Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 4/1 kur. 26-29
  • Jinsi Wakristo Hukabili Shutumu ya Peupe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Wakristo Hukabili Shutumu ya Peupe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kielelezo cha Wakristo Kufuata
  • Je, Uitikie Uchambuzi?
  • Habari za Kwanza Ni Muhimu
  • Usiogopeshwe na Wapinzani
  • Kutetea Imani Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wanachukiwa Bila Sababu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Maoni Yetu Ni Nini Kuelekea Wanaoipinga Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ni Wenye Furaha Ingawa Wanateswa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 4/1 kur. 26-29

Jinsi Wakristo Hukabili Shutumu ya Peupe

UNAHISIJE mtu fulani anapokushutumu au aenezapo uwongo juu yako? Kwa kawaida utaumia moyoni. Mashahidi wa Yehova hupatwa na jambo kama hilo wanapolengewa habari zisizo za kweli au zilizopotoka katika vyombo vya habari. Lakini kama Yesu alivyosema katika Mathayo 5:11, 12, wao bado wana sababu nzuri ya kuwa na shangwe.

Kwa mfano, kichapo kimoja cha Katoliki katika Ujerumani kilidai kwamba “kila Shahidi hulazimishwa kutoa upaji wa kati ya asilimia 17 na 28 ya mapato yake kwa makao makuu ya dhehebu hilo.” Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova si dhehebu, na kazi yao inagharimiwa kabisa kifedha kwa michango ya hiari. Wasomaji wengi walidanganywa na habari hiyo ya uwongo, ambayo inasikitisha sana Mashahidi wa Yehova. Lakini Wakristo wa kweli wanapaswa kuitikiaje shutumu katika vyombo vya habari?

Kielelezo cha Wakristo Kufuata

Mathayo sura ya 23 yafafanua waziwazi jinsi Yesu alivyoshutumu wapinzani wake wa kidini kwa ajili ya unafiki na udanganyifu wao. Je, hilo laandaa kigezo cha kufuata kwa Wakristo leo juu ya jinsi ya kukabili wachambuzi? Sivyo. Mwana wa Mungu alishutumu wapinzani wake wa kidini kwa sababu ya mamlaka yake ya kipekee na utambuzi wa ndani aliokuwa nao, akifanya hivyo kwa manufaa za umati uliokuwa ukimsikiliza.

Mathayo 15:1-11 yaelezea kwamba Yesu alichambuliwa kwa sababu wanafunzi wake walisemwa kuwa walikiuka mapokeo ya Kiyahudi. Yesu aliitikiaje? Yeye alisimama imara. Katika pindi fulani, Yesu alibishana na wachambuzi wake bila kuogopa, akikanusha maoni yao mabaya. Kwa ujumla, si vibaya kwa Wakristo leo kujaribu kusahihisha maoni mabaya ya kazi yao au mafundisho yao, wakijaribu kuelewesha hali hiyo kwa njia sahihi inayopatana na akili. Wao hufanya hivyo ili kusaidia watu wenye mioyo ya kufuata haki watambue kwamba uchambuzi wa Mashahidi wa Yehova haufai na ni wenye kuharibu sifa yao.

Lakini ona jinsi Yesu alivyoitikia muda mfupi baadaye wanafunzi wake walipomwambia: “Wajua ya kuwa Mafarisayo walipolisikia neno lile walichukizwa?” Mafarisayo “walichukizwa”—wao hawakukasirika tu bali wakawa wapinzani wasioweza kurekebishwa ambao Yesu aliwakataa. Kwa hiyo alijibu: “Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu.” Mazungumzo zaidi na wapinzani hao wenye uhasama hayakuwa na maana, hayangenufaisha mtu yeyote, na yangetokeza tu mabishano ya bure. (Mathayo 7:6; 15:12-14; linganisha 27:11-14.) Majibu ya Yesu yaonyesha kwamba kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.”—Mhubiri 3:7.

