“Chukueni Nira Yangu”
1 Katika ulimwengu wenye mikazo na mahangaiko mengi, tumepata kitulizo cha kweli kwa kukubali mwaliko wenye kuchangamsha wa Yesu wa kupata burudisho chini ya nira yake. (Mt. 11:29, 30) Kukubali nira ya kuwa wanafunzi kunatia ndani kufanya kazi fulani ambayo ni ngumu lakini yenye kuburudisha. Kunatia ndani kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwasaidia wengine wapate burudisho pamoja nasi chini ya nira ya Yesu yenye fadhili.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Huduma Inaburudisha: Yesu hakuwaomba wafuasi wake waongeze mzigo wake juu ya mzigo wao. Aliwaalika wachukue mzigo wake mwepesi badala ya kubeba mzigo wao mzito. Hatulemewi tena na mahangaiko na hali ya kukosa tumaini iliyopo katika mfumo huu wa mambo; wala hatujitahidi kupata utajiri usio hakika. (Luka 21:34; 1 Tim. 6:17) Hata ingawa tuna shughuli nyingi na ni lazima tufanye kazi ili tupate vitu vya msingi, jambo kuu maishani mwetu ni kumwabudu Mungu. (Mt. 6:33) Tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu mambo ya maana zaidi, hatutaona huduma kuwa mzigo mzito, bali sikuzote tutaiona kuwa yenye kuburudisha.—Flp. 1:10.
3 Kwa kawaida, tunapenda kuongea kuhusu jambo lolote lile tunalolipenda moyoni. (Luka 6:45) Wakristo wote wanampenda sana Yehova na baraka za Ufalme ambazo ameahidi. Hivyo, inaburudisha kama nini kuzungumza kuhusu “habari njema ya mambo mema” na kusahau mahangaiko yetu tunapokuwa katika huduma! (Rom. 10:15) Bila shaka, kadiri tunavyofanya jambo fulani, ndivyo tunavyopata ustadi zaidi na shangwe zaidi. Kwa hiyo, kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma, ikiwezekana, kutatuburudisha zaidi. Na tunatiwa moyo kama nini tunapoona watu wakikubali ujumbe tunaohubiri! (Mdo. 15:3) Hata watu wasipopendezwa au wakitupinga, tutapata burudisho la kiroho kutokana na huduma tukikumbuka kwamba jitihada zetu zinampendeza Yehova na kwamba matokeo yoyote mazuri tunayopata yanatokana na baraka zake.—Mdo. 5:41; 1 Kor. 3:9.
4 Tunapokubali mwaliko wa Yesu, tunafurahia pendeleo la kutumikia pamoja naye tukiwa Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10; Ufu. 1:5) Hakuna jambo linalotuburudisha zaidi kuliko hilo!