Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 8/15 kur. 12-17
  • Mwaliko Wenye Upendo kwa Wachovu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwaliko Wenye Upendo kwa Wachovu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wale ‘Wanaomenyeka na Kulemezwa Mizigo’
  • Kisababishi Chenyewe cha Magumu
  • Mwaliko wa Yesu Leo
  • Kitulizo na Burudisho
  • Mathayo 11:28-30—“Njoni Kwangu, . . . Nami Nitawapumzisha”
    Mistari ya Biblia Yafafanuliwa
  • ‘Kupata Burudisho la Nafsi Zenu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • “Njooni Kwangu, . . . Nami Nitawaburudisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 8/15 kur. 12-17

Mwaliko Wenye Upendo kwa Wachovu

“Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha.”—MATHAYO 11:28, NW.

1. Yesu aliona nini Galilaya katika safari yake ya tatu ya kuhubiri?

KARIBU na mwanzo wa mwaka wa 32 W.K., Yesu alikuwa katika ziara yake ya tatu ya kuhubiri katika wilaya ya Galilaya. Alisafiri kupitia majiji na vijiji, “akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu.” Alipokuwa akifanya hayo, aliona umati mwingi, naye “alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.”—Mathayo 9:35, 36, NW.

2. Yesu alisaidiaje watu?

2 Hata hivyo, Yesu alifanya zaidi ya kuhurumia tu umati. Baada ya kuagiza wanafunzi wake wasali kwa “Bwana wa mavuno,” Yehova Mungu, aliwatuma waende wasaidie watu. (Mathayo 9:38; 10:1) Kisha akawapa watu uhakikisho wake binafsi juu ya njia ya kupata kitulizo na faraja ya kweli. Aliwapa mwaliko huu wenye kuchangamsha moyo: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia ya upole na wa hali ya chini katika moyo, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:28, 29, NW.

3. Kwa nini mwaliko wa Yesu ni wenye kuvutia leo vilevile?

3 Leo twaishi katika wakati ambapo wengi huhisi wamelemezwa mizigo. (Warumi 8:22; 2 Timotheo 3:1) Kwa wengine, kupata riziki tu huchukua muda mwingi wa wakati wao na nishati zao hivi kwamba hawana wakati na nishati za kutosha kwa ajili ya familia zao, marafiki wao, au kwa jambo lolote. Wengi wamelemezwa mizigo ya magonjwa mabaya, taabu, mshuko wa moyo, na matatizo mengine ya kimwili na kihisia-moyo. Wakihisi mkazo, wengine hujaribu kupata kitulizo kwa kujiingiza kabisa katika ufuatiaji wa raha, kula, kunywa, na hata matumizi ya dawa za kulevya. Bila shaka hilo huwaingiza tu katika matatizo yasiyokoma, likiwaletea matatizo na mikazo zaidi. (Warumi 8:6) Kwa wazi, mwaliko wenye upendo wa Yesu waonekana kuwa wenye kuvutia leo vilevile kama ulivyovutia wakati ule.

4. Ni maswali yapi tunapaswa kufikiria ili kupata manufaa kutokana na mwaliko wenye upendo wa Yesu?

4 Hata hivyo, watu wa siku ya Yesu walikabili hali zipi, hivi kwamba walionekana kama “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku,” hata Yesu akasukumwa kuhisi sikitiko kwa ajili yao? Walilazimika kubeba mizigo gani, na mwaliko wa Yesu ungewasaidiaje? Majibu ya maswali haya yaweza kutusaidia sana katika kunufaika kutokana na mwaliko wenye upendo wa Yesu kwa wachovu.

Wale ‘Wanaomenyeka na Kulemezwa Mizigo’

5. Kwa nini ilifaa kwamba mtume Mathayo aliripoti juu ya tukio hili katika huduma ya Yesu?

5 Ni jambo la kupendeza kwamba ni Mathayo pekee aliyeripoti tukio hili katika huduma ya Yesu. Kwa sababu alikuwa amekuwa mkusanya-kodi, Mathayo, aliyeitwa pia Lawi, alijua vizuri mzigo fulani hasa ambao watu walikuwa wakibeba. (Mathayo 9:9; Marko 2:14) Kitabu Daily Life in the Time of Jesus chasema: “Kodi ambazo [Wayahudi] walilazimika kulipa kwa fedha na kwa vitu na utumishi zilikuwa nzito kwelikweli, nazo zilikuwa nzito hata zaidi kwa sababu kulikuwa na aina mbili za kodi zilizotozwa wakati uleule, kodi za umma na kodi za kidini; na hakuna ile iliyokuwa nyepesi kati ya kodi hizo.”

6. (a) Ni mfumo upi wa kutoza kodi uliotumiwa wakati wa Yesu? (b) Kwa nini wakusanya-kodi walikuwa na sifa mbaya sana hivyo? (c) Paulo alihisi uhitaji wa kukumbusha Wakristo wenzake juu ya nini?

6 Jambo lililofanya hizo zote kuwa hata mzigo zaidi ni mfumo uliotumiwa wakati huo wa kutoza kodi. Maofisa Waroma waliwapa watu ambao wangekusanya kodi nyingi zaidi haki za kukusanya kodi katika mikoa. Wao nao waliajiri watu katika jumuiya zao wasimamie kazi yenyewe ya kukusanya kodi. Kila mtu aliyekuwa katika mfumo huo wa kukusanya kodi alihisi ana haki ya kutoza malipo yake mwenyewe, au kutwaa sehemu yake. Kwa kielelezo, Luka alisimulia kwamba “palikuwa na mwanamume aitwaye Zakayo kwa jina; naye alikuwa mkusanya-kodi-mkuu, na alikuwa tajiri.” (Luka 19:2, NW) Inaonekana “mkusanya-kodi-mkuu” Zakayo na wale waliokuwa chini ya uangalizi wake walirundika mali zao kwa hasara ya watu. Mabaya na ufisadi ulioletwa na mfumo huo ulisababisha watu wawaweke wakusanya-kodi miongoni mwa watenda-dhambi na makahaba, na labda kwa kufaa katika hali nyingi. (Mathayo 9:10; 21:31, 32; Marko 2:15; Luka 7:34) Kwa kuwa watu walihisi mzigo ambao ulikuwa karibu usiweze kuvumilika, si ajabu kwamba mtume Paulo alihisi uhitaji wa kukumbusha Wakristo wenzake wasiudhike chini ya utawala wa Waroma bali ‘wawape wote haki zao; mtu wa kodi, kodi; mtu wa ushuru, ushuru.’—Warumi 13:7a; linganisha Luka 23:2.

7. Sheria za adhabu za Waroma ziliongezeaje mzigo wa watu?

7 Pia Paulo alikumbusha Wakristo kumpa “astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima.” (Warumi 13:7b) Waroma walijulikana kwa ukatili wao na ukali wa sheria zao za adhabu. Kuchapa mijeledi, kucharaza viboko, vifungo vikali vya gerezani, na ufishaji ulitumiwa mara nyingi ili watu watiishwe. (Luka 23:32, 33; Matendo 22:24, 25) Hata viongozi wa Kiyahudi walipewa mamlaka ya kutoza adhabu kama walivyoona inafaa. (Mathayo 10:17; Matendo 5:40) Hakika mfumo huo ulikuwa wenye kukandamiza sana, ikiwa haukuwa wenye ukatili kabisa, kwa mtu yeyote aliyekuwa raia wao.

8. Viongozi wa kidini walitwikaje watu mzigo?

8 Hata hivyo, mbaya zaidi kuliko kodi na sheria za Waroma, ulikuwa ni ule mzigo waliotwikwa watu wa kawaida na viongozi wa kidini wa siku hizo. Inaonekana kwamba hilo ndilo lilikuwa hangaiko kubwa la Yesu alipofafanua watu kuwa ‘wanamenyeka na kulemezwa mizigo.’ Yesu alisema kwamba badala ya kuwapa watu wa hali ya chini tumaini na amani, viongozi wa kidini “hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.” (Mathayo 23:4; Luka 11:46) Mtu hawezi kukosa kuona katika zile Gospeli jinsi viongozi wa kidini wanavyoonyeshwa kwa wazi—hasa waandishi na Mafarisayo—wakiwa kikundi chenye unafiki na kiburi, kisicho na huruma. Wao waliwadharau watu wa kawaida kuwa wasio na elimu na wasio safi, nao waliwadharau wageni waliokuwa miongoni mwao. Maelezo fulani juu ya mtazamo wao yasema hivi: “Siku hizi mtu anayemtwika farasi mzigo kupita kiasi anaweza kushtakiwa mbele ya sheria. Vipi juu ya mtu aliyetwika amri 613 kwa ‘watu wa kawaida’ ambao hawakupata mazoezi yoyote ya kidini; na kisha, kukosa kufanya jambo lolote kuwasaidia, akawashutumu kuwa watu wasiomcha Mungu?” Bila shaka, mzigo halisi haukuwa Sheria ya Kimusa bali ulikuwa yale mapokeo mengi sana yaliyotwikwa watu.

Kisababishi Chenyewe cha Magumu

9. Hali zilizokuwa miongoni mwa watu wa wakati wa Yesu zililinganaje na zile zilizokuwa katika siku za Mfalme Sulemani?

9 Nyakati nyingine mzigo wa kifedha kwa watu ulikuwa mzito sana, hivi kwamba kulikuwa na umaskini wenye kuenea pote. Waisraeli walikuwa lazima walipe kodi za kiasi zilizotajwa na Sheria ya Kimusa. Kisha wakati wa utawala wa Sulemani, watu waligharimia miradi ya kitaifa yenye gharama kubwa sana, kama vile kujenga hekalu na majengo mengine makubwa. (1 Wafalme 7:1-8; 9:17-19) Lakini, Biblia yatuambia kwamba watu walikuwa “wakila, na kunywa, na kufurahi. . . . Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Wafalme 4:20, 25) Ni nini ilitokeza tofauti hiyo?

10. Ni nini iliyotokeza hali ya Israeli kufikia karne ya kwanza?

10 Maadamu taifa hilo lilibaki likiwa imara kwa ajili ya ibada ya kweli, wao walifurahia upendeleo wa Yehova nao walibarikiwa kwa usalama na ufanisi wajapokuwa na matumizi mengi ya kitaifa. Hata hivyo, Yehova alionya kwamba ikiwa ‘wangeghairi, wakiacha kumfuata, wasizishike amri zake,’ wao wangepatwa na matokeo mabaya. Hata ‘Israeli lingekuwa mithali na neno la tusi katika mataifa yote.’ (1 Wafalme 9:6, 7) Mambo yakawa vivyo hivyo. Israeli lilikuja kuwa chini ya utawala wa kigeni, na ule uliokuwa wakati mmoja ufalme wenye utukufu uligeuzwa ukawa koloni tu. Hayo ni matokeo mabaya kama nini kwa sababu walipuuza madaraka yao ya kiroho!

11. Kwa nini Yesu alihisi kwamba watu “walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji”?

11 Haya yote yatusaidia kuelewa ni kwa nini Yesu alihisi kwamba watu aliowaona walikuwa “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku.” Hawa walikuwa Waisraeli, watu wa Yehova, ambao kwa ujumla walikuwa wakijaribu kuishi kulingana na sheria za Mungu na kuendeleza ibada yao kwa njia inayokubalika. Hata hivyo, wao walitumiwa vibaya na kudharauliwa si na wenye mamlaka ya kisiasa na kibiashara tu bali pia na viongozi wa kidini walioasi imani miongoni mwao. Wao walikuwa “kama kondoo wasio na mchungaji” kwa sababu hawakuwa na mtu yeyote wa kuwatunza au kuwatetea. Walihitaji msaada ili wakabili mambo halisi yaliyo magumu sana. Mwaliko wenye upendo na upole wa Yesu ulikuwa wa wakati unaofaa kama nini!

Mwaliko wa Yesu Leo

12. Watumishi wa Mungu na watu wengine wanyoofu huhisi mikazo gani leo?

12 Katika njia nyingi mambo yanafanana hivyo leo. Watu wanyoofu wanaojaribu kupata riziki kwa njia ya haki hupata mikazo na matakwa ya mfumo huu wenye ufisadi kuwa magumu sana kuvumilia. Hata wale ambao wameweka maisha zao wakfu kwa Yehova hawakosi kupatwa na mambo hayo. Ripoti zaonyesha kwamba baadhi ya watu miongoni mwa watumishi wa Yehova wanazidi kupata ugumu wa kutimiza madaraka yao yote, hata ingawa wanataka kufanya hivyo. Wao huhisi wamelemezwa mizigo na kuchoka sana. Wengine hata wanahisi kwamba ingekuwa kitulizo ikiwa wangetupilia mbali kila kitu na kupotelea mbali ili waweze kufikiria mambo upya. Je, umepata kuhisi hivyo? Je, unajua mtu aliye karibu nawe aliye katika hali hiyo? Ndiyo, mwaliko wa Yesu wenye kuchangamsha moyo una umaana mkubwa kwetu leo.

13. Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba Yesu aweza kutusaidia kupata faraja na burudisho?

13 Kabla ya Yesu kutoa mwaliko wake wenye upendo, yeye alisema: “Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.” (Mathayo 11:27) Kwa sababu ya uhusiano huu wa kipekee kati ya Yesu na Baba yake, tunahakikishiwa kwamba kwa kukubali mwaliko wa Yesu na kuwa wanafunzi wake, twaweza kuingia katika uhusiano wa karibu wa kibinafsi pamoja na Yehova, “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3; linganisha Yohana 14:6.) Kwa kuongezea, kwa kuwa ‘amekabidhiwa vyote,’ ni Yesu Kristo pekee aliye na uwezo na mamlaka ya kupunguza mizigo yetu. Mizigo ipi? Ile iliyotwikwa na mifumo yenye ufisadi ya kisiasa, kibiashara, na kidini, na vilevile ile iliyotwikwa na dhambi zetu na kutokamilika kwetu kulikorithiwa. Hilo ni wazo lenye kutia moyo na kufariji kama nini!

14. Yesu angeandaa burudisho kutokana na kumenyeka kupi?

14 Yesu aliendelea kusema hivi: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha.” (Mathayo 11:28, NW) Hakika Yesu hakuwa akipinga kazi ngumu, kwa kuwa mara nyingi aliwashauri wanafunzi wake wajikakamue katika kazi iliyobaki. (Luka 13:24) Lakini “kumenyeka” (“kazi ya taabu,” Kingdom Interlinear) kwadokeza wazo la kazi ngumu ya muda mrefu na yenye uchovu sana, mara nyingi bila matokeo ya kuistahili. Na “kulemezwa mizigo” kunadokeza wazo la kubeba mzigo unaoshinda wa kawaida. Tofauti iliyopo yaweza kulinganishwa na ile iliyopo kati ya mtu anayechimba hazina iliyositirika na yule anayechimba mitaro katika kambi ya kazi ngumu. Wote wanafanya kazi ngumu inayofanana. Kwa mmoja, kazi hiyo inafanywa kwa hamu nyingi, lakini kwa yule mwingine, ni kazi ngumu isiyopendeza na isiyokoma. Jambo linalotokeza tofauti ni kusudi la kazi hiyo au ukosefu wa kusudi la kazi hiyo.

15. (a) Ni maswali yapi tunayopaswa kujiuliza ikiwa tunahisi kwamba tunabeba mzigo mzito mabegani mwetu? (b) Nini laweza kusemwa kuwa chanzo cha mizigo yetu?

15 Je, wahisi kwamba ‘unamenyeka na kulemezwa mizigo,’ kwamba kuna mambo mengi sana yanayodai wakati wako na nishati zako? Je, mizigo unayobeba yaonekana kuwa mizito mno kwako? Ikiwa ndivyo, inaweza kusaidia kujiuliza, ‘Ninamenyekea nini? Ni mzigo wa aina gani ninaobeba?’ Kwa habari hii, mfafanuzi mmoja wa Biblia alionelea hivi zaidi ya miaka 80 iliyopita: “Tukifikiria mizigo ya maisha, hiyo hujigawanya katika sehemu mbili; twaweza kuiita yenye kujitwika wenyewe na isiyoepukika: ile inayotokezwa na matendo yetu, na ile isiyotokezwa na matendo yetu.” Kisha akaongezea: “Wengi wetu wangeshangaa, baada ya kujichunguza kabisa, kuona jinsi sehemu kubwa ya mizigo yetu yote ni yenye kujitwika.”

16. Ni mizigo gani tunaweza kujitwika bila hekima?

16 Ni ipi baadhi ya mizigo tuwezayo kujitwika wenyewe? Leo twaishi katika ulimwengu wenye ufuatiaji wa vitu vya kimwili, wenye kupenda anasa, na wenye kukosa adili. (2 Timotheo 3:1-5) Hata Wakristo waliojiweka wakfu wanakabili mkazo wa kujipatanisha na fashoni na mitindo ya maisha ya ulimwengu. Mtume Yohana aliandika juu ya ‘tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya maisha.’ (1 Yohana 2:16, NW) Hayo ni mavutano yenye nguvu yawezayo kutuathiri kwa urahisi. Imejulikana kwamba watu wengine wamekuwa tayari kujiingiza sana katika deni ili kufurahia anasa zaidi za kilimwengu au kudumisha aina fulani ya mtindo-maisha. Kisha wanapata kwamba ni lazima watumie muda mwingi sana kazini, au kufanya kazi kadhaa, ili wapate pesa za kulipa madeni yao.

17. Ni hali gani iwezayo kufanya iwe vigumu hata zaidi kubeba mzigo, na hali hiyo inaweza kusuluhishwaje?

17 Ingawa mtu aweza kusababu kwamba si vibaya kuwa na vitu fulani ambavyo wengine wanavyo au kufanya mambo fulani ambayo wengine wanafanya, ni muhimu kuchanganua ikiwa anaongezea mzigo wake isivyofaa. (1 Wakorintho 10:23) Kwa kuwa mtu aweza kubeba mzigo wa kiasi fulani tu, ni lazima kitu fulani kiondolewe ili kubeba mzigo mwingine. Mara nyingi, ni mambo muhimu kwa hali-njema yetu ya kiroho—funzo la Biblia la binafsi, kuhudhuria mikutano, na huduma ya shambani—ambayo huondolewa kwanza. Matokeo ni kukosa nguvu ya kiroho, ambayo pia hufanya iwe vigumu hata zaidi kubeba mzigo huo. Yesu Kristo alionya dhidi ya hatari hiyo aliposema: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo.” (Luka 21:34, 35; Waebrania 12:1) Ni vigumu kutambua mtego na kuuponyoka ikiwa mtu amelemezwa mizigo na kuchoka.

Kitulizo na Burudisho

18. Yesu alitolea wale waliomwendea nini?

18 Basi, kwa upendo, Yesu alitoa kitulizo: “Njoni kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha.” (Mathayo 11:28, NW) Maneno ‘burudisha’ hapa na “burudisho” katika mstari wa 29 yatokana na maneno ya Kigiriki yanayolingana na neno ambalo tafsiri ya Septuagint yatumia kutafsiri neno la Kiebrania la “sabato” au “kushika sabato.” (Kutoka 16:23) Hivyo, Yesu hakuahidi kwamba wale waliomwendea hawangekuwa na kazi ya kufanya, bali aliahidi kwamba angewaburudisha ili wawe tayari kwa ajili ya kazi waliyopaswa kufanya kwa kupatana na kusudi la Mungu.

19. Mtu anapataje ‘kumwendea Yesu’?

19 Lakini, mtu anapataje ‘kumwendea Yesu’? Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Ikiwa yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso na kunifuata kwa kuendelea.” (Mathayo 16:24, NW) Hivyo, kumwendea Yesu kwadokeza kunyenyekeza mapenzi ya mtu mwenyewe ili kufanya yale ya Mungu na Kristo, akikubali mzigo fulani wa daraka, na akifanya hivyo kwa kuendelea. Je, hayo yote ni yenye kudai mno? Je, gharama ni kubwa sana? Ebu tufikirie aliyoyasema Yesu baada ya kutoa mwaliko huo wenye upendo kwa wachovu.

Unaweza Kukumbuka?

◻ Watu katika siku ya Yesu walilemezwaje mizigo?

◻ Kisababishi chenyewe cha magumu ya watu kilikuwa nini?

◻ Tunaweza kujichanganuaje ikiwa tunahisi tumelemezwa mizigo sana?

◻ Ni mizigo gani tunayoweza kujitwika wenyewe bila hekima?

◻ Tunaweza kupokeaje burudisho ambalo Yesu aliahidi?

[Picha katika ukurasa wa15]

Ni ipi baadhi ya mizigo ambayo tunaweza kujitwika wenyewe?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 15]

Kwa hisani ya Bahamas Ministry of Tourism

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki