Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 6/15 kur. 28-31
  • Useja Katika Nyakati Ngumu za Kiuchumi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Useja Katika Nyakati Ngumu za Kiuchumi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fanya Yafaayo Zaidi kwa Hali Yako
  • Tazama Upande Ufaao wa Mambo
  • Je, Unaweza Kupanua Huduma Yako?
  • Usalama kwa Wakati Ujao
  • Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Asiyefunga Ndoa Lakini Kamili kwa Utumishi wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Useja—Mlango Uelekeao Kwenye Utendaji Pasipo Kukengeushwa Fikira
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Waseja Ambao Hupata Uradhi Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 6/15 kur. 28-31

Useja Katika Nyakati Ngumu za Kiuchumi

“NILITAKA kuoa nilipokuwa na umri wa miaka 25,” akasema Chuks, aishiye Afrika Magharibi. “Nilikuwa na msichana fulani akilini, naye alikuwa akipendezwa nami. Tatizo lilikuwa pesa. Baba yangu na ndugu yangu mkubwa hawakuwa na kazi, na ndugu na dada zangu wadogo walikuwa shuleni. Kila mmoja katika familia alinitegemea. Halafu, kufanya mambo yawe mabaya zaidi, wazazi wangu wakawa wagonjwa, na hilo likamaanisha kutafuta pesa za ziada kulipia gharama ya tiba.”

Chuks, aliye Shahidi wa Yehova, hakutaka kuingia katika ndoa akiwa hawezi kutunza mke. Alijali maneno ya Paulo yapatikanayo kwenye 1 Timotheo 5:8: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”

“Nilifanya kazi kwa bidii,” Chuks akaendelea, “lakini daima pesa hazikutosha. Kama tokeo, mipango yetu ya ndoa ilibidi iahirishwe kila mara. Mwishowe nikapokea barua kutoka kwa msichana huyo ikisema kwamba mtu mwingine amemwendea baba yake na kuuliza ikiwa anaweza kumwoa. Baba huyo alikubali. Siku chache baada ya barua yake kufika, familia hiyo ikafanya sherehe ya uchumba.”

Kama vile Chuks, wanaume wengi Wakristo wameona mipango yao ya ndoa ikivunjika au kucheleweshwa kwa sababu ya hali mbaya za kiuchumi. Katika nchi nyingi kuna ongezeko kubwa sana la gharama ya maisha. Kwa mfano, katika nchi moja ya Afrika ya kati, bei ya vitu ilipanda kwa asilimia 8,319 katika mwaka mmoja! Katika nchi fulani ni vigumu kupata kazi ya kuajiriwa. Pia, mara nyingi, mishahara ni midogo sana hivi kwamba ni vigumu kwa mtu kujisimamia, asiweze kutunza mke na watoto. Kijana mmoja mwanamume katika Nigeria aliomboleza kwamba kazi ya wakati wote aliyopewa katika kiwanda kimoja ingemlipa dola 17 tu kila mwezi—hizo zikiwa chache kuliko gharama ya kila mwezi ya kulipia basi kwenda na kurudi kutoka mahali pa kazi!

Wanawake wengi Wakristo walio waseja pia wanapata kwamba magumu ya kiuchumi yanaharibu mipango yao ya ndoa. Mara nyingi lazima wafanye kazi kusaidia washiriki wa familia. Wanaume fulani waseja, waonapo hali hiyo, hukawia kuoa, wakitambua kwamba mwanamume aoaye chini ya hali kama hizo angehitaji kupata mshahara wa kutosha ili ategemeze si mke tu bali pia familia ya mkeye. Ayo, mhitimu wa chuo kikuu, hung’ang’ana kujisaidia, kusaidia mama yake, na ndugu na dada zake wachanga. “Nataka kuolewa,” yeye aomboleza, “lakini wengine wajapo na kuona trela yangu ndefu [madaraka ya kifedha], wao huniacha.”

Yajapokuwa matatizo ya kiuchumi, Wakristo wengi waseja hujipata wakisongwa na watu wa ukoo na wengineo waoe na kupata watoto. Nyakati nyingine msongo huo huwa aina fulani ya dhihaka. Kwa mfano, katika sehemu fulani za Afrika, ni desturi wakati unaposalimia mtu mzima kuuliza hali njema ya mke au mume wake na watoto. Nyakati nyingine, salamu kama hizo hutumiwa kudhihaki watu wasiooa. John, aliye katika umri wake wa miaka ya mwishoni-mwishoni mwa 40, asema hivi: “Watu wanichezeapo na kusema, ‘Habari za mke wako?,’ mimi hujibu, ‘Anakuja.’ Ukweli ni kwamba, nawezaje kuoa mke nikiwa siwezi kumtunza?”

Kuhusu John na wengine wengi walio kama yeye, hali hiyo imejumlishwa na mithali hii ya Kiyoruba: “Kuoa haraka si kitu; bei ya chakula ndiyo tatizo.”

