Barabara Pana Iliyo na Uhuru Kidogo
Familia ya watu watatu—baba, mama, na binti mdogo—walikuwa nyumbani katika Sydney, Australia, nyumba iliposhika moto. Walijaribu kuruka kupitia madirisha, lakini yalikuwa na vizuio. Kwa sababu ya vizuio hivyo vya usalama, wazima-moto hawangeweza kuwaokoa. Mama na baba walikufa kwenye moshi na moto. Binti akafa baadaye hospitalini.
NI HUZUNI kama nini kwamba familia hiyo ilikufa kwa sababu ya vizuio vya usalama vilivyokusudiwa kuwakinga! Inasikitisha kwamba nyakati zetu si familia hii pekee inayolinda nyumba yao kwa vizuio na makufuli ya usalama. Majirani walio wengi pia wana nyumba na ploti zenye kufanana na maboma. Kwa nini? Wanatafuta usalama na amani ya akili. Ni huzuni kama nini kwa jamii “huru” ambamo watu huhisi usalama wanapokuwa tu wamezingirwa kama wafungwa nyumbani mwao wenyewe! Katika idadi inayoongezeka ya ujirani, watoto hawawezi tena kucheza kwa usalama kwenye uwanja ulioko karibu au kutembea kwenda shule bila kuandamana na mzazi au mtu mzima mwingine. Katika sehemu nyingi za maisha, uhuru unapotea kama umande wa asubuhi.
Kigezo cha Maisha Kilichobadilika
Siku za wazazi wakuu wetu zilikuwa tofauti. Wakiwa watoto, kwa kawaida wangechezea walipopenda bila hofu. Wakiwa watu wazima, hawakusumbuka kwa makufuli na vizuio. Walihisi huru, na kwa kadiri fulani walikuwa huru. Lakini wazazi wakuu wetu wameona mwelekeo wa jamii ukibadilika muda wa maisha yao. Umebadilika ukawa wenye ubaridi, wenye ubinafsi zaidi; katika sehemu nyingi mahali pa upendo wa jirani pamechukuliwa na woga wa jirani, uliochangia tukio lenye msiba lililotajwa hapo juu. Pamoja na ukosefu huu unaoongezeka wa uhuru kumekuwa na hali ya maadili inayozidi kuzorota. Jamii imefurikwa na “adili mpya,” lakini kihalisi, hali imefikia hatua ambapo ni vigumu kuona adili iwayo yote.
Aliyekuwa mhadhiri wa elimu katika Chuo Kikuu cha Queensland, Dakt. Rupert Goodman, aandika hivi: “Sasa vijana wanaweza kuathiriwa na raha ya aina tofauti . . . mtindo-maisha ambamo ‘ubinafsi’ ndilo jambo kuu: kujiingiza bila kujizuia, kujiona, kujiona kuwa wanatimiza mambo, kujitafutia faida yao wenyewe.” Pia asema hivi: “Maadili kama vile kujidhibiti, kujikana, kazi ya bidii, kufanya kazi ifaavyo, kuheshimu mamlaka, upendo na heshima kwa wazazi . . . ni mawazo yasiyotambuliwa na wengi.”
Njia Pana Kwelikweli
Wale wafahamuo unabii wa Biblia hawashangazwi na kuongezeka huku kwa ubinafsi, kwa kuwa Yesu Kristo aliwaonya wasikilizaji wake hivi: “Mlango ni mpana, na njia [“barabara,” New World Translation] ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia [“barabara,” NW] imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.” (Mathayo 7:13, 14) Barabara ya kwanza, yenye mlango mpana kwa ajili ya wapitaji wengi, ni ‘pana’ kwa sababu haina vizuizi vya kanuni za Biblia zinazohusu adili na maisha ya kila siku. Inavutia wale wanaopenda kufikiri wanachotaka na kuishi kama wapendavyo—bila kanuni, bila masharti.
Kwa kweli, wengi waliochagua njia pana hudai kufurahia uhuru wao. Lakini wengi wao wanasukumwa na mwelekeo uleule mmoja wa ubinafsi. Biblia husema wanatawalwa na ‘roho ile itendayo kazi sasa katika wana wa kuasi.’ Roho hiyo huwasukuma kuishi ‘katika tamaa za miili yao, wakiyatimiza mapenzi ya mwili,’ yawe ni ukosefu wa adili, uzoefu wa dawa za kulevya, au ufuatiaji mno wa mali, umashuhuri, au uwezo.—Waefeso 2:2, 3.
Njia Pana Huongoza Kwenye Uangamivu
Ona kwamba wale wapitao kwenye njia pana wanasukumwa ili kufanya “mapenzi ya mwili.” Hili laonyesha kwamba hawako huru hata kidogo—wana bwana-mkubwa. Wao ni watumwa wa mwili. Na kumtumikia bwana-mkubwa huyu kwaweza kutokeza matatizo mengi—kusambaa kwa maradhi ya kupitishwa kingono, nyumba zilizogawanyika, miili na akili zilizo na ugonjwa kutokana na dawa za kulevya na ulevi, tukitaja machache tu. Hata matendo ya ujeuri, wizi, na kulala kinguvu hutokana na kufikiri kwa ubinafsi kunakoendelezwa na barabara hii yenye kuendekeza. Kwa kadiri ‘barabara hii iendayo upotevuni’ iendeleavyo kuwapo, matunda yayo yatazidi kuwa yenye kuumiza.—Mithali 1:22, 23; Wagalatia 5:19-21; 6:7.
Fikiria vielelezo viwili vya maisha halisi kutoka Australia.a Mary alishindwa na kishawishi, akizoea dawa za kulevya na vilevile kuingia katika ukosefu wa adili. Lakini furaha aliyotafuta ilimfumba. Hata baada ya kupata watoto wawili, maisha yake yalionekana kuwa matupu. Alitwezwa kabisa alipotambua alikuwa amepata UKIMWI.
Tom aliumia kwa njia tofauti. “Nilikulia katika misheni ya kanisa katika kaskazini mwa Queensland,” yeye aandika. “Nikiwa na umri wa miaka 16, nilianza kunywa pombe kupindukia. Baba yangu, wajomba, na marafiki wote walikuwa wanywaji pombe wa kupindukia, hivyo lilionekana kuwa jambo la kawaida kufanya. Nilifikia hatua ambapo ningekunywa chochote, kuanzia pombe hadi alkoholi isiyofaa kunywewa. Pia nikaanza kucheza kamari kwa mashindano ya farasi, mara nyingine nikipoteza mshahara wangu niliofanyia kazi kwa bidii. Huo haukuwa mshahara mdogo, kwa sababu kazi yangu ya kukata miwa ilikuwa yenye mshahara mzuri sana.
“Kisha nikaoa na tukapata watoto. Badala ya kuchukua madaraka yangu, nilifanya vile marafiki wangu walivyofanya—kunywa, kucheza kamari, na kupigana. Mara nyingi nilikuwa nikifungwa gerezani. Lakini hata hilo halikuwa na matokeo kwangu. Maisha yangu yalikuwa mabaya sana. Yalijaa matatizo.”
Ndiyo, kwa kukubali tamaa mbaya, Tom na Mary walijiumiza na kuumiza familia zao. Kwa kusikitisha, vijana wengine wengi hushawishwa na ile roho mbaya ya uhuru inayoendelea kutolewa na barabara pana. Ikiwa tu vijana wangetambua yale madanganyo ya uhuru huo. Ikiwa tu wangeona uhalisi wa njia pana—matokeo yenye uchungu ambayo wote wanaoiendea watapata mwishowe. Kweli, ni pana na nyepesi kuingia. Lakini upana wayo wenyewe ndio laana yayo. Mwendo wa hekima ni kufikiria kwa uzito uhakika usiopuuzika kwamba “yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu.”—Wagalatia 6:8.
Hata hivyo, kuna uchaguzi mzuri zaidi. Huo ni barabara nyembamba. Lakini barabara hiyo ni yenye makatazo kadiri gani, ni yenye kufinyana na nyembamba kadiri gani? Nayo yaelekea wapi?
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa.