Ni Nini Hukuchochea Kumtumikia Mungu?
“Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho [“nafsi,” “NW”] yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”—MARKO 12:30.
1, 2. Ni mambo gani ya kusisimua yanayotimizwa kuhusu kazi ya kuhubiri?
THAMANI ya kweli ya gari haiamuliwi tu na jinsi linavyoonekana. Rangi ya juu yaweza kuongeza uzuri walo wa nje, na muundo walo maridadi waweza kuvutia mtu awezaye kulinunua; lakini vitu muhimu zaidi ni vile visivyoonekana mara hiyo—injini inayoendesha gari hilo, pamoja na vitu vingine vyote vya kuliendesha.
2 Ndivyo ilivyo na utumishi wa Mkristo kwa Mungu. Mashahidi wa Yehova hujawa na kazi za kimungu. Kila mwaka, zaidi ya muda wa saa bilioni moja hutumiwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Isitoshe, mamilioni ya mafunzo ya Biblia yanaongozwa, na wale wanaobatizwa hufikia mamia ya maelfu. Ikiwa wewe ni mtangazaji wa habari njema, umeshiriki katika tarakimu hizo zenye kusisimua hata kama ushirika wako waonekana kuwa kidogo. Na unaweza kuwa na hakika kwamba ‘Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yako, na pendo lile ulilolidhihirisha kwa jina lake.’—Waebrania 6:10.
3. Mbali na matendo, ni nini yapasa kuwa hangaiko kubwa kwa Wakristo, na kwa nini?
3 Hata hivyo, thamani ya kweli ya utumishi wetu—kwa ujumla au tukiwa mmoja-mmo- ja—haipimwi kwa tarakimu pekee. Ni kama Samweli alivyoambiwa, “wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Ndiyo, ni hali yetu ya ndani iliyo muhimu kwa Mungu. Ni kweli kwamba matendo ni muhimu. Matendo ya ujitoaji kimungu hupamba fundisho la Yehova na kuvutia wale wawezao kuwa wanafunzi. (Mathayo 5:14-16; Tito 2:10; 2 Petro 3:11) Lakini, matendo yetu hayafunui mambo yote. Yesu aliyefufuliwa alikuwa na hangaiko kuhusu kutaniko katika Efeso—wajapokuwa na rekodi nzuri ya matendo mema. “Nayajua matendo yako,” akawaambia. “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza.”—Ufunuo 2:1-4.
4. (a) Ni kwa njia gani utumishi wetu kwa Mungu waweza kuwa kama desturi tu ya kufuatwa? (b) Kwa nini kuna uhitaji wa kujichunguza?
4 Kuna hatari. Baada ya muda fulani, utumishi wetu kwa Mungu waweza kuwa desturi tu ya kufuatwa. Mwanamke mmoja Mkristo alifafanua hali yake hivi: “Ningeenda katika utumishi, niende mikutanoni, nijifunze, nisali—lakini nilifanya hayo yote kidesturi tu, bila kuhisi chochote.” Bila shaka watumishi wa Mungu wapaswa kupongezwa wanapojikakamua wajapohisi ‘kutupwa chini’ au ‘unyonge.’ (2 Wakorintho 4:9; 7:6) Hata hivyo, mambo yetu ya kawaida ya Kikristo yakiwa desturi tu, twahitaji kuchungulia ndani katika injini. Hata magari bora zaidi huhitaji kudumishwa kila baada ya muda fulani; vivyo hivyo, Wakristo wote wahitaji kujichunguza kwa ukawaida. (2 Wakorintho 13:5) Wengine waweza kuona kazi zetu, lakini hawawezi kutambua kinachochochea matendo yetu. Basi, kila mmoja wetu apaswa kuhangaikia swali hili: ‘Ni nini hunichochea kumtumikia Mungu?’
Vizuizi vya Uchocheo Ufaao
5. Yesu alisema ni amri gani iliyo ya kwanza kwa zote?
5 Alipoulizwa ni ipi kati ya sheria zilizopewa Israeli iliyokuwa ya kwanza, Yesu alinukuu amri ambayo haikukazia sura yetu ya nje, bali iliyokazia uchocheo wetu wa ndani: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho [“nafsi,” NW] yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:28-30) Hivyo Yesu akataja kinachopasa kuwa msukumo wa utumishi wetu kwa Mungu—upendo.
6, 7. (a) Ni kwa njia gani Shetani ameshambulia kwa hila maisha ya familia, na kwa nini? (2 Wakorintho 2:11) (b) Malezi ya mtu yaweza kuathirije mtazamo wake kuelekea mamlaka ya kimungu?
6 Shetani anataka kuzuia uwezo wetu wa kusitawisha sifa muhimu ya upendo. Ili afaulu, njia moja ambayo ametumia ni kushambulia maisha ya familia. Kwa nini? Kwa sababu hapo ndipo maonyesho yetu ya kwanza na yenye kudumu zaidi ya upendo hufanyizwa. Shetani ajua vema kanuni ya Kibiblia kwamba mambo anayojifunza mtu utotoni yaweza kuwa na manufaa akiwa mtu mzima. (Mithali 22:6) Yeye hujaribu kwa hila kupotosha maana ya upendo kwetu tukiwa na umri mchanga. Akiwa “mungu wa dunia hii,” Shetani huona makusudi yake yakitumiwa vizuri na wengi wanaolelewa katika nyumba zisizo na upendo lakini ambazo ni vituo vya uchungu, ghadhabu, na usemi wenye matukano.—2 Wakorintho 4:4; Waefeso 4:31, 32; 6:4, kielezi-chini, NW; Wakolosai 3:21.
7 Kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha kilisema kwamba njia ambayo baba hushughulikia daraka lake la kimzazi “[yaweza kuathiri sana] maoni ambayo baadaye watoto wake wataonyesha juu ya mamlaka ya kibinadamu na ya kimungu.”a Mwanamume mmoja Mkristo aliyelelewa chini ya mamlaka ya kiimla ya baba yake aliyekuwa mkali sana akiri hivi: “Kwangu, kumtii Yehova ni rahisi; kumpenda ni vigumu zaidi.” Bila shaka, utii ni muhimu, kwa kuwa machoni pa Mungu “kutii ni bora kuliko dhabihu.” (1 Samweli 15:22) Lakini ni nini kiwezacho kutusaidia kufanya zaidi ya kuwa wenye utiifu tu na kitakachotusaidia kusitawisha upendo kwa Yehova ukiwa kani ya kuchochea ibada yetu?
‘Upendo wa Kristo Watubidiisha’
8, 9. Fidia ya dhabihu ya Yesu yapasa kuchocheaje upendo wetu kwa Yehova?
8 Kichocheo kikubwa zaidi cha kusitawisha upendo wa moyo wote kwa Yehova ni kuthamini fidia ya dhabihu ya Yesu Kristo. “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye.” (1 Yohana 4:9) Mara tunapolifahamu na kulithamini, tendo hili la upendo hutokeza itikio la upendo. “Sisi twapenda kwa maana [Yehova] alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.
9 Yesu alikubali kwa hiari mgawo wake wa kutumika akiwa Mwokozi wa mwanadamu. “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu.” (1 Yohana 3:16; Yohana 15:13) Upendo wa Yesu wenye kujidhabihu wapaswa kuamsha itikio lenye uthamini ndani yetu. Kwa kielelezo: Tuseme umeokolewa kutoka majini. Je, ungeenda tu nyumbani, ujipanguse, na kusahau tukio hilo? Bila shaka la! Ungehisi kuwa na deni kwa mtu aliyekuokoa. Kwani, anakuwia uhai wako. Je, Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatuwia jambo dogo kuliko hilo? Bila fidia, kila mmoja wetu angezama katika dhambi na kifo. Badala ya hivyo, kwa sababu ya tendo hili kubwa la upendo, tuna tazamio la kuishi milele katika dunia iliyo paradiso.—Warumi 5:12, 18; 1 Petro 2:24.
