Barabara Nyembamba Iendayo Kwenye Uhuru
NI WATU wachache wenye akili ambao hubisha kwamba ulimwengu wote mzima huendeshwa na sheria za asili. Sheria hizi huendesha kila kitu kuanzia atomi ndogo hadi galaksi zenye nguvu nyingi zilizo na mabilioni ya nyota. Kama hakungekuwa na sheria za asili, hakungekuwa na kupanga wala ufahamu; uhai wenyewe haungekuwapo. Kwa kufahamu sheria za asili na kufanya kazi pamoja nazo, mwanadamu ameweza kutimiza mambo makubwa ajabu, kama vile kutembea mwezini na kuleta picha za rangi kutoka kotekote duniani au hata kutoka nje ya anga la dunia hadi nyumbani mwetu kwenye viwambo vya televisheni.
Lakini vipi juu ya sheria za adili? Je, kuishi kulingana nazo ni kwenye faida na matokeo? Wengi huenda wakahisi kwamba hakuna sheria za adili na kuchagua falsafa au dini yenye kuendekeza inayopatana na tamaa zao wenyewe.
Hata hivyo, kuna wengine wachaguao njia nyingine, ‘njia nyembamba iendayo uzimani’ kama ionyeshwavyo katika Biblia. Hatupaswi kushangaa kwamba ni wachache tu wanaochagua njia hiyo, kwa kuwa Yesu alisema hivi juu ya njia nyembamba: “Waionao ni wachache.” (Mathayo 7:14) Kwa nini ni wachache tu?
Kwa sababu njia nyembamba ina mipaka ya sheria na kanuni za Mungu. Hiyo yaweza kuvutia tu mtu anayetamani kwa unyoofu kupatanisha maisha yake na viwango vya Mungu. Kinyume kabisa na barabara pana, inayotoa uhuru wa uwongo lakini kihalisi inaleta utumwa, barabara nyembamba, inayoonekana kuwa na mipaka, huweka mtu huru kwa kila jambo lifaalo. Mipaka yayo imewekwa na “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.”—Yakobo 1:25.
Jinsi Njia Nyembamba Huleta Uhuru
Kwa kweli, si rahisi sikuzote kukaa katika njia nyembamba. Kila binadamu aishiye si mkamilifu naye ana mwelekeo wa kurithiwa kuelekea kufanya kosa. Hivyo mtu huenda akawa na mwelekeo wa kwenda kombo kidogo. Hata hivyo, faida za kushikamana na ‘barabara yenye kufinyana’ zastahili nidhamu zozote na marekebisho yoyote yanayohitajiwa, kwa kuwa Mungu ‘hutufundisha ili tupate faida.’—Isaya 48:17; Warumi 3:23.
Kwa kielelezo: Wazazi wenye hekima huandaa lishe yenye mipaka kwa watoto wao. Hilo mara nyingine humaanisha wawe thabiti wakati wa chakula. Lakini watoto wakuapo, watathamini nidhamu yenye upendo ya wazazi wao. Wakiwa watu wazima, watakuwa wamesitawisha ladha ya chakula chenye afya. Na kwa sababu kuna chakula kingi mbalimbali chenye lishe bora hawatahisi kamwe kuwa wamewekewa mipaka.
Kwa njia ya kiroho, Mungu hufanya vivyo hivyo kwa wale walioko kwenye barabara nyembamba iendayo kwenye uhai. Yeye husitawisha ndani ya wapole tamaa zenye kujenga ziongozazo kwenye furaha na uhuru wa kweli. Yeye hufanya hilo kwa kuandaa Neno lake, Biblia. Kuongezea hilo, yeye hutualika tuombe roho yake itusaidie, naye hutuamuru tushiriki pamoja na Wakristo wenzetu, wanaoweza kututia moyo tudumu kwenye njia nyembamba. (Waebrania 10:24, 25) Ndiyo, Mungu ni upendo, nayo sifa hii kuu kuliko zote ni msingi wa mambo atakayotenda na njia zake zote.—1 Yohana 4:8.
Wakati upendo, amani, wema, kujidhibiti, na matunda mengineyo ya roho ya Mungu yatokezapo, barabara nyembamba haionekani ikiwa na mipaka. Kama vile andiko lisemavyo, “juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” (Wagalatia 5:22, 23) ‘Ilipo Roho ya Bwana, hapo ndipo penye uhuru.’ (2 Wakorintho 3:17) Hata sasa Wakristo wa kweli wanapata mwonjo wa uhuru huo. Wako huru kutokana na hofu ya aina nyingi inayodhuru watu leo, kama vile hofu juu ya wakati ujao na hofu ya kishirikina juu ya kifo. Ni jambo la kusisimua kama nini kufikiria wakati ujao ambapo “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari”! (Isaya 11:9) Kisha, hata hofu ya uhalifu haitakuwapo tena. Makufuli na vizuio vitakuwa vimeondolewa milele. Wote watahisi huru na salama—usiku na mchana, nyumbani na huko nje. Huo utakuwa uhuru kwelikweli!
Twahakikishiwa Msaada wa Mungu
Kwa kweli, kuishi kulingana na viwango vya Mungu huhitaji jitihada, hata hivyo “amri zake si nzito,” hata kwa binadamu wasiokamilika. (1 Yohana 5:3) Huku tukijipatanisha na njia nyembamba na kuhisi faida za kuitembelea, twasitawisha kutopenda matendo na kufikiri kwa wale walioko kwenye barabara pana. (Zaburi 97:10) Kutii sheria ya Mungu huvutia dhamiri tuliyopewa na Mungu. Badala ya “huzuni ya moyo” na “uchungu wa roho” unaopata wengi, Mungu huahidi: “Tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo.” Ndiyo, moyo uliozoezwa na Yehova ni wenye shangwe na huru.—Isaya 65:14.
Yesu alikufa ili afanye uhuru wa kweli upatikane kwetu. Biblia husema: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Sasa akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu, Yesu anatoa faida za dhabihu hiyo. Muda mfupi, baada ya “dhiki kuu,” wakati barabara pana na wale waiendeao watakapoharibiwa, kwa saburi ataanza kuongoza binadamu wenye utii kupita sehemu iliyobaki ya barabara nyembamba hadi mwisho wayo, ukamilifu wa kibinadamu. (Ufunuo 7:14-17; Mathayo 24:21, 29-31) Mwishowe tutaona kutimizwa kwa ahadi hii tukufu: “Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” Uhuru huo unaotolewa na Mungu hauwezi kulinganika. Hata kifo kitaondolewa.—Warumi 8:21; Ufunuo 21:3, 4.
Kwa kuona na kufahamu waziwazi mahali barabara nyembamba huongoza, mtu aweza kuchagua vizuri zaidi njia hii na kuitembea. Vijana hasa wanasaidiwa ili wasione mambo kwa ufupi na wasiudhiwe na yale wayaonayo kuwa mipaka inayowekwa na viwango vya Mungu. Wajifunze kuona hayo kuwa uthibitisho wa upendo wa Mungu na kinga dhidi ya maovu ya barabara pana. (Waebrania 12:5, 6) Bila shaka, mtu huhitaji saburi, akikumbuka kwamba inachukua muda kusitawisha sifa na tamaa za kimungu, kama vile ichukuavyo muda kwa mti kuzaa matunda mazuri. Lakini mti utazaa ikiwa utapaliliwa na kutiliwa maji.
Hivyo, jifunze Neno la Mungu, shiriki na Wakristo wengineo, na ‘kuomba bila kukoma’ kwa ajili ya roho takatifu. (1 Wathesalonike 5:17) Mtumaini Mungu akusaidie ‘kuyanyosha mapito yako.’ (Mithali 3:5, 6) Lakini je, hayo yote yanatumika? Je, kweli ni yenye faida? Ndiyo, yalifaidi Tom na vilevile Mary, waliotajwa kwenye makala iliyotangulia.
Waliacha Kupitia Barabara Pana
Tom aandika hivi: “Katika miaka ya kati ya 70, tulikutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipotutembelea. Mazungumzo yaliongoza kwenye funzo la Biblia. Nikaanza kurekebisha maisha yangu hatua kwa hatua. Nilibatizwa katika 1982 na sasa ninatumikia katika kutaniko la mahali petu. Mwana wetu pia sasa amebatizwa. Namshukuru mke wangu kwa kunivumilia kwa miaka yote hiyo kabla ya kujifunza kweli. Na zaidi ya yote namshukuru Yehova na Mwanaye, Kristo Yesu, kwa yote waliyotupa na kwa tumaini tulilo nalo sasa la wakati ujao.”
Na vipi juu ya Mary? Yeye alihisi kwamba Mungu hangemsamehe kamwe, lakini alitaka kujifunza juu yake kwa ajili ya watoto wake. Aliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifundisha jirani yake Biblia, yeye pia aliomba asaidiwe. Hata hivyo, mazoea yake mabaya yaliyomshika sana yalifanya maendeleo yawe magumu. Funzo hilo mara liliendelea mara lilikwama. Hata hivyo, binti yake mdogo mwenye umri wa miaka saba, aliendelea kumtia moyo. “Mama, usiache. Utafaulu!” binti huyo angesema. Kisha Mary angefanya bidii zaidi.
Wakati mume wake aliyeishi naye tu bila ndoa, aliyekuwa pia mlevi wa dawa za kulevya, aliporudi nyumbani, yeye pia alijiunga na funzo hilo. Mwishowe wote wawili wakashinda mazoea yao mabaya. Kisha, baada ya kuhalalisha ndoa yao na kukubali ubatizo, walipata furaha kubwa na kuhisi kama familia kwelikweli kwa mara ya kwanza. Kwa kusikitisha, UKIMWI mwishowe ulimuua Mary, lakini alikufa moyo wake ukiwa umewekwa juu ya ahadi ya Biblia ya ufufuo na uhai katika dunia iliyo paradiso, iliyoondolewa kila kitu chenye kudhuru cha barabara pana.
Ndiyo, inawezekana kuondoka kwenye barabara pana yenye nafasi iendayo kwenye uharibifu. Kristo Yesu alisema hivi: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Basi, kwa nini usiazimie kutembea kwenye barabara nyembamba iongozayo kwenye uzima? Kwa kuyatafakari na kutumia yale ujifunzayo kutoka kwa Neno la Mungu, huenda utajionea ahadi hii ya Biblia yenye kuchangamsha moyo: ‘Utaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itakuweka huru.’—Yohana 8:32.