Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 8/15 kur. 17-22
  • “Nira Yangu ni ya Fadhili na Mzigo Wangu ni Mwepesi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nira Yangu ni ya Fadhili na Mzigo Wangu ni Mwepesi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nira ya Fadhili
  • Mzigo Mwepesi
  • “Burudisho kwa Ajili ya Nafsi Zenu”
  • ‘Kupata Burudisho la Nafsi Zenu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Yesu Aliwaburudisha Watu
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2018
  • Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • “Njooni Kwangu, . . . Nami Nitawaburudisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 8/15 kur. 17-22

“Nira Yangu ni ya Fadhili na Mzigo Wangu ni Mwepesi”

“Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu.”—MATHAYO 11:29, NW.

1, 2. (a) Ni ono gani umepata maishani linalokupa burudisho? (b) Ni lazima mtu afanye nini ili apate burudisho aliloahidi Yesu?

KUOGA kwa maji baridi mwishoni mwa siku yenye joto na jasho jingi, au kulala usingizi mnono baada ya safari ndefu yenye kuchosha—huburudisha kama nini! Ndivyo tunavyohisi tunapoondolewa mzigo mzito au tunaposamehewa dhambi na ukiukaji wa sheria. (Mithali 25:25; Matendo 3:19) Burudisho linaloletwa na maono hayo yenye kufariji hutuhuisha, nasi huimarishwa kusonga mbele.

2 Wote wanaohisi wamelemewa mzigo na kuchoka waweza kuja kwa Yesu, kwa sababu aliwaahidi jambo lilelile—burudisho. Hata hivyo, ili kupata burudisho linalotamaniwa sana, ni lazima mtu awe tayari kufanya jambo fulani. “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu,” akasema Yesu, “nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mathayo 11:29, NW) Nira hii ni nini? Nayo inaletaje burudisho?

Nira ya Fadhili

3. (a) Ni aina zipi za nira zilizotumiwa katika nyakati za Biblia? (b) Ni maana gani ya mfano unaohusishwa na nira?

3 Kwa kuwa aliishi katika jamii ya kilimo, Yesu pamoja na wasikilizaji wake walifahamu vizuri nira. Kwa msingi, nira ni boriti ndefu ya mti yenye nafasi mbili upande wa chini zinazotoshea shingo za wanyama wawili wa kufanya kazi, kwa kawaida ng’ombe ndume, ili kuwaweka pamoja wavute jembe, mkokoteni, au mzigo mwingine wowote. (1 Samweli 6:7) Nira za wanadamu zilitumiwa pia. Hizo zilikuwa boriti sahili au fito zilizobebwa mabegani huku mizigo ikiwa imewekwa kwa kila upande. Wakizitumia, wafanyakazi wangeweza kubeba mizigo mizito. (Yeremia 27:2; 28:10, 13) Kwa kushirikishwa sana na mizigo na kazi ngumu, mara nyingi nira hutumiwa kwa njia ya mfano katika Biblia kuwa ishara ya utawala na udhibiti.—Kumbukumbu la Torati 28:48; 1 Wafalme 12:4; Matendo 15:10.

4. Ni nini inayofananishwa na nira ambayo Yesu atolea wale wanaomjia?

4 Basi, ni nini ile nira ambayo Yesu aliambia wale wanaomjia ili kupata burudisho wachukue juu yao? Kumbuka kwamba alisema: “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu.” (Mathayo 11:29, NW) Mtu anayejifunza ni mwanafunzi. Hivyo, kuchukua nira ya Yesu kwamaanisha tu kuwa mwanafunzi wake. (Wafilipi 4:3) Hata hivyo, kufanya hivyo kwahitaji mambo mengi zaidi ya kutambua tu kiakili mafundisho yake. Kwahitaji matendo yanayopatana nayo—kufanya kazi aliyofanya na kuishi njia aliyoishi. (1 Wakorintho 11:1; 1 Petro 2:21) Kwahitaji unyenyekeo wa hiari kwa mamlaka yake na kwa wale ambao amewapa mamlaka. (Waefeso 5:21; Waebrania 13:17) Kwamaanisha kuja kuwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, ukikubali mapendeleo na madaraka yote yanayotokana na wakfu huo. Hiyo ndiyo nira ambayo Yesu atolea wale wote wanaomjia ili kupata faraja na burudisho. Je, u tayari kuikubali?—Yohana 8:31, 32.

5. Kwa nini si jambo gumu kuchukua nira ya Yesu?

5 Kupata burudisho kwa kuchukua nira—je, jambo hilo halipingani? Hasa hapana, kwa sababu Yesu alisema kwamba nira yake ni “ya fadhili.” Neno hilo lamaanisha upole, -a kupendeza, -enye kukubalika. (Mathayo 11:30; Luka 5:39; Warumi 2:4; 1 Petro 2:3) Akiwa seremala stadi, yaelekea sana Yesu alikuwa amepata kutengeneza majembe na nira, naye angejua namna ya kuirekebisha nira ili kazi ifanywe kwa kadiri iwezekanavyo na kwa ustarehe uwezekanao. Angeweza kuweka nguo au ngozi upande wa chini wa nira. Nira nyingi hufanywa hivyo ili zisisugue shingo kupita kiasi. Kwa njia iyo hiyo, nira ya mfano ambayo Yesu atutolea ni “ya fadhili.” Hata ingawa kuwa mwanafunzi wake kwahusisha matakwa na madaraka fulani, hali hiyo ya kuwa mwanafunzi haiwi na ukali au dhuluma bali inaburudisha. Amri za Baba yake wa Kimbingu, Yehova, vilevile si zenye kulemeza.—Kumbukumbu la Torati 30:11; 1 Yohana 5:3.

6. Huenda Yesu alimaanisha nini aliposema: “Chukueni nira yangu juu yenu”?

6 Kuna jambo jingine linalofanya nira ya Yesu iwe “ya fadhili,” au nyepesi kubeba. Aliposema: “Chukueni nira yangu juu yenu,” huenda alimaanisha jambo moja kati ya mawili. Ikiwa alikuwa akifikiria nira yenye sehemu mbili, yaani, ile aina ya kuunganisha pamoja wanyama wawili wa kufanya kazi ya kuvuta mzigo, basi alikuwa anatualika tuingie chini ya nira pamoja naye. Jambo hilo lingekuwa baraka kama nini—kuwa na Yesu kando yetu akivuta mzigo pamoja na sisi! Kwa upande mwingine, ikiwa Yesu alikuwa akifikiria boriti ya nira iliyokuwa ikitumiwa na mfanyakazi wa kawaida, basi alikuwa akitutolea njia ambayo ingefanya mzigo wowote ule tuliolazimika kubeba uwe mwepesi zaidi na rahisi kubeba. Iwe ilikuwa ni nira gani, nira yake ni chanzo cha burudisho kwelikweli kwa sababu anatuhakikishia hivi: “Kwa maana mimi ni mwenye tabia ya upole na wa hali ya chini katika moyo.”

7, 8. Ni kosa gani baadhi ya watu hufanya wanapohisi wana mkazo wa akili?

7 Basi, tufanye nini tukihisi kwamba mzigo wa matatizo ya maisha tunaobeba unazidi kuwa mzito zaidi na kwamba tunakazwa kufikia kikomo? Wengine wanaweza kufikiri kimakosa kwamba nira ya kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo ni ngumu sana au ni yenye kudai mno, ingawa ni shughuli za maisha ya kila siku zinazowalemeza. Watu fulani katika hali hiyo huacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo, au kuacha kushiriki katika huduma, wakihisi kwamba labda watapata kitulizo fulani. Lakini, hilo ni kosa baya sana.

8 Tunajua kwamba nira ambayo Yesu anatoa ni “ya fadhili.” Ikiwa hatukuibeba vizuri, inaweza kutusugua. Ikiwa ndivyo ilivyo tunapaswa kuchunguza zaidi nira tuliyobeba mabegani mwetu. Ikiwa, kwa sababu fulani, nira hiyo inahitaji kurekebishwa au haijawekwa vizuri, kuitumia haitahitaji tu jitihada zaidi kwa upande wetu bali pia itasababisha uchungu. Kwa maneno mengine, utendaji wa kitheokrasi ukianza kuonekana kama mzigo kwetu, ni lazima tuchunguze tuone ikiwa tunaushughulikia ifaavyo. Madhumuni yetu ya kufanya mambo tunayofanya ni nini? Je, sisi hujitayarisha vizuri tuendapo mikutanoni? Je, sisi hujitayarisha vizuri kimwili na kiroho tunapokuwa katika huduma ya shambani? Je, sisi hufurahia uhusiano wa karibu ulio mzuri pamoja na wengine katika kutaniko? Na zaidi ya yote, uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, ukoje?

9. Kwa nini nira ya Mkristo haipasi kamwe kuwa mzigo usioweza kubebeka?

9 Tukubalipo kwa moyo wote nira anayotutolea Yesu na kujifunza kuibeba ifaavyo, hakuna sababu yoyote kamwe inayoifanya ionekane kuwa mzigo usioweza kubebeka. Tukiweza kuweka picha hii akilini—Yesu akiwa chini ya nira pamoja na sisi—si vigumu kwetu kuona ni nani kwa kweli anabeba sehemu kubwa ya mzigo. Ni kama mtoto mdogo anayebatabata akiegemea kishikio cha kitembezi chake, akifikiri kwamba anakisukuma mbele, lakini kumbe ni mzazi anayekisukuma. Akiwa Baba mwenye upendo, Yehova Mungu ajua vema mipaka yetu na udhaifu wetu mbalimbali naye huitikia mahitaji yetu kupitia Yesu Kristo. ‘Mungu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu,’ akasema Paulo.—Wafilipi 4:19; linganisha Isaya 65:24.

10. Mtu anayechukua hali ya kuwa mwanafunzi kwa uzito hupata ono gani?

10 Wakristo wengi waliojiweka wakfu wamekuja kutambua jambo hilo kupitia maono yao ya binafsi. Kwa kielelezo, kuna Jenny, anayeona kwamba akitumikia akiwa painia-msaidizi kila mwezi na kufanya kwa wakati wote kazi ya kimwili yenye mikazo mingi humfanya awe na mkazo mkubwa wa akili. Lakini anahisi kwamba kazi ya upainia hasa humsaidia kudumisha usawaziko wake. Akisaidia watu kujifunza kweli ya Biblia na kuwaona wakibadili maisha zao ili wapate kibali cha Mungu—hilo ndilo humletea shangwe kuu katika maisha yake yenye shughuli nyingi. Anakubaliana kabisa na maneno ya mithali isemayo hivi: “Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—Mithali 10:22.

Mzigo Mwepesi

11, 12. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Mzigo wangu ni mwepesi”?

11 Kwa kuongezea ahadi yake ya nira “ya fadhili,” Yesu atuhakikishia hivi: “Mzigo wangu ni mwepesi.” Nira “ya fadhili” tayari inafanya kazi iwe rahisi; mzigo pia ukifanywa uwe mwepesi, hakika kazi inakuwa yenye raha. Lakini, Yesu alifikiria nini aliposema hayo?

12 Fikiria kile ambacho mkulima angefanya kama angetaka kubadili kazi ya wanyama wake, kwa mfano kuacha kulima shamba na kuanza kukokota mkokoteni. Kwanza angeondoa jembe kisha aunganishe mkokoteni. Ingeshangaza sana ikiwa angeunganisha jembe pamoja na mkokoteni kwa wanyama hao. Vilevile, Yesu hakuwa akiambia watu waweke mzigo wake juu ya ule ambao tayari walikuwa wakibeba. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Hakuna mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili.” (Luka 16:13) Hivyo, Yesu alikuwa akiwapa watu uchaguzi. Je, wangeendelea kubeba mzigo mzito waliokuwa nao, au wangeuweka chini na kukubali ule aliowatolea? Yesu aliwapa motisha hii yenye upendo: “Mzigo wangu ni mwepesi.”

13. Watu wa siku za Yesu walikuwa wakibeba mzigo gani, na kwa matokeo gani?

13 Katika siku za Yesu, watu walikuwa wakimenyana na mzigo mzito waliotwikwa na watawala Waroma wenye kudhulumu na viongozi wa kidini wenye kufuatia mambo madogo-madogo na wenye unafiki. (Mathayo 23:23) Katika jaribio la kuondosha mzigo wa Waroma, watu fulani walijaribu kujifanyia marekebisho wenyewe. Walijihusisha katika harakati za kisiasa, wakapatwa na misiba. (Matendo 5:36, 37) Wengine waliazimia kuboresha hali zao kwa kujiingiza sana katika miradi ya ufuatiaji wa vitu vya kimwili. (Mathayo 19:21, 22; Luka 14:18-20) Yesu alipowaonyesha njia ya kupata kitulizo kwa kuwaalika wawe wanafunzi wake, si wote walikuwa tayari kukubali. Wao walisita kuweka chini mzigo waliokuwa wakibeba, ingawa ulikuwa mzito kama nini, na kuchukua mzigo wa Yesu. (Luka 9:59-62) Hilo lilikuwa kosa lenye msiba kama nini!

14. Mahangaiko ya maisha na tamaa za vitu vya kimwili zinawezaje kutulemeza mzigo?

14 Tusipokuwa waangalifu, twaweza kufanya kosa hilo leo. Kuwa wanafunzi wa Yesu kwatuweka huru kutokana na kufuatia miradi na maadili yaleyale yanayofuatwa na watu wa ulimwengu. Ingawa bado ni lazima tuendelee kufanya kazi kwa bidii ili kupata riziki, hatufanyi mambo hayo kuwa jambo kuu la maisha zetu. Na bado, mahangaiko ya maisha na uvutio wa starehe inayoletwa na vitu vya kimwili waweza kutushika kwa nguvu sana. Tukiziruhusu, tamaa hizo zaweza hata kuondoa kweli ambayo tumekubali kwa shauku. (Mathayo 13:22) Twaweza kushughulikia mno kutimiza tamaa hizo hivi kwamba madaraka yetu ya Kikristo yawe matakwa yenye kuchosha tutake kuyapitia tu haraka iwezekanavyo. Hakika hatungeweza kutarajia kupata burudisho lolote kutokana na utumishi wetu kwa Mungu ikiwa unafanywa kwa roho hiyo.

15. Yesu alitoa onyo gani kuhusu tamaa ya vitu vya kimwili?

15 Yesu alitaja kwamba maisha ya uradhi hayaji kwa kufuatia kutimiza mahitaji yetu yote, bali kwa kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi maishani. “Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini,” akahimiza. “Maisha je! si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?” Kisha akaelekeza uangalifu kwa ndege wa mbinguni na kusema: “Hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao.” Akirejezea maua ya shambani, alisema: “Hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.”—Mathayo 6:25-29.

16. Maono yameonyesha nini kwa habari ya matokeo ya kufuatia vitu vya kimwili?

16 Je, twaweza kujifunza jambo lolote kwa somo hili la vitu vinavyoonekana? Ni jambo la kawaida kwamba kadiri mtu ajitahidivyo kuboresha hali yake ya maisha kiuchumi, ndivyo anavyozidi kujifunga katika miradi ya kilimwengu na ndivyo ule mzigo uwavyo mzito mabegani mwake. Ulimwengu umejaa wafanya biashara waliopatwa na hasara ya familia zilizovunjika, ndoa zilizoharibika, afya mbaya, na mengi zaidi kwa sababu ya ufanisi wao wa vitu vya kimwili. (Luka 9:25; 1 Timotheo 6:9, 10) Albert Einstein, aliyepata tuzo la Nobel, alisema hivi pindi moja: “Mali, ufanisi wa nje, umashuhuri, anasa—kwangu, siku zote vitu hivyo vimekuwa vya kudharaulika. Naamini kwamba njia ya maisha iliyo sahili na kiasi ndiyo bora zaidi kwa kila mtu.” Jambo hilo larudia tu shauri sahili la mtume Paulo: “Huo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji kimungu huu pamoja na ujitoshelevu.”—1 Timotheo 6:6, NW.

17. Biblia hupendekeza njia gani ya maisha?

17 Kuna jambo fulani muhimu hatutaki kupuuza. Ingawa “njia ya maisha iliyo sahili na kiasi” ina mafaa mengi, si hiyo yenyewe inayotokeza uradhi. Kuna wengi ambao njia yao ya maisha ni sahili kwa sababu ya kulazimishwa na hali, lakini hawana uradhi na furaha hata kidogo. Biblia haituhimizi tukatae furaha ya mambo ya kimwili na kuishi maisha ya utawa. Mkazo unatiliwa ujitoaji kimungu, si ujitoshelevu. Ni kwa kujumuisha zote mbili ndipo tunapopata ile “njia ya kupata faida kubwa.” Faida gani? Mbele kidogo katika barua hiyo, Paulo aeleza kwamba wale ‘wasioutumaini utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu’ watakuwa “wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Timotheo 6:17-19.

18. (a) Mtu anaweza kupataje burudisho la kweli? (b) Tuoneje mabadiliko ambayo huenda ikawa lazima tufanye?

18 Tutapata burudisho ikiwa tutajifunza kuweka chini mzigo wetu binafsi ulio mzito ambao huenda tunabeba na kuchukua mzigo mwepesi anaotutolea Yesu. Wengi ambao wamepanga upya maisha zao ili waweze kushiriki kikamilifu zaidi katika utumishi wa Ufalme wamepata njia ya maisha yenye furaha na uradhi. Bila shaka, imani na moyo mkuu wahitajika ili mtu afanye hivyo, na huenda kukawa na vizuizi njiani. Lakini Biblia yatukumbusha hivi: “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; naye ayatazamaye mawingu hatavuna.” (Mhubiri 11:4) Kwa kweli mambo mengi si magumu kama inavyofikiriwa ikiwa tumefanya maamuzi ya kuyafanya. Inaonekana kwamba sehemu ngumu zaidi ni kufikia uamuzi. Tunaweza kujichosha kwa kupambana na wazo hilo au kulipinga. Tukiimarisha akili zetu na kukubali mwito huo, tunaweza kushangaa kuona jinsi inavyogeuka kuwa baraka. Mtunga-zaburi alihimiza hivi: “Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema.”—Zaburi 34:8; 1 Petro 1:13.

“Burudisho kwa Ajili ya Nafsi Zenu”

19. (a) Tunaweza kutarajia nini hali ya ulimwengu izidipo kuwa mbaya zaidi? (b) Tukiwa chini ya nira ya Yesu, twahakikishiwa nini?

19 Mtume Paulo aliwakumbusha wanafunzi wa karne ya kwanza hivi: “Imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi.” (Matendo 14:22) Na bado hali ni hivyo leo. Hali za ulimwengu ziendeleapo kuwa mbaya, mikazo inayowajia wote ambao wameazimia kuishi maisha ya uadilifu na ujitoaji kimungu itakuwa mingi hata zaidi. (2 Timotheo 3:12; Ufunuo 13:16, 17) Na bado twahisi jinsi Paulo alivyohisi aliposema hivi: “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi.” Sababu ni kwamba twaweza kumtegemea Yesu Kristo atupe nguvu ipitayo ya kawaida. (2 Wakorintho 4:7-9) Kwa kukubali nira ya kuwa mwanafunzi kwa moyo wote, tutafurahia utimizo wa ahadi hii ya Yesu: “Nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:29, NW.

Je, Waweza Kueleza?

◻ Nira ya fadhili ambayo Yesu alitoa ilikuwa nini?

◻ Tufanye nini ikiwa tunahisi kwamba nira yetu inakuwa mzigo wenye kulemeza?

◻ Yesu alimaanisha nini aliposema: “Mzigo wangu ni mwepesi”?

◻ Tunaweza kuwaje na hakika kwamba mzigo wetu wabaki ukiwa mwepesi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki