo na ulimwengu ili likubali daraka la kijamii na akalisaidia kanisa lishinde jamii ya kipagani.”
Dini ya Serikali
Baada ya Konstantino, Maliki Juliano (361-363 W.K.) alijaribu kuupinga Ukristo na kurudisha upagani. Lakini akashindwa, na baada ya miaka 20 hivi, Maliki Theodosius 1 alipiga marufuku upagani akauweka “Ukristo” wa Utatu kuwa dini ya Serikali ya Milki ya Roma. Mwanahistoria Mfaransa Henri Marrou aliandika hivi kwa usahihi kamili: “Kufikia mwisho wa utawala wa Theodosius, Ukristo, au kwa usahihi zaidi, Ukatoliki halali, ulikuja kuwa dini rasmi ya ulimwengu wote wa Kiroma.” Ukatoliki halali ulikuwa umechukua mahali pa Ukristo wa kweli na ukaja kuwa “sehemu ya ulimwengu.” Dini hiyo ya Serikali ilikuwa tofauti mno na ile dini ya wafuasi wa Yesu wa mapema, ambao aliwaambia hivi: “Ninyi si wa [si sehemu ya, NW] ulimwengu.”—Yohana 15:19.
Mwanahistoria na mwanafalsafa Mfaransa Louis Rougier aliandika hivi: “Ukristo ulipoenea, ulibadilika kwa njia za ajabu ukafikia hatua ya kutoweza kutambulika. . . . Kanisa la zamani lenye maskini, lililoishi kwa kupewa michango ya msaada, lilikuja kuwa kanisa lenye nguvu nyingi lililokubaliana na mamlaka za kimwili zilizopo liliposhindwa kuzitawala.”
Mapema katika karne ya tano W.K., “Mtakatifu” wa dini ya Roma Katoliki Augustino aliandika kitabu chake mashuhuri The City of God (Jiji la Mungu). Ndani yacho alitoa usimulizi wa majiji mawili, “lile la Mungu na lile la ulimwengu.” Je! kitabu hicho kilikazia mtengano kati ya Wakatoliki na ulimwengu? Sivyo hasa. Profesa Latourette asema hivi: “Augustino alitambua waziwazi [kwamba] yale majiji mawili, la kidunia na la kimbingu, yanashirikiana.” Augustino alifundisha kwamba “Ufalme wa Mungu umeanza tayari katika ulimwengu huu tangu mwanzo wa kanisa [Katoliki].” (The New Encyclopædia Britannica, Macropædia, Buku 4, ukurasa 506) Hivyo, iwe kusudi la Augustino la kwanza lilikuwa nini, nadharia zake zilihusisha Kanisa Katoliki zaidi na mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu.
Milki Iliyogawanyika
Katika 395 W.K., Theodosius 1 alipokufa, Milki ya Roma iligawanywa kirasmi katika sehemu mbili. Jiji kuu la ile Milki ya Mashariki, au ya Bizantino lilikuwa Konstantinopo (zamani Bizantio, sasa Istanbul), na jiji kuu la Milki ya Magharibi lilikuwa katika Ravenna, Italia, (baada ya 402 W.K.). Tokeo ni kwamba, Jumuiya ya Wakristo ikaja kugawanyika kisiasa na kidini pia. Kwa habari ya uhusiano kati ya Kanisa na Serikali, kanisa katika Milki ya Mashariki ilifuata nadharia ya Eusebio wa Kaisaria (aliyeishi wakati wa Konstantino Mkuu). Akipuuza ile kanuni ya Kikristo ya kujitenga na ulimwengu, Eusebio alisababu kwamba ikiwa maliki na milki ingekuwa ya Kikristo, Kanisa na Serikali ingekuwa jamii moja ya Kikristo, maliki akitenda akiwa mwakilishi wa Mungu duniani. Kwa ujumla, uhusiano huo kati ya Kanisa na Serikali umefuatwa na Makanisa ya Orthodox ya Mashariki kwa muda wote wa karne ambazo zimepita. Katika kitabu chake The Orthodox Church, Timothy Ware, ambaye ni askofu wa dini ya Orthodox, alionyesha tokeo la hilo: “Utaifa ndio umeyaua Mafundisho Halali kwa muda wa karne kumi ambazo zimepita.”
Katika Magharibi maliki wa mwisho wa Roma alipinduliwa katika 476 W.K. kwa kushambuliwa na makabila ya Kijerumani. Hilo lilitia alama mwisho wa Milki ya Roma ya Magharibi. The New Encyclopædia Britannica yasema hivi kuhusu hali iliyofuata ya kutokuwa na milki: “Mamlaka mpya ilifanyizwa: Kanisa la Roma, kanisa la askofu wa Roma. Kanisa hilo lilijiona kuwa mwandamizi wa Milki ya Roma iliyotoweka.” Ensaiklopedia hiyo inaendelea kusema hivi: “Mapapa wa Roma . . . walinyoosha dai hilo la serikali ya kanisa kupita mipaka ya kanisa na serikali wakaanzisha ile iliyoitwa eti nadharia ya panga mbili, wakisema kwamba Kristo hakumpa papa mamlaka ya kiroho tu juu ya kanisa bali pia mamlaka ya kimwili juu ya falme za kilimwengu.”
Makanisa ya Protestanti ya Kitaifa
Muda wote wa Enzi za Kati, dini ya Orthodox na ya Roma Katoliki pia iliendelea kujihusisha sana na siasa, shughuli za kilimwengu, na vita. Je! yale Mapinduzi Makubwa ya Protestanti ya karne ya 16 yalitia alama kurudi kwa Ukristo wa kweli, uliojitenga na ulimwengu?
La. Twasoma hivi katika The New Encyclopædia Britannica: “Wanamapinduzi Waprotestanti wenye kufuata mapokeo ya Luther, Kalvin, na ya Kianglikana . . . walibaki wakiwa wameshika sana maoni ya Augustino, ambaye walipendelea sana nadharia zake. . . . Kila moja ya mapokeo hayo makuu matatu ya Kiprotestanti ya Ulaya ya karne ya 16 . . . yalipata utegemezo kutoka kwa mamlaka za kimwili katika Saxony [Ujerumani ya kati], Uswisi, na Uingereza yakabaki katika hali ile ile ya kuwa pamoja na serikali kama vile kanisa la enzi za kati lilivyokuwa.”
Badala ya kurudisha Ukristo wa Kweli, Mapinduzi Makubwa ya Kidini yalitokeza makanisa mengi ya kitaifa au ya kieneo ambayo yamejipendekeza kwa serikali za kisiasa na kuziunga mkono kwa bidii katika vita vyazo. Kwa kweli, makanisa ya Katoliki na ya Protestanti pia yameanzisha vita vya kidini. Katika kitabu chake An Historian’s Approach to Religion, Arnold Toynbee aliandika hivi kuhusu vita hivyo: “Viliwaonyesha Wakatoliki na Waprotestanti katika Ufaransa, Uholanzi, Ujerumani, na Ailandi, na madhehebu ya ushindani ya Waprotestanti katika Uingereza na Uskochi, wakiwa katika tendo katili la kujaribu kukandamizana kwa nguvu za silaha.” Mapigano ya siku hizi yanayogawanya Ailandi na Yugoslavia ya zamani yanaonyesha kwamba makanisa ya Roma Katoliki, Orthodox, na Protestanti yangali yanajihusisha sana katika mambo ya ulimwengu huu.
Je! hayo yote yamaanisha kwamba Ukristo wa kweli, uliojitenga na ulimwengu, hauko tena duniani? Makala ifuatayo itajibu swali hilo.
[Sanduku/Picha katika kurasa za 10 and 11]
JINSI “UKRISTO” ULIVYOKUJA KUWA DINI YA SERIKALI
UKRISTO haukukusudiwa kamwe uwe sehemu ya ulimwengu huu. (Mathayo 24:3, 9; Yohana 17:16) Lakini, vitabu vya historia vyatuambia kwamba katika karne ya nne W.K., “Ukristo” ulikuja kuwa dini rasmi ya Serikali ya Milki ya Roma. Hilo lilitukiaje?
Tangu wakati wa Nero (54-68 W.K.) hadi miaka ya baadaye sana ya karne ya tatu W.K., maliki wote Waroma ama waliwanyanyasa Wakristo kwa bidii ama waliruhusu wanyanyaswe. Gallienus (253-268 W.K.) alikuwa maliki Mroma wa kwanza kuwatolea julisho la uvumilivu. Hata hivyo, Ukristo ulikuwa dini iliyokatazwa kotekote katika milki hiyo. Baada ya Gallienus, mnyanyaso uliendelea, na chini ya Diocletian (284-305 W.K.) na wale waandamizi wake wa karibu-karibu, mnyanyaso huo uliongezeka hata zaidi.
Badiliko lilikuja mapema katika karne ya nne wakati wa kule kulikoitwa eti kugeuka kwa Maliki Konstantino 1 kwenye Ukristo. Kuhusu “kugeuka” huko, kitabu kimoja cha Kifaransa Théo—Nouvelle encyclopédie catholique (Théo—Ensaiklopedia Mpya ya Katoliki) chasema hivi: “Konstantino alidai kuwa maliki Mkristo. Kwa kweli, alibatizwa tu akiwa karibu kufa kitandani.” Hata hivyo, katika 313 W.K., Konstantino na maliki mwenzake, Licinius, walitoa amri iliyowapa Wakristo na wapagani pia uhuru wa kidini. New Catholic Encyclopedia yasema hivi: “[Tendo] la Konstantino la kuwanyooshea Wakristo uhuru wa ibada, lililomaanisha kwamba Ukristo ulitambuliwa kirasmi kuwa religio licita [dini halali] zaidi ya upagani, lilikuwa tendo lenye kuleta mabadiliko makubwa.”
Hata hivyo, The New Encyclopædia Britannica yajulisha hivi: “Yeye [Konstantino] hakufanya Ukristo uwe dini ya milki yote.” Mwanahistoria Mfaransa Jean-Rémy Palanque, mshiriki wa Taasisi ya Ufaransa, aandika hivi: “Hata hivyo, Serikali ya Roma . . . ilibaki, ya kipagani kirasmi. Na Konstantino, alipokuwa akishikamana na dini ya Kristo, hakukomesha hali hiyo.” Katika kile kitabu The Legacy of Rome, Profesa Ernest Barker alisema hivi: “[Ushindi wa Konstantino] haukusababisha Ukristo usimamishwe mara iyo hiyo ikiwa dini ya Serikali. Konstantino aliridhika kutambua Ukristo ukiwa mojawapo ibada za peupe za milki hiyo. Kwa muda wa miaka sabini iliyofuata desturi za zamani za kipagani zilifanywa kirasmi katika Roma.”
Kwa hiyo kufikia hapo “Ukristo” ulikuwa dini halali katika Milki ya Roma. Ilikujaje kuwa dini rasmi ya Serikali, katika maana kamili ya usemi huo? Twasoma hivi katika New Catholic Encyclopedia: “Sera ya [Konstantino] iliendelezwa na waandamizi wake isipokuwa Juliano [361-363 W.K.], ambaye mnyanyaso wake wa Ukristo ulikomeshwa ghafula kwa kifo chake. Mwishoni, katika robo ya mwisho ya karne ya 4, Theodosius Mkuu [379-395 W.K.] alifanya Ukristo uwe dini rasmi ya Milki akakandamiza ibada ya peupe ya kipagani.”
Akithibitisha hilo na kufunua dini hiyo mpya ya Serikali ilikuwa ni nini hasa, msomi na mwanahistoria wa Biblia F. J. Foakes Jackson aliandika hivi: “Chini ya Konstantino Ukristo na milki ya Roma zilikuwa marafiki. Chini ya Theodosius zilikuwa na umoja. . . . Tangu wakati huo na kuendelea jina Katoliki liliwekewa wale waliomheshimu sana Baba, Mwana, na Mzuka Mtakatifu kwa kicho icho hicho. Sera yote ya kidini ya maliki huyo ilikusudiwa kutimiza hilo, tokeo likawa kwamba, Imani ya Katoliki ikawa dini moja halali ya Waroma.”
Jean-Rémy Palanque aliandika hivi: “Theodosius, alipokuwa akipigana na upagani, tokeo pia lilikuwa kwamba alipendelea Kanisa la orthodox [la Katoliki]; amri yake ya 380 W.K. liliwaamuru raia wake wote wafuate imani ya Papa Damasus na ya askofu [Mwamini wa Utatu] wa Aleksandria nayo iliwanyima uhuru wa ibada wale waliokataa. Ile Baraza kubwa la Konstantinopo (381) liliwalaumu tena wazushi wote, na maliki akahakikisha kwamba hakuna askofu yeyote ambaye angewaunga mkono. Ukristo wa Nisea [wa Utatu] ulikuwa umekuwa dini ya Serikali kikamili na kikweli. . . . Kanisa lilijiunga na Serikali kwa ukaribu sana nalo likapata utegemezo wayo wa pekee.”
Hivyo, dini iliyokuja kuwa dini ya Serikali ya Milki ya Roma, haikuwa ule Ukristo usioghoshiwa wa siku za mitume. Ulikuwa Ukatoliki wa Utatu wa karne ya nne, uliowekwa kwa nguvu na Maliki Theodosius 1 na kuzoewa na Kanisa Roma Katoliki, ambalo lilikuwa kama lilivyo sasa, sehemu kwelikweli ya ulimwengu huu.
[Hisani]
Maliki Theodosius 1: Real Academia de la Historia, Madrid (Foto Oronoz)
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Scala/Art Resource, N.Y.