Kisanduku cha Mlo Chatoa Ushahidi
WATU katika eneo lililoathiriwa walikuwa na shida ya kupata chakula katika siku zilizofuata tetemeko la dunia katika Kobe, Japani, Januari uliopita. Na bado, Mashahidi wa Yehova hawakupungukiwa na riziki, yote hayo kwa ajili ya utegemezo wenye fadhili wa rafiki zao. Kwa siku mbili au tatu hivi baada ya tetemeko hilo, makutaniko ya karibu-karibu yaliandaa wali wa mviringo. Upesi, marafiki wenye kujali walitoa visanduku vya milo. Wengi waliambatanisha barua fupi kwenye kisanduku cha milo zikionyesha kujali walioathiriwa. Waliopokea milo hiyo walisema kwamba kila mlo “uliliwa kwa machozi” kwa kuwa hawakuweza kuzuilia machozi yao walipokuwa wakisoma barua hizo fupi.
Mashahidi wa Yehova walishiriki chakula chao na wengine waliokuwa na uhitaji. Shahidi mmoja alikuwa akila chakula chake cha mchana huku akisafiri kwa gari pamoja na mfanyakazi-mwenzi asiye Shahidi waliyefanya kazi pamoja naye katika kampuni moja. Hivyo alimgawia kisanduku kimoja cha milo alichokuwa amepokea.
“Ulinunua wapi kisanduku hiki cha mlo wa mchana?” huyo mfanyakazi-mwenzi akauliza. Ndugu akaeleza kazi ya kutoa msaada ya Mashahidi. “Sijala mboga kwa siku nyingi. Nitabakisha kingine nipelekee familia yangu nyumbani,” mtu huyo akasema kwa uthamini.
Mara ya tatu alipopewa kisanduku cha mlo, yule mfanyakazi-mwenzi alimpa huyo Shahidi pesa za Japani yen 3,000 (karibu dola za Marekani 35) na kusema: nafahamu utendaji wenu mbalimbali, hivyo tafadhali acha nitoe mchango kwa kazi yenu. Nathamini kushiriki chakula chako cha mchana pamoja nami. Kwa kweli, marafiki zenu wote ni watu wazuri sana.”