Konstantino Mkubwa Je, Alikuwa Mtetezi wa Ukristo?
Maliki Mroma Konstantino yu miongoni mwa wanaume wachache ambaye historia imelirembesha jina lake kwa neno “Mkubwa.” Jumuiya ya Wakristo imeongeza semi “mtakatifu,” “mtume wa kumi na tatu,” “mtakatifu aliye sawa na mitume,” na ‘aliyechaguliwa kwa Mwongozo wa Mungu ili kutimiza mgeuzo ulio mkubwa zaidi katika ulimwengu wote.’ Kinyume cha hayo maoni, wengine humfafanua Konstantino kuwa mtu “mwenye kuhusika na uchinjaji, mwenye kushutumiwa kwa uhalifu mwingi usiohesabika na mwenye kujaa udanganyi, . . . mwonezi mwenye kuchukiza, mwenye hatia ya uhalifu wenye kutisha.”
WENGI wanaodai kuwa Wakristo wamefundishwa kwamba Konstantino Mkubwa alikuwa mmojawapo wa wafadhili wakubwa zaidi wa Ukristo. Wao humsifu kuwa aliwakomboa Wakristo kutoka katika taabu ya kunyanyaswa na Waroma na kuwapa uhuru wa kidini. Isitoshe, yaaminiwa sana kwamba alikuwa mfuasi mwaminifu wa hatua za Yesu Kristo akiwa na tamaa yenye nguvu ya kuendeleza harakati za Kikristo. Kanisa Othodoksi la Mashariki na Kanisa Koptiki yamemtangaza Konstantino na mama yake, Helena, kuwa “watakatifu.” Msherehekeo wao huadhimishwa Juni 3 au kulingana na kalenda ya kanisa, Mei 21.
Konstantino Mkubwa kwa kweli alikuwa nani? Alikuwa na fungu gani katika kusitawisha Ukristo wa baada ya mitume? Inaelimisha sana kuacha historia na wasomi wajibu maswali hayo.
Konstantino wa Kihistoria
Konstantino, mwana wa Konstantio Klorasi, alizaliwa katika Naissus huko Serbia wapata mwaka wa 275 W.K. Baba yake alipopata kuwa maliki wa majimbo ya magharibi ya Roma mwaka wa 293 W.K., alikuwa akipigana kwenye Danube chini ya maagizo kutoka kwa Maliki Galeriasi. Mwaka wa 306 W.K., Konstantino alirudi upande wa baba yake aliyekuwa akielekea kufa huko Uingereza. Mara baada ya kifo cha baba yake, Konstantino aliinuliwa na jeshi kwenye cheo cha maliki.
Wakati huo, watu wengine watano walidai kwamba walikuwa Maliki. Kipindi cha kati ya mwaka wa 306 na 324 W.K., ambacho baada yacho Konstantino alipata kuwa maliki wa pekee, kilikuwa kipindi cha vita ya daima ya wenyewe kwa wenyewe. Ushindi katika kampeni mbili za kijeshi ulimhakikishia Konstantino sehemu katika historia ya Roma na kumfanya kuwa mtawala wa pekee wa Milki ya Roma.
Mwaka wa 312 W.K., Konstantino alimshinda mpinzani wake Maksentio, katika pigano la Daraja Milvia nje ya Roma. Watetezi wa Kikristo walidai kwamba wakati wa kampeni hiyo, kulionekana msalaba wenye kuwaka mwali chini ya jua ukiwa na maneno ya Kilatini In hoc signo vinces, yanayomaanisha “Katika ishara hii shinda.” Pia yaaminiwa kwamba katika ndoto, Konstantino aliambiwa achore zile herufi mbili za kwanza za jina la Kristo katika Kigiriki kwenye ngao za askari wake. Hata hivyo, kisa hicho kina mambo mengi yasiyopatana na kronolojia. Kitabu A History of Christianity chataarifu hivi: “Kuna kuhitilafiana kwa uthibitisho kuhusu wakati barabara, mahali na maelezo ya kinaganaga ya ono hilo.” Likimkaribisha Konstantino huko Roma, Baraza Kuu la kipagani lilimtangaza kuwa Augusto mkuu na Askofu Mkuu (Pontifex Maximus), yaani, kuhani wa cheo cha juu wa dini ya kipagani ya hiyo milki.