Fanya Yafaayo Zaidi kwa Hali Yako

Ni rahisi kama nini kuhuzunika tutamanipo kitu ambacho hakiji. Mithali 13:12 husema: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” Pengine hivi ndivyo wewe huhisi ikiwa unatamani kuoa lakini hujiwezi kifedha. Jambo hili huenda likawa kweli ikiwa wewe ni mmoja wa wale mtume Paulo alieleza kuwa wenye “kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9.

Kukabili hali hiyo huenda isiwe rahisi, lakini kuna mambo unayoweza kufanya uvumilie na hata upate shangwe katika hali yako. Yesu Kristo, mwanamume asiyeoa, aliandaa kanuni ya Biblia yenye kutumika inayoweza kukusaidia kushinda hali ya kukata tamaa inayoletwa na kukawia kwa kilichotarajiwa. Yeye alisema hivi: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.”—Matendo 20:35.

Unaweza kutumia shauri hili kwa kufanyia familia yako na wengine kutanikoni matendo mazuri. Pengine unaweza kuongeza utendaji wako katika huduma ya Kikristo. Ukijishughulisha kabisa na kutoa kusiko na ubinafsi, huenda ukapata kwamba unakuwa ‘umesimama kwa uthabiti wa moyo wako, bila sharti, lakini waweza kuyatawala mapenzi yako.’—1 Wakorintho 7:37.

Mwanamume mwingine asiyeoa, mtume Paulo, aliandika shauri hili lenye kusaidia: “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Wakristo wengi waseja wamepata ‘raha nafsini mwao’ kwa kutumia wakati wao kumkaribia Yehova zaidi kupitia sala, funzo la Neno la Mungu, na kushiriki katika mikutano ya Kikristo. (Mathayo 11:28-30) Ukifanya hivi, utaweza kukabili hali ngumu ya kiuchumi kwa mafanikio zaidi. Pia itakusaidia udhihirishe hali nzuri zaidi ya kiroho, ikikufanya mume au mke bora ikiwa mwishowe utakuja kuoa.

Usisahau kamwe kwamba Yehova hujali wale wote wamtumikiao. Yeye anajua matatizo na magumu unayopata. Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo pia anajua ni nini hatimaye kikufaacho kabisa, katika hali ya kiroho na ya kihisia-moyo. Ukitumia kwa saburi kanuni za Neno lake katika maisha yako ya kila siku, unaweza kuwa na hakika kwamba atatoa msaada wakati wake ufikapo na kutimiza mahitaji na tamaa yako kwa hali njema yako ya milele. Biblia huhakikisha kwamba: “BWANA . . . hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu.”—Zaburi 84:11.

Tazama Upande Ufaao wa Mambo

Pia, ukumbuke kwamba kuna faida hususa za kuwa mseja. Mtume Paulo aliandika hivi: “Aozaye ubikira wake afanya vema, lakini yeye asiyeuoza atafanya bora.”—1 Wakorintho 7:38, NW.

Kwa nini useja ni “bora” kuliko ndoa? Paulo aeleza hivi: “Yeye asiyeoa hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; bali yeye aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe. Tena iko tofauti hii kati ya mke na mwanamwali. Yeye asiyeolewa hujishughulisha na mambo ya Bwana, apate kuwa mtakatifu mwili na roho. Lakini yeye aliyeolewa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mumewe.”—1 Wakorintho 7:32-34.

Kwa maneno mengine, Wakristo waliooa wana haki ya kujali juu ya mahitaji, mapendezi, na mambo yasiyompendeza mwenzi wao wa ndoa. Lakini Wakristo waseja wanaweza kukazia fikira utumishi wa Yehova kwa uangalifu mwingi zaidi. Wakilinganishwa na wale waliooa, Wakristo waseja wako katika hali bora ya “kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine.”—1 Wakorintho 7:35.

Paulo hasemi kwamba Mkristo mseja hana mambo ya kumvuta fikira. Ikiwa umelemewa na matatizo ya kiuchumi, huenda ukahisi kwamba kuna mambo mengi ambayo hukutatiza yakikuondosha fikira kutoka hudumani. Hata hivyo, uhuru wa kibinafsi wa kumtumikia Mungu kwa kawaida huwa mwingi zaidi kwa mwanamume au mwanamke asiyeolewa kuliko ulivyo kwa wale walio katika ndoa.

Alipokuwa akipendekeza useja kuwa njia bora, mtume Paulo hakusema lilikuwa kosa kuoa. Yeye aliandika hivi: “Lakini, kama ukioa, huna hatia.” Hata hivyo, alitahadhari hivi: “Lakini watu kama hao [wenye kuoa] watakuwa na dhiki katika mwili.”—1 Wakorintho 7:28.

Yeye alimaanisha nini kwa kusema hivyo? Ndoa huleta masumbufu fulani. Katika nyakati ngumu za kiuchumi, dhiki kama hiyo huenda ikatia ndani hangaiko la baba kuhusu kutunza mahitaji ya mkeye na watoto wake. Ugonjwa pia unaweza kuleta mzigo mkubwa wa kifedha na wa kihisia-moyo kwa familia.

Kwa hiyo ingawa huenda usipendelee hali yako, huenda ukawa katika hali bora kuliko vile ungekuwa ikiwa ungekuwa umeoa na kuwa na daraka la kutunza watoto. Matatizo unayokabili sasa ni ya muda tu; yataondolewa katika mfumo mpya wa Mungu—na mengine labda hivi karibuni.—Linganisha Zaburi 145:16.

Je, Unaweza Kupanua Huduma Yako?

Ingawa si kila mtu awezaye kufanya hivyo, wengine wameweza kuingia katika utumishi wa wakati wote wajapokuwa na matatizo ya kiuchumi. Chuks, aliyetajwa awali, alifanya biashara ya kuuza vifaa vya ofisi ili asaidie familia yao. Karibu na wakati ambapo mipango yake ya ndoa ilivunjika, alipokea barua iliyomwalika kufanya kazi ya ujenzi kwa muda fulani katika ofisi ya tawi ya kwao ya Watch Tower Society. Akihangaikia pesa, ndugu yake mkubwa alimvunja moyo kutokwenda. Hata hivyo, Chuks akasababu kwamba Yehova alikuwa amemsaidia kusimamisha biashara yake ya kuuza vifaa vya ofisi, hivyo lazima aweke masilahi ya Ufalme kwanza na kutumaini katika uwezo wa Mungu wa uandalizi. (Mathayo 6:25-34) Isitoshe, akafikiri, ni kwa muda wa miezi mitatu tu.

Chuks alikubali mwaliko huo akamwachia ndugu yake biashara hiyo. Miaka sita baadaye, Chuks amebaki katika utumishi wa wakati wote, ni mzee katika kutaniko la Kikristo, na yuko tayari kifedha kuoa. Je, anasikitikia jinsi mambo yalivyotukia katika maisha yake? Chuks asema: “Nilihisi vibaya niliposhindwa kuoa wakati nilipotaka, lakini hali imerekebika kwa faida yangu. Nimepata aina nyingi za shangwe na mapendeleo ya utumishi ambayo huenda singeweza kufurahia kama ningalioa na kuwa na familia wakati huo.”

Usalama kwa Wakati Ujao

Katika nyakati ngumu wengi hutafuta usalama wa ndoa kama ulinzi dhidi ya magumu ya kifedha ya wakati ujao. Nchi fulani, zikiwa zimelemewa na mzigo wa deni, hutolea wazee-wazee msaada mdogo au hata hazitoi. Hivyo wazazi mara nyingi hutegemea familia zao, na hasa watoto wao, kuwasaidia katika umri wao wa uzeeni. Kama tokeo, wanaume na wanawake waseja mara nyingi wanasongwa waoe na kupata watoto, hata wakati hali yao ya kifedha si nzuri.

Lakini ndoa na kulea watoto hakuhakikishi usalama. Watoto fulani wa kilimwengu hawataki kusaidia wazazi wao walio wazee-wazee, wengine hawana uwezo, huku wengine wakifa kabla ya wazazi wao. Wakristo hasa hutafuta usalama mahali penginepo, wakijua ahadi hii ya Mungu: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”—Waebrania 13:5.

Wale walioahirisha ndoa ili watumikie Yehova wakati wote hawajaachwa. Christiana ni mseja mwenye umri wa miaka 32. Yeye ametumika akiwa painia wa kawaida katika Nigeria kwa miaka tisa iliyopita. Yeye asema hivi: “Mimi huweka tumaini langu katika Yehova, anayetuhakikishia kwamba hatawaacha kamwe watumishi wake. Ahadi yake ni tumaini langu. Yehova hunitunza kiroho na kifedha. Amethibitika kuwa Baba mkarimu. Kwa mfano, nilihama nikapainie katika eneo lililo na uhitaji mkubwa zaidi wa Mashahidi. Ingawa kuna vitu vichache vya kimwili, nimejifunza kukabili hali. Nilipolazwa hospitali kwa ajili ya homa kali ya vipindi, ndugu katika kutaniko letu la awali walinitembelea kunisaidia.

“Nimeridhika sana na utumishi wa wakati wote. Nauona kuwa pendeleo tukufu kufanya kazi pamoja na Muumba wa ulimwengu wote mzima pamoja na ndugu na dada wengi sana ulimwenguni pote. Naona wachanga wengi walioshindwa la kufanya na wasio na tumaini kwa sababu ya mambo yanayotendeka kuwazunguka. Kwangu, maisha yangu yana maana; ninatazamia mbele nikiwa na uhakika. Najua kwamba kuwa karibu na Yehova ndilo suluhisho bora zaidi kwa matatizo tunayokabili leo.”

Ikiwa unatamani kuoa lakini unashindwa kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi, uwe na moyo mkuu! Hauko peke yako. Kuna wengi wanaovumilia majaribu kama hayo kwa msaada wa Yehova. Fanya yafaayo zaidi kwa hali yako kwa kufanyia wengine mambo mazuri na kufanyia maendeleo hali yako ya kiroho. Mkaribie Mungu; yeye atakusaidia kwa sababu kwa kweli anakujali.—1 Petro 5:7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki