‘Kupata Burudisho la Nafsi Zenu’
“Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemewa na mizigo, . . . nyinyi mtapata burudisho la nafsi zenu. kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—MATHAYO 11:28-30, NW.
1, 2. Hali ya jamaa ya kibinadamu imekuwa nini kwa karne nyingi, na hii inatofautianaje na vile Mungu alivyokusudia hapo kwanza?
“TWAJUA ya kuwa viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” Hivyo ndivyo mwanamume mmoja alivyoandikia marafiki katika Roma karne kadhaa zilizopita. (Warumi 8:22) Katika miaka ya tangu wakati huo, uuguaji na umivu la jamaa ya kibinadamu kwa ujumla limezidi tu kuongezeka. Ubaguzi, umaskini, uhalifu, na njaa ni mambo ambayo yameumiza watu wengi sana kila mahali. Mfumo wa kiuchumi usio na haki hulazimisha mamilioni ya watu kutoka katika kazi zao na hata katika nyumba zao, na mavutano ya kishetani hubomoa jitihada za kulea watoto wafuate njia iwapasayo.
2 Lakini labda msiba ulio mkubwa zaidi hutukia wakati ugonjwa, maradhi, au uzee unapofyonza watu nguvu zao na kuwanyang’anya heshima yao wanapokuwa vizee vilivyobakia mifupa na ngozi tu. Umivu kali sana na mteseko uliopo, ambao mara nyingi huendelea kwa majuma, miezi, na nyakati nyingine hata miaka, hufanya mioyo iume na kusababisha machozi yatiririke kama mito. Loo, maelezo hayo ya maisha yahuzunishaje! Kuhusu shida kubwa ya mwanadamu, mfalme mmoja mwenye hekima wa zamani za kale alisema: “Siku zake zote ni masikitiko [umivu, NW], na kazi yake ni huzuni.” (Mhubiri 2:23; 4:1) Kwa uhakika maisha leo hayako kama vile Mungu alivyoyakusudia hapo kwanza!—Mwanzo 2:8, 9.
3. Mungu aliumba mwanadamu akiwa na uwezekano gani, na kwa sasa unatimizwaje kwa kadiri ndogo?
3 Yehova Mungu aliumba mwanadamu akiwa mkamilifu, akiwa na uwezekano wa kuona shangwe ya kweli maishani. (Kumbukumbu 32:4, 5) Ebu ufikirie ufurahishi wa kuonja mlo mzuri, kupumua hewa safi kwa njia yenye shangwe, au kuona machweo ya kupendeza sana! “Nimeiona shughuli ambayo Mungu amewapa wana wa aina ya binadamu ili washughulike humo,” akasema mfalme uyo huyo mwenye hekima zamani za kale. “Kila kitu yeye amekifanya kikiwa na umbo zuri katika wakati wacho. . . . Mimi nimepata kujua kwamba hakuna kitu chochote kilicho bora kwao kuliko kushangilia na kutenda wema wakati wa maisha ya mtu; na pia kwamba kila mwanadamu apaswe kula na kwa kweli anywe na kuona wema kwa ajili ya kazi yake yote ya bidii. Hiyo ni zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 3:10-13, NW.
4. (a) Kama ilivyoonyeshwa na matukio yaliyohusu Yesu, watu wengi sana wana hali gani ya kuhuzunisha? (b) Yesu alitoa mwaliko gani wa kuchangamsha moyo, na hii yatokeza maswali gani?