10. (a) Twaweza kufanyaje fidia ituhusu binafsi? (b) Upendo alio nao Kristo watubidiishaje?
10 Tafakari juu ya fidia. Uitumie binafsi maishani mwako, kama alivyofanya Paulo: “Uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu, ambaye alinipenda akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu.” (Wagalatia 2:20) Kutafakari kwa njia hiyo kutaamsha uchocheo unaotoka moyoni, kwa kuwa Paulo aliandikia Wakorintho hivi: “Upendo wa Kristo watubid[i]isha . . . alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.” (2 Wakorintho 5:14, 15) The Jerusalem Bible yasema kwamba upendo wa Kristo “hutushurutisha sana.” Tunapotafakari upendo wa Kristo, tunabidiishwa, kusukumwa sana na moyo, hata kushurutishwa sana. Unagusa mioyo yetu na kutuchochea tutende. Na kama linavyofasiriwa na tafsiri ya J. B. Phillips, “chanzo chenyewe cha matendo yetu ni upendo wa Kristo.” Uchocheo wowote wa aina nyingine hautatokeza matunda ya kudumu ndani yetu, kama uonyeshwavyo na kielelezo cha Mafarisayo.
“Jilindeni na Chachu ya Mafarisayo”
11. Fafanua mtazamo wa Mafarisayo kuelekea matendo ya kidini.
11 Mafarisayo walitoa uhai wote kutoka kwa ibada ya Mungu. Badala ya kukazia upendo kwa Mungu, wao walikazia matendo kuwa kipimo cha hali ya kiroho. Kazi yao ya kushughulikia sana sheria ndogo-ndogo iliwafanya waonekane kuwa waadilifu kwa nje, lakini ndani, wao ‘walijaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.’—Mathayo 23:27.
12. Baada ya Yesu kumponya mtu fulani, Mafarisayo walijionyeshaje kuwa wagumu katika mioyo?
12 Katika pindi moja, kwa huruma-nyororo Yesu alimponya mtu ambaye mkono wake ulikuwa umenyauka. Ni lazima mtu huyo awe alifurahi kama nini kuponywa mara moja ugonjwa ambao bila shaka ulimfanya asihisi vizuri kimwili na kihisiamoyo! Lakini Mafarisayo hawakushangilia pamoja naye. Badala ya hivyo, walitafuta kijikosa—kwamba Yesu alikuwa ametoa msaada katika siku ya Sabato. Wakishughulikia mno ufasiri wao wa mambo madogo-madogo ya Sheria, Mafarisayo walikosa kabisa kusudi la Sheria. Si ajabu kwamba Yesu ‘aliona huzuni kwa ajili ya ugumu wa mioyo yao’! (Marko 3:1-5) Na zaidi, aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Jilindeni na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo.” (Mathayo 16:6) Matendo yao na mitazamo yao inafunuliwa katika Biblia kwa manufaa yetu.
13. Kuna somo gani kwetu katika kielelezo cha Mafarisayo?
13 Kielelezo cha Mafarisayo chatufundisha kwamba twahitaji kuwa wenye kiasi kwa habari ya matendo. Ni kweli kwamba matendo ni muhimu, kwa kuwa “imani pasipo matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Hata hivyo, wanadamu wasiokamilika wana mwelekeo wa kuhukumu wengine kwa yale wanayofanya kuliko kwa jinsi walivyo. Huenda hata nyakati nyingine tukajihukumu hivyo. Huenda tukawa na kichaa cha kuwa watendaji, kana kwamba hicho ndicho kipimo cha pekee cha hali yetu ya kiroho. Twaweza kusahau umuhimu wa kuchunguza uchocheo wetu mbalimbali. (Linganisha 2 Wakorintho 5:12.) Huenda tukawa watu wa kushikilia sheria mno ‘wanaochuja mbu na kumeza ngamia,’ tukitii sheria huku tukivunja kusudi layo.—Mathayo 23:24.
14. Mafarisayo walikuwaje kama kikombe au kombe chafu?
14 Mafarisayo hawakujua kwamba ikiwa mtu anampenda Yehova kikweli, kwa kawaida matendo ya ujitoaji kimungu yangefuata yenyewe. Hali ya kiroho hutoka ndani ikielekea nje. Yesu alishutumu vikali Mafarisayo kwa jinsi walivyofikiri kimakosa kwa habari hii, akisema: “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang’anyi na kutokuwa na kiasi. Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi.”—Mathayo 23:25, 26.
15. Taja mifano ionyeshayo kwamba Yesu hutazama zaidi ya sura.
15 Jinsi kikombe, kombe, au hata jengo linavyoonekana kwa nje haifunui mengi zaidi. Wanafunzi wa Yesu waliduwazwa na umaridadi wa hekalu la Yerusalemu, ambalo Yesu aliliita “pango la wanyang’anyi” kwa sababu ya mambo yaliyokuwa yakiendelea humo. (Marko 11:17; 13:1) Ukweli kuhusu hekalu ndio ukweli unaohusu mamilioni ya watu wanaodai kuwa Wakristo, kama ambavyo rekodi ya Jumuiya ya Wakristo inavyoonyesha. Yesu alisema kwamba angewahukumu baadhi ya watu ambao walifanya “miujiza mingi” katika jina lake kuwa ‘watendao maovu.’ (Mathayo 7:22, 23) Tofauti kabisa, yeye alisema hivi kuhusu mjane aliyetoa mchango kidogo sana wa pesa hekaluni: “Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina . . . huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia.” (Marko 12:41-44) Je, ni kutoa hukumu kwa njia isiyopatana? La. Katika hali zote mbili, Yesu alionyesha maoni ya Yehova. (Yohana 8:16) Yeye aliona vichocheo vya matendo na kuhukumu kupatana navyo.
“Kila Mtu kwa Kadiri ya Uwezo Wake”
16. Kwa nini hatuhitaji kulinganisha utendaji wetu sikuzote na ule wa Mkristo mwingine?
16 Tukichochewa na mambo mazuri, hakuna haja ya kufanya milinganisho sikuzote. Kwa kielelezo, ni kazi bure kujaribu kushindana kwa kutumia muda uleule wa saa katika huduma ambao Mkristo mwingine hutumia au kufikia matimizo ya huyo katika kuhubiri. Yesu alisema umpende Yehova kwa moyo wako wote, akili zako zote, nafsi yako yote, na nguvu zako zote—si za mtu mwingine. Uwezo, nguvu, na hali za kila mtu hutofautiana. Hali yako ikiruhusu, upendo utakuchochea kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma—labda hata ukiwa mhudumu painia wa wakati wote. Hata hivyo, ikiwa unang’ang’ana na ugonjwa, muda unaotumia katika huduma waweza kuwa kidogo kuliko jinsi ungependa. Usivunjike moyo. Uaminifu kwa Mungu haupimwi kwa muda wa saa. Ukichochewa na mambo mazuri, utakuwa na sababu nzuri ya kuwa na shangwe. Paulo aliandika: “Kila mtu na aipime kazi yake mwenyewe, ndipo atakapokuwa na sababu ya kujisifu ndani ya nafsi yake tu, wala si kwa mwenzake.”—Wagalatia 6:4.
17. Katika maneno yako mwenyewe, eleza kifupi mfano wa talanta.
17 Ebu fikiria mfano wa Yesu wa talanta, kama ulivyorekodiwa kwenye Mathayo 25:14-30. Mtu mmoja aliyekuwa karibu kusafiri mbali aliwaita watumwa wake na kuwapa mali zake. “Akampa mmoja talanta tano, na mmoja talanta mbili, na mmoja talanta moja; kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake.” Bwana-mkubwa aliporudi kutoza hesabu watumwa wake, alipata nini? Mtumwa aliyekuwa amepewa talanta tano alipata talanta tano zaidi. Vivyo hivyo, mtumwa aliyekuwa amepewa talanta mbili alipata talanta mbili zaidi. Mtumwa aliyekuwa amepewa talanta moja aliizika ardhini naye hakufanya lolote ili kuongeza mali ya bwana-mkubwa wake. Bwana-mkubwa alichanganuaje hali hiyo?
18, 19. (a) Kwa nini bwana-mkubwa hakumlinganisha mtumwa aliyepewa talanta mbili na yule aliyepewa talanta tano? (b) Mfano wa talanta watufundisha nini kuhusu pongezi na milinganisho? (c) Kwa nini mtumwa wa tatu alipata hukumu ya adhabu?
18 Kwanza, ebu tufikirie mtumwa aliyepewa talanta tano na yule aliyepewa talanta mbili. Kwa kila mmoja wao, bwana-mkubwa alisema: “Vema, mtumwa mwema na uaminifu.” Je, angemwambia hivyo mtumwa mwenye talanta tano kama mtumwa huyo angepata talanta mbili tu? Haielekei hivyo! Kwa upande mwingine, hakumwambia mtumwa aliyepata talanta mbili: ‘Kwa nini hukupata talanta tano? Ona mtumwa mwenzako na jinsi alivyopata nyingi kwa niaba yangu!’ La, bwana-mkubwa mwenye huruma-nyororo, aliyefananisha Yesu, hakuwalinganisha. Yeye aliwapa talanta “kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake,” naye hakutarajia kupata zaidi ya uwezo wa kila mmoja wao. Watumwa wote wawili walipata pongezi sawa, kwa kuwa wote wawili walifanya kazi kwa nafsi yote kwa bwana-mkubwa wao. Sote twaweza kujifunza kwa hayo.
19 Bila shaka, mtumwa wa tatu hakupongezwa. Hata alitupwa katika giza la nje. Baada ya kupokea talanta moja tu, yeye hakutazamiwa kutokeza talanta nyingi kama yule mtumwa mwenye talanta tano. Lakini, yeye hata hakujaribu! Alipewa hukumu ya adhabu kwa sababu ya mtazamo wa moyo wake ulio “mbaya na ulegevu,” ulioonyesha ukosefu wa upendo kwa bwana-mkubwa.
20. Yehova huonaje vizuizi vyetu?
20 Yehova atazamia kila mmoja wetu kumpenda kwa nguvu zetu zote, lakini inachangamsha moyo kama nini kwamba “yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi”! (Zaburi 103:14) Mithali 21:2 lasema kwamba “BWANA huipima mioyo”—si tarakimu. Yeye huelewa vizuizi vyovyote ambavyo hatuwezi kudhibiti, viwe vya kifedha, kimwili, kihisia-moyo, au vingine. (Isaya 63:9) Na wakati uo huo, anatutarajia tutumie kikamili mali zote ambazo huenda tunazo. Yehova ni mkamilifu, lakini anaposhughulika na waabudu wake wasiokamilika, yeye hawatazamii kuwa wakamilifu. Yeye ni mwenye kukubali sababu katika shughuli zake na asiyepitisha kiasi kwa matazamio yake.
21. Utumishi wetu kwa Mungu ukichochewa na upendo, twaweza kupata matokeo gani mazuri?
21 Kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili zetu zote, na nguvu zetu zote “kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa.” (Marko 12:33) Tukichochewa na upendo, basi tutafanya yote tuwezayo katika utumishi wa Mungu. Petro aliandika kwamba sifa za kimungu, kutia ndani upendo, ‘zikiwa kwenu na kujaa tele, zitawafanya ninyi kuwa si wavivu wala si watu wasio na matunda, kwa kumjua Bwana wetu Yesu Kristo.’—2 Petro 1:8.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Kwa Kupitia
◻ Ni nini chapasa kuchochea utumishi wetu kwa Mungu?
◻ Upendo wa Kristo watubidiishaje kumtumikia Yehova?
◻ Ni lazima tuepuke mambo yapi ya Mafarisayo?
◻ Kwa nini si hekima kulinganisha sikuzote utumishi wetu na ule wa Mkristo mwingine?
[Picha katika ukurasa w16]
Uwezo, nguvu, na hali za watu mmoja-mmoja hutofautiana