Mwaka wa 313 W.K., Konstantino alipanga kushirikiana na Maliki Lisinio, mtawala wa majimbo ya mashariki. Kupitia ile Amri ya Milan, kwa pamoja walitoa uhuru wa kuabudu na haki sawa kwa vikundi vyote vya kidini. Hata hivyo, wanahistoria wengi hupunguza umaana wa hati hiyo, wakisema kwamba ilikuwa barua ya kawaida tu wala si hati kuu ya kimaliki yenye kuonyesha badiliko la sera kuelekea Ukristo.
Katika miaka kumi iliyofuata, Konstantino alimshinda Lisinio, mshindani wake wa mwisho aliyebaki, na kuwa mtawala asiyepingwa wa ulimwengu wa Roma. Mwaka wa 325 W.K., akiwa bado hajabatizwa, alisimamia baraza kubwa la kwanza la muungano wa kanisa la “Kikristo” ambalo lililaumu ufuatiaji wa mafundisho ya Ariasi na kutayarisha taarifa ya itikadi muhimu ziitwazo Imani za Nisea.
Konstantino aliugua ugonjwa wa kufisha mwaka wa 337 W.K. Katika saa hiyo ya mwisho-mwisho ya uhai wake, alibatizwa, kisha akafa. Baada ya kifo chake lile Baraza Kuu lilimteua kuwa miongoni mwa miungu ya Roma.
Dini Katika Mkakati wa Konstantino
Kuhusu mtazamo wa ujumla ambao maliki wa Roma wa karne ya tatu na ya nne walikuwa nao kuelekea dini, kitabu Istoria tou Ellinikou Ethnous (Historia ya Taifa la Kigiriki) chasema hivi: “Hata wakati ambapo wale waliokalia kiti cha ufalme cha hiyo milki hawakuwa na mielekeo ya kidini yenye kina sana, wakikubaliana na kufikiri kwa nyakati hizo, waliliona kuwa jambo la lazima kuitanguliza dini katika muundo wao wa mipango ya kisiasa, ili angalau kuyapa matendo yao sifa ya kidini.”
Bila shaka, Konstantino alikuwa mtu aliyepatanisha maisha yake na nyakati ambamo aliishi. Mwanzoni mwa kazi-maisha yake, alihitaji tegemezo fulani la “kimungu,” na hilo halingeweza kuandaliwa na miungu ya Roma iliyokuwa ikififia. Hiyo milki kutia na dini yake na mashirika mengine, ilikuwa ikishuka, na jambo fulani jipya na lenye kutia nguvu lilihitajiwa ili kuiimarisha tena. Ensaiklopedia Hidria yasema hivi: “Konstantino hasa alipendezwa na Ukristo kwa sababu haukutegemeza tu ushindi wake bali pia kule kutengeneza upya milki yake. Makanisa ya Kikristo yaliyokuwako kila mahali yakawa tegemezo lake la kisiasa. . . . Alijiweka karibu na maaskofu wakubwa wa hizo nyakati . . . , akaomba kwamba watunze muungano wao ukiwa kamili.”
Konstantino alihisi kwamba dini ya “Kikristo”—hata ingawa ilikuwa yenye kuasi na kufisidiwa sana kufikia wakati huo—ingeweza kutumiwa kwa matokeo ikiwa kani yenye kutia nguvu mpya na yenye kuunganisha ili kuusaidia mpango wake mkubwa wa utawala wa kimaliki. Akikubali kirasmi misingi ya Ukristo wenye kuasi imani ili kupata tegemezo katika kuendeleza malengo yake mwenyewe ya kisiasa, aliamua kuunganisha watu chini ya “katoliki,” au dini ya watu wote. Desturi na sherehe za kipagani zilipewa majina ya “Kikristo.” Na makasisi wa “Kikristo” wakapewa hadhi, mshahara, na uwezo wenye kuvutia sawa na makasisi wa kipagani.
Akitafuta upatano wa kidini kwa sababu za kisiasa, upesi Konstantino alinyamazisha kabisa hoja zenye kupinga, sio kwa msingi wa kweli ya mafundisho, bali kwa msingi wa kibali cha walio wengi. Tofauti kubwa sana za kimafundisho ndani ya kanisa la “Kikristo” lililokuwa limegawanyika vibaya, zilimpa fursa ya kuingilia kati akiwa mpatanishi “mwenye kutumwa na Mungu.” Kupitia shughuli zake na Wadonati katika Afrika Kaskazini na wafuasi wa Ariasi katika sehemu ya mashariki ya hiyo milki, aligundua upesi kwamba kushawishi hakukutosha kufanyiza imani thabiti, yenye kuungamanishwa.a Ilikuwa ni kwa kujaribu kutatua ule ubishi wa Kiaria kwamba alifanya mkutano wa baraza la kwanza la muungano wa kidini katika historia ya kanisa.—Ona sanduku “Konstantino na Baraza la Nisea.”
Kumhusu Konstantino, mwanahistoria Paul Johnson ataarifu hivi: “Huenda mojawapo ya sababu zake kuu za kuuvumilia Ukristo ikawa kwamba ulimpa yeye mwenyewe na Serikali fursa ya kudhibiti kabisa sera ya Kanisa juu ya mafundisho.”
Je, Alipata Kuwa Mkristo?
Johnson asema hivi: “Konstantino hakuacha kamwe kuabudu jua na alihifadhi jua kwenye sarafu zake.” Kichapo Catholic Encyclopedia chasema hivi: “Konstantino alionyesha dini zote mbili upendeleo sawa. Akiwa askofu mkuu aliitunza ibada ya kipagani na kuhami haki zake.” Konstantino hakupata kamwe kuwa Mkristo,” yataarifu ensaiklopedia Hidria, ikiongeza hivi: “Eusebius wa Kaisaria, aliyeandika wasifu wa Konstantino, asema kwamba Konstantino alipata kuwa Mkristo katika dakika za mwisho za uhai wake. Jambo hilo halisadikishi, kwa kuwa siku iliyotangulia, [Konstantino] alikuwa amemtolea Zeo dhabihu kwa sababu alikuwa pia na jina la cheo Askofu Mkuu.”
Hadi siku ya kufa kwake mwaka wa 337 W.K., Konstantino alikuwa na jina la cheo la Askofu Mkuu, kiongozi mkuu wa mambo ya kidini. Kwa habari ya ubatizo wake, yafaa kuuliza, Je, ulitanguliwa na toba ya kweli na kugeuka kabisa, kama itakwavyo katika Maandiko? (Matendo 2:38, 40, 41) Je, ulikuwa uzamisho kamili wa maji ukiwa wonyesho wa wakfu wa Konstantino kwa Yehova Mungu?—Linganisha Matendo 8:36-39.
Je, Alikuwa “Mtakatifu”?
Kichapo Encyclopædia Britannica chataarifu hivi: “Konstantino alikuwa na haki ya kuitwa Mkubwa si kwa sababu ya vile alivyokuwa bali kwa sababu ya yale aliyofanya. Kwa kweli, ikiwa angetahiniwa kwa sifa, angekuwa mmojawapo wa wale wenye sifa ndogo sana za ustahili kati ya wale ambao neno [Mkubwa] limetumiwa kwao nyakati za kale na za kisasa.” Nacho kitabu A History of Christianity chataarifu hivi: “Kulikuwa na ripoti za mapema juu ya hamaki yake yenye jeuri na ukatili wake alipokuwa na hasira. . . . Hakuwa na staha yoyote kwa uhai wa kibinadamu . . . Maisha yake ya faraghani yalikuwa yenye ukatili sana alipozeeka.”
Kwa wazi Konstantino alikuwa na matatizo mazito ya utu. Mtafiti wa historia ataarifu kwamba “sifa yake ya kukasirika upesi ndiyo mara nyingi iliyokuwa sababu ya kufanya kwake uhalifu.” (Ona sanduku “Uuaji Kimakusudi Mbalimbali wa Nasaba ya Wafalme.”) Konstantino hakuwa na “utu wa Kikristo,” abisha mwanahistoria H. Fisher katika kitabu chake History of Europe. Mambo ya hakika hayampi sifa ya kuwa Mkristo wa kweli aliyekuwa amevaa “utu mpya” na ambaye ndani yake kungeonekana matunda ya roho takatifu ya Mungu—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.—Wakolosai 3:9, 10; Wagalatia 5:22, 23.
Matokeo ya Jitihada Zake
Akiwa Askofu Mkuu mpagani—na kwa hiyo kiongozi wa kidini wa Milki ya Roma—Konstantino alijaribu kuwashawishi maaskofu wa kanisa lenye kuasi imani. Aliwatolea nyadhifa za mamlaka, umashuhuri, na mali wakiwa maofisa wa dini ya Serikali ya Roma. Kichapo Catholic Encyclopedia chakubali: “Maaskofu fulani, wakiwa wamepofushwa na fahari ya hiyo staha, hata walithubutu kumsifu huyo maliki kuwa malaika wa Mungu, kuwa mtu mtakatifu, na kutabiri kwamba angetawala mbinguni, sawa na Mwana wa Mungu.”
Ukristo wenye kuasi imani ulipopendelewa na serikali ya kisiasa, ulipata kuwa zaidi na zaidi sehemu ya ulimwengu huu, sehemu ya mfumo huu wa kilimwengu, na kuchukuliwa pole kwa pole kutoka katika mafundisho ya Yesu Kristo. (Yohana 15:19; 17:14, 16; Ufunuo 17:1, 2) Tokeo ni kwamba, “Ukristo” uliunganishwa na mafundisho na mazoea yasiyo ya kweli—Utatu, hali ya kutokufa kwa nafsi, moto wa helo, purgatori, sala kwa ajili ya wafu, utumizi wa rozari, sanamu, mifano, na mambo ya namna hiyo.—Linganisha 2 Wakorintho 6:14-18.
Kutoka kwa Konstantino, kanisa lilirithi mwelekeo wenye kulazimisha utii. Wasomi Henderson na Buck wasema hivi: “Ule usahili wa Gospeli ulifisidiwa, sherehe za ibada zenye fahari za madaha na sherehe mbalimbali zikaanzishwa, heshima za kilimwengu na mishahara ikakabidhiwa walimu wa Ukristo, na wa Ufalme wa Kristo ambao kwa kiwango kikubwa ulikuwa umegeuzwa kuwa ufalme wa ulimwengu huu.”
Ukristo wa Kweli Uko Wapi?
Mambo ya hakika ya kihistoria hufunua sababu ya kweli ya “ukubwa” wa Konstantino. Badala ya kuanzishwa na Yesu Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko la Kikristo la kweli, Jumuiya ya Wakristo kwa kiwango fulani ni tokeo la kujinufaisha kisiasa na la mbinu zenye ujanja za maliki mpagani. Kwa kufaa sana, mwanahistoria Paul Johnson auliza hivi: “Je, milki ilijisalimisha kwa Ukristo, au Ukristo ulitumiwa vibaya na milki?”
Wale wote watakao kikweli kushikamana sana na Ukristo ulio safi waweza kusaidiwa kutambua na kushirikiana na kutaniko la Kikristo la kweli leo. Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wako tayari kabisa kuwasaidia watu wenye moyo wa haki watambue Ukristo wa kweli na kuabudu Mungu katika njia yenye kukubalika kwake.—Yohana 4:23, 24.
[Maelezo ya Chini]
a Udonati ulikuwa farakano la “Kikristo” la karne ya nne na ya tano W.K. Wafuasi wake walidai kwamba uhalali wa matendo ya kidini hutegemea sifa za kiadili za mhudumu na kwamba ni lazima kanisa liondoe kutoka kwa washiriki wake watu wenye hatia ya dhambi nzito. Uaria ulikuwa harakati ya “Kikristo” ya karne ya nne ambao ulikana uungu wa Yesu Kristo. Ariasi alifundisha kwamba Mungu hakuzaliwa wala hana mwanzo. Kwa sababu Mwana amezaliwa, hawezi kuwa Mungu katika maana sawa na vile Baba alivyo. Mwana hakuwako tangu umilele wote lakini aliumbwa na huwako kwa mapenzi ya Baba.
[Sanduku katika ukurasa wa 28]
Konstantino na Baraza la Nisea
Maliki Konstantino asiyebatizwa alitimiza fungu gani kwenye Baraza la Nisea? Kichapo Encyclopædia Britannica chataarifu hivi: “Konstantino mwenyewe alisimamia, akiongoza kwa bidii mazungumzo . . . Wakiwa wameogofywa na huyo maliki, maaskofu wote, isipokuwa wawili tu, walitia sahihi hizo itikadi za kidini, wengi wao wakifanya hivyo kinyume cha mwelekeo wao.”
Baada ya miezi miwili ya mjadala wa kidini wenye hasira, mwanasiasa huyo mpagani aliingilia kati na kuamua kwa kupendelea wale waliosema kwamba Yesu alikuwa Mungu. Lakini kwa nini? “Kimsingi Konstantino hakuwa na uelewevu wowote wa maswali yaliyokuwa yakiulizwa katika theolojia ya Kigiriki,” chasema kitabu A Short History of Christian Doctrine. Alielewa kwamba mgawanyiko wa kidini ulikuwa tisho kwa milki yake, naye alikuwa ameazimia kuiimarisha milki yake.
Kwa habari ya hati ya mwisho iliyoandikwa huko Nisea kwa msaada wa Konstantino, kitabu Istoria tou Ellinikou Ethnous (Historia ya Taifa la Kigiriki) chasema hivi: “Yaonyesha ubaridi wa [Konstantino] kuelekea mambo ya kimafundisho, . . . kudumu kwake kwa ushupavu katika kujaribu kurudisha muungano ndani ya kanisa kwa vyovyote, na mwishowe kusadiki kwake kwamba akiwa ‘askofu wa wasio Wakristo’ alikuwa na kauli ya mwisho kuhusu jambo lolote lile la kidini.” Je, yawezekana kwamba roho ya Mungu ilitegemeza maamuzi yaliyofanywa kwenye baraza hilo?—Linganisha Matendo 15:28, 29.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
Uuaji Kimakusudi Mbalimbali wa Nasaba ya Wafalme
Chini ya kichwa hicho, kitabu Istoria tou Ellinikou Ethnous (Historia ya Taifa la Kigiriki) chafafanua kile ambacho hukiita “uhalifu wa nyumbani wenye kuchukiza sana ambao Konstantino alifanya.” Upesi baada ya kuanzisha utawala wake wa kinasaba, alisahau jinsi ya kuonea shangwe mafanikio yasiyotazamiwa, akajua hatari zilizomzunguka. Akiwa mtu mwenye kushuku na labda mwenye kuchochewa na wenye kujipendekeza, kwanza alimshuku mpwa wake wa kiume, Lisinianasi—mwana wa Augusto mwenzake ambaye tayari alikuwa amemfisha—ambaye angeweza kuwa mshindani wake. Kuuawa kimakusudi kwake kulifuatwa na kufishwa kwa Krispo, mwana mzaliwa wa kwanza wa Konstantino mwenyewe, aliyeuawa na mama yake wa kambo Fausta, kwa sababu alionekana kuzuia uzao wake mwenyewe kupata mamlaka kamili.
Mwishowe tendo hilo la Fausta lilikuwa sababu ya kifo chake mwenyewe chenye kutazamisha. Yaonekana kwamba Augusta Helena, aliyekuwa na uvutano juu ya mwana wake Konstantino mpaka mwisho, alihusika katika uuaji kimakusudi huo. Hisia zisizopatana kiakili, ambazo mara nyingi zilimwongoza Konstantino pia zilichangia kufishwa kwa wingi kwa wengi wa marafiki na washiriki wake. Kitabu History of the Middle Ages chamalizia hivi: “Kufishwa—sio kusema kuua kimakusudi—kwa mwana wake mwenyewe na mke wake kwaonyesha kwamba hakuguswa na uvutano wowote wa kiroho katika Ukristo.”
[Picha katika ukurasa wa 30]
Tao hili katika Roma limetumiwa kumtukuza Konstantino
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Musée du Louvre, Paris