Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Ni mtazamo gani upasao kuonyeshwa kwenye ubatizo wa Kikristo?
Hilo ni swali lenye kupendeza, kwani ingawa wengi wa wasomaji wetu tayari wamebatizwa, wao wanahusika, kama vile wale wanaobatizwa. Kwanza, acheni tutoe maelezo juu ya wale wanaobatizwa, wanaozamishwa kabisa. Mtazamo wao wapasa uwe nini?
Kwenye Mathayo 28:19, 20, Yesu aliwaambia wafuasi wake waende wakafanye watu kuwa wanafunzi, wakiwafundisha na kuwabatiza. Yeye hakuonyesha ubatizo kuwa ono la kusisimukiwa kupita kiasi, likiwa jambo linalotokana na msisimuko wa muda. Ni hatua nzito, kama vile tuonavyo kutokana na kielelezo cha Yesu. Luka 3:21 husema: ‘Yesu naye akabatizwa, naye alipokuwa anaomba, mbingu zilifunuka.’ Ndiyo, Kielelezo chetu alichukua ubatizo kwa uzito, kwa sala. Hatuwezi kumwazia akitoa ishara ya ushindi baada ya kutoka majini, akitoa kelele ya ushindi, au akitupa-tupa mikono yake hewani, ingawa wengine wamefanya mambo kama hayo hivi karibuni. La, akiwa pamoja na Yohana Mbatizaji peke yake, Yesu alimwendea Baba yake kwa sala.
Hata hivyo, Biblia haidokezi kwamba ni lazima ubatizo uwe tukio lisilochangamkiwa au lisilo la furaha, likitaka vikao vya pekee au vya kurudia-rudia maneno, kama vile baadhi ya makanisa katika Jumuiya ya Wakristo hutaka leo. Kwani, fikiria siku ya Pentekoste, wakati maelfu ya Wayahudi na waongofu walipopata ubatizo wa Kikristo. Tayari walikuwa wamejifunza Sheria ya Mungu na kuingia katika uhusiano naye. Kwa hiyo walihitaji tu kujifunza juu ya, na kukubali Mesiya, Yesu. Mara walipofanya hivyo, wao wangebatizwa.
Matendo 2:41 (NW) yaripoti hivi: “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa.” Tafsiri ya Biblia ya Weymouth yasomeka hivi: “Basi, wale waliolikaribisha neno lake kwa shangwe walibatizwa.” Walipata shangwe katika zile habari zenye kusisimua juu ya Mesiya, na bila shaka shangwe hiyo ya kuhisiwa moyoni ilienea hadi kwenye ubatizo wenyewe, ubatizo uliofanywa mbele ya mamia na mamia ya watazamaji wenye furaha. Hata malaika mbinguni walikuwa wakitazama na kushangilia. Kumbuka maneno ya Yesu: “Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.”—Luka 15:10.
Kuna njia mbalimbali ambazo kwazo kila mmoja wetu aweza kuonyesha uzito na pia shangwe ya ubatizo. Katika makanisa fulani wale wanaobatizwa huvaa kanzu nyeupe au nyeusi. Hakuna Andiko lolote linalounga mkono takwa hilo. Isitoshe, mavazi ya kuogea yenye kufunua uchi yasingefaa hata kidogo, kwa wanaume au kwa wanawake. Na kama vile imesemwa, baada ya kutoka majini, Mkristo mpya hapaswi kutoa ishara za kipekee wala kusisimuka sana kana kwamba alikuwa amepata ushindi mkubwa. Sehemu nyingine ya udugu wa Kikristo ina furaha kwamba mtu mpya alibatizwa. Yeye apaswa kutambua kwamba wonyesho huo wa imani ni hatua ya mwanzo tu katika ule mwendo mrefu wa uaminifu-maadili ili kupata kibali cha Mungu.—Mathayo 16:24.
Sisi, tukiwa watazamaji katika ubatizo wa hadharani, hushiriki shangwe ya pindi hiyo, hasa ikiwa mtu anayebatizwa ni mtu wa ukoo au mtu fulani tuliyejifunza Biblia pamoja naye. Hata hivyo, ili kushiriki kikamili, twapaswa kusikiliza hotuba yote pamoja na wataka-kubatizwa, tuwasikie wakijibu hadharani yale maswali waliyoulizwa, na kujiunga katika sala. Kufanya hivyo kutatusaidia tuwe na maoni yafaayo juu ya ubatizo wenyewe; tutakuwa na maoni ya Mungu juu ya huo. Baada ya ubatizo kwisha, shangwe yetu haihitaji wonyesho wa ushindi wenye madoido, shada la maua, au karamu kwa heshima ya yule aliyebatizwa. Lakini tungeweza kumwendea ndugu au dada yetu mpya ili kuonyesha furaha kwa sababu ya hatua hiyo nzuri ajabu aliyochukua na kumkaribisha kwa uchangamfu sana katika udugu wetu wa Kikristo.
Basi, kwa muhtasari, sisi sote, kutia na wale wanaojitiisha kwa uzamisho wa maji, twapaswa kuona ubatizo kwa uzito ufaao. Huo si wakati wa kupaaza sauti kwa hisiamoyo, wa kufanya karamu, au wa kushangilia kwa kelele nyingi. Wala huo si wakati wa mtu kukosa uchangamshi au furaha. Twaweza kuwa wenye shangwe kwa kufaa kwamba wapya wamejiunga nasi kwenye njia ya uhai wa milele. Na twaweza kuwakaribisha kwa shangwe ndugu na dada zetu wapya.
[Picha katika ukurasa wa 31]