4 Hata hivyo, ni watu wachache kama nini wawezao kuonea shangwe vitu vyema ambavyo Mungu alitukusudia! Yesu Kristo alikuwa na habari kwamba aina ya binadamu ilikuwa katika hali ya kimaskini kabisa, ya kusikitikiwa sana. Biblia yasema, “wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake.” Lo, Yesu aliwahurumia wanyonge hao kwa huruma iliyoje! (Mathayo 9:36; 15:30) Katika pindi moja, aliwatolea mwaliko huu wenye kuchangamsha moyo: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha nyinyi. Bebeni nira yangu na kujifunza kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia pole na hali ya kujishusha katika moyo, na nyinyi mtapata burudisho la nafsi zenu.” (Mathayo 11:28, 29, NW) Kwa uhakika, haya ni maneno yenye kuvuvia tumaini! Lakini Yesu alikuwa akiongea juu ya burudisho gani? Nasi twaweza kulipataje?
Ukweli Ambao Huburudisha
5. Yesu alionyeshaje njia ya kupata uhuru wa kweli na burudisho la nafsi zetu?
5 Yesu alipohudhuria Sikukuu ya Tabenakulo (Mahema) karibu miezi sita kabla ya kifo chake, alionyesha njia ya kuwa huru na hivyo kupokea burudisho la kweli. Akiambia wale waliokuwa wamemwamini, yeye alisema: “Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:31, 32) Yesu alikuwa akiongea juu ya ukweli gani? Huo utatuweka huru kutoka kwenye nini? Wasikilizaje wake walikuwaje watumwa?
6. (a) Wapinzani wa kidini walitokeza ubishi gani, na kwa nini? (b) Sisi sote ni watumwa kwa njia gani?
6 Wapinzani wa kidini walimkatiza Yesu, wakikazania hivi: “Sisi ni wazao wa Abrahamu na hatujapata kamwe kuwa watumwa kwa mtu yeyote. Imekuwaje wewe wasema, ‘Nyinyi mtakuwa huru’?” Wapinzani hao Wayahudi walijivunia urithi wao. Hata ingawa taifa hilo lilikuwa limekuja chini ya utawala wa kigeni mara nyingi, Wayahudi walikataa kuitwa watumwa. Lakini Yesu alionyesha ni kwa njia gani walikuwa watumwa, akisema: “Kwa ukweli kabisa mimi nasema kwa nyinyi, Kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.” Ndiyo, wasikilizaji wake wote walikuwa ‘watendaji wa dhambi,’ hata kama vile sisi sote tulivyo leo. Hii ni kwa sababu sisi sote tumerithi dhambi kutoka kwa wazazi wetu wa asili. Lakini Yesu aliahidi hivi: “Mwana akiwaweka nyinyi huru, nyinyi mtakuwa huru kikweli.”—Yohana 8:33-36; Warumi 5:12, NW.
7. Uhuru wa kweli unaweza kupatikanaje, na ukweli ambao hutuweka huru ni nini?
7 Hivyo uhuru wa kweli waweza kupatikana kwa njia ya Mwana wa Mungu tu, Yesu Kristo, aliyetoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu ya ukombozi. Dhabihu hii ndiyo hutuweka huru kutoka kwenye dhambi inayoua, na kufanya iwezekane tuuonee shangwe uhai wa milele katika afya na furaha kamilifu katika ulimwengu mpya wa Mungu ulio na uadilifu. (Yohana 3:16; 1 Yohana 4:10) Kwa hiyo, ukweli ambao hutuweka huru ni ukweli ule unaohusu Yesu Kristo na fungu lake katika kutimiza makusudi ya Mungu. Ufalme, ambao Mfalme wao ni Kristo, ndio utakaotimiza penzi la Mungu kwa dunia, na kwa uendelevu Yesu alitoa ushuhuda kuhusu ukweli huu.—Yohana 18:37.
Jinsi Ukweli Huburudisha
8. Njia ambayo ukweli huandaa burudisho yaweza kutolewa kielezi jinsi gani?
8 Njia ambayo ukweli huandaa burudisho yaweza kutolewa kielezi na mwanamke ambaye ameambiwa ana namna fulani ya kansa yenye kuenea haraka sana. Mzigo wa kujua hivyo unaponda roho ya mwanamke huyo afikiriapo yale matokeo yenye maumivu mengi, yanayoweza kuvunja sana hisia zake. Hata hivyo, bila kuchelewa anaendea daktari mwingine na kufanyiwa michunguzo zaidi. Matokeo ya michunguzo hiyo yaonyeshapo kwamba uchunguzi wa kwanza ulikuwa na makosa au kwamba mwanamke huyo amepona kwa njia ya kustaajabisha, ebu wazia hisia ya kitulizo kizuri ajabu anachokuwa nacho. Nafsi yake inaburudikaje!
9. Yesu aliandaaje kitulizo kwa kufundisha watu ukweli?
9 Vivyo hivyo, Yesu alipokuja duniani, watu walikuwa wamelemewa na ile mifumo ya bure tu ya siku hiyo. Yesu alisema hivi kwa habari ya waandishi na Mafarisayo wenye madaraka: “Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.” (Mathayo 23:4; Marko 7:2-5) Kilikuwa kitulizo kilichoje Yesu alipowaandalia watu ukweli uliowaweka huru kutoka kwenye mapokeo hayo yenye kuwatumikisha! (Mathayo 15:1-9) Mambo si tofauti leo.
10. Watu wengi wamebeba mizigo gani yenye kuwanyang’anya furaha, na huenda mtu akahisije mizigo hii ikiondolewa kwa kujifunza ukweli?
10 Labda wewe ulikuwa mmoja ambaye aliishi kwa kutetemekea kuteswa motoni au katika pargatori baada ya kifo, kwa sababu ya ule mzigo mzito wa mafundisho bandia ya kidini. Au mpendwa alipokufa, huenda ukawa ulipondeka roho wakati kasisi alipokuambia kwamba Mungu amechukua mtoto kipenzi chako kwa sababu Yeye alihitaji malaika mwingine—kana kwamba Mungu ndiye aliyemhitaji mtoto wako kuliko wewe. Nyakati fulani makasisi huwaambia watu wenye ugonjwa fulani mkubwa kwamba hii ni laana kutoka kwa Mungu. Je! haiburudishi kweli kweli kujifunza kweli za Biblia ambazo huondolea mtu maneno hayo ya ubandia wa kidini wenye kulemea? Hii huleta hisia ya kitulizo kilichoje!—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4; Yohana 9:2, 3.
11. (a) Mmoja wa mizigo iliyo mikubwa zaidi ni nini, nao unaweza kuondolewaje? (b) Ni burudisho gani ambalo Yesu aliwaletea watenda dhambi alipokuwa duniani?
11 Mmoja wa mizigo mikubwa zaidi ambayo mtu aweza kubeba ni ule wa kuwa na hatia kwa sababu ya dhambi ambazo tumetenda. Inatuliza kujua kwamba dhambi hizi zinaweza kuondolewa kwa sababu ya ustahili wa dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Biblia yatuhakikishia kwamba, ‘Damu yake Yesu yatusafisha dhambi yote.’ (1 Yohana 1:7) Tujapokuwa tumefanya mabaya yoyote makubwa sana, ikiwa tumetubu kweli kweli na kutengeneza njia zetu, twaweza kuonea shangwe kitulizo chenye burudisho la kuwa na dhamiri safi na uhakikishio wa kwamba Mungu hatakumbuka tena dhambi zetu. (Zaburi 103:8-14; 1 Wakorintho 6:9-11; Waebrania 10:21, 22) Kristo aliwaburudisha kama nini wenye kulemewa na mzigo wa dhambi, kama vile makahaba na wakusanya-kodi kama Zakayo! Yesu aliwafariji kwa kweli za Biblia alipokuwa akila pamoja nao.—Luka 5:27-32; 7:36-50; 19:1-10.
12. (a) Yesu aliwaletea burudisho watu waliokuwa katika hali gani zenye kutaabisha sana? (b) Katika karne ya kwanza, Yesu alionyesha nani kwa njia ya kutazamisha sana kwamba yeye ndiye “njia na ukweli na uhai”?