Mashahidi wa Yehova hawatarajii kila mtu aseme vyema juu yao. Wao huzingatia maneno ya Yesu: “Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.” (Luka 6:26) Pindi moja C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, aliulizwa ni kwa nini yeye hakujitetea dhidi ya shutumu. Yeye alijibu: “Ukisimama kumpiga teke kila mbwa anayekubwekea, hutafika mbali.”

Hivyo, hatupaswi kuacha maneno ya wapinzani wenye bidii yatukengeushe kutoka kwa utumishi wetu kwa Mungu. (Zaburi 119:69) Na tuzingatie kazi ya Wakristo wa kweli, yaani, kueneza evanjeli. Matokeo ya kawaida yatakuwa kwamba tutakuwa na fursa za kujibu maswali na kueleza umuhimu wa kazi yetu, kama vile kuboresha maadili ya mtu na kumfunza katika Neno la Mungu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Je, Uitikie Uchambuzi?

Yesu alisema hivi juu ya wafuasi wake: “Ninyi si wa ulimwengu . . . Kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.” (Yohana 15:19) Ripoti nyingi za vyombo vya habari ambazo hushutumu sana Mashahidi wa Yehova ni wonyesho wa chuki hiyo, na ripoti kama hizo zapaswa kupuuzwa. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda vyombo vya habari vitoe habari zisizo za kweli juu ya Mashahidi au zenye kupotoa au zisizoelewesha vizuri mambo fulani ya hakika. Huenda waandikaji fulani wa magazeti wakapata habari kutoka kwa watu wanaotubagua. Tuwe tunapuuza habari za uwongo katika vyombo vya habari au tuwe tunatetea kweli kwa njia ifaayo yategemea hali, mchocheaji wa uchambuzi, na lengo lake.

Nyakati nyingi mambo ya hakika yaweza kusahihishwa kwa barua iliyoandikwa vizuri kwa mhariri iwapo barua hiyo itachapishwa yote. Lakini barua kama hiyo yaweza kuleta matokeo tofauti kabisa na yale yaliyokusudiwa. Kwa njia gani? Ule uwongo wa awali waweza kupata utangazaji mwingi hata zaidi, au wapinzani waweza kupewa fursa zaidi ya kupata uwongo au matukano ya kuchapisha. Katika hali nyingi ni afadhali kuacha suala la barua kwa mhariri lishughulikiwe na wazee wanaohusika. Ikiwa habari mbaya za vyombo vya habari zatokeza chuki, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society yaweza kujulisha makutaniko katika nchi hiyo mambo ya hakika, hivyo ikiwezesha wahubiri wote kutoa maelezo mazuri kwa watu wanaouliza.

Je, wewe binafsi unahitaji kujihusisha hata kidogo na mashtaka hayo yaliyopotoka? Shauri la Yesu la “waacheni,” wapuuzeni, kwa wazi latumika kwa kikundi hiki cha wapinzani. Wakristo waaminifu-washikamanifu wana sababu za Kibiblia za kupuuza waasi-imani na maoni yao. (1 Wakorintho 5:11-13; Tito 3:10, 11; 1 Yohana 2:19; 2 Yohana 10, 11) Ikiwa mtu fulani anapendezwa kujua kwa moyo wa unyoofu kama uchambuzi dhidi ya Mashahidi wategemea mambo ya hakika au ya uwongo, mara nyingi ujuzi wako mwenyewe wenye msingi mzuri hutosha kumjibu.—Ona Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1986, kurasa 13 na 14.

Ukikabiliwa na habari zilizopotoka katika vyombo vya habari, zingatia shauri la Mithali 14:15: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Katika Uswisi, watu wengi waliudhika wakati ripoti fulani zenye kugusa hisia katika vyombo vya habari zilipotaja kwamba msichana mmoja Shahidi alikufa kwa sababu watu wake wa ukoo walikataza wafanyakazi wa hospitali kumtia damu mshipani. Lakini, je, ndivyo mambo yalivyokuwa? La. Mgonjwa huyo alikataa kutiwa damu mshipani kwa sababu za kidini, lakini alikubali tiba ya badala isiyohusu damu. Tiba hiyo ingeanzishwa mara hiyo bila mambo mengi na yaelekea hiyo ingeokoa uhai wake. Lakini, hospitali ilikawia isivyofaa kumtibu mpaka kulipochelewa mno. Ripoti za vyombo vya habari hazikutaja mambo hayo ya hakika.

Kwa hiyo, upime kwa uangalifu kadiri ya ukweli wa ripoti hizo. Twaweza kueleza watu wanaouliza maswali kwamba wazee wenyeji hushughulikia visa kama hivyo kwa njia yenye upendo na kwa kupatana na miongozo ya Biblia. Kwa kushikilia kanuni tunapojibu maswali hutuzuia kurukia maamuzi.—Mithali 18:13.

Habari za Kwanza Ni Muhimu

Katika karne ya kwanza, watu walieneza uwongo juu ya Yesu Kristo ili kuharibu sifa yake, wengine hata wakimtaja kuwa mhaini. (Luka 7:34; 23:2; linganisha Mathayo 22:21.) Baadaye, kutaniko changa la Kikristo lilikabili upinzani mkubwa kutoka kwa watu wa kidini na kilimwengu. Kwa kuwa “Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia,” wengi waliwadharau watumishi wake. (1 Wakorintho 1:22-29) Wakristo wa kweli leo ni lazima wafikirie shutumu, ambayo ni namna ya mnyanyaso.—Yohana 15:20.

Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova huthamini wakati mtu wanayesema naye habagui naye aonyesha mtazamo uleule wa baadhi ya wageni wa Paulo katika Roma, waliotangaza hivi: “Tunataka kusikia kwako uonavyo wewe; kwa maana katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.”—Matendo 28:22.

Eleza watu waliopata habari za uwongo, ukifanya hivyo kwa upole. (Warumi 12:14; linganisha 2 Timotheo 2:25.) Uwaalike wapate habari za kwanza kuhusu Mashahidi wa Yehova, jambo linalowawezesha kuona mashtaka ya uwongo. Pia unaweza kutumia maelezo yaliyochapishwa na Watch Tower Society yanayotoa habari nyingi juu ya tengenezo, historia, na mafundisho yalo.a Pindi moja Filipo alimjibu Nathanaeli kwa kusema hivi tu: “Njoo uone.” (Yohana 1:46) Twaweza kufanya vivyo hivyo. Mtu yeyote anayetaka anakaribishwa kwa uchangamfu kuzuru Jumba la Ufalme la kwao ili ajionee mwenyewe Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani na yale wanayoamini.

Usiogopeshwe na Wapinzani

Ni jambo la kutia moyo kama nini kujua kwamba shutumu haizuii watu kuwa Mashahidi! Katika kipindi kimoja cha mazungumzo ya televisheni nchini Ujerumani, waasi-imani walisema uwongo mwingi juu ya Mashahidi. Mtazamaji mmoja alitambua shutumu hizo za uasi-imani kuwa mambo yasiyo ya kweli naye alisukumwa na moyo aanze tena kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Ndiyo, nyakati nyingine shutumu ya peupe hutokeza matokeo mazuri!—Linganisha Wafilipi 1:12, 13.

Mtume Paulo alijua kwamba wengine wangeelekeza fikira zaidi kwa “hadithi za uongo” kuliko kweli. Kwa hiyo yeye aliandika: “Uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.” (2 Timotheo 4:3-5) Kwa hiyo usijiruhusu ukengeushwe, na kamwe ‘usiogope’ wapinzani. (Wafilipi 1:28) Dumisha utulivu bila kuwa na wasiwasi na uhubiri habari njema kwa shangwe, nawe utakabili kwa ujasiri shutumu ya peupe. Ndiyo, kumbuka ahadi ya Yesu: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”—Mathayo 5:11, 12.

[Maelezo ya Chini]

a Ona vichapo Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote, Mashahidi wa Yehova Katika Karne ya 20, na Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Alipokabiliwa na wapinzani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Waacheni.” Alimaanisha nini?

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu.”—Mathayo 5:11

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki