Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 1/1 kur. 24-28
  • Yehova Hakutuacha Kamwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Hakutuacha Kamwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Kweli ya Biblia
  • Kuhubiri Ujapokuwa Upinzani
  • Magumu Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2
  • Kutahiniwa Juu ya Suala la Kutokuwamo
  • Kurudi Kijijini Kwetu
  • Ugavi wa Fasihi Wakatizwa
  • Magumu Yaongezeka
  • Mabadiliko Makubwa Sana
  • Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu Pekee
  • Yehova Amenipa “Nguvu Ipitayo Iliyo ya Kawaida”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Nchini Albania na Kosovo
    Masimulizi ya Mashahidi wa Yehova
  • Jinsi Mahitaji Yangu ya Kiroho Yalivyotoshelezwa
    Amkeni!—2003
  • Mashariki na Magharibi, Yehova Huwaimarisha Watu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 1/1 kur. 24-28

Yehova Hakutuacha Kamwe

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA NASHO DORI

Mbreshtan ni kijiji kidogo cha mlimani kusini mwa Albania, kisicho mbali na Ugiriki. Mimi nilizaliwa huko 1907. Nilipokuwa na miaka mitano, nilianza kwenda shule ya Kigiriki, lakini masomo yangu yalikatizwa wakati majeshi ya Kiitalia yaliposhambulia Albania wakati wa Vita ya Ulimwengu 1. Baada ya vita, nilianza masomo yangu tena lakini kwa lugha ya Kialbania.

INGAWA wazazi wangu hawakuwa watu wa kidini sana, wao walifuata mapokeo ya Kanisa Othodoksi la Kialbania. Ndugu ya babu yangu alikuwa padri katika Mbreshtan, kwa hiyo nilifanya kazi kanisani kisha nikajionea mwenyewe utendaji walo mbalimbali. Desturi zilionekana kuwa bila faida yoyote, na unafiki walo uliniudhi.

Wakitenda kulingana na desturi za kwetu, wazazi wangu walinichagulia mwanamke kijana ili nimwoe. Argjiro alitoka kijiji cha karibu cha Grabova, nasi tukaoana 1928, alipokuwa na miaka 18.

Kujifunza Kweli ya Biblia

Karibu na wakati huo nililalamika juu ya Kanisa Othodoksi kwa binamu yangu aliyekuwa akitembelea kutoka Marekani. “Katika Marekani, karibu na nyumba yangu,” yeye akajibu, “kuna kikundi cha watu ambao hawana kanisa, lakini wao hujifunza Biblia.” Wazo la kujifunza Biblia bila kuwa na kanisa lilinivutia. Kwa hiyo nilimwomba kama angeweza kunipelekea baadhi ya fasihi za Biblia.

Nilisahau kabisa juu ya mazungumzo yetu mpaka karibu mwaka mmoja baadaye nilipopokea kifurushi kutoka Milwaukee, Wisconsin. Ndani yacho mlikuwa kitabu The Harp of God katika Kialbania na Mnara wa Mlinzi katika Kigiriki. Nilisoma kitabu hicho kijuujuu nikaona mtajo kuhusu kanisa la kweli. Huo uliniudhi. ‘Sitaki lolote kuhusiana na kanisa,’ nikajiambia mwenyewe. Kwa hiyo sikukisoma kitabu hicho kikamili.

Katika 1929, nilijiunga na jeshi nikatumwa kwenye jiji la Tiranë, jiji kuu la Albania. Nikiwa huko nilikutana na Stathi Muçi, aliyekuwa akisoma Biblia ya Kigiriki. “Je, wewe huenda kanisani?” nikauliza. “La,” yeye akajibu. “Nililiacha kanisa. Mimi ni mmoja wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa.” Jumapili, askari-jeshi mwingine nami tukaenda kwenye mkutano pamoja na Stathi. Huko nilijifunza kwamba kanisa la kweli si jengo wala dini fulani, bali limefanyizwa na watumishi watiwa-mafuta wa Kristo. Sasa nikaelewa kile ambacho kitabu The Harp of God kilikuwa kikisema.

Nasho Idrizi na Spiro Vruho walikuwa wamerudi Albania kutoka Marekani katika miaka ya katikati ya 1920 nao walikuwa wakieneza kweli za Biblia ambazo walikuwa wamejifunza huko. Nilianza kuhudhuria mikutano katika Tiranë, pamoja na wale Wanafunzi wa Biblia wachache. Upesi ikawa wazi kwangu kwamba nilikuwa nimelipata tengenezo la Yehova. Kwa hiyo mnamo Agosti 4, 1930, nilibatizwa katika mto wa karibu.

Baadaye nilirudi Mbreshtan ili kufuatia kazi yangu ya ushonaji wa viatu. Lakini la maana zaidi, nilianza pia kushiriki na wengine kweli za Biblia nilizokuwa nimejifunza. Nilikuwa nikiwaambia: “Yesu Kristo si kama zile sanamu kanisani. Yeye yu hai!”

Kuhubiri Ujapokuwa Upinzani

Ahmed Bey Zogu alitwaa utawala kwa nguvu katika 1925, akajifanya mwenyewe Mfalme Zog wa 1 katika 1928, akatawala hadi 1939. Waziri wake wa haki za kibinadamu alitoa kibali kwa kazi yetu ya Kikristo. Hata hivyo, tulikuwa na matatizo. Hiyo ilikuwa kwa sababu Musa Juka, waziri wa mambo ya kitaifa, alikuwa rafiki wa karibu wa papa katika Roma. Juka aliamuru kwamba dini tatu pekee zitambuliwe kirasmi—Uislamu, Othodoksi, na Katoliki ya Kiroma. Polisi wakajaribu kutunyang’anya vitabu vyetu na kukomesha kazi yetu ya kuhubiri, lakini hawakufaulu.

Katika miaka ya 1930, nilitembelea Berat mara nyingi, jiji lililo kubwa zaidi katika Albania ambako Mihal Sveci alielekeza kazi yetu ya kuhubiri. Tulipanga ziara za kuhubiri kotekote nchini. Wakati mmoja nilitumwa kwenye mji wa Shkodër kwa majuma mawili, nami nikaweza kuacha fasihi nyingi. Katika 1935 sisi tukiwa kikundi tulikodi basi ili kuhubiri katika mji wa Këlcyrë. Halafu ziara kubwa zaidi ya Albania ikapangwa kwenye miji ya Përmet, Leskovik, Ersekë, Korçë, Pogradec, na Elbasan. Tulimaliza ziara hiyo katika Tiranë wakati barabara ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Ugavi wa chakula cha kiroho ulitusaidia tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho, kwa hiyo hatukuhisi kamwe kuwa tumeachwa. Tangu 1930 hadi 1939, nilipokea Mnara wa Mlinzi la Kigiriki kwa ukawaida. Lengo langu lilikuwa pia kuisoma Biblia kwa angalau muda wa saa moja kila siku, jambo ambalo nilifanya kwa miaka ipatayo 60 kabla ya macho yangu kushindwa kuona. Ni karibuni tu kwamba Biblia nzima ilipatikana katika lugha ya Kialbania, kwa hiyo ninafurahi kwamba nilijifunza Kigiriki nikiwa mtoto. Mashahidi wengine Waalbania katika siku hizo za mapema walijifunza Kigiriki pia ili waweze kuisoma Biblia nzima.

Katika 1938, Argjiro alibatizwa. Kufikia 1939 saba wa watoto wetu kumi walikuwa wamezaliwa. Kwa kuhuzunisha, watatu wa watoto wetu wa kwanza saba walikufa walipokuwa wachanga.

Magumu Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2

Katika Aprili 1939, kabla tu ya mwanzo wa Vita ya Ulimwengu 2, vikosi vya Ufashisti vya Kiitalia vilishambulia Albania. Upesi baada ya hilo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku, lakini kikundi chetu kidogo cha wapiga-mbiu wa Ufalme karibu 50 kiliendelea kuhubiri. Vitabu na vijitabu vyetu vipatavyo 15,000 vilitwaliwa na kuharibiwa wakati wa Vita ya Ulimwengu 2.

Jani Komino alikuwa na ghala kubwa ya fasihi iliyoshikana na nyumba yake. Majeshi ya Kiitalia yalipopata kujua kwamba hivyo vitabu vilikuwa vimechapishwa Marekani, yaliudhika. “Nyinyi ni waenezaji wa propaganda! Marekani inapinga Italia!” wao wakasema. Wale ndugu vijana wenye bidii Thomai na Vasili Cama walikamatwa, na ilipojulikana kwamba hivyo vitabu walivyokuwa wakigawanya vilikuwa vimetoka kwa Komino, yeye pia akakamatwa. Upesi mimi nikaitwa na polisi ili kuhojiwa.

“Je, wawajua wanaume hawa?” wakaniuliza.

“Ndiyo,” nikajibu.

“Je, wewe hufanya kazi nao?”

“Ndiyo,” nikajibu. “Sisi ni Mashahidi wa Yehova. Hatuzipingi serikali. Sisi hatuungi mkono upande wowote.”

“Je, umekuwa ukigawanya fasihi hizi?”

Nilikubali, walinifunga pingu, nami nikatiwa gerezani mnamo Julai 6, 1940. Humo nilijiunga na wengine watano kutoka kijiji changu—Josef Kaci, Llukan Barko, Jani Komino, na wale ndugu (wa kimwili) akina Cama. Tukiwa gerezani tulikutana na Mashahidi wengine watatu—Gori Naçi, Nikodhim Shyti, na Leonidas Pope. Sote tisa tulikuwa tumesongamana katika jela yenye ukubwa wa meta 1.8 kwa meta 3.7!

Baada ya siku chache, tulifungwa pamoja kwa mnyororo na kupelekwa jiji la Përmet. Miezi mitatu baadaye tulihamishwa hadi gereza lililoko Tiranë na kufungwa kwa miezi mingine minane bila kuhukumiwa.

Hatimaye, tulipelekwa mbele ya mahakama ya kijeshi. Ndugu Shyti nami tulihukumiwa kifungo cha miezi 27, Ndugu Komino miezi 24, na wale wengine waliachiliwa huru baada ya miezi 10. Sisi tulihamishwa hadi gereza la Gjirokastër, ambako Ndugu Gole Flloko alisaidia kufanya tupate kibali cha kuachiliwa katika 1943. Baadaye familia yetu ilifanya makao katika jiji la Përmet, ambako nikawa mwangalizi wa kutaniko lile dogo.

Hata ingawa kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku na Vita ya Ulimwengu 2 iliendelea katika nchi zilizotuzunguka, tuliendelea kufanya kile ambacho tungeweza ili kutimiza utume wetu wa kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Mathayo 24:14) Katika 1944 jumla ya Mashahidi 15 walikuwa gerezani. Hata hivyo, katika nyakati hizo ngumu, hatukuhisi kamwe kuwa tumeachwa na Yehova.

Kutahiniwa Juu ya Suala la Kutokuwamo

Ingawa vita iliisha 1945, magumu yetu yaliendelea nayo hata yakawa mabaya zaidi. Kupiga kura kwa lazima kulitekelezwa wakati wa uchaguzi wa Desemba 2, 1946. Yeyote yule aliyethubutu kutopiga kura alionwa kuwa adui wa Serikali. Wale wa kutaniko letu katika Përmet wakaanza kuuliza, “Twapaswa tufanyeje?”

“Ikiwa mwamtumainia Yehova,” nikajibu, “hampaswi kuniuliza jambo la kufanya. Tayari mwajua kwamba watu wa Yehova hawaungi mkono upande wowote. Wao si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:16.

Siku ya uchaguzi ikaja, na wajumbe wa serikali wakaja nyumbani kwetu. Wakaanza hivi kwa utulivu, “Ah, acheni tunywe kikombe cha kahawa na kuongea. Je, wajua leo ni siku gani?”

“Ndiyo, uchaguzi unafanywa leo,” nikajibu.

“Ni afadhali uharakishe, au utachelewa,” ofisa mmoja akasema.

“La, sina nia ya kwenda. Kura yetu ni kwa Yehova,” nikajibu.

“Haya basi, njoo upigie kura upinzani.”

Nikaeleza kwamba Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote kabisa. Msimamo wetu ulipojulikana na wengi, tuliwekewa mkazo zaidi. Tuliamuriwa tuache kufanya mikutano yetu, kwa hiyo tukaanza kukutana kwa siri.

Kurudi Kijijini Kwetu

Katika 1947 familia yangu nami tukarudi Mbreshtan. Muda mfupi baadaye, katika alasiri moja ya Desemba yenye ubaridi sana, niliitwa ofisini mwa Sigurimi (polisi wa siri). “Je, wajua ni kwa nini nimekuita?” huyo ofisa akauliza.

“Nawazia ni kwa sababu umesikia mashtaka dhidi yangu,” nikajibu. “Lakini Biblia husema kwamba ulimwengu ungetuchukia, kwa hiyo mashtaka hayanishangazi.”—Yohana 15:18, 19.

“Usiongee juu ya Biblia nami,” akaitikia kwa ukali. “Nitakupiga vibaya sana.”

Huyo ofisa na watu wake wakaondoka lakini wakaniamuru nisimame nje katika baridi. Baada ya muda fulani akaniita tena ofisini mwake na kuniamuru niache kufanya mikutano nyumbani kwetu. “Ni wangapi wanaoishi kijijini mwako?” yeye akauliza.

“[Watu] mia na ishirini,” nikasema.

“Wao ni wa dini gani?”

“Othodoksi ya Kialbania.”

“Na wewe?”

“Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”

“Watu mia moja na ishirini hufuata njia moja na wewe hufuata nyingineyo?” Kisha akaniamuru niwashe mishumaa kanisani. Nilipomwambia kuwa nisingefanya hivyo, akaanza kunipiga kwa ufito. Ilikuwa karibu saa saba usiku nilipoachiliwa hatimaye.

Ugavi wa Fasihi Wakatizwa

Baada ya Vita ya Ulimwengu 2 kuisha, tulianza kupokea Mnara wa Mlinzi tena kupitia posta, lakini hatimaye magazeti hayakuwa yakipokewa tena. Halafu, usiku mmoja saa nne, niliitwa na polisi wa siri. “Gazeti la Kigiriki limewasili,” nikaambiwa, “nasi tungependa utueleze yote ambayo linahusu.”

“Mimi sijui Kigiriki vizuri sana,” nikasema. “Jirani yangu akijua vizuri zaidi. Labda yeye aweza kuwasaidia.”

“La, twataka wewe ueleze jambo hili,” ofisa mmoja akasema huku akitoa baadhi ya nakala za Kigiriki za Mnara wa Mlinzi.

“Ah, haya ni yangu!” nikapaaza sauti. “Bila shaka, naweza kueleza jambo hili. Mwaona, magazeti haya hutoka Brooklyn, New York. Hapo ndipo mahali makao makuu ya Mashahidi wa Yehova yapo. Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini yaonekana kama kwamba walikosea juu ya anwani. Magazeti haya yangalipaswa kupelekwa kwangu, si kwenu.”

Wao walikataa kunipa hayo magazeti, na tangu wakati huo hadi 1991, zaidi ya miaka 40 baadaye, sisi hatukupokea fasihi zozote za Biblia Albania. Wakati wa miaka hiyo yote, tuliendelea kuhubiri, tukitumia Biblia zetu pekee. Karibu Mashahidi 20 walikuwa gerezani katika 1949; wengine walikuwa na vifungo vya miaka mitano.

Magumu Yaongezeka

Katika miaka ya 1950, watu waliamuriwa wabebe hati za kuonyesha kwamba waliunga mkono jeshi. Lakini Mashahidi wa Yehova walikataa kubeba hati hizo. Kwa sababu hiyo, Ndugu Komino nami tulikaa katika jela kwa miezi mingine miwili.

Wakati ambapo Serikali iliruhusu kuwapo kwa dini fulani-fulani, tulikuwa na kadiri fulani ya uhuru. Hata hivyo, katika 1967 dini zote zilipigwa marufuku, hilo likifanya Albania iwe kirasmi nchi isiyoamini kabisa kuwako kwa Mungu. Mashahidi waliendelea kujaribu kufanya mikutano, lakini hilo likawa jambo gumu sana. Wengine wetu tukashonelea bitana zetu za koti kifuko cha pekee ili tuweze kuficha Biblia ndogo. Halafu tulikuwa tukienda kwenye shamba fulani ili kuisoma.

Mashahidi katika Tiranë wakashikwa, na watatu wakapewa kifungo cha miaka mitano katika kambi ya kufanyia kazi nzito iliyokuwa mbali. Likiwa tokeo, familia zao ziliteseka. Wale kati yetu tuliotoka vijiji vidogo, vya mbali, hatukupelekwa mbali kwa sababu hatukuonwa kuwa tisho kubwa. Lakini kutokuwamo kwetu kuliongoza kwenye kuondoshwa kwa majina yetu katika orodha za wale wa kupewa chakula. Kwa hiyo, maisha yalikuwa magumu sana. Pia, wengine wawili wa watoto wetu wakafa. Hata hivyo hatukuhisi kamwe kuwa tumeachwa na Yehova.

Hofu ilienea Albania. Kila mtu alikuwa akitazamwa, na polisi wa siri waliandika ripoti juu ya yeyote aliyethubutu kueleza wazo lililo tofauti na lile la chama chenye kutawala. Kwa hiyo tulikuwa waangalifu sana juu ya kuandika ripoti juu ya utendaji wetu. Hatukuweza kukutana kwa ajili ya kitia-moyo cha kiroho katika vikundi vilivyo vikubwa zaidi ya watu wawili au watatu. Bado, hatukuacha kamwe kuhubiri.

Wakijitahidi kusababisha mvurugo miongoni mwa akina ndugu, polisi wa siri walieneza uvumi kwamba Shahidi fulani mashuhuri katika Tiranë alikuwa mpelelezi. Hilo lilifanya wengine wapoteze uhakika wao nalo likavuruga muungano wetu kwa kadiri fulani. Kwa sababu ya kutokuwa na fasihi zozote za Biblia za karibuni na kutoweza kuwasiliana na tengenezo la Yehova lionekanalo, wachache waliruhusu hofu iwashinde.

Kwa kuongezea, wenye mamlaka walieneza uvumi kwamba Spiro Vruho, aliyekuwa mzee Mkristo mwenye kustahiwa sana katika Albania, alikuwa amejiua. “Mwaona,” wao wakasema, “hata Vruho amekata tamaa.” Baadaye ikawa wazi kwamba Ndugu Vruho alikuwa kwa kweli ameuawa kimakusudi.

Katika 1975, Argjiro nami tulikaa na mwana wetu katika Tiranë kwa miezi michache. Wakati wa uchaguzi, wenye mamlaka jijini walituwekea mkazo kwa kututisha hivi: “Msipopiga kura, tutamnyang’anya mwana wenu kazi yake.”

“Mwanangu amekuwa akifanya kazi kwa miaka 25,” nikajibu. “Nyinyi mna rekodi za kibinafsi zenye mambo mengi juu yake na familia yake. Mimi sijapiga kura kwa zaidi ya miaka 40. Kwa kawaida habari hiyo huwa katika rekodi za wafanyakazi. Ikiwa haimo, basi rekodi zenu zina kasoro. Ikiwa imo katika rekodi zenu, basi hamjawa waaminifu-washikamanifu kwa chama kwa kumruhusu afanye kazi kwa miaka mingi hivyo.” Waliposikia hilo, wenye mamlaka wakasema kwamba ikiwa tungerudi Mbreshtan, wao wasingesisitiza juu ya jambo hilo.

Mabadiliko Makubwa Sana

Katika 1983 tulihama Mbreshtan hadi jiji la Laç. Muda mfupi baadaye, katika 1985, yule mtawala wa kimabavu akafa. Yeye alikuwa ametawala tangu ule uchaguzi wa lazima wa kwanza katika 1946. Hatimaye, sanamu yake, iliyokuwa mahali mashuhuri pa uwanja mkubwa katika Tiranë, pamoja na ile ya Stalin zilibomolewa.

Wakati wa miongo ya kupigwa marufuku kwa utendaji wetu, Mashahidi wengi walitendewa kikatili, na wengine wakauawa. Mtu mmoja aliwaambia Mashahidi wengine barabarani hivi: “Wakati wa Wakomunisti, sisi sote tulikuwa tumemwacha Mungu. Ni Mashahidi wa Yehova pekee walioendelea kuwa waaminifu kwake yajapokuwa majaribu na magumu.”

Kadiri uhuru zaidi uliporuhusiwa, watu tisa waliripoti utendaji katika huduma ya Kikristo katika Juni 1991. Katika Juni 1992, mwezi mmoja baada ya marufuku kuondolewa, watu 56 walishiriki katika kazi ya kuhubiri. Mapema mwaka huo tulijawa na shangwe kuwa na watu 325 wakihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Tangu wakati huo idadi ya wanaohubiri imeongezeka hadi zaidi ya 600, na jumla ya watu 3,491 walihudhuria Ukumbusho mnamo Aprili 14, 1995! Katika miaka ya juzijuzi imekuwa shangwe kubwa kwangu kuona vijana wengi wakiongezwa katika makutaniko yetu.

Argjiro ameendelea akiwa mwaminifu kwa Yehova na amekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwangu miaka hii yote mingi. Nilipokuwa gerezani au nikisafiri katika kazi ya kuhubiri, yeye alitunza mahitaji ya familia yetu kwa subira bila lalamiko. Mmoja wa wana wetu na mke wake walibatizwa 1993. Hilo lilitufurahisha sana.

Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu Pekee

Ninafurahi kuona tengenezo la Yehova katika Albania likiwa lenye muungano sana na likiwa na ufanisi wa kiroho. Nahisi kama yule Simeoni aliyezeeka katika Yerusalemu ambaye kabla ya kufa alipewa pendeleo lenye thamani sana la kumwona yule Mesiya aliyeahidiwa kwa muda mrefu. (Luka 2:30, 31) Sasa niulizwapo ni serikali ya namna ipi ninayopendelea, mimi husema hivi: “Sipendelei wala Ukomunisti wala ubepari. Iwe ni watu au ni Serikali wanaoimiliki nchi hiyo si jambo la maana. Serikali hujenga barabara, huleta nguvu za umeme hadi vijiji vya mbali, na huandaa kadiri fulani ya utaratibu. Hata hivyo, serikali ya Yehova, Ufalme wake wa kimbingu, ndilo suluhisho pekee kwa matatizo magumu yanayokabili Albania na pia sehemu nyinginezo za ulimwengu.”

Kile ambacho watumishi wa Mungu wanafanya duniani pote katika kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu si kazi ya binadamu yeyote. Hii ni kazi ya Mungu. Sisi ni watumishi wake. Ingawa tumekuwa na magumu mengi Albania na kwa muda mrefu hatukuweza kuwasiliana na tengenezo la Yehova lionekanalo, hatukuachwa kamwe naye. Roho yake ilikuwapo sikuzote. Yeye alituongoza kwenye kila hatua njiani. Nimeona hili muda wote wa maisha yangu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki