Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 10/1 kur. 13-18
  • Wazazi na Watoto: Mtangulizeni Mungu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazazi na Watoto: Mtangulizeni Mungu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Daraka la Kikristo
  • Daraka la Msingi
  • Kuandaa Utegemezo Unaohitajika
  • Wazazi, Mnatanguliza Nini?
  • Watoto—Mtampendeza Nani?
  • Wazazi, Waandalieni Mahitaji Watu wa Familia Zenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kutumia Neno la Mungu Katika Jamaa Zetu Wenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 10/1 kur. 13-18

Wazazi na Watoto: Mtangulizeni Mungu!

“Mhofu Mungu wa kweli na kuzishika amri zake.”—MHUBIRI 12:13, NW.

1. Wazazi na watoto wanahitaji kusitawisha hofu gani, nayo itawaletea nini?

UNABII kuhusu Yesu Kristo ulisema kwamba “furaha yake itakuwa katika kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.” (Isaya 11:3) Hofu yake hasa ilikuwa staha na kicho kikubwa kwa Mungu, hofu ya kutompendeza Mungu kwa sababu alimpenda. Wazazi na watoto wahitaji kusitawisha hofu hiyo kama ya Kristo kwa Mungu, itakayowaletea shangwe kama Yesu. Wao wahitaji kumtanguliza Mungu katika maisha zao kwa kutii amri zake. Kulingana na mwandikaji mmoja wa Biblia, “huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13, NW.

2. Ni amri ipi ya Sheria iliyokuwa ya maana zaidi, nayo ilipewa akina nani hasa?

2 Amri ya maana zaidi ya Sheria, yaani, kwamba ‘tumpende Bwana kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, na kwa nguvu zetu zote,’ ilitolewa hasa kwa wazazi. Hilo laonyeshwa na maneno zaidi ya Sheria: “Uwafundishe watoto wako kwa bidii [maneno haya ya kumpenda Yehova], na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:4-7; Marko 12:28-30) Basi, wazazi waliamriwa wamtangulize Mungu kwa kumpenda wao wenyewe na kwa kuwafundisha watoto wao wafanye hivyo.

Daraka la Kikristo

3. Yesu alionyeshaje umaana wa kuwapa watoto uangalifu?

3 Yesu alionyesha umaana wa kuwapa hata watoto wachanga uangalifu. Katika pindi moja kuelekea mwisho wa huduma ya kidunia ya Yesu, watu walianza kumletea vitoto vyao. Kwa wazi wakiona kwamba Yesu alikuwa na shughuli mno asisumbuliwe, wanafunzi walijaribu kuwakataza watu. Lakini Yesu aliwakemea wanafunzi wake: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie.” Yesu hata ‘aliwakumbatia,’ hivyo akionyesha kwa njia ya kugusa moyo umaana wa kuwapa uangalifu watoto wachanga.—Luka 18:15-17; Marko 10:13-16.

4. Ni nani waliopewa amri ya ‘kufanya mataifa yote kuwa wanafunzi,’ na kufanya hivyo kungemaanisha wafanye nini?

4 Yesu pia alielewesha wazi kwamba wafuasi wake walikuwa na daraka la kuwafundisha wengine mbali na watoto wao wenyewe. Baada ya kifo na ufufuo wake, Yesu “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano”—kutia ndani baadhi ya wazazi. (1 Wakorintho 15:6) Yaonekana hilo lilitukia kwenye mlima fulani katika Galilaya ambako mitume wake 11 walikuwa wamekusanyika pia. Wakiwa huko Yesu aliwahimiza wote: “Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, . . . na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:16-20, italiki ni zetu.) Hakuna Mkristo awezaye kwa haki kupuuza amri hii! Ili baba na mama waitekeleze wao wanahitaji kutunza watoto wao na vilevile kushiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha peupe.

5. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba wengi wa mitume, kama si wote, walikuwa wameoa na labda walikuwa na watoto? (b) Vichwa vya familia walihitaji kutii shauri gani kwa uzito?

5 Jambo la maana ni kwamba hata mitume walikuwa wasawazishe madaraka ya familia zao na wajibu wa kuhubiri na vilevile kuchunga kundi la Mungu. (Yohana 21:1-3, 15-17; Matendo 1:8) Hii ni kwa sababu wengi wao, kama si wote, walikuwa wameoa. Hivyo mtume Paulo alieleza: “[Je!] hatuna uwezo kuchukua pamoja nasi mke aliye ndugu, kama wao mitume wengine, na ndugu wa Bwana, na Kefa?” (1 Wakorintho 9:5, italiki ni zetu; Mathayo 8:14) Huenda mitume wengine walikuwa na watoto. Wanahistoria wa mapema, kama vile Eusebio, wasema kwamba Petro alikuwa nao. Wazazi wote waliokuwa Wakristo wa mapema walihitaji kutii shauri hili la Kimaandiko: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”—1 Timotheo 5:8.

Daraka la Msingi

6. (a) Wazee Wakristo wenye familia wanakabili mwito gani? (b) Ni lipi daraka la msingi la mzee?

6 Wazee Wakristo wenye familia leo wamo katika hali inayofanana na ile ya mitume. Ni lazima wasawazishe daraka lao la kutunza mahitaji ya familia ya kiroho na ya kimwili pamoja na wajibu wao wa kuhubiri peupe na kuchunga kundi la Mungu. Ni utendaji gani unaopaswa kutangulizwa? Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1964, Kiingereza, lilisema: “Daraka la kwanza [la Baba] ni familia yake, naye hakika hawezi kutumikia [akiwa mzee] kama hawezi kutunza wajibu huu.”

7. Baba Wakristo humtangulizaje Mungu?

7 Kwa hiyo, ni lazima akina baba wamtangulize Mungu kwa kutii amri ya ‘kuwalea watoto wao katika adabu na maonyo ya Bwana.’ (Waefeso 6:4) Daraka hilo haliwezi kuachiwa mtu mwingine, hata kama baba anaweza kuwa na migawo mingine ya kusimamia utendaji katika kutaniko la Kikristo. Baba hao wanaweza kutunzaje madaraka yao—wakiandalia washiriki wa familia kimwili, kiroho, na kihisia-moyo—na wakati uo huo, kusimamia na kuangalia kutaniko?

Kuandaa Utegemezo Unaohitajika

8. Mke wa mzee anaweza kumtegemezaje?

8 Kwa wazi, wazee wenye madaraka ya familia wanaweza kunufaika wakitegemezwa. Mnara wa Mlinzi lililonukuliwa hapo juu lilisema kwamba mke Mkristo anaweza kumtegemeza mume wake. Lilisema: “Anaweza kufanya hali iwe ya kumfaa kwa kadiri iwezekanavyo ili atayarishe migawo yake mbalimbali, na kusaidia kuokoa wakati muhimu kwa mume wake na kwake mwenyewe kwa kuwa na ratiba nzuri nyumbani, kutayarisha mlo kwa wakati, kuwa tayari kwenda mikutanoni haraka. . . . Akiwa chini ya mwelekezo wa mume wake, mke Mkristo anaweza kusaidia sana kulea watoto katika njia iwapasayo ili kumpendeza Yehova.” (Mithali 22:6) Ndiyo, mke aliumbwa kuwa “msaidizi,” na kwa hekima mume wake atafurahia msaada wake. (Mwanzo 2:18) Utegemezo wake waweza kumsaidia kutunza madaraka yake ya familia na ya kutaniko kwa njia ya mafanikio zaidi.

9. Ni akina nani katika kutaniko la Thesalonike waliotiwa moyo kusaidia washiriki wengine wa kutaniko?

9 Hata hivyo, si wake wa wazee wa Kikristo peke yao wanaoweza kushiriki katika utendaji unaotegemeza mwangalizi ambaye lazima awe ‘mchungaji wa kundi la Mungu’ na vilevile kutunza familia yake. (1 Petro 5:2) Ni akina nani pia wawezao? Mtume Paulo aliwahimiza ndugu katika Thesalonike kuwa na staha kwa wale ‘wanaowasimamia.’ Lakini, akiendelea kusema na ndugu haohao—hasa wale wasiosimamia—Paulo aliandika: “Twawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, waonyeni kwa upole wale wasio na utaratibu, semeni kwa kufariji nafsi zilizoshuka moyo, tegemezeni walio dhaifu, iweni wenye ustahimilivu kuelekea wote.”—1 Wathesalonike 5:12-14, NW.