12 Watu wengine wengi hubeba mizigo mizito ya ugonjwa na maradhi, kushuka moyo vikali, na kihoro kingi ajabu kinacholetwa na kifo cha mpendwa. Hata hivyo, Yesu aliwaletea burudisho wote hao waliokuwa ‘wakimenyeka na kulemewa na mizigo.’ (Mathayo 4:24; 11:28, 29, NW) Aliponya mwanamke mmoja aliyekuwa ametafuta msaada kwa watabibu kwa miaka 18 asipate mafanikio. Yesu aliponya mwanamume mmoja pia aliyekuwa amekuwa mgonjwa kwa miaka 38, na mwingine aliyekuwa amezaliwa kipofu. Je! waweza kuwazia kitulizo walichopata walipoponywa na Yesu? (Luka 13:10-17; Yohana 5:5-9; 9:1-7) Uhakika ni kwamba wote wale waliomjia Yesu kwa imani walikuja kwenye chanzo cha ukweli, burudisho halisi, na uhai. Kwa yule mjane aliyepokea mwanaye pekee kutoka kwa wafu na kwa wale wazazi ambao walirudishiwa binti yao wa miaka 12 akiwa hai, Yesu alithibitisha kwa njia yenye kutazamisha kweli kweli kwamba yeye ndiye “njia na ukweli na uhai.”—Yohana 14:6, NW; 17:3; Luka 7:11-17; 8:49-56.
13. Yesu alitufundisha kugeukia nani ili tupate msaada, na ni nini hutokea tutumiapo shauri lake?
13 Bila shaka kuna nyakati ambapo wewe hukabiliwa na matatizo makubwa usiyoyaweza binafsi. Yesu alitufundisha kumgeukia Yehova tupate msaada, hata kama vile yeye mwenyewe alivyofanya. (Luka 22:41-44; Waebrania 5:7) Tukimgeukia Mungu katika sala kwa ukawaida, twashiriki hisia za mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Na ahimidiwe Bwana [Yehova, NW], siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; Mungu ndiye wokovu wetu.” (Zaburi 55:22; 68:19) Ndiyo, kuujua ukweli huleta burudisho kweli kweli. Hutuvuta karibu zaidi na Yehova na kutusaidia tuthamini kwamba tukiwa na msaada wake yawezekana kushughulikia hata hali zilizo ngumu zaidi maishani.
Twaburudishwa na Tumaini la Ufalme
14. Ni nini kilichotegemeza Yesu katika majaribu yake, na ni kitu gani cha muhimu ili tupate burudisho la nafsi zetu?
14 Ili tupate burudisho la kweli kwa nafsi zetu, ni lazima tuwe na tumaini imara. Tumaini ndilo lililomtegemeza Yesu. Biblia yasema hivi: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake yeye alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kulia wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:2, NW) Tumaini lenye shangwe ambalo lilimtegemeza Yesu ni lile la kuchangia kutakaswa kwa jina la Baba yake kwa kushika ukamilifu, na pia la kujithibitisha kuwa anastahiki kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kudumisha mwono wazi wa tumaini letu, tukiwa mtawala mwenzi wa Kristo mbinguni ama mmoja wa raia zake wenye kuishi katika dunia Paradiso, kutatutegemeza sisi pia katika utumishi wa Mungu. Kweli kweli, tumaini hilo ni muhimu ili kupata burudisho la nafsi zetu.—Warumi 12:12.
15. Maisha yetu yana matazamio gani bila tumaini la Ufalme?
15 Fikiria ni matazamio gani ya maisha ambayo tungekuwa nayo bila tumaini la Ufalme. Urefu wa maisha asilia ni miaka 70 tu au yawezekana 80. Na siku hizo hupita mbio sana, kama vile atakavyokuambia mtu yeyote anayeendelea kupata umri! Ndiyo, Biblia yasema kwa ukweli hivi kuhusu maisha: ‘Hupita upesi tukatokomea mara.’ (Zaburi 90:10) Hata hivyo, sisi twataka siku zetu ziendelee. Twataka kuishi. Kuna mengi sana ya kufanya na kuonea shangwe.
16. Twahitaji kufanya nini ili tupate burudisho la nafsi zetu?
16 Kwa hiyo, ni muhimu kama nini kwamba tumjie kwa imani “Kristo Yesu, tumaini letu”! (1 Timotheo 1:1, NW) Kama yeye alivyosema: “Hili ndilo penzi la Baba yangu, kwamba kila mmoja ambaye huona Mwana na hujizoeza imani katika yeye apaswe kuwa na uhai wa milele.” (Yohana 6:40, 51, NW) Je! sisi twaamini hilo? Ili tupate burudisho la nafsi zetu, ni lazima tuamini hivyo kabisa. Hatuwezi kufanikiwa bila imani. Kweli kweli, ni lazima tuvae “tumaini letu la wokovu kama kofia ya chuma.” (1 Wathesalonike 5:8, HNWW; linganisha Waebrania 6:19.) Ni lazima tumaini hilo lilinde akili yetu, kufikiri kwetu. Ama sivyo, tutalemewa sana na mizigo na taabu hata tuchoke na kupoteza uhai wa milele. Kwa hiyo, ili ulionee shangwe burudisho la nafsi yako, hakikisha kuliweka tumaini lako la Ufalme likiwa imara.
Burudisho kwa Kufanya Kazi ya Mungu
17. (a) Ni jambo gani linalotakwa ili kupata burudisho, na kwa nini hilo si takwa la kupita kiasi kwetu? (b) Kukubali nira ya Kristo kunahusisha nini?
17 Lakini mengi zaidi ya kumjia Yesu tu yanatakiwa ili kupata burudisho. Yeye aliongezea hivi: “Bebeni nira yangu [au, “Ingieni chini ya nira yangu pamoja nami”] na kujifunza kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia pole na hali ya kujishusha katika moyo, na nyinyi mtapata burudisho la nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:29, 30, NW) Kubeba nira humaanisha kazi. Lakini angalia kwamba Yesu hatuombi tubebe nira hiyo na kuifanya kazi yote tukiwa peke yetu. Sisi twapaswa kwenda chini ya nira hiyo pamoja naye. Katika kisa hiki, kuikubali nira ambayo Kristo anatoa kwahusisha kujiweka wakfu kwa Mungu, kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji, halafu kutwaa daraka la kuwa mwanafunzi wa Kristo. Lakini nira hiyo ya uanafunzi yaweza kuletaje burudisho?
18. (a) Kwa nini kukubali nira ya Kristo huleta burudisho? (b) Kazi ya kuhubiri yatuleteaje shangwe na burudisho?
18 Kukubali nira ya Kristo huleta burudisho kwa sababu Yesu ni mwenye tabia pole na hali ya kujishusha moyoni. Kwa kuwa yeye hatazamii mambo ya kupita kiasi, inaburudisha kufanya kazi pamoja naye chini ya nira ile ile. Yeye hufikiria mapungukiwa yetu na udhaifu mbalimbali. Kama alivyosema, “Nira yangu ni ya fadhili.” Ni kweli kwamba nira ya uanafunzi yahusisha kazi, kazi ile ile ya kuhubiri na kufundisha ambayo Yesu alifanya na kuzoeza wafuasi wake wa mapema waifanye. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Hata hivyo, ni kazi yenye kuburudisha kama nini kuambia wengine juu ya Mungu wetu mwenye upendo, Mwana wake, na Ufalme! Inaburudisha kama nini kuambia watu jinsi wanavyoweza kuishi milele katika Paradiso! Nao wanapoitikia ujumbe wa Ufalme wenye kutolea watu uhai, na kujiunga nasi katika kumtumikia Yehova Mungu, shangwe yetu huwa kubwa kama nini!—1 Timotheo 4:16.
19. Kwa nini shauri lililotolewa na baba-mkwe wa Musa linastahiki kuangaliwa na wazee wa kundi leo?
19 Katika miaka ya majuzi, mamilioni ya watu wamekuja kwenye tengenezo la Yehova nao wahitaji msaada katika kukubali nira ya Kristo, na hii yaongezea mzigo wa kazi wa wapiga mbiu ya Ufalme na wale wenye kuwachunga. Wachungaji hao wa kiroho wanastahiki kuangalia shauri ambalo mnabii Musa alipokea kutoka kwa baba-mkwe wake. Yeye alimpa Musa ushauri huu: “Jambo hili ufanyalo si jema. Huna budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni zito mno kwako; huwezi wewe kulitenda peke yako.” Kwa hiyo akamshauri Musa achague wanaume wengine hodari waishiriki kazi ya kuwachunga watu. Ushauri huu ulithibitika kuwa wenye mafanikio ulipofuatwa. (Kutoka 18:17-27) Leo, mazoezi ya uendelevu yatatokeza wanaume wengi wenye uwezo, “zawadi katika wanaume,” wawezao kushiriki kuchunga kundi la kondoo ili wazee wa kundi wasidhoofike.—Waefeso 4:8, 16, NW.
20. Yesu Kristo na Baba yake hutaka nini kwetu?
20 Ingawa Kristo alihimiza wafuasi wake wajitahidi sana, wala yeye wala Baba yake hakutaka kwamba watu wowote kati yetu wafanye mambo ya kupita kiasi. Wakati mmoja, watu fulani walipomchambua Mariamu dada ya Lazaro kwa jitihada alizomfanyia Yesu, yeye aliwakaripia, akisema: “Mwacheni . . . ametenda alivyoweza.” (Marko 14:6-8; Luka 13:24) Na hilo tu ndilo linalotazamiwa kwetu—kufanya tuwezalo. Utendaji huo wa Kikristo si mzigo bali ni burudisho. Kwa nini? Kwa sababu huleta uradhi wa kweli sasa na tumaini hakika la kupata manufaa za milele wakati ujao.
21. (a) Ni nini mzigo mwepesi wa Kristo, na mara nyingi ni nini hufanya kazi ya kuhubiri iwe ngumu? (b) Twapaswa kuwa na azimio gani imara, na tukiwa na tazamio gani hakika?
21 Ni kweli kwamba Shetani atahakikisha tunanyanyaswa, hata kama vile mwananira mwenzetu, Yesu Kristo, alivyonyanyaswa. (Yohana 15:20; 2 Timotheo 3:12) Lakini kumbuka kwamba kinacholemea si ule mzigo mwepesi wa Kristo. Bali, upinzani wa Sheta-ni na mawakili wake ndio hufanya kazi yetu iwe ngumu mara nyingi. Mzigo wa Kristo ni wa kuishi kulingana na matakwa ya Mungu tu, nayo hayalemei. (1 Yohana 5:3) Basi, sisi na tuendelee kukaa chini ya nira ya Yesu Kristo pamoja naye, tukijitahidi sana katika kazi ya kuhubiri na kufundisha, hata kama vile yeye alivyofanya. Kama alivyoahidi, kwa kufanya hivyo ‘tutapata burudisho la nafsi zetu.’
Wewe Ungejibuje?
◻ Kulingana na Warumi 8:22, hali ya aina ya binadamu imekuwaje?
◻ Kuujua ukweli huleta burudisho kwa njia gani mbalimbali?
◻ Kwa nini tumaini la Ufalme linaburudisha sana?
◻ Nira ya Yesu ni nini, na kwa nini ni ya fadhili?
◻ Ni kubeba mzigo gani kutatuletea burudisho?