Faraja kwa Wale Wenye “Roho Iliyovunjika”
LEO, ulimwengu wa Shetani umefikia “kuishiwa na utambuzi wote wa adili.” (Waefeso 4:19, NW; 1 Yohana 5:19) Uzinzi na uasherati zimeenea. Katika nchi nyingi asilimia 50 au zaidi za ndoa huishia talaka. Ugoni-jinsia-moja unakubalika katika sehemu nyingi. Jeuri ya kingono—kulala kinguvu—huripotiwa mara nyingi katika vyombo vya habari. Ponografia ni biashara inayofanyiza mabilioni ya dola.—Warumi 1:26, 27.
Miongoni mwa mambo maovu sana ni kutenda vibaya watoto wasio na hatia. Kama vile hekima ya ulimwengu wa Shetani ilivyo, hali ya kutenda vibaya watoto ni “ya kinyama, ya roho waovu.” (Yakobo 3:15, NW) Katika Marekani pekee, gazeti la Time lasema, “zaidi ya ripoti 400,000 zinazoweza kuthibitishwa za mashambulizi ya kingono huorodheshwa na walimu na madaktari kwa wenye mamlaka kila mwaka.” Waliotendwa vibaya wanapokuwa watu wazima, wengi bado hubeba majeraha yenye uchungu, na majeraha hayo ni halisi! Biblia husema: “Roho [mwelekeo wa akilini, hisia na mawazo za ndani] ya mtu itastahimili udhaifu wake; bali roho iliyovunjika [iliyotiwa jeraha, iliyotaabishwa] nani awezaye kuistahimili?”—Mithali 18:14.
Habari njema ya Ufalme wa Mungu huvutia watu wa aina zote, kutia ndani “waliovunjika moyo” na walio na “roho nzito.” (Isaya 61:1-4) Si ajabu kwamba wengi wenye uchungu wa kihisia-moyo huitikia mwaliko huu: “Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufunuo 22:17) Kwa hawa kutaniko la Kikristo laweza kuwa mahali pa faraja. Wanafurahi kujua kwamba karibuni kuteseka kutakuwa jambo lililopita. (Isaya 65:17) Hata hivyo, hadi wakati huo, wanaweza kuhitaji ‘kufarijiwa’ na majeraha yao ‘kugangwa.’ Kwa kufaa Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Semeni kwa kufariji nafsi zilizoshuka moyo, tegemezeni walio dhaifu, iweni wenye ustahimilivu kuelekea wote.”—1 Wathesalonike 5:14, NW.
“Kumbukumbu Zilizothibitiwa”
Katika miaka ya majuzi watu fulani ‘wamevunjwa moyo’ kwa sababu ambazo watu wengine huona vigumu kuzielewa. Wao ni watu wazima ambao, kwa msingi wa zile zifafanuliwazo kuwa “kumbukumbu zilizothibitiwa,” wanasema kwamba walitendwa vibaya kingono walipokuwa watoto.a Wengine hawana wazo la kuwa waliwahi kunyanyaswa kingono hadi, kwa ghafula, wapatapo mawazo yenye kurudi na “kumbukumbu” la kutendewa vibaya na mtu mzima (au watu wazima) walipokuwa wachanga. Je, katika kutaniko la Kikristo kuna yeyote aliye na mawazo yenye kusumbua kama hayo? Katika nchi kadhaa, wapo, na hawa waliojiweka wakfu huenda wakahisi fadhaiko kubwa, hasira, hatia, aibu, au upweke. Kama Daudi huenda wakahisi kutengwa na Mungu na kupaaza sauti wakisema: “Ee BWANA, kwa nini wasimama mbali? Kwani kujificha nyakati za shida?”—Zaburi 10:1.
Namna nyingi za “kumbukumbu” hizi hazieleweki vizuri na wataalamu wa afya ya akili. Na bado, “kumbukumbu” hizo zaweza kuathiri hali ya kiroho ya Wakristo waliojiweka wakfu. Hivyo twatazamia kwa uhakika Neno la Mungu litupe mwongozo katika kuzishughulikia. Biblia huandaa “ufahamu katika mambo yote.” (2 Timotheo 2:7, 3:16, NW) Pia huwasaidia wote wanaohusika kuwa na imani katika Yehova, ‘Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote.’—2 Wakorintho 1:3, 4.
Je, Kweli Kulitendeka?
Ulimwenguni, mna ubishi mwingi juu ya “kumbukumbu” hizi kuwa ni nini na ni kwa kadiri gani zinawakilisha mambo yaliyotendeka kwa kweli. Mashahidi wa Yehova “si wa ulimwengu” nao hawashiriki katika ubishi huo. (Yohana 17:16) Kulingana na ripoti zilizoandikwa, nyakati nyingine “kumbukumbu” zimethibitika kuwa za kweli. Kwa kielelezo, baada ya mfanyakazi mmoja wa bima Frank Fitzpatrick “kukumbuka” akinyanyaswa kingono na kasisi fulani, karibu watu wengine mia moja walidai kwamba wao pia walikuwa wametendwa vibaya na kasisi huyo huyo. Kasisi aliyeripotiwa akakubali kutenda vibaya.
Hata hivyo, yafaa kuangaliwa kwamba idadi fulani ya watu wameshindwa kuthibitisha “kumbukumbu” zao. Wengine wakitaabika kwa njia hiyo wamepata kukumbuka vizuri mtu fulani akiwatenda vibaya au akitendwa vibaya mahali fulani hususa. Hata hivyo, baadaye uthibitisho halali ulio kinyume ulionyesha wazi kwamba mambo haya yote “yaliyokumbukwa” hayangeweza kuwa ya kweli.
Kuandaa Kimbilio
Walakini, faraja yaweza kutolewaje kwa wale walio na “roho iliyovunjika” kwa sababu ya “kumbukumbu” hizo? Kumbuka mfano wa Yesu wa Msamaria mwenye ujirani. Mtu fulani alishambuliwa na wanyang’anyi, akapigwa, na kunyang’anywa mali zake. Msamaria alipokuwa akipita, akamhurumia mtu huyo aliyejeruhiwa. Alifanya nini? Je, alisisitiza kusikia habari zote hususa juu ya kupigwa huko? Au je, Msamaria huyo alitaka ufafanuzi wa wezi hao na kuwafuata haraka? La. Mtu huyo alikuwa ameumizwa! Hivyo Msamaria huyo akamfunga mtu huyo majeraha yake kwa utaratibu na kwa upendo akambeba hadi mahali salama kwa hoteli iliyokuwa karibu na ambapo angeweza kupona.—Luka 10:30-37.
Bila shaka, kuna tofauti kati ya majeraha ya mwilini na “roho iliyovunjika” inayosababishwa na hasa kutendwa vibaya kingono wakati wa utotoni. Lakini yote mawili husababisha kuteseka kwingi sana. Hivyo, yale Msamaria huyo aliyomfanyia Myahudi huyo aliyejeruhiwa yaonyesha yale yawezayo kufanywa ili kusaidia Mkristo mwenzi aliyeumia. Jambo la kwanza ni kutoa faraja ya upendo na kumsaidia kupata nafuu.
Ibilisi alimtaabisha Ayubu mwaminifu, yaonekana akiwa na uhakika kwamba ama uchungu wa kihisia-moyo ama wa kimwili ungeweza kuvunja uaminifu-maadili wake. (Ayubu 1:11; 2:5) Tangu wakati huo, Shetani amejaribu mara nyingi kutumia mateso—awe anayasababisha moja kwa moja au la—kudhoofisha imani ya watumishi wa Mungu. (Linganisha 2 Wakorintho 12:7-9.) Je, tunaweza kuwa na shaka kwamba sasa Shetani anatumia kutenda vibaya watoto na “roho iliyovunjika” ya watu wazima walio wengi waliopatwa na jambo hilo (au wanaosumbuliwa na “kumbukumbu” za kutendwa hivyo) kujaribu kudhoofisha imani ya Wakristo? Mkristo auguaye lakini ambaye kwa uthabiti anakataa kuacha uaminifu-maadili wake anasema hivi kama Yesu alipokuwa akishambuliwa na Shetani: “Nenda zako, Shetani”!—Mathayo 4:10.
Uwe na Nguvu za Kiroho
“Mtumwa mwaminifu mwenye akili” ameandika habari ili kusaidia kushughulikia maumivu ya kiroho na kihisia-moyo yanayosababishwa na kutenda vibaya watoto. (Mathayo 24:45-47) Mambo yaliyoonwa yaonyesha kwamba mwenye kuteseka anasaidiwa ikiwa anaweza kutegemea ‘nguvu za Bwana na uwezaji wa nguvu zake,’ akivaa “suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” (Waefeso 6:10-17, NW) Silaha hii inatia ndani “kweli” ya Biblia, ambayo inamfunua Shetani kuwa adui wa mwisho na inaondoa kabisa giza ambalo katika hilo yeye na wamuungao mkono hutenda. (Yohana 3:19) Halafu, kuna “bamba la kifuani la uadilifu.” Mwenye kutaabika apaswa kujitahidi kushikilia viwango vya maadili. Kwa kielelezo, wengine wana tamaa yenye nguvu ya kujiumiza au kutenda ukosefu wa adili. Kila wakati wanapokinza tamaa hizi, wanapata ushindi!
Silaha ya kiroho pia inatia ndani “habari njema ya amani.” Kuzungumza na wengine juu ya makusudi ya Yehova humtia nguvu anayezungumza na vilevile yeyote asikilizaye. (1 Timotheo 4:16) Ikiwa ni wewe una “roho iliyovunjika,” jambo hilo likifanya iwe vigumu kwako kuzungumza juu ya habari njema, jaribu kwenda na Mkristo mwingine anayeenda kufanya kazi hii muhimu. Na usisahau “ngao kubwa ya imani.” Uwe na imani kwamba Yehova anakupenda na kwamba atarudisha yote uliyopoteza. Uwe na imani isiyo na shaka kwamba Yesu pia anakupenda, naye alithibitisha hilo kwa kufa kwa ajili yako. (Yohana 3:16) Sikuzote Shetani amedai kwa uwongo kwamba Yehova hawajali watumishi wake. Huo ni uwongo mwingine wake mbaya, uliopotoka.—Yohana 8:44; linganisha Ayubu 4:1, 15-18; 42:10-15.
Ikiwa uchungu wa moyo unafanya iwe vigumu kwako kuamini kwamba Yehova anakujali, kushirikiana na wengine ambao wana imani thabiti kwamba anajali kutasaidia. (Zaburi 119:107, 111; Mithali 18:1; Waebrania 10:23-25) Kataa kumruhusu Shetani akunyang’anye thawabu ya uhai. Kumbuka, “kofia ya chuma ya wokovu” ni sehemu ya silaha hiyo; ndivyo na “upanga wa roho.” Biblia imepuliziwa kwa roho takatifu, ambayo Shetani hawezi kushinda. (2 Timotheo 3:16; Waebrania 4:12) Maneno yayo yenye kuponya yaweza kutuliza uchungu wa kihisia-moyo.—Linganisha Zaburi 107:20; 2 Wakorintho 10:4, 5.
Mwishowe, sali bila kukoma upate nguvu za kuvumilia. (Warumi 12:12; Waefeso 6:18) Sala ya kuhisiwa moyoni ilimtegemeza Yesu kupitia maumivu makali ya kihisia-moyo, nayo inaweza kukusaidia pia. (Luka 22:41-43) Je, ni vigumu kusali? Waombe wengine wasali pamoja nawe na kusali kwa ajili yako. (Wakolosai 1:3; Yakobo 5:14) Roho takatifu itategemeza sala zako. (Linganisha Warumi 8:26, 27.) Kama vile maumivu ya kimwili yenye uchungu mwingi yalivyo, wengine walio na majeraha makubwa ya kihisia-moyo huenda wasiponeshwe kabisa katika mfumo huu wa mambo. Lakini kwa msaada wa Yehova twaweza kuvumilia, nao uvumilivu ni ushindi, kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu. (Yohana 16:33) “Enyi watu, mtumainini [Yehova] sikuzote, ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu.”—Zaburi 62:8.
Vipi Anayesemwa Kuwa Alitenda Vibaya?
Kwa kweli mtu atendaye vibaya mtoto kingono ni mlala-kinguvu na yapasa aonwe hivyo. Yeyote atendwaye kwa njia hii ana haki ya kumshtaki mwenye kumtenda vibaya. Hata hivyo, shtaka halipaswi kufanywa upesi ikiwa msingi walo pekee ni “kumbukumbu zilizothibitiwa” za kutendwa vibaya. Katika kisa cha namna hiyo jambo la muhimu kabisa kwa mwenye kuugua ni kupata kadiri fulani ya uthabiti wa kihisia-moyo. Baada ya wakati fulani kupita, huenda akawa katika hali nzuri ya kuweza kupima “kumbukumbu” hizo na kuamua atakalo kufanya juu yazo, ikiwa kuna jambo la kufanya.
Fikiria kisa cha Donna. Inaripotiwa kwamba alikuwa na tatizo la ulaji akamwendea mshauri—yaonekana asiyekuwa na ustadi wa kutosha. Mara akamshtaki baba yake kwa ngono ya kiukoo na baba yake akapelekwa mahakamani. Kamati ya hukumu haikufikia uamuzi, hivyo huyo baba hakufungwa gerezani, lakini ilimbidi kulipa dola 100,000 za gharama ya mahakama. Kisha, baada ya hayo yote, Donna akawaambia wazazi wake kwamba haamini tena kwamba alitendwa vibaya!
Kwa hekima, Sulemani alisema: “Usiharakishe kufanya kesi ya kisheria.” (Mithali 25:8, NW) Ikiwa kuna sababu fulani nzuri za kushuku kwamba yule anayedhaniwa alitenda jambo hilo bado anatenda vibaya watoto, huenda onyo likahitaji kutolewa. Wazee wa kutaniko waweza kusaidia katika kisa kama hicho. La sivyo, usifanye mambo haraka. Huenda mwishowe ukaridhika na kuacha jambo hilo liishe. Hata hivyo, ikiwa unataka kumwendea huyo mtenda vibaya anayedhaniwa (baada ya kupima kwanza jinsi utahisi juu ya jinsi anavyoweza kuitikia), una haki ya kufanya hivyo.
Wakati ambapo yule anayepatwa na “kumbukumbu” hizo anapopata nafuu, hali za kutatanisha huenda zikatokea. Kwa kielelezo, mtu fulani anaweza kuwa na maono ya wazi ya akilini ya kunyanyaswa kingono na mtu fulani amwonaye kila siku. Hakuna sheria ziwezazo kuwekwa za kushughulikia jambo hilo. “Kila mmoja atachukua mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5, NW) Wakati mwingine mtu aweza kuhisi kwamba mtu wa ukoo au mshiriki wa familia anahusika. Kumbuka hali ya kutilika shaka ya baadhi ya “kumbukumbu zilizothibitiwa” unapokuwa utamtambulisha yule anayeshukiwa kuwa alitenda jambo hilo. Katika hali kama hiyo, maadamu jambo hilo halijathibitishwa, kudumisha uhusiano na familia—angalau kwa kuwatembelea mara kwa mara, kwa kuwaandikia barua, au kuwapigia simu—kwaweza kuonyesha kwamba unajaribu kufuata mwelekezo wa Kimaandiko.—Linganisha Waefeso 6:1-3.
Wazee Wanaweza Kufanya Nini?
Wazee wakiendewa na mshiriki wa kutaniko anayepatwa na mawazo yanayorudi au “kumbukumbu zilizothibitiwa” za kutendwa vibaya alipokuwa mtoto, kwa kawaida wawili wao wanapewa mgawo wa kusaidia. Wazee hawa wapaswa kumtia moyo kwa fadhili mwenye kufadhaika kwa wakati huu aweke fikira zake juu ya kukabili fadhaiko la kihisia-moyo. Majina ya mtenda vibaya yeyote “anayekumbukwa” yapasa iwe siri kabisa.
Kazi ya msingi ya wazee ni kutenda wakiwa wachungaji. (Isaya 32:1, 2; 1 Petro 5:2, 3) Ni lazima hasa wawe waangalifu ‘kujivika moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.’ (Wakolosai 3:12) Na wasikilize kwa njia ya fadhili kisha watoe maneno yenye kuponya kutoka kwa Maandiko. (Mithali 12:18) Wengine ambao wametaabishwa na “kumbukumbu” zenye kuumiza wameonyesha uthamini kwa wazee ambao wanawatembelea mara kwa mara au hata kuwapigia simu kuona jinsi wanavyoendelea. Mambo kama hayo hayapaswi kuchukua muda mrefu, lakini yanaonyesha kwamba tengenezo la Yehova hujali. Mwenye kutaabika atambuapo kwamba ndugu zake Wakristo wanampenda kwa kweli, huenda akasaidiwa kupata kadiri fulani ya usawaziko wa kihisia-moyo.
Vipi ikiwa mwenye maumivu aamua kwamba anataka kushtaki?b Basi wale wazee wawili waweza kumshauri kwamba, kupatana na kanuni iliyoko kwenye Mathayo 18:15, yeye mwenyewe apaswa kumwendea mshtakiwa na kumweleza habari hiyo. Ikiwa mwenye shtaka hana uwezo wa kihisia-moyo wa kumkabili mshtakiwa uso kwa uso, aweza kufanya hivyo kwa kupiga simu au labda kwa kuandika barua. Kwa njia hiyo yule anayeshtakiwa anapewa fursa ya kutaarifu mbele ya Yehova kwa kujibu shtaka hilo. Huenda pia akaweza kutoa uthibitisho wa kwamba hangaliweza kutenda ubaya huo. Au labda yule anayeshtakiwa atatubu, na kuwe na upatanisho. Hilo laweza kuwa baraka kama nini! Ikiwa toba imefanywa, wale wazee wawili waweza kushughulikia mambo hayo zaidi kulingana na kanuni za Maandiko.
Shtaka hilo likikanushwa, wazee wapaswa kueleza mwenye shtaka kwamba hakuna jambo jingine liwezalo kufanywa kwa njia ya kihukumu. Na kutaniko litaendelea kumwona mshtakiwa kuwa asiye na hatia. Biblia husema kwamba ni lazima kuwe na mashahidi wawili au watatu kabla ya tendo la kihukumu liweze kufanywa. (2 Wakorintho 13:1; 1 Timotheo 5:19) Hata ikiwa zaidi ya mtu mmoja “akumbuka” kutendwa vibaya na mtu yuleyule, hali ya kumbukumbu hizi si yenye kutegemeka hivi kwamba haiwezekani kuwekewa msingi wa maamuzi ya kihukumu bila uthibitisho mwingine unaoziunga mkono. Hilo halimaanishi kwamba “kumbukumbu” kama hizo zinaonwa kuwa za uwongo (au kwamba zinaonwa kuwa za kweli). Lakini kanuni za Biblia lazima zifuatwe katika kufanya jambo liwe la kihukumu.
Vipi ikiwa mshtakiwa—ingawa anakataa kosa—kwa kweli ni mwenye hatia? Je, “anaepuka hukumu”? Bila shaka sivyo! Swali la kuwa kwake na hatia au bila hatia laweza kuachwa mikononi mwa Yehova. “Dhambi za watu wengine zi dhahiri, zatangulia kwenda hukumuni; wengine dhambi zao zawafuata.” (1 Timotheo 5:24; Warumi 12:19; 14:12) Kitabu cha Mithali husema: “Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha; bali kutaraji kwao wasio haki kutapotea.” “Mtu mwovu atakapokufa, taraja lake lapotea.” (Mithali 10:28; 11:7) Hatimaye, Yehova Mungu na Kristo Yesu hutoa hukumu idumuyo milele yenye haki.—1 Wakorintho 4:5.
Kumkinza Ibilisi
Nafsi zilizojiweka wakfu zivumiliapo zinapokabili maumivu mengi ya kimwili au ya kihisia-moyo, ni uthibitisho ulioje wa nguvu zao za ndani na upendo kwa Mungu! Na ni ushuhuda ulioje wa uwezo wa roho ya Yehova yenye kutegemeza!—Linganisha 2 Wakorintho 4:7.
Maneno haya ya Petro yahusu watu kama hao: “Mpingeni huyo [Shetani], mkiwa thabiti katika imani.” (1 Petro 5:9) Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Wakati mwingine huenda ikawa vigumu kufikiri vizuri na kwa akili. Lakini usivunjike moyo! Karibuni, Ibilisi na matendo yake ya ujanja hatakuwapo. Kwa kweli, tunatazamia kwa hamu nyingi wakati huo ambapo “Mungu mwenyewe . . . atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
[Maelezo ya chinis]
a “Kumbukumbu zilizothibitiwa” na maneno yanayofanana na hayo yamefungwa ndani ya alama za mnukuo ili kuyatofautisha na kumbukumbu za kawaida tulizo nazo sisi sote.
b Huenda pia ikawa lazima hatua inayoelezwa katika fungu hili ichukuliwe ikiwa jambo hilo limejulikana kutanikoni.