10. Ni matokeo gani mazuri ambayo msaada wenye upendo wa ndugu wote huleta kutanikoni?

10 Ni vema jinsi gani ndugu katika kutaniko wanapokuwa na upendo unaowasukuma kufariji walioshuka moyo, kutegemeza walio dhaifu, kuonya kwa upole wasio na utaratibu, na kuwa na ustahimili kwa wote! Ndugu katika Thesalonike, waliokuwa wamekubali kweli ya Biblia majuzi wajapokabili dhiki kubwa, walitumia shauri la Paulo la kufanya hivyo. (Matendo 17:1-9; 1 Wathesalonike 1:6; 2:14; 5:11) Fikiria matokeo mazuri ambayo ushirika wao wenye upendo ulitokeza katika kuimarisha na kuungamanisha kutaniko lote! Vivyo hivyo, ndugu wanapofarijiana, kutegemezana, na kuonyana leo, hilo lafanya madaraka ya uchungaji ya wazee, ambao mara nyingi wana familia za kutunza, kuwa rahisi kushughulikia.

11. (a) Kwa nini yafaa kukata kauli kwamba wanawake walitiwa ndani katika neno “akina ndugu”? (b) Ni msaada gani mwanamke Mkristo aliyekomaa anaweza kuwatolea wanawake wachanga leo?

11 Je, wanawake walikuwa miongoni mwa “akina ndugu” ambao mtume Paulo alikuwa akiwazungumzia? Ndiyo, walikuwamo, kwa kuwa wanawake wengi walikuja kuwa waamini. (Matendo 17:1, 4; 1 Petro 2:17; 5:9) Wanawake hawa wangetoa msaada gani? Kulikuwa na wanawake wachanga katika makutaniko waliokuwa na tatizo la kudhibiti ‘misukumo ya kingono’ au ‘walioshuka moyo.’ (1 Timotheo 5:11-13, NW) Wanawake wengine leo wana matatizo kama hayo. Huenda jambo wanalohitaji zaidi ni mtu wa kusikiliza matatizo yao tu na kuonyesha hisia mwenzi. Mara nyingi ni mwanamke Mkristo aliyekomaa ndiye afaaye zaidi kuandaa msaada huo. Kwa mfano, yeye anaweza kuzungumzia matatizo yake ya binafsi pamoja na mwanamke mwingine ambayo mwanamume Mkristo hawezi kushughulikia ifaavyo. Akikazia thamani ya kuandaa msaada kama huo, Paulo aliandika: “Na wazee wa kike [“Wanawake wenye umri mkubwa,” NW] wawe . . . wafundishao mema; ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Tito 2:3-5.

12. Ni muhimu kwamba wote kutanikoni wafuate mwelekezo wa nani?

12 Dada hao wanyenyekevu ni baraka iliyoje katika kutaniko wanapotegemeza waume zao na wazee kwa ushirikiano! (1 Timotheo 2:11, 12; Waebrania 13:17) Wote kutanikoni wanaposhirikiana ili kusaidiana kwa roho ya upendo na wote wanaponyenyekea mwelekezo wa wachungaji waliowekwa rasmi, wazee wenye madaraka ya familia hasa hufaidika.—1 Petro 5:1, 2.

Wazazi, Mnatanguliza Nini?

13. Baba wengi hushindwaje kushughulikia familia zao?

13 Miaka mingi iliyopita mtumbuizaji mmoja mashuhuri alisema hivi: “Mimi huona watu wenye mafanikio wakiendesha makampuni yenye mamia ya watu; wao hujua kushughulikia kila hali, jinsi ya kutoa nidhamu na kuthawabisha katika ulimwengu wa biashara. Lakini shughuli kubwa zaidi wanayoendesha ni familia yao nao hushindwa.” Kwa nini? Je, si kwa sababu wao hutanguliza biashara na mapendezi mengine na kupuuza shauri la Mungu? Neno lake lasema: “Maneno haya ninayokuamuru . . . , uwafundishe watoto wako kwa bidii.” Jambo hilo lilikuwa lifanywe kila siku. Wazazi wahitaji kutoa wakati wao bila kuzuia—na hasa upendo wao na hangaiko lao.—Kumbukumbu la Torati 6:6-9.

14. (a) Wazazi wanapaswa kuwatunzaje watoto wao? (b) Malezi yafaayo ya watoto yatia ndani nini?

14 Biblia yatukumbusha kwamba watoto ni urithi kutoka kwa Yehova. (Zaburi 127:3) Je, wewe hutunza watoto wako kama mali ya Mungu, zawadi aliyokukabidhi? Yaelekea mtoto wako ataitikia ukiwa unamchukua katika mikono yako, hivyo ukionyesha utunzi na uangalifu wako wenye upendo. (Marko 10:16) Lakini ‘kulea mtoto katika njia impasayo’ kwahitaji zaidi ya kumkumbatia na kumbusu tu. Ili awe na hekima ya kuepuka mitego ya maisha, mtoto vilevile huhitaji nidhamu yenye upendo. Mzazi huonyesha upendo wa kweli kwa ‘kumrudi mapema.’—Mithali 13:1, 24; 22:6.

15. Ni nini kinachoonyesha umuhimu wa nidhamu ya wazazi?

15 Umuhimu wa nidhamu ya mzazi waweza kuonwa kutokana na ufafanuzi wa mshauri mmoja wa shule juu ya watoto ambao huja ofisini mwake: “Wao ni wa kuhurumiwa, wenye kushuka moyo, na wasiojitumaini. Wao hulia wanaposema jinsi mambo yalivyo hasa. Wengi wao—wengi zaidi kuliko mtu awezavyo kufikiria—wamejaribu kujiua, si kwa sababu wao ni wenye furaha hivi kwamba hawawezi kuivumilia; bali kwa sababu wao hukosa furaha sana, hawatunzwi, na kukazwa akili kwa sababu kwa umri huo mchanga wao ndio ‘wenye madaraka’ na hiyo inawashinda kabisa kushughulikia.” Aliongezea hivi: “Laogopesha kwa kijana kuhisi kwamba ni yeye anayeshughulikia mambo.” Ni kweli kwamba watoto waweza kukataa kutiwa nidhamu, lakini kwa kweli wao huthamini miongozo na vizuizi vya wazazi. Wao hufurahi kwamba wazazi wao wanajali kiasi cha kuwawekea mipaka. “Imeniondolea mzigo mkubwa kabisa akilini,” akasema kijana mmoja ambaye wazazi wake walimwekea vizuizi.

16. (a) Ni nini hupata watoto fulani waliolelewa katika familia za Kikristo? (b) Kwa nini mwenendo mpotovu wa mtoto si lazima uonyeshe kwamba mazoezi aliyopewa na wazazi hayakuwa mazuri?

16 Lakini, wajapokuwa na wazazi wanaowapenda na wanaoandaa mazoezi mazuri, vijana fulani, kama yule mwana mpotevu wa kielezi cha Yesu, hukataa mwongozo wa wazazi na kukengeuka. (Luka 15:11-16) Hata hivyo, hilo lenyewe halimaanishi kwamba wazazi hawakutimiza daraka lao la kuzoeza mtoto wao ifaavyo, kama Mithali 22:6 ielekezavyo. Ile taarifa ya ‘kumlea mtoto katika njia impasayo naye hataiacha’ ilitolewa kwa ujumla. Kwa kusikitisha, kama mwana mpotevu, watoto fulani ‘hudharau kumtii mzazi.’—Mithali 30:17.

17. Wazazi wa watoto wapotovu waweza kupata faraja kwa jambo gani?

17 Baba mmoja wa mtoto mpotovu aliomboleza hivi: “Nimejaribu sana kufikia moyo wake. Nimeshindwa jambo la kufanya kwa sababu nimejaribu njia nyingi sana. Hakuna njia iliyofaulu.” Twatumaini kwamba watoto hao wapotovu baadaye watakumbuka mazoezi yenye upendo waliyopokea na kurudi kama alivyofanya yule mwana mpotevu. Hata hivyo, uhakika ni kwamba watoto wengine huasi na kufanya mambo yasiyo ya adili na kuwaumiza sana wazazi wao. Wazazi waweza kufarijika kwa kujua kwamba hata yule mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani alisalitiwa na mwanafunzi wake wa muda mrefu Yuda Iskariote. Na bila shaka Yehova mwenyewe alihuzunishwa wakati wana wake wengi wa roho walipokataa shauri lake na kuwa waasi bila kosa lolote kwa upande wa Yehova.—Luka 22:47, 48; Ufunuo 12:9.

Watoto—Mtampendeza Nani?

18. Watoto wanaweza kuonyeshaje kwamba wanamtanguliza Mungu?

18 Yehova anawahimiza enyi vijana: “Watiini wazazi wenu katika Bwana.” (Waefeso 6:1) Vijana humtanguliza Mungu kwa kufanya hivyo. Usiwe mpumbavu! “Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye,” Neno la Mungu lasema. Wala usidhanie kwa kiburi kwamba huwezi kutiwa nidhamu. Ukweli ni kwamba “kuna kizazi cha watu walio safi machoni pao wenyewe; ambao hawakuoshwa uchafu wao.” (Mithali 15:5; 30:12) Kwa hiyo tiini mwelekezo wa kimungu—‘zisikilizeni,’ ‘mziweke akiba,’ ‘msizisahau,’ “toeni uangalifu,” (NW), ‘zishikeni,’ na ‘msiziache’ sheria na nidhamu za wazazi.—Mithali 1:8; 2:1; 3:1; 4:1; 6:20.

19. (a) Watoto wana sababu zipi zenye nguvu za kumtii Yehova? (b) Wachanga wanaweza kuonyeshaje kwamba wao ni wenye shukrani kwa Mungu?

19 Una sababu zenye nguvu za kumtii Yehova. Anakupenda, naye ametoa sheria zake, kutia ndani sheria ya watoto kutii wazazi wao, ili kukulinda na kukusaidia uwe na maisha yenye furaha. (Isaya 48:17) Pia ametoa Mwana wake afe kwa ajili yako ili uokolewe kutoka kwa dhambi na kifo na kupata uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Je, unashukuru? Mungu anatazama kutoka mbinguni, akichunguza moyo wako aone kama unampenda kikweli na kuthamini maandalio yake. (Zaburi 14:2) Shetani anatazama pia, naye anamdhihaki Mungu, akidai kwamba wewe hutamtii Mungu. Unafanya Shetani afurahi na ‘kumhuzunisha’ Yehova unapokosa kumtii Mungu. (Zaburi 78:40, 41) Yehova anakusihi: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu [kwa kuwa mtiifu kwangu]; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Ndiyo, swali ni, Utampendeza nani, Shetani au Yehova?

20. Kijana mmoja amedumishaje moyo mkuu wa kumtumikia Yehova hata anapohisi woga?

20 Si rahisi kufanya mapenzi ya Mungu ukikabili mikazo ambayo Shetani na ulimwengu wake anakuwekea. Inaweza kuogopesha. Kijana mmoja alisema: “Kuwa mwoga ni kama kuhisi baridi. Unaweza kufanya kitu uiondoe.” Akaeleza: “Unapohisi baridi unavaa sweta. Ukiendelea kuhisi baridi, unavaa nyingine. Na utaendelea kuvaa kitu mpaka baridi ipotee usiihisi tena. Kwa hiyo kusali kwa Yehova unapohisi woga ni kama kuvaa sweta unapohisi baridi. Nikiwa bado mwoga baada ya sala moja, ninasali tena, na tena, na tena, mpaka sihisi woga tena. Na inafaulu. Imenitenga na matatizo!”

21. Yehova atatutegemezaje tukijaribu kweli kweli kumtanguliza maishani mwetu?

21 Tukijaribu kwa kweli kumtanguliza Mungu maishani mwetu, Yehova atatutegemeza. Atatuimarisha, akiandaa msaada wa malaika unapohitajika, kama alivyofanya na Mwana wake. (Mathayo 18:10; Luka 22:43) Enyi nyote wazazi na watoto, iweni na moyo mkuu. Mwe na hofu kama ya Kristo, nayo itawaletea furaha. (Isaya 11:3) Ndiyo, “mhofu Mungu wa kweli na kuzishika amri zake, kwa sababu huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13, NW.

Je, Waweza Kujibu?

◻ Wafuasi wa mapema wa Yesu walihitaji kusawazisha madaraka gani?

◻ Ni lazima wazazi Wakristo watimize daraka gani?

◻ Ni msaada gani unaopatikana kwa wazee Wakristo wenye familia?

◻ Ni utumishi gani wenye thamani ambao dada wanaweza kufanya kutanikoni?

◻ Ni shauri gani na mwelekezo upi ulio muhimu kwa watoto kutii?

[Picha katika ukurasa wa15]

Mara nyingi mwanamke Mkristo aliyekomaa anaweza kuandalia mwanamke mchanga msaada unaohitajiwa

[Picha katika ukurasa wa17]

Wazazi wa watoto wapotovu wanaweza kupata faraja gani katika Maandiko?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki